Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Watu Waaminifu wa Zamani Walijiacha Waongozwe na Roho ya Mungu

Watu Waaminifu wa Zamani Walijiacha Waongozwe na Roho ya Mungu

Watu Waaminifu wa Zamani Walijiacha Waongozwe na Roho ya Mungu

“Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe amenituma, ndiyo, roho yake.” —ISA. 48:16.

1, 2. Tunahitaji nini ili tuwe na imani, na tutatiwa moyo namna gani tunapofikiria watu waaminifu wa zamani?

 TANGU siku za Abeli, watu wengi wameonyesha imani, hata hivyo, “imani si mali ya watu wote.” (2 The. 3:2) Kwa nini basi mutu anapaswa kuwa na sifa hiyo, na ni nini kinachoweza kumusaidia awe mwaminifu? Mara nyingi, imani inatokana na mambo tunayosikia katika Neno la Mungu. (Rom. 10:17) Ni sehemu ya tunda la roho takatifu ya Mungu. (Gal. 5:22, 23) Kwa hiyo, ili mutu awe na imani na kuionyesha, anahitaji roho takatifu.

2 Ni makosa kufikiri kwamba wanaume na wanawake walio na imani, wamezaliwa nayo. Watumishi waaminifu wa Mungu wanaozungumuziwa katika Biblia walikuwa watu ‘wenye hisia kama zetu.’ (Yak. 5:17) Walikuwa na mashaka, na uzaifu mbalimbali, walijisikia kuwa hawana uwezo, lakini “walifanywa kuwa wenye nguvu” kupitia roho ya Mungu ili kushindana na matatizo. (Ebr. 11:34) Tunapofikiria jinsi roho ya Yehova ilivyowasaidia, tunaweza pia kutiwa moyo ili tuendelee kuwa waaminifu hasa wakati huu ambao imani yetu inajaribiwa na mambo mengi.

Roho ya Mungu Ilimutia Musa Nguvu

3-5. (a) Namna gani tunajua kwamba roho takatifu ilimusaidia Musa atimize madaraka yake? (b) Mufano wa Musa unatufundisha nini kuhusu jinsi Yehova anavyotutolea roho yake?

3 Kati ya watu walioishi katika mwaka wa 1513 mbele ya Kristo, Musa alikuwa ‘mupole zaidi.’ (Hes. 12:3) Mungu alimupa mutumishi wake huyo daraka kubwa la kuongoza taifa la Israeli. Roho ya Mungu ilimupatia uwezo wa kutabiri, kuhukumu, kuandika, kuongoza, na kufanya miujiza. (Soma Isaya 63:11-14.) Lakini, siku fulani, Musa alinungunika kwamba daraka lake lilikuwa nzito sana kwake. (Hes. 11:14, 15) Kwa hiyo, Yehova ‘akaondoa sehemu ya roho’ iliyokuwa juu ya Musa na akaiweka juu ya wanaume wengine 70 ili wamusaidie kubeba muzigo huo. (Hes. 11:16, 17) Ijapokuwa Musa alifikiri kwamba daraka lake lilikuwa nzito sana, kwa kweli, hakuwa akiubeba muzigo huo yeye mwenyewe—na hata wanaume hao 70 waliochaguliwa ili kumusaidia, hawangeubeba muzigo huo wao wenyewe.

4 Musa alikuwa amepewa roho takatifu yenye kutosha ili atimize daraka lake. Hata kisha kuwatolea wanaume hao 70 sehemu fulani ya roho, Musa aliendelea kuwa na roho aliyohitaji. Musa hakubaki na sehemu ndogo ya roho wala wazee hao 70 hawakupokea sehemu ya roho yenye kuzidi. Vivyo hivyo, Yehova anatutolea kiasi cha roho tunachohitaji kulingana na hali zetu. Yeye “Hatoi roho kwa kipimio” lakini anatoa “kutokana na wingi alio nao.”—Yoh. 1:16; 3:34.

5 Je, unavumilia majaribu? Je, madaraka yako yanaongezeka na unaona kwamba yanakuchukua wakati mwingi? Je, unajikaza kutosheleza mahitaji ya kiroho na ya kimwili ya familia yako wakati ambapo vitu vinazidi kupanda bei na afya yako inazidi kuwa mbaya? Je, una madaraka mazito katika kutaniko? Uwe hakika kwamba kupitia roho yake, Mungu anaweza kukupatia nguvu unayohitaji ili kupambana na kila hali.—Rom. 15:13.

Roho Takatifu Ilimusaidia Bezaleli

6-8. (a) Roho ya Mungu iliwasaidia Bezaleli na Oholiabu kufanya nini? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Bezaleli na Oholiabu waliongozwa na roho ya Mungu? (c) Kwa nini mufano wa Bezaleli ni wenye kutia moyo kabisa?

6 Bezaleli aliishi wakati wa Musa; mambo aliyotimiza yanatusaidia kuona jinsi roho ya Mungu inavyoweza kumusaidia mutu. (Soma Kutoka 35:30-35.) Bezaleli alichaguliwa ili aongoze kazi ya kutengeneza vitu vya lazima kwa ajili ya maskani. Je, alikuwa na ufundi wa mambo hayo mbele apewe mugawo huo? Labda, lakini inaonekana kwamba kazi aliyofanya hapo mbele ilikuwa ya kutengenezea Wamisri matofali. (Kut. 1:13, 14) Namna gani basi, Bezaleli angetimiza kazi ile ngumu aliyopewa? Yehova ‘alimujaza roho yake katika hekima, katika uelewaji na katika ujuzi na katika kila aina ya ufundi na kwa ajili ya kubuni vyombo, ili kufanya vifaa sanifu vya kila namna.’ Hata ikiwa Bezaleli alizaliwa na uwezo wa ufundi fulani, roho takatifu ilimuongezea uwezo huo. Ilikuwa hivyo pia kuhusu Oholiabu. Ni wazi kwamba Bezaleli na Oholiabu walifikia kuijua vizuri kazi yao, kwa kuwa zaidi ya kutimiza kazi yao waliwafundisha pia wengine namna ya kufanya kazi vizuri. Ndiyo, Mungu alichochea mioyo yao ili wawafundishe wengine.

7 Ushuhuda mwengine unaoonyesha kwamba Bezaleli na Oholiabu waliongozwa na roho ya Mungu ni kwamba kazi waliyofanya ilidumu. Vitu walivyotengeneza viliendelea kutumiwa miaka 500 baadaye. (2 Nya. 1:2-6) Tofauti na mafundi wengi wa leo wanaoandika majina yao juu ya vitu walivyofanya ao wanaopenda majina yao yajulikane, Bezaleli na Oholiabu hawakufanya hivyo. Wao walipenda kwamba heshima zote zimuendee Yehova.—Kut. 36:1, 2.

8 Leo, tunaweza kupewa kazi inayoogopesha na inayoomba ufundi wa pekee, kama vile kujenga, kutumia mashini za kuchapisha, kusimamia mikusanyiko, kusimamia kazi ya kutolea misaada ndugu waliopatwa na misiba, na kupashana habari na madaktari ili kutetea musimamo wetu kuhusu damu. Wakati fulani, kazi hizo zinafanywa na ndugu wenye ufundi, lakini mara nyingi zinafanywa na ndugu wanaojitolea ambao hawakupata ujuzi wa pekee kuhusu kazi hizo. Roho ya Mungu inawasaidia kufanya kazi hizo vizuri. Je, umewahi kukataa mugawo fulani katika utumishi wa Yehova, ukifikiri kwamba wengine ndio wanaweza kuutimiza vizuri zaidi kuliko wewe? Kumbuka kwamba, roho ya Yehova inaweza kukuongezea ujuzi na uwezo na inaweza kukusaidia utimize mugawo wowote unaopewa.

Roho ya Mungu Ilimusaidia Yoshua Kuongoza

9. Waisraeli walijikuta katika hali gani baada ya kutoka Misri, na hilo lilitokeza ulizo gani?

9 Roho ya Mungu iliongoza pia mwanaume mwengine aliyeishi wakati wa Musa na Bezaleli. Muda mufupi baada ya kutoka Misri, Waamaleki walianza kuwashambulia watu wa Mungu. Wao walilazimika kupigana. Ijapokuwa hawakuzoea vita, Waisraeli walilazimika kupigana vita kwa mara ya kwanza tangu watoke katika utumwa. (Kut. 13:17; 17:8) Walihitaji kiongozi wa jeshi. Ni nani ambaye angeliongoza?

10. Kwa nini Yoshua na Waisraeli walipata ushindi?

10 Yehova alimuchagua Yoshua. Lakini ikiwa angeulizwa kazi aliyokuwa akifanya huko Misri ambayo ingemufanya astahili daraka hilo, unajua yeye angesema nini? Mutumwa? Mutengeneza matofali? Muokota mana? Yoshua hakujua jambo lolote kuhusu vita. Ni wazi kwamba, babu ya Yoshua Elishama alikuwa kapita wa kabila la Efraimu na labda aliongoza jeshi la watu 108,100 wa kabila moja kati ya makabila tatu ya Israeli. (Hes. 2:18, 24; 1 Nya. 7:26, 27) Hata hivyo, Yehova hakumwambia Musa amuchague Elishama ao mwana wake Nuni, lakini alimuchagua Yoshua ili aliongoze jeshi na kushinda maadui zake. Mapigano yalichukua muda murefu siku hiyo. Kwa kuwa Yoshua alimutii kabisa Mungu na alikubali mwongozo wa roho takatifu, Waisraeli walipata ushindi.—Kut. 17:9-13.

11. Namna gani tunaweza kutimiza utumishi mutakatifu kama Yoshua?

11 Baada ya muda, Yoshua, “mwenye kujaa roho ya hekima,” alichukua nafasi ya Musa. (Kum. 34:9) Roho takatifu haikumutolea uwezo wa kufanya miujiza na kutoa unabii kama Musa, lakini ilimusaidia kuongoza Israeli katika vita ili kuchukua inchi ya Kanaani. Leo, tunaweza kujisikia hatuna uwezo ao hatustahili kutimiza sehemu fulani ya utumishi wetu mutakatifu. Lakini kama Yoshua, tuko hakika kwamba tutaweza ikiwa tunafuata kwa ukaribu maagizo ya Yehova.—Yos. 1:7-9.

‘Roho ya Yehova Ilimufunika Gideoni’

12-14. (a) Ushindi wa waaskari 300 juu ya majeshi ya Wamidiani unatuhakikishia nini? (b) Namna gani Yehova alimuhakikishia Gideoni ushindi? (c) Leo, Mungu anatuhakikishia nini?

12 Baada ya kifo cha Yoshua, Yehova aliendelea kutumia roho yake ili kuwatia nguvu watumishi wake waaminifu. Kitabu cha Waamuzi kinajaa masimulizi ya watu ambao “kutoka hali ya uzaifu walifanywa kuwa wenye nguvu.” (Ebr. 11:34) Kupitia roho takatifu, Mungu alimuchochea Gideoni apiganie Israeli. (Amu. 6:34) Hesabu ya jeshi la Wamidiani ilizidi mara ine Jeshi la Gideoni. Machoni pa Yehova, ilionekana kwamba kikundi kidogo hicho kilikuwa bado na watu wengi sana. Yehova alimwambia Gideoni mara mbili apunguze hesabu ya jeshi lake hivi kwamba hesabu ya Wamidiani ilizidi mara 450 jeshi la Israeli. (Amu. 7:2-8; 8:10) Hilo jeshi ndogo ndilo Yehova alikubali. Kwa hiyo, Waisraeli watakaposhinda vita, hakuna mutu ambaye angesema kwa majivuno eti tumeshinda kwa sababu tuna akili ao nguvu ya vita.

13 Gideoni na jeshi lake walikuwa tayari kwa ajili ya vita. Ikiwa ungekuwa mumoja wa kikundi hicho kidogo, je, ungejisikia salama huku ukiona kwamba wenzako wamerudishwa nyumbani kwa sababu walikuwa na woga ao kwa sababu hawakuwa waangalifu? Ao je, ungekuwa na woga kidogo kwa kufikiria jinsi mambo yatakavyokuwa? Gideoni alimutegemea Mungu. Alifanya yale Mungu alimwamuru kufanya! (Soma Waamuzi 7:9-14.) Yehova hakukasirika Gideoni alipomwomba amuonyeshe alama fulani ili awe hakika kwamba atakuwa pamoja naye. (Amu. 6:36-40) Lakini alimusaidia ili awe na imani yenye nguvu.

14 Uwezo wa Yehova wa kuwaokoa watu wake hauna mipaka. Anaweza kuwaokoa na kila hali ngumu akitumia hata wale ambao wanaonekana kuwa wazaifu ao wasio na uwezo. Wakati fulani tunaweza kufikiri kwamba maadui wetu ni wengi sana ao tunaweza kuwa katika hali isiyo na tumaini. Hatutazamii Yehova atutolee alama za kimuujiza kama alivyomufanyia Gideoni, lakini anaweza kututolea mwongozo na kutufariji kupitia Neno lake na tengenezo lake linaloongozwa na roho yake. (Rom. 8:31, 32) Ahadi zake zenye upendo zinatia nguvu imani yetu na zinatuhakikishia kwamba yeye ni Musaidizi wetu kabisa!

“Roho ya Yehova Ikaja juu ya Yefta”

15, 16. Kwa nini binti ya Yefta alikubali kujinyima, na hilo linawafundisha wazazi nini?

15 Tufikirie mufano mwingine. Waisraeli walipopigana na Waamoni, roho ya Yehova “ikaja juu ya Yefta.” Kwa kuwa alitaka kupata ushindi ili Mungu atukuzwe, Yefta alifanya naziri. Alimuahidi Mungu kwamba akimupatia ushindi juu ya Waamoni, atakaporudi, yule atakayetoka inje wa kwanza ili kuja kumupokea, atakuwa wa Yehova. Yefta aliporudi kisha kushinda Waamoni, binti yake akatoka inje kumupokea. (Amu. 11:29-31, 34) Je, hilo lilimushangaza Yefta? Labda hapana, kwa kuwa alikuwa na mutoto mumoja tu. Alitimiza naziri yake kwa kumutoa binti yake amutumikie Yehova mahali pake patakatifu maisha yake yote. Kwa kuwa binti ya Yefta alikuwa mwabudu mwaminifu wa Yehova, alikubali kwamba baba yake atimize naziri aliyofanya. (Soma Waamuzi 11:36.) Roho ya Yehova iliwatolea wote wawili nguvu walizohitaji.

16 Binti ya Yefta alifikia namna gani kuwa na roho hiyo ya kujinyima? Ni wazi kwamba imani yake ilijengwa alipokuwa akiona bidii ya baba yake na jinsi alivyojitolea kwa Mungu. Enyi wazazi, jueni kwamba watoto wenu wanawatazama. Maamuzi munayochukua yanawaonyesha kwamba munaamini mambo munayosema. Watoto wenu wanasikiliza sala zenu na kufuata kwa uangalifu mambo munayowafundisha na kuona jinsi munavyojikaza kumutumikia Mungu kwa moyo wote. Yote hayo yatachochea watoto wenu watamani sana kumutumikia Yehova na hilo litawaletea ninyi furaha.

“Roho ya Yehova Ikaanza Kutenda Kazi juu” ya Samsoni

17. Samsoni alifanya nini kwa musaada wa roho ya Mungu?

17 Mufano mwingine ni ule wa Samsoni. Wakati Waisraeli walichukuliwa mateka na Wafilisti, ‘Baada ya muda roho ya Yehova ikaanza kumuchochea’ Samsoni ili kuokoa Israeli. (Amu. 13:24, 25) Yehova alimupatia Samsoni nguvu ambayo hakuna mutu mwingine alikuwa nayo, ili kutimiza kazi za ajabu. Wafilisti walipowachochea Waisraeli wengine wamukamate Samsoni “roho ya Yehova ikaanza kutenda kazi juu yake, na zile kamba zilizokuwa kwenye mikono yake zikawa kama nyuzi za kitani ambazo zimeunguzwa kwa moto, nazo pingu zake zikayeyuka kutoka kwenye mikono yake.” (Amu. 15:14) Hata wakati Samsoni alipoteza nguvu zake kwa sababu alichukua uamuzi usiofaa, Mungu alimutolea nguvu “kupitia imani.” (Ebr. 11:32-34; Amu. 16:18-21, 28-30) Kwa sababu ya hali ya taabu iliyomupata, roho ya Yehova ilimusaidia Samsoni kwa njia ya pekee. Kwa kweli, masimulizi hayo yanatutia moyo sana. Namna gani?

18, 19. (a) Habari kuhusu Samsoni inatuhakikishia jambo gani? (b) Katika habari hii, namna gani mifano ya watu waaminifu wa zamani imekusaidia?

18 Leo, sisi pia tunategemea roho hiyo iliyomusaidia Samsoni. Tunaitegemea tunapotimiza kazi ambayo Yesu aliwapatia wafuasi wake; ‘kuhubiria watu na kuwatolea ushahidi kamili.’ (Mdo. 10:42) Wakati fulani inaweza kuwa vigumu kwetu kutimiza kazi hiyo. Lakini, sisi ni wenye shukrani kwa Yehova kwa kuwa anatumia roho yake ili itusaidie kutimiza kazi mbalimbali ambazo ametukabizi! Kwa hiyo, tunapotimiza kazi hiyo, tunaweza kusema kama nabii Isaya: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe amenituma, ndiyo, roho yake.” (Isa. 48:16) Bila shaka, ni roho ya Mungu ndiyo imetutuma! Tunatimiza kazi hiyo tukiwa hakika kwamba Yehova atatuongezea uwezo tunaohitaji kama alivyomufanyia Musa, Bezaleli, na Yoshua. Tunatumia “upanga wa roho, yaani, neno la Mungu,” tukiwa hakika kwamba atatupa nguvu kama alivyofanyia Gideoni, Yefta, na Samsoni. (Efe. 6:17, 18) Kwa kutegemea musaada wa Yehova ili kushinda vipingamizi, tunaweza kuwa nguvu kiroho, kama vile Samsoni alivyokuwa nguvu kimwili.

19 Kwa kweli, tumeona kwamba Yehova anawabariki walio na bidii kuhusu ibada ya kweli. Tukijiacha tuongozwe na roho ya Mungu, imani yetu itaongezeka. Katika Maandiko ya Kigiriki kuna mifano ya watu wengine waliojiacha waongozwe na roho ya Mungu. Katika habari inayofuata, tutafurahi kujifunza jinsi roho ya Mungu ilivyowasaidia watu waaminifu wakati wa mitume, yaani, mbele ya Pentekoste ya mwaka wa 33 na baada ya hapo.

Kwa nini ni jambo lenye kutia moyo kujua jinsi roho ya Mungu ilivyowasaidia . . .

• Musa?

• Bezaleli?

• Yoshua?

• Gideoni?

• Yefta?

• Samsoni?

[Maulizo ya Funzo]

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 22]

Roho ya Mungu inaweza kutusaidia tuwe nguvu kiroho kama vile Samsoni alivyokuwa nguvu kimwili

[Picha katika ukurasa wa 21]

Wazazi, mufano wenu muzuri unaweza kuchochea watoto wenu watamani sana kumutumikia Yehova