Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Nathani—Alitetea Ibada Safi kwa Uaminifu

Nathani—Alitetea Ibada Safi kwa Uaminifu

Nathani—Alitetea Ibada Safi kwa Uaminifu

Si rahisi kumusadikisha mutu mwenye mamlaka nyingi kwamba amejiendesha vibaya na kwamba anastahili kubadilika. Je, unaweza kukutana na mutu kama huyo ikiwa unajua kwamba alimuua mutu fulani ili asipoteze heshima yake?

Mufalme Daudi wa Israeli alifanya uzinifu na Bath-sheba, na mwanamuke huyo akapata mimba. Ili kuficha zambi yao, Daudi akamuuisha bwana yake na kisha akamuchukua Bath-sheba kuwa bibi yake. Kwa muda wa miezi mingi Daudi aliendelea kuishi maisha ya unafiki, hata hivyo aliendelea pia kuwa mufalme. Lakini, Yehova hakuruhusu zambi za mufalme zibaki bila kujulikana. Akamutuma nabii wake Nathani ili akutane na Daudi.

Huo haukuwa mugawo rahisi. Ujitie pa nafasi ya Nathani. Kwa kuwa Nathani alikuwa mwaminifu kwa Yehova na alishikamana na kanuni za Mungu, bila shaka hilo lilimuchochea amukumbushe Daudi zambi zake. Namna gani nabii angemusadikisha Mufalme Daudi kwamba alihitaji kutubu?

ALIKUWA MWALIMU MWENYE BUSARA

Kwa nini usitumie dakika chache ili kusoma 2 Samweli 12:1-25? Wazia kwamba ulikua mwenye kusimama karibu na Nathani alipokuwa akimuelezea Daudi hadisi hii: ‘Palikuwa na wanaume wawili waliokuwa katika jiji moja, mumoja alikuwa tajiri na yule mwingine alikuwa maskini. Yule mwanamume tajiri alikuwa na kondoo na ngombe wengi sana; lakini yule mwanamume maskini hakuwa na chochote isipokuwa mwana-kondoo jike mumoja, aliye mudogo, ambaye alikuwa amenunua. Naye alikuwa akimuhifazi hai, na huyo kondoo alikuwa akikua pamoja naye na wanawe, wote pamoja. Kondoo huyo alikuwa akila tonge lake, na kunywa kutoka katika kikombe chake, naye alikuwa akilala kifuani pake, na kondoo huyo akawa kama binti kwake. Baada ya muda, mugeni akaja kwa yule mwanamume tajiri, lakini hakuchukua kutoka kati ya kondoo zake na ngombe zake ili kumwandalia yule musafiri aliyekuja kwake. Kwa hiyo akachukua yule mwana-kondoo jike wa yule mwanamume maskini, akamwandalia yule mutu aliyekuja kwake.’​—2 Sam. 12:1-4.

Bila shaka, kwa kuwa Daudi aliwahi kuwa muchungaji wa kondoo​—aliamini hadisi hiyo. Mufafanuzi mumoja alitoa maelezo haya: “Labda Nathani alizoea kuja kwa Daudi ili kuwatetea watu ambao walitendewa bila haki kwa sababu hawakuwa na mutu wa kuwatetea, na Daudi alifikiri kwamba Nathani alikuja kumuona kwa kusudi hilo.” Hata ikiwa ilikuwa hivyo, iliomba Nathani awe mwaminifu kwa Mungu na kuwa na ujasiri ili azungumuze na mufalme kama alivyofanya. Hadisi ya Nathani ilimukasirisha Daudi. Kwa hasira Daudi akasema: ‘Kama Yehova anavyoishi, mutu huyo aliyefanya hivyo anastahili kufa!’ Ndipo Nathani akamuelezea: “Wewe mwenyewe ndiye yule mwanamume!” Jambo hilo lilimuhuzunisha sana Daudi.​—2 Sam. 12:5-7.

Fikiria kwa nini Nathani alitumia njia hiyo. Mara nyingi mutu aliyemutendea mwengine vibaya ni vigumu aone kosa lake. Sisi wote tunakuwa na mwelekeo wa kutafuta visababu ikiwa matendo yetu yanatiliwa shaka. Lakini hadisi ya Nathani ilimufanya Daudi ajihukumu bila kujua. Mufalme alitambua waziwazi kwamba mwenendo wa mutu ambaye Nathani alieleza ulikuwa wenye kuhuzunisha. Kwa hiyo, kisha tu Daudi kuhukumu mutu huyo, ndipo Nathani alimufunulia mufalme kwamba mutu huyo aliyezungumuziwa katika hadisi ni yeye. Ndipo Daudi aliona uzito wa zambi aliyofanya. Hilo lilimufanya akubali karipio. Alikubali kwamba ‘alimuzarau’ Yehova kupitia mwenendo wake kuhusiana na Bath-sheba, na alikubali karipio.​—2 Sam. 12:9-14; Zab. 51, maandishi ya utangulizi.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na habari hiyo? Kusudi la mutu anayefundisha Biblia ni kusaidia wasikilizaji wafikie uamuzi unaofaa. Nathani alimuheshimu Daudi na kwa hiyo alizungumuza naye kwa busara. Nathani alijua kwamba moyo wa Daudi ulipenda uadilifu na haki. Kwa hiyo alitumia hadisi ambayo alijua ingevutia mutu aliyekuwa na sifa hizo. Sisi pia tunaweza kusaidia watu walio na moyo muzuri waelewe maoni ya Yehova. Namna gani? Kwa kuwachochea watumie mambo ambayo wanajua kuwa ni sawa, lakini tutafanya hivyo bila kuwaonyesha kwamba sisi ndio watu wazuri kuliko wao ao kwamba tunajua mambo mengi ya kiroho kuliko wao. Biblia, ndiyo inapaswa kutuonyesha jambo la haki na lisilo la haki, wala si maoni yetu wenyewe.

Zaidi ya yote, uaminifu kwa Mungu ulimusaidia Nathani kumukaripia mufalme huyo mwenye mamlaka nyingi. (2 Sam. 12:1) Uaminifu kama huo utatufanya tuwe na ujasiri wa kutetea kanuni za Yehova zenye haki.

ALITEGEMEZA IBADA SAFI

Inaonekana kwamba Nathani na Daudi walikuwa marafiki, kwa kuwa Daudi alimupatia mutoto wake mumoja jina la Nathani. (1 Nya. 3:1, 5) Anapozungumuziwa kwa mara ya kwanza katika Biblia, Nathani yuko kati ya watu waliokuwa pamoja na Daudi. Wote wawili walimupenda Yehova. Mufalme alimutumaini kabisa Nathani kwa kuwa alimufunulia nabii huyo nia yake ya kumujengea Yehova hekalu. Daudi alisema hivi: “‘Tazama, mimi ninakaa katika nyumba ya mierezi, lakini sanduku la Mungu wa kweli linakaa katikati ya vitambaa vya mahema.’ Basi Nathani akamwambia mufalme: ‘Kila jambo lililo moyoni mwako​—nenda, lifanye, kwa sababu Yehova yupo pamoja nawe’”​—2 Sam. 7:2, 3.

Kwa kuwa Nathani alikuwa mwabudu mwaminifu wa Yehova, alikubali kwa shauku mupango huo wa Daudi wa kujenga mara ya kwanza duniani mahali pa ibada safi penye kudumu. Kwenye pindi hiyo, inaelekea kwamba Nathani alitoa maoni yake mwenyewe kuliko kutoa maoni ya Yehova. Usiku huo, Mungu alimuagiza nabii wake amupelekee mufalme ujumbe tofauti: Daudi hangestahili kujenga hekalu la Yehova. Mutu atakayelijenga atakuwa mumoja wa wana wa Daudi. Nathani alimutangazia Daudi kwamba Mungu alikuwa akifanya agano pamoja naye, kwamba kiti chake cha ufalme kitafanywa ‘imara mupaka wakati usio na kipimo.’​—2 Sam. 7:4-16.

Mawazo ya Nathani kuhusu kujenga hekalu hayakupatana na mapenzi ya Mungu. Hata hivyo, bila kunungunika, nabii huyo munyenyekevu alikubali na kuunga mukono kusudi la Yehova. Ni mufano muzuri wa kuiga kabisa ikiwa Mungu anaturekebisha katika njia fulani! Mambo ambayo nabii Nathani alifanya baadaye yanaonyesha kwamba aliendelea kukubaliwa na Mungu. Kwa kweli, inaonekana kwamba Yehova alimupatia Nathani nabii na pia Gadi mwonaji wa mufalme, roho yake, ili wamushauri Daudi kuweka wanamuziki 4 000 katika hekalu.​—1 Nya. 23:1-5; 2 Nya. 29:25.

ALITETEA UFALME

Nathani alijua kwamba ni Sulemani atakayekua mufalme mahali pa Daudi aliyekuwa amezeeka. Kwa hiyo, Nathani alitenda mara moja wakati Adoniya alipojaribu kuchukua ufalme kwa kinguvu wakati Daudi alipokuwa muzee sana. Wakati huo tena Nathani alitenda kwa busara na uaminifu. Kwanza, alimushauri Bath-sheba aende kumukumbusha Daudi kiapo chake cha kumufanya Sulemani mwana wao awe mufalme. Kisha Nathani yeye mwenyewe aliingia kumuona mufalme Daudi ili kumuuliza ikiwa ni yeye aliyemuruhusu Adoniya kuwa mufalme mahali pake. Alipoona uzito wa jambo hilo, mufalme aliyekuwa amezeeka, alimutolea Nathani na watumishi wengi waaminifu maagizo ili kumutia Sulemani mafuta na kumutangaza kuwa mufalme. Adoniya alizuiwa kuchukua ufalme kinguvu.​—1 Fal. 1:5-53.

ALIKUWA MWANA-HISTORIA MUNYENYEKEVU

Ni Nathani na Gadi walioandika kitabu cha Samweli wa 1 sura ya 25 mupaka 31 na kitabu chote cha Samweli wa 2. Kuhusiana na historia zilizoongozwa na roho ya Mungu zilizoandikwa katika vitabu hivyo, inasemwa hivi: ‘Na mambo ya Daudi mufalme, ya kwanza na ya mwisho, yameandikwa katika maneno ya Samweli mwonaji na katika maneno ya nabii Nathani na katika maneno ya Gadi mwonaji.’ (1 Nya. 29:29) Inasemwa pia kwamba ni Nathani aliyeandika habari kuhusu ‘mambo ya Sulemani.’ (2 Nya. 9:29) Inaelekea sana kwamba Nathani aliendelea kutumika kwenye makao ya kifalme hata kisha kifo cha Daudi.

Mambo mengi tunayojua kuhusu Nathani labda yaliandikwa naye mwenyewe. Hata hivyo, kubaki kwake kimya kuhusiana na mambo fulani kunatufundisha mengi kumuhusu. Ni wazi kwamba Nathani alikuwa mwana​-historia munyenyekevu. Hakupenda kujifanyia jina. Kulingana na maneno ya kamusi moja ya Biblia, Nathani anaonekana katika Biblia “bila kujitambulisha na bila habari yoyote kuhusu familia yake.” Hatujue lolote kuhusu ukoo wake ao maisha yake ya pekee.

ALICHOCHEWA NA UAMINIFU KWA YEHOVA

Kupitia mambo machache ambayo Biblia inaeleza kuhusu Nathani, ni wazi kwamba alikuwa munyenyekevu lakini pia muteteaji mwenye bidii wa mipango ya kimungu. Yehova Mungu alimupatia madaraka mazito. Tafakari juu ya sifa za Nathani, kama vile uaminifu kwa Mungu na kupendezwa sana na matakwa ya Mungu. Ujikaze kuiga sifa hizo.

Labda hautatumwa ili kwenda kumukaripia mufalme ambaye amefanya uzinifu ao kuzuia mupango wa mutu fulani anayependa kuwa mutawala. Hata hivyo, Mungu anaweza kukusaidia ili ubaki mwaminifu kwake na kutegemeza kanuni zake za haki. Unaweza pia kufundisha ukweli kwa ujasiri lakini pia kwa busara na kutegemeza ibada safi.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kwa kuwa Nathani alikuwa muteteaji wa ufalme, alizungumuza na Bath-sheba kwa busara