Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Wakristo wa Kweli Wanaliheshimu Neno la Mungu

Wakristo wa Kweli Wanaliheshimu Neno la Mungu

Wakristo wa Kweli Wanaliheshimu Neno la Mungu

“Neno lako ni kweli.”​—YOH. 17:17.

TAFUTA MAJIBU KWA MAULIZO HAYA:

Namna gani mukutano uliofanywa huko Yerusalemu katika mwaka wa 49 ni tofauti na mikutano ya viongozi wa kidini ya miaka iliyofuata?

Ni watu fulani gani walitetea Neno la Mungu walioishi kuanzia kipindi cha miaka ya 1000 mupaka ya 1400?

Ni njia gani ya kujifunza Biblia Wakristo waaminifu walitumia mwishoni mwa miaka ya 1800, na kwa nini njia hiyo ilikuwa na matokeo mazuri?

1. Taja jambo la maana lililokuhakikishia kwamba Mashahidi wa Yehova ni tofauti na dini zingine.

 FIKIRIA siku ambayo ulizungumuza kwa mara ya kwanza na Shahidi wa Yehova. Ni jambo gani unalokumbuka kuhusu mazungumuzo yenu? Watu wengi wanajibu, ‘Nilishangaa kuona kwamba Shahidi alitumia Biblia ili kujibu maulizo yangu yote.’ Lilikuwa jambo lenye kufurahisha kujua kusudi la Mungu kuhusu dunia, kujua hali ya watu waliokufa, na kujua kwamba watu tunaowapenda sana watafufuliwa wakati ujao!

2. Ni sababu gani zilizokufanya uheshimu Biblia?

2 Hata hivyo, tulipojifunza zaidi Biblia, tulitambua kwamba zaidi ya kujibu maulizo yetu kuhusu uzima, kifo, na wakati wetu ujao, Biblia inatufunulia mambo mengine mengi. Tulielewa kwamba ulimwenguni pote Biblia ndicho kitabu kilicho na mashauri yenye kusaidia kuliko vitabu vingine. Mashauri yake hayachuye, na wale wanaofuata mashauri hayo wanakuwa na maisha yenye furaha. (Soma Zaburi 1:1-3.) Wakristo wa kweli hawaioni Biblia, “kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.” (1 The. 2:13) Kuzungumuzia kwa kifupi maisha ya watu fulani wa wakati uliopita, kutatuonyesha tofauti iliyo kati ya wale wanaoliheshimu Neno la Mungu na wale wasioliheshimu.

TATIZO KUBWA LINATATULIWA

3. Ni tatizo gani lililohatarisha umoja wa Wakristo wa wakati wa mitume, na kwa nini ilikuwa vigumu kulitatua?

3 Miaka 13 kisha Kornelio kutiwa mafuta kulitokea tatizo kubwa lililohatarisha umoja wa Wakristo. Watu wengi wa Mataifa walianza kumukubali Kristo. Jambo hilo lilitokeza ulizo; Je, wanaume walipaswa kutahiriwa kulingana na desturi ya Wayahudi mbele wabatizwe? Haikuwa rahisi kwa Muyahudi kujibu ulizo hilo. Wayahudi walioshika Sheria ya Musa hawangesubutu kuingia katika nyumba ya watu wa Mataifa, wala hata kufanya urafiki nao. Wayahudi waliokubali kuwa Wakristo walikuwa tayari wamekwisha kuteswa vikali kwa sababu walikuwa wameiacha dini yao. Kukaribisha watu wa Mataifa wasiotahiriwa kama ndugu zao kulipaswa kuwakasirisha Wayahudi zaidi, na kufanya wasielewane hata kidogo.​—Gal. 2:11-14.

4. Ni nani waliokutana ili kutatua tatizo la kutahiriwa, na hilo lingetokeza maulizo gani?

4 Katika mwaka wa 49, mitume na wazee huko Yerusalemu, wao wenyewe wakiwa Wayahudi wenye kutahiriwa, ‘walikusanyika pamoja ili waliangalie jambo hilo.’ (Mdo. 15:6) Katika mukutano wao hakukuwa mabishano ya kiteolojia kuhusu mambo ya dini ao mambo yasiyo ya lazima, lakini mazungumuzo yenye kupendeza kuhusu mafundisho ya Biblia. Kila mutu alitoa maoni yake kuhusu tatizo hilo. Je, waliruhusu maamuzi yao yaongozwe na mapendezi yao ao ubaguzi? Je, wanaume wazee hao wangengojea mupaka wakati hasira kuhusu Wakristo katika Israeli ingetulia, ndipo wachukue uamuzi? Ao mwishowe wangekubaliana tu kuhusu jambo fulani ambalo hapo mbele hawakuamini kuwa ni sawa ili tu kufanya uamuzi wa mwisho wa mambo ambayo hawakubaliane?

5. Namna gani mukutano uliofanywa huko Yerusalemu mwaka wa 49 ulikuwa tofauti na mikutano ya wakubwa wa kidini iliyofanywa miaka iliyofuata?

5 Kwenye mikutano ya wakubwa wa kidini, ni kawaida watu wakubali mambo ambayo kwa kweli hawakukubaliana nayo. Lakini haikuwa hivyo kwenye mukutano uliofanywa huko Yerusalemu. Wote walikubaliana kwa umoja kuhusu uamuzi uliochukuliwa. Namna gani? Hata ikiwa mawazo yao yalikuwa tofauti, wote waliokuwa hapo waliheshimu Neno la Mungu, na hivyo maandishi hayo matakatifu yaliwasaidia kutatua tatizo hilo.​—Soma Zaburi 119:97-101.

6, 7. Namna gani maandiko yalisaidia ili kutatua tatizo linalohusu kutahiriwa?

6 Andiko lililosaidia kutatua tatizo hilo ni Amosi 9:11, 12. Andiko la Matendo 15:16, 17 linarudilia andiko hilo la Amosi na linasema hivi: ‘Nitarudi na kukijenga upya kibanda cha Daudi ambacho kimeanguka chini; nami nitayajenga upya mabomoko yake na kukisimamisha tena, ili watu wanaobaki wamutafute Yehova kwa bidii, pamoja na watu wa mataifa yote, watu wanaoitwa kwa jina langu, asema Yehova.’

7 Lakini mutu anaweza kusema, ‘andiko hilo halisemi kwamba haikuwa lazima watu wasio wa Mataifa walioamini kutahiriwa.’ Ni kweli, lakini hivyo ndivyo Wayahudi waliokubali kuwa Wakristo wangeelewa jambo hilo. Kwa nini? Kwa kuwa Wayahudi waliwaona ‘watu wa mataifa’ waliotahiriwa kuwa ndugu zao. (Kut. 12:48, 49) Kwa mufano, kulingana na tafsiri ya Bagster katika Septuajinti, Esteri 8:17 inasema hivi: ‘Watu wengi wasio Wayahudi wakatahiriwa, na wakawa Wayahudi.’ Kwa hiyo, wakati Maandiko yalitabiri kwamba mabaki ya nyumba ya Israeli (Wayahudi na watu wasio Wayahudi waliotahiriwa) pamoja na “watu wa mataifa yote” (wasiotahiriwa) wangekuwa taifa moja linaloitwa kwa jina la Mungu, mambo yalieleweka. Watu wasio Wayahudi waliotaka kuwa Wakristo hawakuombwa kutahiriwa.

8. Kwa nini iliomba ujasiri ili kuchukua uamuzi kuhusu tatizo la kutahiriwa?

8 Wanaume hao Wakristo waliongozwa na Neno la Mungu na roho yake ili “wafikie kauli moja.” (Mdo. 15:25) Hata ikiwa uamuzi huo ungetokeza mateso zaidi kwa Wayahudi waliokubali kuwa Wakristo, wanaume hao waaminifu walifanya uamuzi wao utegemee kabisa Biblia.​—Mdo. 16:4, 5.

TOFAUTI INAKUWA WAZI

9. Ni nini lililochafua ibada ya kweli, na ni fundisho gani la musingi ambalo lilipotoshwa?

9 Mutume Paulo alitabiri kwamba baada ya kifo cha mitume, mafundisho ya kweli ya Kikristo yangechafuliwa na mafundisho ya uwongo. (Soma 2 Wathesalonika 2:3, 7.) Kati ya wale ambao hawakufuata “fundisho lenye afya” kulikuwa na wale waliokuwa na madaraka katika kutaniko. (2 Tim. 4:3) Paulo aliwaonya wazee wa siku zake hivi: “Kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Mdo. 20:30) The New Encyclopædia Britannica inaeleza sababu kubwa iliyowaongoza kwenye mafikiri yaliyopotoka: ‘Wakristo waliofundishwa filozofia fulani ya Kigiriki walianza kutumia maneno ya filozofia hiyo ili kufasiria mafundisho ya Kikristo. Walifanya hivyo ili wajionyeshe kuhusu ujuzi waliopata na ili wageuze wapagani wenye elimu wawe Wakristo.’ Fundisho la musingi ambalo lilipotoshwa na mawazo ya kipagani lilihusu kujua ikiwa Yesu Kristo ni nani. Biblia inamwita Mwana wa Mungu; lakini wapenda filozofia ya Kigiriki walikazia kwamba yeye ni Mungu.

10. Namna gani fundisho la kutaka kujua ikiwa Yesu Kristo ni nani lingepata jibu?

10 Jambo hilo la kujua ikiwa Yesu Kristo ni nani lilifanyiwa ubishi sana kwenye mikutano mikubwa ya viongozi wa kidini ya kuamua mambo. Walioshiriki mikutano hiyo, wangepata jibu kwa urahisi ikiwa wangechunguza kwa uzito yale Maandiko yanasema, lakini wengi hawakufanya hivyo. Wengi walikuwa tayari wamechukua uamuzi mbele hata mukutano kuanza, na walingangania tu mawazo yao. Sheria zinazohusu mafundisho ya dini na maamuzi waliyokuwa wakichukua hayakutegemea sana Maandiko Matakatifu.

11. Ni mamlaka gani wale wanaoitwa eti Mababa wa kwanza wa Kanisa wamepewa, na kwa nini?

11 Kwa nini viongozi hao wa kidini hawakuchunguza Maandiko sana? Mutu mwenye elimu anayetafsiri maneno ya Biblia Charles Freeman anasema kwamba wale wanaoamini kwamba Yesu ni Mungu ‘wana magumu ya kukataa maneno mengi ya Yesu yanayoonyesha kwamba Mungu Baba ni mukuu kuliko yeye.’ Kwa hivyo, desturi za kidini na maoni ya wakubwa wa kidini yalichukua nafasi ya Injili. Mupaka leo, viongozi wengi wa kidini, wanategemea sana maneno ya wale wanaoitwa eti Mababa wa kwanza wa Kanisa kuliko kutegemea Neno la Mungu! Ikiwa umekwisha kuzungumuzia fundisho la utatu pamoja na mutu aliyesomea kwenye seminere, labda umeona akifanya hivyo.

12. Mutawala wa Roma alikuwa na mamlaka gani yasiyofaa juu ya kanisa?

12 Mutawala wa Roma alikuwa na mamlaka sana katika mikutano hiyo. Kuhusiana na hilo, Profesa Richard E. Rubenstein anaandika hivi kuhusu Baraza la Nicée: ‘Constantin, mutawala mupya, alipendelea [maaskofu] na kuwatajirisha sana kuliko walivyowazia. Kabla ya mwaka mumoja, Constantin aliwarudishia makanisa yao yote ao kuwajengea mapya, na hivyo aliwasaidia waanze tena kufanya kazi na kupewa heshima waliyopoteza. Aliwatolea viongozi wa dini mapendeleo ambayo yalikuwa yakipewa mapadri wapagani.’ Matokeo yakawa nini? ‘Constantin akawa na mamlaka juu ya Baraza la Nicée, labda hata ya kuwaamulia maaskofu.’ Charles Freeman alihakikisha hivi: ‘Baraza hilo likaamua kwamba kuanzia hapo mutawala anapaswa kuingilia mambo ya Kanisa si tu kwa kulitegemeza lakini pia kuchukua uamuzi wa mwisho kuhusu mafundisho fulani.’​—Soma Yakobo 4:4.

13. Unafikiri ni mambo gani yaliyochochea wakubwa wa kidini walioishi kisha wakati wa mitume, wapuuze mafundisho yaliyo wazi ya Biblia?

13 Wakuu wa kidini walikuwa na tatizo la kujua vizuri ikiwa Yesu Kristo ni nani, lakini watu wengi wa hali ya chini hawakuwa na tatizo hilo. Watu wa hali ya chini walielewa na kukubali mambo waliyosoma katika Maandiko. Kwa kuwa hawakutamani feza na mamlaka ambayo mutawala alikuwa akitolea viongozi wa kidini, walijua bila matatizo cheo cha Yesu kupitia Maandiko. Mwanateolojia wa wakati huo, Grégoire wa Nysse, alitoa maelezo ya kuwazarau watu hao wa hali ya chini: ‘Wao ni wachuuzi wa mavazi, wabadilisha-feza, na wanauzisha chakula, wote ni wanateolojia. Ukiuliza mambo ya feza wanakuonyesha ni wapi imeandikwa kwamba Mwana ni tofauti na Baba. Ukiuliza bei ya mukate, jibu ni Baba ni mukubwa kuliko Mwana. Ukitaka kujua ikiwa mahali pa kuogea ni tayari, jibu unalopata ni Mwana aliumbwa.’ Kwa kweli, tofauti na wakubwa wa kidini, watu wa hali ya chini walikuwa na uwezo wa kueleza habari hizo kwa kutumia Biblia. Ikiwa Grégoire na wenzake wangewasikiliza ingekuwa vizuri!

“NGANO” NA “MAGUGU” ZINAKUA PAMOJA

14. Kwa nini tunaweza kusema kwamba kuanzia wakati wa mitume na kuendelea Wakristo watiwa-mafuta fulani wamekuwapo duniani?

14 Katika mufano mumoja, Yesu alionyesha kwamba kuanzia wakati wa mitume na kuendelea, Wakristo watiwa-mafuta wa kweli wamekuwapo duniani. Aliwalinganisha na “ngano” inayoendelea kukua pamoja na “magugu.” (Mt. 13:30) Bila shaka, hatuwezi kusema kwa uhakika ni watu gani waliokuwa watiwa-mafuta wanaofananishwa na ngano, lakini tunaweza kuhakikisha kwamba siku zote kumekuwa na watu waliotetea Neno la Mungu kwa ujasiri na kufunua mafundisho ya uwongo ya kidini. Acheni tuzungumuzie mifano fulani.

15, 16. Taja watu fulani walioliheshimu Neno la Mungu.

15 Askofu Mukuu Agobard wa Lyons, Ufaransa (779-840), alipinga ibada ya sanamu, kuweka makanisa wakfu kwa watakatifu, liturujia, na mazoea mengine yaliyo kinyume na maandiko. Askofu mwenzake Claudius, alikataa pia desturi za kanisa na akapinga mazoea ya kutolea watakatifu sala na ya kuabudu vitu vinavyofikiriwa kuwa vitakatifu. Katika miaka ya 1100, Kasisi mukuu Berengarius wa Tours, Ufaransa, alifukuzwa katika kanisa kwa kuwa alikataa fundisho la kanisa Katoliki la kwamba mukate na divai vinabadilika kimuujiza kuwa mwili na damu halisi ya Kristo. Pia, aliamini kwamba Biblia ni ya maana sana kuliko desturi za kanisa.

16 Katika miaka hiyo, kulitokea watu wawili wengine waliopenda ile kweli ya Biblia, Peter wa Bruys na Henry wa Lausanne. Peter aliacha upadri kwa kuwa hakukubali fundisho la kanisa Katoliki kuhusu kubatiza watoto wadogo, kufikiri kwamba mukate na divai vinabadilika kimuujiza kuwa mwili na damu halisi ya Kristo, sala kwa ajili ya wafu, na ibada ya musalaba. Katika mwaka wa 1140, Peter aliuawa kwa sababu ya mambo aliyoamini. Mutawa Henry, alipinga mazoea ya kupokea rushwa katika kanisa na mazoea mengine yanayohusiana na liturujia yaliyo kinyume na maandiko. Alikamatwa katika mwaka wa 1148 na akabaki katika gereza mupaka kifo.

17. Ni hatua gani za maana ambazo Waldo pamoja na wafuasi wake walichukua?

17 Karibu na wakati ambapo Peter wa Bruys alichomwa akiwa hai kwa kuwa alipinga mazoea fulani ya kanisa, mutu fulani alizaliwa ambaye baadaye alisaidia sana kutangaza ukweli wa Biblia. Jina lake lilikuwa Valdès, ao Waldo. * Tofauti na Peter wa Bruys na Henry wa Lausanne, Waldo hakuwa na cheo katika kanisa, lakini aliliheshimu sana Neno la Mungu hivi kwamba aliacha mambo ya biashara na akafanya mupango ili sehemu za Biblia zitafsiriwe katika luga za watu wa hali ya chini walioishi kusini-mashariki mwa Ufaransa. Watu fulani walifurahia ujumbe wa Biblia katika luga zao za kuzaliwa hivi kwamba wakaachia wengine mali yao na kujitoa katika kazi ya kutangazia wengine ukweli wa Biblia. Kanisa lilichukizwa sana na jambo hilo. Katika mwaka wa 1184, papa aliwafukuza katika kanisa wanaume na wanawake hao wenye bidii ambao baadaye waliitwa Wafuasi wa Waldo, na askofu aliwafukuza katika nyumba zao. Hilo liliwapatia nafasi ya kutangaza ujumbe wa Biblia mahali pengine. Mwishowe, Wafuasi wa Waldo, Peter wa Bruys, na Henry wa Lausanne na wengine waliowaunga mukono walisambaa katika sehemu mbalimbali za Ulaya. Watu wengine waliotetea ukweli wa Biblia walitokea katika miaka iliyofuata: John Wycliffe (1330-1384), William Tyndale (1494-1536), Henry Grew (1781-1862), na George Storrs (1796-1879).

“NENO LA MUNGU HALIFUNGWI”

18. Eleza njia ambayo wanafunzi wa Biblia walitumia mwishoni mwa miaka ya 1800 na kwa nini ilikuwa na matokeo mazuri.

18 Hata ikiwa walijikaza namna gani, maadui wa Biblia wameshindwa kabisa kuzuia kutangazwa kwa ile kweli ya Biblia. Andiko la 2 Timotheo 2:9 linasema, “Neno la Mungu halifungwi.” Katika mwaka wa 1870 kikundi cha wanafunzi wa Biblia walianza kutafuta ile kweli. Walitumia njia gani? Mutu fulani kati yao alikuwa akitokeza fundisho fulani. Walilizungumuzia. Waliangalia maandiko yote yenye kuhusiana na fundisho hilo, walipokuwa wakitosheka jinsi maandiko hayo yalivyopatana, walichukua uamuzi wao na kuandika mambo hayo. Je, hilo halituhakikishie kwamba wanaume hao waaminifu, “mababu wetu wa kiroho” mwishoni mwa miaka ya 1800, waliazimia kupatanisha kabisa mafundisho yao na Neno la Mungu, kama mitume na wanaume wazee wa wakati wa mitume?

19. Andiko la mwaka wa 2012 ni gani, na kwa nini ni lenye kufaa?

19 Leo mafundisho yetu yanategemea Biblia. Kwa hiyo, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova limechagua maneno ya Yesu yenye kutegemeka kuwa andiko la mwaka wa 2012: “Neno lako ni kweli.” (Yoh. 17:17) Kwa kuwa kila mutu anayetaka kukubaliwa na Mungu anapaswa kutembea katika ile kweli, acheni sisi wote tuendelee kujikaza ili tujiache kuongozwa na Neno la Mungu.

[Maelezo ya chini]

^ Valdès ameitwa wakati fulani Pierre Valdès ao Peter Waldo, lakini hatuna uhakika kuhusu jina lake la kwanza.

[Maulizo ya Funzo]

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 8]

Andiko la mwaka wa 2012 ni: “Neno lako ni kweli.”—Yohana 17:17

[Picha katika ukurasa wa 7]

Waldo

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wycliffe

[Picha katika ukurasa wa 7]

Tyndale

[Picha katika ukurasa wa 7]

Grew

[Picha katika ukurasa wa 7]

Storrs