Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yeye ni Mufano Muzuri wa Kuiga Lakini Pia ni Onyo Kwetu

Yeye ni Mufano Muzuri wa Kuiga Lakini Pia ni Onyo Kwetu

Yeye ni Mufano Muzuri wa Kuiga Lakini Pia ni Onyo Kwetu

“Mungu wa Yakobo . . . atatufundisha njia zake, nasi tutatembea katika mapito yake.”—ISA. 2:3.

1, 2. Namna gani tunaweza kufaidika na mifano ya watu wanaozungumuziwa katika Biblia?

 BILA shaka unakubali kwamba unaweza kufaidika na mambo yaliyoandikwa katika Biblia. Humo utakuta mifano ya wanaume na wanawake waaminifu ambao walikuwa na mwenendo muzuri na pia sifa nzuri ambazo utafurahia kuiga. (Ebr. 11:32-34) Hata hivyo, katika Biblia utakuta pia mifano ya watu ambayo inaweza kuwa onyo, yaani, matendo na namna ya kufikiri unayopaswa kuepuka.

2 Kwa kweli, watu fulani wanaozungumuziwa katika Biblia wanaweza kuwa wakati huohuo mufano muzuri wa kuiga, na pia mufano wa kuepuka. Fikiria Daudi, alikuwa muchungaji munyenyekevu na kisha akawa mufalme mwenye nguvu. Yeye alipenda kweli na alimutegemea Yehova, katika njia hiyo alikuwa mufano muzuri. Hata hivyo, Daudi alifanya makosa mazito, alifanya uzini na Bath-sheba, alimuuwisha Uria, na aliwahesabu watu isivyofaa. Acheni tuzungumuzie mwana wake Sulemani, aliyekuwa mufalme na mwandishi wa Biblia. Kwanza tuone ni katika njia gani mbili alikuwa mufano muzuri.

“Hekima ya Sulemani”

3. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Sulemani ni mufano muzuri kwetu?

3 Sulemani Mukuu, Yesu Kristo, alisema kwamba Mufalme Sulemani ni mufano muzuri wa kuiga. Yesu aliwaambia Wayahudi fulani wenye mashaka, hivi: ‘Malkia wa kusini atasimama katika hukumu pamoja na kizazi hiki naye atakihukumu kuwa chenye hatia; kwa sababu alikuja kutoka miisho ya dunia kuisikia hekima ya Sulemani, lakini, tazama! mutu mukuu kuliko Sulemani yuko hapa.’ (Mt. 12:42) Ndiyo, Sulemani alijulikana sana kwa sababu ya hekima yake, naye alitutia moyo tutafute hekima hiyo.

4, 5. Namna gani Sulemani alipata hekima, lakini namna gani sisi tunaweza kuipata?

4 Sulemani alipoanza kutawala, Mungu alimutokea katika ndoto na akamwambia aombe anachotaka. Sulemani aliona kwamba haelewi mambo mengi; kwa hiyo aliomba hekima. (Soma 1 Wafalme 3:5-9.) Mungu alifurahia ombi lake. Kwa hiyo akamupatia Sulemani “moyo wenye hekima na wenye uelewaji” na mali. (1 Fal. 3:10-14) Kama Yesu alivyoonyesha, hekima ya Sulemani ilikuwa kubwa sana hivi kwamba malkia wa Sheba alisikia kuhusu hekima yake na akafunga safari ndefu ili aje kumwona Sulemani na kusikiliza hekima yake.—1 Fal. 10:1, 4-9.

5 Hatutazamie kupata hekima ya kimuujiza kama ile ya Sulemani. Yeye mwenyewe alisema, “Yehova mwenyewe anatoa hekima,” lakini aliandika pia kwamba tunapaswa kujikaza ili kuipata. Aliandika hivi: “Kwa sikio lako usikilize hekima kwa makini, ili uelekeze moyo wako kwenye utambuzi.” Alitumia pia maneno kama vile ‘kuita,’ na ‘kuendelea kutafuta’ hekima. (Met. 2:1-6) Bila shaka, tunaweza kupata hekima.

6. Ni katika mambo gani tunaweza kuonyesha kwamba tunaiga mufano muzuri wa Sulemani kuhusu hekima?

6 Ni vizuri kujiuliza, ‘Je, ninaipenda kabisa hekima ya Mungu kama Sulemani?’ Kwa sababu ya matatizo ya feza watu wengi wanajitolea sana kuhusu kazi yao, wanatafuta sana feza ao wanabadili maamuzi yao kuhusu aina ya masomo na miaka wanayopaswa kusoma. Wewe na familia yako muna maoni gani juu ya mambo hayo? Je, maamuzi yenu yanaonyesha kwamba munaipenda kabisa hekima ya Mungu na munaitafuta? Je, munaweza kubadilisha mawazo yenu kuhusu feza na mambo ya masomo ili muweze kutafuta hekima zaidi? Kwa kweli, kupata hekima na kuitumia kutatuletea faida milele. Sulemani aliandika hivi: “Ndipo utakapoelewa uadilifu na hukumu na unyoofu, njia yote ya yaliyo mema.”—Met. 2:9.

Sulemani Alitia Ibada ya Kweli pa Nafasi ya Kwanza Akavuna Amani

7. Namna gani Mungu alijengewa hekalu nzuri?

7 Sulemani alipoanza kutawala, muda kidogo baada ya hapo, aliamua kubadili maskani iliyokuwa ikitumiwa wakati wa Musa, na kujenga hekalu nzuri. (1 Fal 6:1) Hata ikiwa linaitwa hekalu la Sulemani, yeye hakulijenga ili ajulikane sana kuwa mutu mwenye akili ya mambo ya ujenzi ao mutu mwenye feza. Si yeye aliyekuwa mutu wa kwanza kutoa wazo la kujenga hekalu hilo; ni Daudi baba yake. Naye Yehova alimutolea Daudi maagizo kuhusu jinsi ya kulijenga hekalu na vifaa vyake vyote. Daudi alitoa feza nyingi na vitu vingi kwa ajili ya ujenzi wa hekalu. (2 Sam. 7:2, 12, 13; 1 Nya. 22:14-16) Lakini, Sulemani ndiye aliyepewa daraka la kujenga hekalu hilo na kazi hiyo ilichukua muda wa miaka saba na nusu.—1 Fal. 6:37, 38; 7:51.

8, 9. (a) Ni mufano gani Sulemani ametuachia kuhusu kutokuacha kufanya kazi njema? (b) Kwa kuwa Sulemani alitia ibada ya kweli pa nafasi ya kwanza, jambo hilo lilitokeza baraka gani?

8 Hivyo, Sulemani alituachia mufano muzuri wa kutokuacha kufanya kazi njema na kutia mambo ya maana pa nafasi ya kwanza. Hekalu lilipomalizika na kisha kuweka sanduku la agano ndani yalo, Sulemani alitoa sala mbele ya watu wote. Katika sala alimwambia Yehova hivi: “Macho yako yafunguliwe kuielekea nyumba hii usiku na muchana, kuelekea mahali ambapo ulisema hivi kupahusu, ‘Jina langu litakuwa hapo,’ ili kusikiliza sala ambayo mutumishi wako anatoa kuelekea mahali hapa.” (1 Fal. 8:6, 29) Waisraeli na wageni wangeweza kusali wakielekea hekalu hilo, lililojengwa ili kuliheshimisha jina la Mungu.—1 Fal. 8:30, 41-43, 60.

9 Kwa kuwa Sulemani alitia ibada ya kweli pa nafasi ya kwanza, jambo hilo lilitokeza baraka gani? Kisha sherehe ya kufungua hekalu, watu ‘walishangilia na kufurahi moyoni mwao kutokana na wema wote ambao Yehova alikuwa ametenda kwa ajili ya Daudi mutumishi wake na kwa ajili ya Israeli.’ (1 Fal. 8:65, 66) Utawala wa miaka 40 wa Sulemani ulikuwa wa amani na watu walikuwa na vitu vingi vizuri. (Soma 1 Wafalme 4:20, 21, 25.) Zaburi ya 72 inashuhudia jambo hilo na inatusaidia tufikiri kuhusu baraka tutakazopata kutokana na uongozi wa Yesu Kristo, Sulemani Mukuu.—Zab. 72:6-8, 16.

Mufano wa Sulemani Ni Onyo Kwetu

10. Tunapozungumuza kuhusu Sulemani ni kosa gani nzito alilofanya tunalofikiria mara moja?

10 Kwa nini tunaweza kusema kwamba maisha ya Sulemani ni onyo pia kwetu? Huenda ukafikiria mara moja wake wa kigeni ambao Sulemani alioa na masuria wake. Tunasoma hivi: ‘Ikawa kwamba wakati Sulemani alipokuwa muzee, wake zake wakawa wameugeuza moyo wake ukaifuata miungu mingine; na moyo wake haukuwa mukamilifu kwa Yehova.’ (1 Fal. 11:1-6) Bila shaka hautapenda hata kidogo kufuata mufano huo mubaya. Lakini je, ni onyo hilo moja tu tunalopata katika maisha ya Sulemani? Acheni tuone mambo mengine kuhusu maisha yake tunayoweza kusahau kwa urahisi, na ambayo yanaweza kuwa onyo kwetu.

11. Tunajifunza nini kutokana na ndoa ya kwanza ya Sulemani?

11 Sulemani alitawala kwa muda wa miaka 40. (2 Nya. 9:30) Basi, tunaweza kujifunza nini kutokana na 1 Wafalme 14:21? (Soma.) Andiko hilo linatuonyesha kwamba Sulemani alipokufa, mwana wake Rehoboamu alianza kutawala akiwa na miaka 41, na jina la mama yake lilikuwa “Naama Mwamoni.” Hilo linaonyesha kwamba mbele Sulemani awe mufalme, alioa mwanamuke mugeni kutoka taifa adui lililokuwa likiabudu miungu ya uongo. (Amu. 10:6; 2 Sam. 10:6) Je, mwanamuke huyo aliendelea kuiabudu miungu hiyo? Hatujui ikiwa aliendelea kuabudu miungu hiyo ao ikiwa aligeuka na kuwa mwabudu wa kweli, kama walivyofanya Rahabu na Rutu. (Rut. 1:16; 4:13-17; Mt. 1:5, 6) Kwa hivyo, inaonekana kwamba Sulemani alikuwa na wakwe na watu wa jamaa kupitia muke huyo ambao hawakuwa wakimwabudu Yehova.

12, 13. Sulemani alichukua uamuzi gani mubaya alipoanza kutawala, na labda alifikiri namna gani?

12 Sulemani alipokuwa mufalme mambo yaliharibika zaidi. Alifanya ‘mapatano ya ndoa pamoja na Farao mufalme wa Misri, akamuchukua binti ya Farao, akamuleta katika Jiji la Daudi.’ (1 Fal. 3:1) Je, mwanamuke huyo Mumisri alianza kumwabudu Yehova kama Rutu alivyofanya? Biblia haisemi lolote kuhusu jambo hilo. Hata hivyo baadaye, Sulemani alimujengea nyumba (na labda aliwajengea pia wajakazi wake) inje ya Jiji la Daudi. Kwa nini? Maandiko yanasema kwamba alifanya hivyo kwa sababu mwabudu wa uongo hakustahili kuishi karibu ya sanduku la agano.—2 Nya. 8:11.

13 Labda Sulemani alifunga ndoa na binti wa mufalme wa Misri kwa sababu ya faida fulani za politike. Lakini hiyo haikuwa sababu yenye kukubalika. Tangu zamani, Mungu alikataza Waisraeli wasifunge ndoa na Wakanaani, aliwatolea hata majina ya mataifa hayo ya Wakanaani. (Kut. 34:11-16) Labda Sulemani alifikiri kwamba angeweza kufanya hivyo kwa sababu Misri haikutajwa kati ya mataifa hayo. Hata hivyo, je, Mungu angekubali sababu hiyo? Kwa kweli, alipuuza hatari iliyokuwa wazi ambayo Yehova alionyesha, yaani ya kumugeuza Mwisraeli aache ibada ya kweli.—Soma Kumbukumbu 7:1-4.

14. Tunaweza kufaidika na onyo gani kutokana na mufano mubaya wa Sulemani?

14 Je, mufano wa Sulemani unaweza kuwa onyo kwetu? Dada fulani anaweza kutoa visababu anapokosa kutii agizo la Mungu la kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Kor. 7:39) Pia, ndugu anaweza kuanza kutoa visabu ili kushiriki katika michezo ao kushirikiana na vikundi fulani kwenye masomo hata ikiwa halazimishwe kabisa, ao kuficha mapato yake ili asilipe kodi kama inavyoombwa, ao kusema uongo anapoulizwa jambo fulani la haya alilofanya. Tukumbuke kwamba tunaweza kujikuta katika hatari ya kutoa visababu ili tusimutii Mungu, kama alivyofanya Sulemani.

15. Namna gani Yehova alimwonyesha Sulemani rehema? Hata hivyo, ni jambo gani tunalopaswa kukumbuka?

15 Jambo lingine ni kwamba hata ikiwa Sulemani alifunga ndoa na binti huyo wa mufalme wa Misri, Biblia inaeleza kwamba Mungu alimutolea hekima aliyoomba, na Akamwongezea pia utajiri. (1 Fal. 3:10-13) Sulemani alipuuza maagizo ya Mungu, lakini hakuna andiko linaloonyesha kwamba Yehova alimukataa mara moja asiwe mufalme ao kwamba alimuazibu vikali. Sababu ni kwamba Mungu anajua kuwa sisi ni wanadamu wasiokamilika pia sisi ni mavumbi. (Zab. 103:10, 13, 14) Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba mambo tunayofanya yanaweza kuwa na matokeo mabaya sasa ao baadaye.

Sulemani Alikuwa na Wake Wengi Sana!

16. Sulemani alipuuza sheria gani kwa kuchukua wake wengi?

16 Katika kitabu cha Wimbo wa Sulemani, mufalme anamusifu binti fulani aliye bikira, kwamba alikuwa murembo sana kupita malkia 60 na masuria 80. (Wim. 6:1, 8-10) Ikiwa hesabu hiyo inaonyesha wake wa Sulemani na maasuria wake, basi alikuwa na wanawake wengi wakati huo wa utawala wake. Hata ikiwa wengi kati yao ao wote walikuwa waabudu wa kweli, Mungu alimwagiza Musa kwamba mufalme wa Israeli hapaswi ‘kuzidisha wake kwa ajili yake, ili moyo wake usigeuke kando.’ (Kum. 17:17) Hata hivyo, wakati huo pia Yehova hakumukataa Sulemani. Mungu aliendelea kumubariki Sulemani, na hata akamutumia ili kuandika kitabu cha Biblia cha Wimbo wa Sulemani.

17. Ni ukweli gani tunapaswa kila mara kukumbuka?

17 Je, hilo linaonyesha kwamba Sulemani angepuuza sheria ya Mungu na akose kuazibiwa na kwamba sisi pia tunaweza kufanya hivyo? Hapana. Hilo linaonyesha tu kwamba Mungu anaweza kumuvumilia mutu kwa muda fulani. Hata hivyo, ikiwa hatupatwe na matokeo mabaya papo hapo, hilo halimaanishe kwamba mambo yatabaki hivyo wakati wote. Tukumbuke maneno haya ya Sulemani: “Kwa maana hukumu juu ya kazi mbaya haikutekelezwa upesi, ndiyo sababu moyo wa wana wa binadamu umeazimia kabisa ndani yao kutenda yaliyo mabaya.” Pia akaongeza: “Ninajua pia kwamba mambo yatawaendea vyema wale wanaomwogopa Mungu wa kweli, kwa sababu walimwogopa.”—Mhu. 8:11, 12.

18. Namna gani mambo yaliyomupata Sulemani yanaonyesha ukweli wa Wagalatia 6:7?

18 Ni sikitiko kwamba Sulemani yeye mwenyewe hakufuata kwa uangalifu ukweli huo! Ni kweli kwamba alifanya mambo mengi mazuri na alipata baraka za Mungu. Lakini baada ya muda, alianza kufanya mabaya na mabaya. Akawa na tabia ya kutotii sheria za Mungu. Hilo linaonyesha ukweli wa maneno haya ambayo mutume Paulo aliandika: ‘Musipotoshwe: Mungu si wa kuzihakiwa. Kwa maana lolote lile analopanda mutu, atavuna hilo pia’! (Gal. 6:7) Mwishowe, Sulemani alivuna matunda mabaya kwa sababu hakufuata mwongozo wa Mungu. Biblia inasema: ‘Mufalme Sulemani akawapenda wake wengi wageni pamoja na binti ya Farao, wanawake Wamoabu, Waamoni, Waedomu, Wasidoni na Wahiti.’ (1 Fal. 11:1) Labda wengi kati ya wake hao waliendelea kuabudu miungu yao, na hivyo walimuharibu Sulemani. Alipotoshwa na hakukubaliwa tena na Mungu wetu mwenye uvumilivu.—Soma 1 Wafalme 11:4-8.

Tujifunze Kutokana na Mufano Wake Muzuri ao Mubaya

19. Kwa nini tunaweza kusema kwamba katika Biblia tuna mifano mingi mizuri tunayoweza kuiga?

19 Yehova alimwongoza Paulo kupitia roho yake aandike: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” (Rom. 15:4) Katika mambo hayo yaliyoandikwa tunakuta wanaume na wanawake wengi waliokuwa mifano mizuri na wenye imani kubwa. Ndiyo sababu Paulo aliandika: ‘Nami nitasema nini zaidi? Kwa maana nitakosa wakati nikiendelea kusimulia juu ya Gideoni, Baraka, Samsoni, Yeftha, Daudi na vilevile Samweli na wale manabii wengine, ambao kupitia imani walishinda falme katika mapambano, wakatenda uadilifu, wakapata ahadi, kutoka hali ya uzaifu wakafanywa kuwa wenye nguvu.’ (Ebr. 11:32-34) Tunaweza kufaidika na mifano mizuri iliyo katika Maandiko, na tunapaswa kuwaiga watu hao.

20, 21. Kwa nini unaazimia kuendelea kujifunza kutokana na mifano iliyo katika Neno la Mungu?

20 Hata hivyo, maisha ya watu fulani wanaozungumuziwa katika Biblia ni onyo kwetu. Kati ya watu hao kuna wale ambao wakati fulani walikubaliwa na Yehova kuwa watumishi wake. Tunaposoma Biblia tunaweza kutambua ni wapi na namna gani watumishi fulani wa Mungu walipotoka, na hivyo wakawa mifano ya kuonya. Tunaweza kutambua namna wengine, hatua kwa hatua, walianza kuwa na mawazo mabaya, na namna walivyochukua maamuzi ambayo mwishowe yaliwaletea matokeo mabaya. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mifano hiyo? Kila mumoja wetu anaweza kujiuliza: ‘Namna gani mutu huyo alianza kuwa na mawazo mabaya? Je, hilo linaweza pia kunipata? Ninaweza kufanya nini ili kuepuka jambo hilo na kufaidika na onyo hili?’

21 Bila shaka, tunapaswa kufikiria kwa uangalifu mifano hiyo, kwa kuwa Paulo aliandika hivi: “Mambo hayo yaliendelea kuwapata kuwa vielelezo, nayo yaliandikwa ili kuwa onyo kwetu sisi ambao tumefikiwa na miisho ya mifumo ya mambo.”—1 Kor. 10:11.

Umejifunza Nini?

• Kwa nini katika Biblia kuna mifano ya kufuata na mifano ambayo ni onyo?

• Namna gani Sulemani alifikia kuwa na mwenendo mubaya katika maisha yake?

• Makosa ya Sulemani yanatupatia onyo gani?

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Sulemani alitumia hekima aliyopewa na Mungu

[Picha katika ukurasa wa 12]

Je, unajifunza kutokana na makosa ya Sulemani?