Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Mambo ya Kufikiria Unapoombwa Mashauri

Mambo ya Kufikiria Unapoombwa Mashauri

Mambo ya Kufikiria Unapoombwa Mashauri

Je, mutu fulani amekwisha kukuomba wewe mashauri? Kwa mufano, mutu fulani amekwisha kukuuliza hivi: ‘Naweza kufanya nini? Niende kwenye karamu hiyo ao hapana? Je, nikubali kazi hiyo ao hapana? Ninaweza kurafikiana naye nikiwa na kusudi la kufunga ndoa naye ao hapana?’

Watu wasio na mawazo mabaya wanaweza kukuomba musaada mbele ya kuchukua uamuzi fulani​—uamuzi huo unaweza kuwa na matokeo fulani juu ya uhusiano wao pamoja na rafiki, watu wa familia ao Yehova. Majibu yako yatategemea nini? Kwa kawaida wewe unafanya nini unapowashauria watu wengine? Iwe ulizo linaonekana kuwa la maana ao hapana, Methali 15:28 inasema hivi: “Moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu.” Fikiria jinsi kanuni tano za Biblia zifuatazo zinavyoweza kukusaidia unaposhauria wengine.

1 Jua Kwanza Hali ya Mutu Anayeomba Shauri.

“Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.”​—MET. 18:13.

Ili kumutolea mutu shauri nzuri, ni lazima kuelewa hali na mawazo yake. Kwa mufano, ikiwa mutu anakuita kwenye telefone na kuuliza njia anayoweza kufuata ili kufika nyumbani kwako, wewe ungepaswa kujua nini kwanza ili uweze kumuongoza? Je, utamushauri afuate njia fulani inayofaa zaidi bila kujua kwanza mahali alipo? Hapana, sivyo? Vivyo hivyo, ili kumutolea mutu musaada unaofaa anapoomba shauri, ni lazima kutambua kwanza “mahali” alipo sasa, yaani, hali yake na mawazo yake. Je, kuna mambo fulani yanayofanya ajikute katika hali hiyo; mambo tunayopaswa kufikiria mbele ya kumutolea shauri? Ikiwa hatujui vizuri hali ya yule anayetuomba shauri, tunaweza kumutolea shauri ambalo linaweza kumupoteza zaidi.​—Luka 6:39.

Tafuta Kujua jitihada Ambazo Amefanya ili Kupata Jibu. Inaweza pia kuwa jambo la hekima kumuuliza yule anayeomba musaada maulizo yafuatayo: “Ni kanuni gani za Biblia unafikiri zinahusika?” “Kuamua kama unavyofikiri kunaweza kuwa na matokeo gani mazuri ao mabaya?” “Mupaka sasa ni mambo gani ambayo umesoma kuhusu jambo hilo?” “Ni mashauri gani umekwisha kutolewa na wazee wa kutaniko, wazazi wako, ao yule anayekufundisha Biblia?”

Majibu kwa maulizo hayo yanaweza kutusaidia tutambue mutu huyo amejikaza kadiri gani ili kupata jibu. Pia, tunapomutolea shauri ni vizuri tufikirie yale ambayo wengine wamekwisha kumuambia. Tunaweza pia kutambua ikiwa mutu huyo anatafuta tu mushauri ambaye ‘atafurahisha masikio’ yake na mashauri anayopenda.​—2 Tim. 4:3.

Epuka Kujibu Haraka.

‘Kila mutu lazima awe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.’​—YAK. 1:19.

Kwa nia nzuri, tunaweza kujibu haraka. Lakini, kufanya hivyo si hekima, zaidi sana ikiwa tunazungumuzia habari ambayo hatujafanyia utafiti kabisa, sivyo? Methali 29:20 inasema hivi: ‘Je, umemuona mutu mwenye haraka kwa maneno yake? Kuna tumaini zaidi kwa mujinga kuliko kwake.’

Chukua wakati ili uhakikishe kwamba shauri lako linapatana kabisa na hekima ya Mungu. Jiulize, “Je, mawazo yangu yameingiliwa na mawazo ao ‘roho ya ulimwengu’ inayotuzunguka?” (1 Kor. 2:12, 13) Kumbuka kwamba kuwa na nia nzuri hakutoshi. Kisha kujulishwa magumu yaliyomungojea Yesu, mutume Petro alimushauria hivi: ‘Jitendee kwa fazili, Bwana; wewe hutapatwa hata kidogo na jambo hili.’ Tunaweza kujifunza nini kutokana na shauri hilo la Petro? Tunajifunza kwamba hata mutu mwenye nia nzuri anaweza kutoa shauri ambalo, “si fikira za Mungu, bali za wanadamu.” (Math. 16:21-23) Ni lazima kabisa tufikiri mbele ya kusema! Kwa vyovyote, ujuzi wetu ni mufupi sana unapolinganishwa na hekima ya Mungu, sivyo?​—Ayu. 38:1-4; Met. 11:2.

3 Onyesha Unyenyekevu Kwa Kutumia Neno la Mungu.

“Sifanyi jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; bali kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.”​—YOH. 8:28.

Je, utasema, “Ikiwa ni mimi ninge . . .”? Hata ikiwa unaelewa jibu la ulizo, ni vizuri kujifunza kutoka mufano wa Yesu, ambaye alionyesha unyenyekevu na kiasi. Hata ikiwa Yesu alikuwa na ujuzi na uzoevu wa juu sana kuliko mutu yeyote; yeye alisema hivi: ‘Sijasema kutokana na musukumo wangu mwenyewe, bali Baba mwenyewe . . . aliyenituma amenipa amri kuhusu jambo la kutangaza na la kusema.’ (Yoh. 12:49, 50) Siku zote, mafundisho na mashauri ya Yesu yalitegemea mapenzi ya Baba yake.

Kwa mufano, tunasoma kwenye Luka 22:49 kwamba wanafunzi wa Yesu walimuuliza ikiwa wanaweza kupigana wakati maadui walikaribia kumukamata. Hata hivyo, mumoja kati yao alitumia upanga. Kuhusu habari hiyohiyo, kwenye Mathayo 26:52-54 tunasoma kwamba hata katika hali ngumu kama hizo, Yesu alichukua wakati wa kufikiri pamoja na wanafunzi wake kuhusu mapenzi ya Mungu. Kwa kuwa alijua kanuni zilizo kwenye Mwanzo 9:6 na unabii wa Zaburi 22 na pia ule wa Isaya 53, Yesu alikuwa na uwezo wa kutoa mashauri yenye hekima ambayo bila shaka yaliokoa maisha ya wengi na kumupendeza Yehova.

4 Tumia Vitabu vya Kikristo.

‘Ni nani kwa kweli mutumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimuweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani, awape chakula chao kwa wakati unaofaa?’​—MATH. 24:45.

Yesu alimuchagua mutumwa mwaminifu ambaye anatoa chakula cha kiroho cha maana. Unapotoa shauri ao mwongozo kuhusu mambo ya maana, je, unachukua wakati wa kufanya utafiti katika vichapo vya mutumwa vinavyofasiria mambo yaliyo katika Biblia?

Index na Watchtower Library * vinatutolea nafasi ya kupata habari nyingi na zilizo wazi bila magumu. Ni kukosea kabisa ikiwa tunapuuza vifaa hivyo vyenye kujaa habari nyingi za maana! Kuna vichwa mbalimbali vinavyotajwa, vikiwa na habari tofauti-tofauti ili kusaidia mutu anayetafuta shauri. Je, una ufundi wa kuwasaidia wengine wachunguze kanuni za Biblia na kufikiri juu ya Neno la Mungu? Kama vile karte ao busole inavyoweza kumusaidia mutu atambue mahali alipo na kumuongoza mahali anapokwenda, vivyo hivyo, vichapo vya mutumwa vinaweza kumusaidia mutu aone njia anayochukua na kutambua jinsi ya kubaki katika njia ya uzima.

Wazee wengi wamewazoeza wahubiri kupata habari kwa kutumia Index ao Watchtower Library, kwa hiyo wanasaidia ndugu na dada jinsi ya kufikiri kupitia maandiko. Kufanya hivyo kunawasaidia wahubiri kabisa kupata majibu ya maulizo yanayowasumbua, na pia wanakuwa na zoezi la kufanya utafiti na kutegemea chakula cha kiroho ambacho Yehova anatutolea. Kwa kufanya hivyo, ‘nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’​—Ebr. 5:14.

5 Epuka Kuchukulia Wengine Uamuzi.

‘Kila mumoja ataubeba muzigo wake mwenyewe.’​—GAL. 6:5.

Mwishowe, ni daraka la kila mutu kuchagua shauri la kufuata. Sisi wote, Yehova ametupa uhuru wa kuamua ikiwa tutajiacha kuongozwa na kanuni zake ao hapana. (Kum. 30:19, 20) Hali fulani zinaomba kufikiria kanuni nyingi za Biblia, lakini, ni yule mutu anayeomba shauri ndiye anapaswa kuchukua uamuzi wa mwisho. Tunapofikiria shauri linaloombwa ao miaka ya yule anayeomba shauri, ni vizuri pia kujiuliza hivi, ‘Je, nina mamlaka kabisa ya kutoa shauri kuhusu jambo hilo?’ Kuna mambo ambayo ni wazee wa kutaniko ndio walio na mamlaka ya kuyashugulikia ao ikiwa yule anayeomba shauri ni kijana, wazazi wake wanaweza kumusaidia.

[Maelezo ya chini]

^ CD-ROM Watchtower Library inapatikana katika luga 39. Index inapatikana katika luga 45.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 8]

Kutafuta Habari ya Kuzungumuzia Kwenye Ibada ya Familia

Kwenye Ibada ya familia, munaweza kutafuta majibu kwa maulizo muliyoulizwa hivi karibuni. Utapa habari ao kanuni za Biblia wapi ili kumusaidia mutu anayeuliza maulizo? Kwa mufano, tuseme ndugu ao dada anakuuliza kuhusu kufanya urafiki na mutu fulani akiwa na kusudi la kuoana naye. Unapotumia Index ao Watchtower Library, tafuta habari zinazohusiana moja kwa moja na jambo hilo kwanza. Kwa mufano, katika Index unaweza kutafuta kichwa cha habari “Fréquentation” ao “Mariage.” Kisha chunguza vichwa vidogo-vidogo ili upate habari inayohusiana na jambo hilo. Unapopata kichwa kikubwa, tazama ikiwa kuna kichwa kidogo karibu ya kichwa hicho kikubwa ambacho kinaandikwa “Voir aussi,” kichwa hicho kidogo kinaweza kukuelekeza kwenye kichwa kingine kinachohusiana sana na jambo unalotafuta.

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Kupitia tengenezo lake, Yehova anatutolea vifaa vinavyoweza kutusaidia kutoa ao kupokea mashauri yanayofaa kabisa. Andiko la Mhubiri 12:11 linasema hivi: ‘Maneno ya wenye hekima ni kama michokoo ya kuongoza ngombe, na kama tu misumari iliyopigiliwa ndani, ndivyo walivyo wale wanaoshugulika mno kukusanya maneno; wametolewa kutoka kwa muchungaji mumoja.’ Kama vile “michokoo”​—fimbo ndefu iliyotumiwa ili kuongoza wanyama wanaokokota mizigo​—mashauri mazuri yanayochochewa na upendo yanawaongoza watu waaminifu wafuate njia inayofaa. “Misumari iliyopigiliwa” inafanya kitu kiwe imara. Vivyo hivyo, kutolea wengine shauri nzuri kunaweza kuwasaidia. Wenye hekima wanafurahi sana wanapofikiria ‘mukusanyiko wa maneno’ yanayoonyesha hekima ya ‘muchungaji wao mumoja,’ Yehova.

Sikiliza muchungaji anapokushauria. Ni pendeleo kabisa kumutolea mutu anayetega sikio mashauri yenye kusaidia tunapopewa nafasi hiyo! Ikiwa kwa kweli mashauri yetu yanategemea kanuni za Biblia, mashauri hayo yatakuwa mazuri na yanaweza kumuletea musikilizaji faida zenye kudumu.