Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Kuna Uzuri Upande wa Mukono Wako wa Kuume Milele’

‘Kuna Uzuri Upande wa Mukono Wako wa Kuume Milele’

Masimulizi Kuhusu Maisha ya Watu

‘Kuna Uzuri Upande wa Mukono Wako wa Kuume Milele’

Lois Didur Anaeleza Maisha Yake

Ni mara ngapi katika maisha yako umekwisha kusema hivi, ‘Ningelijua singechukua uamuzi huo’? Kisha kupitisha miaka 50 katika utumishi wa wakati wote, sikumbuki kupatwa na jambo mbaya kwa sababu ya kuwa upande wa mukono wa kuume wa Yehova. Acheni niwaelezee kwa nini.

NILIZALIWA mwaka wa 1939 na nilikomalia katika sehemu za mashambani huko Saskatchewan, Canada, pamoja na dada zangu wane na mudogo yangu mumoja. Tulifurahia kuishi katika sehemu za mashambani. Siku moja, Mashahidi wa Yehova walikuja kwetu ili kuzungumuza na baba yangu, niliwauliza ikiwa Mungu ana jina. Wakatuonyesha jina Yehova katika Zaburi 83:18. Hilo likanifanya nitake kujua mengi kumuhusu Mungu na kuhusu Neno lake.

Katika miaka hiyo, watoto walioishi sehemu za mashambani walisomea katika chumba kimoja mupaka somo la nane. Walifanya safari ndefu kwa miguu ao kwa farasi ili kufika kwenye masomo. Walimu walikuwa wakiishi katika familia mbalimbali ambazo zilikuwa zinatosheleza mahitaji yao ya kila siku. Mwaka mumoja, wazazi wangu ndio walipaswa kumupangisha na kutosheleza mahitaji ya mwalimu mupya, John Didur.

Sikujua kwamba kijana huyo pia alipendezwa sana na Neno la Mungu. Wakati fulani nilipokuwa nikisifu serikali za Ulaya-Mashariki (usosialisti na ukoministi), ambazo baba yangu alitegemeza wakati huo, John akasema hivi kwa utulivu: “Hakuna mwanadamu aliye na haki ya kutawala wanadamu wengine. Ni Mungu tu aliye na haki hiyo.” Wazo hilo likatokeza mazungumuzo yenye kupendeza.

Kwa kuwa alizaliwa katika mwaka wa 1931, John alijua taabu ya vita. Wakati vita ya Wakorea ilianza katika mwaka wa 1950, aliuliza viongozi mbalimbali wa kidini kwa nini walijiingiza katika vita. Wote walimujibu kwamba si vibaya Wakristo kutumia silaha. Baadaye, aliuliza Mashahidi wa Yehova ulizo hilohilo. Wao walimuonyesha yale Maandiko yanasema na musimamo ambao Wakristo wa kwanza walichukua kuhusu vita. John alibatizwa katika mwaka wa 1955. Mwaka uliofuata, mimi pia nilibatizwa. Sisi wote wawili tuliazimia kumutumikia Yehova maisha yetu yote na kwa nguvu zetu zote. (Zab. 37:3, 4) Katika mwezi wa 7 mwaka wa 1957, tulioana.

Kwa kuwa katika eneo letu mikusanyiko ilikuwa ikifanyika mwezi wa 7, mara nyingi tarehe ya ukumbusho wa ndoa yetu ilikuwa ikikutana na tarehe ya mikusanyiko. Wakati huo tulifurahi kuwa kati ya ndugu na dada wengine wengi ambao waliheshimu mupango wa ndoa. Katika mwaka wa 1958 tulihuzuria kwa mara ya kwanza mukusanyiko wa kimataifa. Tulikuwa watano ambao tulichukua motokari kutoka Saskatchewan mupaka New York City. Muda wa juma moja tulikuwa tukisafiri muchana, na kila usiku tulilala katika hema. Wazia jinsi tulivyoshangaa wakati ndugu mumoja tuliyekutana naye huko Bethlehem, Pennsylvania, alipotualika tukae katika familia yake usiku huo! Ukarimu wake ulifanya tufike katika muji wa New York City tukiwa safi na wenye kuvalia vizuri. Mukusanyiko huo mukubwa ulitusaidia tufurahie kabisa pendeleo la ajabu la kumutumikia Yehova! Kama mutunga-zaburi alivyoandika, ‘kuna uzuri upande wa mukono wako wa kuume milele.’​—Zab. 16:11.

KAZI YA UPAINIA

Mwaka mumoja baadaye, katika 1959, tulianza kazi ya upainia na tuliishi katika nyumba ndogo iliyokuwa mulimani katika eneo la mashambani huko Saskatchewan. Kutoka hapo ungeweza kuona sehemu za mbali, na sehemu fulani kati ya hizo zilikuwa ndiyo eneo letu.

Siku moja, tulipokea barua moja yenye kufurahisha kutoka biro ya tawi. Nikaenda mbio mahali John alipokuwa akitembeza mashini ya kulima mashamba. Katika barua hiyo tuliombwa kuwa mapainia wa pekee katika Red Lake, Ontario. Kwa kuwa hatukujua mahali muji huo unapatikana, tulienda mbio kuangalia kwenye karte ili kujua mahali eneo hilo linapopatikana.

Mahali hapo palikuwa tofauti kabisa na sehemu za mashambani! Kulikuwa misitu mikubwa na miji midogo midogo iliyojengwa pembeni ya mahali palipochimbwa zahabu. Tulipokuwa tukitafuta mahali pa kupanga siku yetu ya kwanza, binti mumoja mudogo alisikia mazungumuzo yetu pamoja na jirani yao. Akaenda mbio kumuelezea mama yake naye akakubali kututolea makao usiku huo. Kitanda kilikuwa katika chumba kidogo kichafu. Siku iliyofuata, tulihamia katika nyumba yenye vyumba viwili isiyo na maji na vitu vingine vya lazima, isipokuwa tu mahali pa kuleta joto nyumbani. Tulinunua vitu vidogo mahali panapouzishwa vitu ambavyo vimekwisha kutumikishwa na tukatosheka na vitu hivyo.

Kutaniko lilikuwa umbali wa kilometa 209. Wafanyakazi wengi waliotumika mahali pa kuchimba zahabu walitoka Ulaya, na walituomba Biblia katika luga yao. Kwa wakati kidogo, tulikuwa na mafunzo ya Biblia 30 yenye kuendelea vizuri. Katika miezi sita, kutaniko ndogo likaundwa.

Mume wa muke mumoja tuliyekuwa tukijifunza naye alimuita padiri wao kupitia telefone ili aje kumusadikisha muke wake kwamba mambo anayojifunza ni ya uongo. Tulipokutana na padiri huyo, yeye alisema kwamba tunapaswa kufundisha pia Utatu. Mwanamuke huyo akachukua Biblia yao ya Kikatoliki na kumuambia padiri huyo aonyeshe katika Biblia mambo aliyokuwa akitetea. Padiri huyo akatupa Biblia hiyo mezani, akisema kwamba halazimishwi kuonyesha andiko lolote. Padiri huyo alipokuwa akiondoka, alisema katika luga ya Kiukrenia kwamba tulipaswa kufukuzwa katika nyumba hiyo na hatupaswi kamwe kukaribishwa tena. Hakujua kwamba John alielewa luga hiyo!

Baadaye, kisha muda kidogo, tukatoka katika muji wa Red Lake kwa kuwa John alipaswa kupata mazoezi ya kuwa mwangalizi wa muzunguko. Mwaka mumoja hivi baadaye, John alipokuwa akitoa hotuba ya ubatizo kwenye mukusanyiko wa wilaya, mume huyo alikuwa kati ya wale waliopenda kubatizwa! Jinsi padiri huyo alivyojiendesha siku hiyo ilimufanya mume huyo aanze kutafuta yeye mwenyewe ukweli katika Biblia.

MENGI YA KUFANYA KATIKA KAZI YA MUZUNGUKO

Katika kazi ya muzunguko, tulikuwa na pendeleo moja la pekee la kubaki pamoja na familia tofauti-tofauti. Tukawa marafiki sana wa ndugu na dada waliotutolea makao na mambo mengine. Siku moja, tulikuwa kwenye chumba cha juu ambacho hakikukua na mahali pa joto katika kipindi cha baridi kali. Asubuhi mapema, tulisikia dada mumoja muzee akiingia kwa utulivu katika chumba chetu ili kuwasha moto kwenye mafiga ndogo. Kisha alituletea beseni yenye maji ya moto ili tuoge mbele ya kwenda katika mahubiri. Nilijifunza mengi kutokana na hali yake ya utulivu na upole.

Kazi ya muzunguko ilinisaidia nimukaribie Yehova. Muzunguko mumoja katika Alberta ulitia ndani miji iliyokuwa karibu na mahali pa kuchimba majiwe ya beyi katika Far North, mahali ambapo dada mumoja alikuwa akiishi. Je, tengenezo la Yehova lilimufikiria dada huyo aliyekuwa Shahidi peke yake huko? Kila miezi sita, tulienda huko kupitisha juma moja katika utumishi na kufanya mikutano pamoja naye, kama tu inavyoendeshwa katika kutaniko la muji wenye watu wengi. Hilo lilitukumbusha jinsi Yehova anavyohangaikia sana kila mutu aliye mufano wa kondoo.

Tuliendelea kupashana habari na wengi waliotutolea makao. Hilo lilinikumbusha moja kati ya zawadi za kwanza ambayo John alinitolea​—kibweta cha rangi-rangi kilichojaa makaratasi ya kuandikia barua. Tuliendelea kuwaandikia marafiki zetu tukitumia makaratasi hayo. Sijasahau kibweta hicho.

Tulipokuwa katika muzunguko huko Toronto, ndugu mumoja kutoka Betheli ya Canada alituita kwa njia ya telefone na kutuuliza ikiwa tunaweza kwenda kutumikia kwenye Betheli. Alipenda tujibu siku iliyofuata! Na alipata jibu letu siku hiyo.

UTUMISHI WA BETHELI

Kila mugawo tuliopewa ulitusaidia tuone sehemu mbalimbali za mambo mazuri yanayotoka katika mukono wa Yehova. Tulijionea jambo hilo pia tulipohamia Betheli katika mwaka wa 1977. Kutumika pamoja na watiwa​-mafuta fulani kulitusaidia tuone si utu wao tofauti-tofauti tu lakini pia jinsi walivyoliheshimu sana Neno la Mungu.

Tulifurahia maisha yasiyobadilika-badilika ya Betheli. Kwa mufano, mavazi yetu yalikuwa sasa katika kabati la mavazi na si katika sanduku la mavazi, na tulibaki sasa katika kutaniko moja. Zaidi ya mugawo wangu, nilifurahi kila wakati nilipoitwa ili kutembeza watu waliokuja kutembelea Betheli. Nilifurahia kuwaelezea jinsi kazi inavyoendeshwa kwenye Betheli, nilisikiliza maoni yao na kujibu maulizo yao.

Miaka ilipita haraka, basi, katika mwaka wa 1997, John alialikwa ili kuhuzuria Masomo ya Washiriki wa Halmashauri ya Tawi huko Patterson, New York. Baadaye, tuliulizwa ikiwa tungependa kutumikia Ukraine. Tulitiwa moyo kufikiria jambo hilo kwa uangalifu katika sala. Mangaribi hiyo tulijua tayari kwamba tutakubali.

MUGAWO MWINGINE​—UKRAINE

Tulihuzuria mukusanyiko mukubwa wa kimataifa katika Saint​-Pétersbourg, Russie, katika mwaka wa 1992, na kisha mukusanyiko wa Kiev, Ukraine, katika mwaka wa 1993. Mikusanyiko hiyo ilitufanya tuwapende ndugu zetu wa Ulaya-Mashariki. Makao yetu mapya katika Lviv, Ukraine, yalikuwa kwenye orofa (etaje) ya pili ya nyumba moja ya zamani. Kutoka madirisha mutu aliona vizuri uwanja ulio na bustani ndogo, jogoo mukubwa mwekundu, na vitoto vya kuku. Mahali hapo palifanana na Saskatchewan. Tulikuwa watu 12 walioishi katika nyumba hiyo. Kila asubuhi mapema tulivuka muji ili kwenda kutumika kwenye Betheli.

Tulijisikia namna gani huko Ukraine? Kuwa kati ya watu wengi waliopata majaribu, waliopigwa marufuku, na kufungwa, lakini ambao waliendelea kuwa na imani yenye nguvu lilikuwa jambo lenye kufunza unyenyekevu. Tulipowapongeza, walisema, “Tulifanya hivyo kwa ajili ya Yehova.” Hawakufikiri hata kidogo kwamba waliachwa. Hata sasa, ikiwa unamushukuru ndugu ao dada fulani kwa ajili ya wema wake, anajibu, “Sifa zimwendee Yehova,” akitambua kwamba ni Yehova aliye chanzo cha mambo yote mema.

Katika Ukraine, wengi wanatembea kwa muguu ili kwenda kwenye mikutano, kwa hiyo wana wakati wa kuzungumuza na kutiana moyo. Wanatembea muda wa saa moja ao zaidi. Kuna zaidi ya makutaniko 50 katika Lviv, kati ya makutaniko hayo, 21 yanatumia Jumba la Ufalme kubwa lenye majumba mengi. Siku ya Yenga, inapendeza kuona ndugu na dada wengi wakimiminika kuja kwenye mikutano.

Haikutuchukua muda murefu ili kujisikia vizuri, kwa kuwa tulikuwa pamoja na ndugu na dada wenye adabu na tayari kuwahangaikia wengine. Ninapokuwa na magumu ya kuelewa luga, wananisaidia kwa uvumilivu. Kupitia macho yao na maneno yao utaona kweli kwamba wanakuhangaikia.

Jambo moja lililotokea mwaka wa 2003 kwenye mukusanyiko wa kimataifa huko Kiev, linaonyesha kwamba ndugu wanatumainiana kabisa. Tuliposhuka katika sehemu iliyo chini ya udongo mahali treni inapopita, kulikuwa na watu wengi, kisha tukaona binti mumoja akija mahali tulipokuwa na kusema kwa utulivu, “Nimepotea. Simuone nkambo yangu.” Binti huyo alijua kwamba tuko Mashahidi wa Yehova kwa kuwa tulivaa karte zetu za utambulisho. Alikuwa binti hodari na hakulia. Muke wa mwangalizi wa muzunguko aliyekuwa pamoja nasi akamupeleka binti huyo katika stade kwenye biro inayoshugulikia Vitu Vilivyopotea na Kupatikana. Mwishowe binti huyo akamupata nkambo (tate) yake. Niliguswa sana moyo kuona jinsi binti huyo mudogo alivyotutumainia kabisa, hata katikati ya watu wengi sana.

Ndugu na dada wengi kutoka sehemu za mbali walikuja Ukraine katika mwezi wa 5 mwaka wa 2001 ili kusikiliza hotuba ya kufungua majengo mapya ya Betheli. Kisha hotuba ya pekee katika stade Siku ya Yenga asubuhi, ndugu na dada walimiminika ili kuja kutembelea Betheli mupya. Sijasahau hata kidogo kipindi hicho! Kuwaona ndugu na dada hao wakitembea kwa ukimya na kwa utaratibu, kulinivutia sana. Hilo liliongeza furaha yangu kuhusu mambo mazuri yanayotokana na kumutumikia Mungu.

BADILIKO KUBWA

Jambo la kuhuzunisha ni kwamba katika mwaka wa 2004, John alipatwa na magonjwa ya kansere. Tulienda Canada ili apate matunzo. Mwili wake haukuvumilia matunzo ya kwanza aliyopata hivi kwamba alipitisha majuma fulani akitunzwa kwa uangalifu sana. Jambo la kufurahisha ni kwamba alirudiwa na akili. Ijapokuwa alikuwa akisema kwa magumu, macho yake yalikuwa yakionyesha shukrani yake kwa wote waliokuja kumuona.

Lakini afya yake iliendelea kuwa mbaya, na akafa. Nikasikia kwamba nimekosewa sehemu kubwa ya mwili wangu. John nami tulifurahi sana kumutumikia Yehova pamoja. Ningefanya nini? Nikaamua kurudi Ukraine. Ninashukuru sana familia ya Betheli na kutaniko kwa upendo wenye shauku ambao wamekuwa wakinionyesha huko.

Katika maisha yetu hatukuhuzunika hata kidogo kwa sababu ya maamuzi tuliyochukua. Watu tulioshirikiana nao walifanya tuwe na maisha yenye furaha. Ninajua kwamba kungali mengi ya kujifunza kuhusu wema wa Yehova, na ninatumaini kwamba nitaendelea kumutumikia milele kwa kuwa nimepata kabisa ‘uzuri upande wa mukono wa kuume wa Yehova.’

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 6]

“Katika maisha yetu hatukuhuzunika hata kidogo kwa sababu ya maamuzi tuliyochukua”

[Picha katika ukurasa wa 3]

Tulipooana na John

[Picha katika ukurasa wa 4]

Nilipokuwa painia wa pekee katika Red Lake, Ontario

[Picha katika ukurasa wa 5]

Pamoja na John katika Ukraine, mwaka wa 2002