Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tabia Inayoweza Kuharibu Mawazo Yako—Wivu

Tabia Inayoweza Kuharibu Mawazo Yako—Wivu

Tabia Inayoweza Kuharibu Mawazo Yako​—Wivu

Napoléon Bonaparte alikuwa nao. Jules César alikuwa nao. Alexandre le Grand alikuwa nao. Ijapokuwa walikuwa na nguvu na utukufu, wanaume hao walikuwa na wivu katika mioyo yao; tabia inayoweza kuharibu mawazo ya mutu. Kila mumoja wa wanaume hao watatu alisikilia ao kuonea mwengine wivu.

Filozofe mumoja Muingereza, Bertrand Russell aliandika hivi: ‘Napoléon alimusikilia César wivu, César alimusikilia Alexandre le Grand wivu, na labda Alexandre alimusikilia Hercule wivu, Hercule ambaye hakuwahi kuishi.’ Kila mutu anaweza kuambukizwa na wivu, iwe mutu ana mali nyingi, iwe ana sifa za namna gani, iwe amepata nini maishani.

Wivu ni hali ya kuonea kijicho ao kuwa na kinyongo kuelekea wengine kwa sababu ya vitu vyao, mali yao, faida fulani wanazopata, na kazalika. Kitabu kimoja kinachofasiria maneno ya Biblia kinasema kwamba wivu ni tamaa ya kupenda kuwa sawasawa na mwengine, na kutamani kuwa na kitu cha mwengine. Zaidi ya kutamani vitu vya mutu mwingine, mutu mwenye sifa hiyo mbaya anapenda kitu cha mwengine kiwe chake.

Kwa hiyo, ni jambo la hekima kujua jinsi wivu unavyoweza kuanza katika mioyo yetu na matokeo yake. Ni lazima hasa tujue mambo tunayopaswa kufanya ili wivu usitutawale.

ROHO INAYOWEZA KUCHOCHEA WIVU

Wanadamu wasio wakamilifu wana “mwelekeo wa kuona wivu.” Lakini kuna tabia zinazoweza kuchochea na kukomaza mwelekeo huo. (Yak. 4:5) Mutume Paulo anazungumuzia jambo moja alipoandika hivi: ‘Na tusiwe wenye kujisifu, wenye kuchochea mashindano juu ya mutu na mwenzake, tukioneana wivu.’ (Gal. 5:26) Roho ya mashindano inaweza kutufanya tuwe watu wenye wivu sana. Dada Cristina na ndugu José * walijionea ukweli wa jambo hilo.

Dada Cristina, ambaye ni painia wa kawaida anasema: “Mara nyingi ninajikuta nikiwasikilia wivu wengine. Ninalinganisha mambo waliyo nayo na yale ambayo mimi sina.” Siku moja, Cristina alikuwa akila chakula pamoja na mwangalizi mwenye kusafiri na bibi yake. Akijua kwamba yeye na bwana yake Eric, walikuwa na miaka ya kuzaliwa karibu moja na mwangalizi mwenye kusafiri na bibi yake na kwamba wao pia walikuwa na migawo hiyo wakati uliopita, Cristina akawaambia: “Bwana yangu pia ni muzee! Basi, kwa nini ninyi muko katika utumishi wa kusafiri lakini sisi hatuna pendeleo hilo?” Roho ya ushindani ndiyo iliyochochea wivu wake, ikamupofusha akili ili asione kazi nzuri ambayo yeye na bwana yake walikuwa wakifanya na kujisikia kuwa hatosheki na maisha yao.

José alitamani sana kuwa mutumishi wa huduma katika kutaniko lao. Wengine walipotiwa kuwa watumishi wa huduma, akawasikilia wivu na akamuchukia muratibu wa baraza la wazee. José anakubali hivi: “Wivu ulinifanya nimuchukie ndugu huyo na kumuwazia vibaya. Wivu unapomutawala mutu hawezi tena kufikiri vizuri, anakuwa mwenye kujifikiria tu.”

MIFANO ILIYO KATIKA BIBLIA INATUFUNDISHA NINI?

Katika Biblia tuna mifano mingi inayotuonya. (1 Kor. 10:11) Mifano fulani inatuonyesha jinsi wivu unavyoanza na jinsi unavyowaharibu wale wanaojiacha kutawaliwa nao.

Tuchukue mufano wa Kaini, mwana wa kwanza wa Adamu na Hawa. Aliwaka hasira wakati Yehova hakukubali zabihu yake lakini akakubali zabihu ya Abeli. Kaini angeweza kuamua kufanya yaliyo sawa, lakini wivu ukamupofusha akili hivi kwamba akamuua ndugu yake. (Mwa. 4:4-8) Si ajabu kwamba Biblia inamutaja Kaini kuwa mutu “aliyetokana na yule mwovu,” Shetani!​—1 Yoh. 3:12.

Ndugu kumi wa Yosefu walimusikilia wivu kwa sababu ya uhusiano wa pekee aliokuwa nao na baba yao. Walimuchukia Yosefu hata zaidi wakati aliwaelezea ndoto zake za kiunabii alizoota. Walitaka hata kumuua. Mwishowe, walimuuzisha akawa mutumwa, na bila huruma wakamudanganya baba yao kwamba Yosefu amekufa. (Mwa. 37:4-11, 23-28, 31-33) Miaka mingi baadaye, walikubali zambi yao, wakaambiana hivi: “Bila shaka tuna hatia kuhusiana na ndugu yetu, kwa sababu tuliona nafsi yake ikitaabika alipotuomba kwa bidii tumwonee huruma, lakini sisi hatukusikiliza.”​—Mwa. 42:21; 50:15-19.

Wivu wa Kora, Dathani, na Abiramu, ulichochewa walipolinganisha mapendeleo yao na yale ya Musa na Haruni. Walimushitaki Musa kwamba alipenda ‘kujifanya mukuu’ juu ya wengine. (Hes. 16:13) lakini, shtaka hilo lilikuwa la uongo. (Hes. 11:14, 15) Yehova yeye mwenyewe ndiye aliyemuchagua Musa. Lakini waasi hao walimusikilia wivu Musa kwa sababu ya pendeleo lake. Mwishowe, Yehova aliwaua kwa sababu ya wivu wao.​—Zab. 106:16, 17.

Mufalme Sulemani alijionea matendo mabaya sana ambayo mutu anaweza kufanya kwa sababu ya wivu. Mwanamuke mumoja aliyefiwa mutoto alijaribu kusema uongo; alimufanya mwanamuke mwenzake akubali kwamba mutoto aliyekufa ni wake. Mufalme alipoamua kwamba mutoto huyo aliyekuwa muzima auawe, mwanamuke huyo muongo alikubaliana na uamuzi huo. Ndipo, Sulemani akaamua mutoto huyo apewe mama yake wa kweli.​—1 Fal. 3:16-27.

Wivu unaweza kuwa na matokeo mabaya sana. Mifano hiyo inayotoka katika Maandiko inaonyesha kwamba wivu unaweza kuongoza kwenye chuki, ukosefu wa haki, na mauaji. Pia, katika kila mufano yule aliyeonewa wivu hakufanya jambo lolote lililomufanya astahili kutendewa vibaya. Je, kuna jambo fulani tunaloweza kufanya ili wivu usitutawale? Tunaweza kuchukua hatua gani ili kushinda wivu?

JINSI YA KUSHINDA WIVU KABISA!

Tuwe na upendo na shauku ya kindugu. Mutume Petro alitolea Wakristo shauri hili: ‘Sasa kwa kuwa mumezitakasa nafsi zenu kwa kuwa watiifu kwa ile kweli tokeo likiwa ni upendo wa kindugu usio na unafiki, pendaneni sana kutoka moyoni.’ (1 Pet. 1:22) Basi, upendo ni nini? Mutume Paulo aliandika: ‘Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fazili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya.’ (1 Kor. 13:4, 5) Je, hauoni kwamba kuwa na upendo kama huo kunaweza kutuzuia tusiwasikilie wengine wivu? (1 Pet. 2:1) Kuliko kumusikilia Daudi wivu, Yonatani ‘alimupenda kama nafsi yake mwenyewe.’​—1 Sam. 18:1.

Shirikiana na watu wanaomuogopa Mungu. Mutungaji wa Zaburi ya 73 aliwasikilia wivu waovu waliokuwa na maisha ya starehe na yasiyo na matatizo. Lakini alishinda wivu huo kwa kwenda katika “patakatifu pakuu pa Mungu.” (Zab. 73:3-5, 17) Kushirikiana na waabudu wenzake, kulimusaidia mutunga-zaburi apate baraka zinazotokana na ‘kumukaribia Mungu.’ (Zab. 73:28) Kuhuzuria mikutano kwa ukawaida pamoja na waamini wenzetu Wakristo kunaweza kuwa na matokeo mazuri pia kwetu.

Tenda mema. Kisha kuona kwamba Kaini alikuwa ameingiwa na wivu na chuki, Mungu alimwambia: ‘Geuka utende mema.’ (Mwa. 4:7) ‘Kutenda mema’ kunamaanisha nini kwa Wakristo? Yesu alisema kwamba ‘tunapaswa kumupenda Yehova Mungu wetu kwa moyo wetu wote na kwa nafsi yetu yote na kwa akili yetu yote na tunapaswa kumupenda jirani yetu kama sisi wenyewe.’ (Mt. 22:37-39) Furaha tunayopata kwa kutia utumishi wa Yehova pa nafasi ya kwanza na kuwasaidia wengine ni dawa yenye nguvu ya kushinda wivu. Kuhubiri kwa bidii Ufalme na kufanya wanafunzi ni njia nzuri ya kumutumikia Mungu na kuhangaikia jirani; kufanya hivyo kunatuletea “baraka ya Yehova.”​—Met. 10:22.

‘Shangilia pamoja na watu wanaoshangilia.’ (Rom. 12:15) Yesu alifurahi wanafunzi wake walipopata matokeo mazuri katika mahubiri, na akawaambia kwamba watatimiza mengi zaidi kuliko yale ambayo yeye alitimiza. (Luka 10:17, 21; Yoh. 14:12) Watumishi wa Yehova ni wenye umoja. Ikiwa ndugu ao dada anapata matokeo mazuri, hiyo ni baraka kwetu sisi wote. (1 Kor. 12:25, 26) Kwa hiyo, tunapaswa kufurahi kuliko kusikia wivu wakati wengine wanapata mapendeleo makubwa.

SI RAHISI KUSHINDA WIVU!

Pigano tunalofanya ili kushinda wivu linaweza kuchukua muda murefu. Dada Cristina anasema hivi: “Ningali na mwelekeo wa kusikilia wengine wivu. Hata ikiwa ninachukia tabia hiyo, lakini bado ingali, na lazima niimalize kabisa.” Ndugu José pia alipigana pigano hilohilo. Anasema hivi: “Yehova alinisaidia ili nipendezwe na sifa nzuri za muratibu wa baraza la wazee. Uhusiano muzuri pamoja na Mungu umenifaidi sana.”

Wivu ni moja kati ya “matendo ya mwili,” ambayo kila Mukristo anapaswa kuepuka. (Gal. 5:19-21) Ikiwa haturuhusu wivu ututawale, tunaweza kuwa na maisha yenye furaha na kumufurahisha Baba wetu wa mbinguni, Yehova.

[Maelezo ya chini]

^ Majina yamebadilishwa.

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 17]

‘Shangilia pamoja na watu wanaoshangilia’