Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Walitangaza Neno la Mungu kwa Uhodari!

Walitangaza Neno la Mungu kwa Uhodari!

Walitangaza Neno la Mungu kwa Uhodari!

Unapopambana na upinzani, inaomba uhodari na pia ujasiri. Wakristo wa kweli wanaonyesha sifa hizo, kama inavyoonyeshwa katika vitabu kama vile “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu na Mashahidi wa Yehova​—Wapiga Mbiu wa Ufalme wa Mungu. Wakristo wa kwanza walipambana na upinzani. Hata hivyo, walimuomba Yehova awapatie roho yake ili iwasaidie kusema neno lake kwa ujasiri, sisi pia tunapaswa kufanya hivyo.​—Mdo. 4:23-31.

Kuhusu kazi yetu ya kuhubiri wakati wa vita ya kwanza ya ulimwengu, ndugu mumoja aliandika hivi: “Watumishi wa Mungu walikuwa wakigawia watu kwa bidii buku la saba Études des Écritures, ya kitabu chenye kichwa Le mystère de Dieu accompli. Kiligawanywa kuliko vitabu vingine vyote ambavyo vimewahi kugawanywa mupaka wakati huo. Trakti Habari za Ufalme Na. 1 ilitolewa mwaka wa 1918. Kisha Trakti Habari za Ufalme Na. 2 ikatokea. Trakti hiyo ilieleza kwa nini kitabu Le mystère de Dieu accompli kilikatazwa na wakuu wa serikali. Baada ya hapo, trakti Habari za Ufalme Na. 3 ikatolewa. Wakristo watiwa-mafuta waaminifu waligawa sana vichapo hivyo. Iliomba kuwa na imani na uhodari ili kugawia watu trakti Habari za Ufalme.”

Leo, wahubiri wa Ufalme wapya wanazoezwa katika mahubiri, lakini haikuwa hivyo hapo zamani. Ndugu mumoja wa Pologne, mukaaji wa huko Amerika alikumbuka siku ambayo alitokea katika mahubiri kwa mara ya kwanza, katika mwaka wa 1922. Aliandika hivi: “Siku hiyo nilisimama mbele ya biro ya muganga ao daktari na nikagonga kwenye mulango. Sikujua jinsi ya kumutolea mutu kichapo, na sikuwa nikizungumuza luga ya Kiingereza vizuri. Musaidizi wa muganga wa kike akafungua mulango. Siwezi kusahau siku hiyo, kwa kuwa nilikuwa mwenye wasiwasi na woga. Nilipofungua sakoshe yangu, vitabu vyote vikaanguka kwenye miguu ya musaidizi huyo. Sijui jambo nililosema, lakini nakumbuka kwamba nilimutolea kichapo kimoja. Mbele ya kuondoka nilijisikia tayari nikiwa mwenye ujasiri kwamba Yehova alinibariki. Siku hiyo, niligawa vijitabu vingi katika eneo hilo la biashara.”

Dada mumoja alisema kwamba “katika mwaka wa 1933 hivi, ndugu wengi walitumia motokari zilizokuwa na vikuza sauti ili kueneza ujumbe wa Ufalme.” Siku moja, dada huyo pamoja na ndugu mumoja na muke wake, walikuwa wakihubiri katika eneo lenye milima la California, huko Amerika. Dada huyo anakumbuka: “Ndugu alipandisha motokari hiyo iliyokuwa na kikuza sauti kwenye milima, nasi tukabaki chini mujini. Sauti ya ujumbe uliorekediwa ilipoanza kusikika, watu walifikiri kwamba ni sauti iliyokuwa ikitoka mbinguni. Watu wa muji walimutafuta ndugu huyo huku na huku, lakini hawakumupata. Ujumbe huo ulipofikia mwisho, tuliwaendea watu na kuwatolea ushahidi. Nilitumika na motokari zingine mbili zilizokuwa na vikuza sauti, lakini watu wengi hawakutaka kusikiliza ujumbe. Hata hivyo, walilazimishwa kusikiliza hotuba hizo kwa kuwa ujumbe uliotoka kwenye motokari hizo waliusikia wazi katika nyumba zao. Tulitambua kwamba Yehova aliruhusu namna ya kuhubiri inayofaa itumiwe kwa wakati unaofaa. Iliomba kuwa na uhodari ili kuhubiri kwa kutumia njia hiyo, jambo la maana ni kwamba njia hiyo ilitimiza kusudi lake, yaani jina la Yehova lilitukuzwa.”

Katika miaka ya 1930 na mwanzoni mwa miaka ya 1940, fono na hotuba za Biblia zilizorekodiwa zilitumiwa katika mahubiri. Dada mumoja anakumbuka: “Dada mumoja kijana alikuwa akihubiri nyumba kwa nyumba akitumia fono. Alipoanza kumusikilizisha mwenye nyumba kwenye mulango fulani, mwanaume huyo alikasirika sana hivi kwamba akaipiga fono teke na ikarushwa mupaka kwenye veranda ya inje. Hata hivyo, hakuna diske iliyovunjika. Wanaume watatu waliokuwa wakila chakula chao katika motokari iliyokuwa pembeni walikuwa wakiwatazama, hivi wakamwalika dada aje awasikilizishe rekodi hiyo, na walichukua vichapo fulani. Hilo likamutuliza.” Iliomba kuwa na uhodari ili kuvumilia majaribu kama hayo.

Dada huyo anaongeza: “Nakumbuka wakati tulipoanza kuwagawia watu magazeti barabarani katika mwaka wa 1940. Mbele ya hapo, kulikuwa maandamano ya kutangaza habari. Wakiwa kwenye mustari, ndugu na dada walitembea kandokando ya barabara wakibeba vikaratasi vyenye maandishi ‘Dini Ni Mutego na Uibaji’ na ‘Mutumikie Mungu na Kristo Mufalme.’ Wakati huohuo walitolea watu trakti tatu. Iliomba uhodari ili kushiriki katika aina hiyo ya kazi, lakini walifikia kusudi lao la kuendelea kujulisha watu jina la Mungu na kuwafanya wafahamiane na watu wake.”

Dada mwengine anasema hivi: “Haikuwa rahisi kutolea watu magazeti barabarani katika miji midogomidogo. Wakati huo Mashahidi walipambana na upinzani mukali. . . . Iliomba kuwa hodari kabisa kusimama pembeni ya barabara ukiwa na magazeti mukononi, na kuita kwa sauti ukitumia maneno fulanifulani ya kukumbukwa yaliyopendekezwa. Hata hivyo, hatukukosa mara nyingi kuhubiri Siku ya Posho. Wakati fulani, watu walikubali ujumbe wetu. Wakati mwengine vikundi vya watu wenye hasira vilituzunguka, na wakati fulani tuliondoka kwa uficho ili kuepuka kushambuliwa na vikundi hivyo.”

Ijapokuwa Mashahidi wa Yehova waliteswa wakati wa vita ya pili ya ulimwengu, waliendelea kuhubiri kwa ujasiri. Kampanye ya siku 43 iliyoanza tarehe 1 mwezi wa 12, 1940 mupaka tarehe 12 mwezi wa 1, 1941, karibu wahubiri 50 000 katika Amerika, waligawia watu vijitabu milioni 8 katika kampanye iliyoitwa “Uhodari” wakati wa kipindi cha kutoa ushuhuda.

Ndugu na dada wengi katika tengenezo la Yehova ambao leo wamezeeka wanakumbuka magumu waliyopata hapo zamani yaliyowaomba watende kwa uhodari. Wengine wanakumbuka kwamba uhodari wao ulionekana kupitia maneno waliyotumia kila mara kama vile “sukuma adui mupaka kwenye mulango wake,” ili kuonyesha kwamba waliazimia kuendelea kuhubiri kwa bidii mupaka mwisho. Hatujue ni njia gani nyingine tutatumia ili kuwatolea watu ujumbe wa Mungu mbele ya mwisho wa ulimwengu huu muovu. Iwe njia gani itatumiwa, kwa musaada wa Mungu, tutaendelea kutangaza neno la Yehova kwa imani na uhodari.

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 9]

Siku zote uhodari umehitajiwa ili kushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme