Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tuwasaidie Watu ‘Waamuke Kutoka Katika Usingizi’

Tuwasaidie Watu ‘Waamuke Kutoka Katika Usingizi’

Tuwasaidie Watu ‘Waamuke Kutoka Katika Usingizi’

‘Munajua majira, kwamba tayari ni saa ya ninyi kuamuka kutoka katika usingizi.’​—ROM. 13:11.

JE, UNAWEZA KUELEZA?

Kwa nini ni jambo la lazima kwa Wakristo kukaa macho kiroho?

Kwa nini wahubiri wenye kukaa macho kiroho wanapaswa kuwa wasikilizaji na watazamaji wazuri?

Wema na adabu vinaweza kutusaidia namna gani katika kazi ya kuhubiri?

1, 2. Kwa nini watu wengi wanahitaji kuamuka?

 KILA mwaka, watu wengi wanakufa kwa sababu wanasinzia ao labda wanalala wanapotembeza motokari. Wengine wanafukuzwa kazini kwa kuwa hawafike kazini pa wakati kwa sababu ya usingizi ao kwa kuwa wanalala wanapokuwa kazini. Lakini usingizi wa kiroho unaweza kuwa hatari hata zaidi. Ndiyo sababu Biblia inasema: “Mwenye furaha ni yule anayekaa macho.”​—Ufu. 16:14-16.

2 Kadiri siku kuu ya Yehova inavyokaribia, wanadamu kwa ujumla ni wenye kulala kiroho. Hata viongozi wa dini fulani zinazojiita kuwa za Kikristo wamewaita waamini wao kuwa ‘majitu wenye kulala.’ Usingizi wa kiroho ni nini? Kwa nini ni lazima Wakristo wa kweli waendelee kukaa macho? Namna gani tunaweza kuwasaidia wengine waamuke kiroho?

USINGIZI WA KIROHO NI NINI?

3. Mutu anayelala usingizi wa kiroho ni mutu anayefanya nini?

3 Kwa kawaida watu wanaolala usingizi hawafanye jambo lolote. Lakini, wale wanaolala usingizi wa kiroho wanaweza kuwa na shuguli nyingi, lakini si shuguli za kiroho. Wanaweza kujishugulisha sana na mahangaiko ya kila siku ya maisha, kutafuta raha, sifa, ao utajiri. Kwa sababu ya kutafuta mambo hayo, hawahangaikie kabisa-kabisa mahitaji yao ya kiroho. Lakini, watu wanaokaa macho kiroho, wanatambua kwamba tunaishi “katika siku za mwisho,” kwa hiyo wanatenda kwa bidii kadiri wawezavyo ili kufanya mapenzi ya Mungu.​—2 Pet. 3:3, 4; Luka 21:34-36.

4. Shauri la kutoendelea kulala usingizi kama wengine, linatusaidia namna gani?

4 Soma 1 Wathesalonike 5:4-8. Katika andiko hili mutume Paulo aliwatia moyo waamini wenzake ‘wasilale usingizi kama wengine.’ Alimaanisha nini? Tunaweza ‘kulala usingizi’ ikiwa tunapuuza kanuni za Mungu zinazohusiana na mwenendo safi. Pia, tunaweza ‘kulala usingizi’ ikiwa tunasahau kuwa siku ambayo Yehova ataharibu watu wasiomuogopa imekaribia. Tunapaswa kuwa macho ili watu wasiomuogopa Mungu wasituvute kufuata njia zao na namna yao ya kufikiri.

5. Wale walio katika usingizi wa kiroho wana maoni gani?

5 Watu fulani wanafikiri kwamba hakuna Mungu atakayewahukumu. (Zab. 53:1) Wengine wanafikiri kwamba Mungu hawahangaikie wanadamu, kwa hiyo si lazima sisi pia tumuhangaikie. Lakini wengine wanafikiri kwamba kuwa waamini wa dini fulani kunawafanya wawe marafiki wa Mungu. Watu wote hao wako katika usingizi wa kiroho na wanahitaji kuamushwa. Tunaweza kuwasaidia namna gani?

NI LAZIMA SISI WENYEWE TUWE MACHO

6. Kwa nini sisi Wakristo tunapaswa kujikaza kukaa macho kiroho?

6 Ili kuwaamusha wengine, ni lazima sisi wenyewe tuwe macho. Hilo linamaanisha nini? Neno la Mungu linaonyesha kwamba mutu anayesinzia kiroho anajishugulisha na “matendo ya giza,” yaani, karamu za kupindukia, vipindi vya kulewa, uasherati, mwenendo mupotovu, mizozo na wivu. (Soma Waroma 13:11-14.) Si rahisi kuepuka matendo hayo. Kwa hiyo, ni lazima kuwa waangalifu. Ikiwa shofere anatembeza motokari akiwa mwenye kusinzia anatia maisha yake katika hatari. Ni lazima kabisa Mukristo ajue pia kwamba usingizi wa kiroho unaweza kuongoza kwenye kifo!

7. Namna gani kuwazia vibaya watu wa eneo letu kunaweza kutufanya tusifurahie kazi ya kuhubiri?

7 Kwa mufano, Mukristo anaweza kufikiri kwamba watu wote wa eneo lake hawapendi kusikia kabisa habari njema. (Met. 6:10, 11) Anaweza kufikiri hivi, ‘Ikiwa hakuna mutu atakayenisikiliza, kwa nini nijikaze kuwahubiria ao kuwasaidia watu?’ Kwa kweli, hata ikiwa watu wengi wanalala usingizi wa kiroho sasa, hali na namna yao ya kufikiri vinaweza kubadilika. Kwa hiyo, wengine kati yao wanaweza kutusikiliza. Tunaweza kuwasaidia ikiwa sisi wenyewe tunakaa macho kwa kujaribu njia zingine za kutoa ujumbe wa Ufalme kwa namna yenye kuvutia. Kukaa macho kunamaanisha pia kukumbuka kwamba kazi yetu ya kuhubiri ni ya lazima sana.

KWA NINI KAZI YETU YA KUHUBIRI NI YA MAANA SANA?

8. Kwa nini kazi yetu ya Kuhibiri ni ya maana sana?

8 Tukumbuke kwamba iwe watu wanatusikiliza ao hapana, kazi yetu ya kuhubiri inamuletea Yehova sifa na inasaidia sana katika kutimiza kusudi lake. Hivi karibuni, wale wasiotii habari njema watahukumiwa. Watu watahukumiwa kulingana na jinsi wanavyoitikia mahubiri yetu. (2 Thes. 1:8, 9) Zaidi ya hilo, ni kosa kwa Mukristo kufikiri kwamba si lazima kuhubiri kwa bidii kwa kuwa “kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Mdo. 24:15) Neno la Mungu linatusaidia kujua kwamba wale watakaoonwa kuwa ‘mbuzi watakatiliwa mbali milele.’ Kazi yetu ya kuhubiri inawasaidia watu wafaidike na rehema ya Mungu, na inawatolea nafasi ya kubadilika ili kupata “uzima wa milele.” (Math. 25:32, 41, 46; Rom. 10:13-15) Ikiwa hatuhubiri, namna gani watu watapata nafasi ya kusikiliza ujumbe unaoweza kuokoa uzima?

9. Namna gani kuhubiri habari njema kumefaidi wewe na wengine?

9 Kuhubiri habari njema kunatufaidi sisi pia. (Soma 1 Timotheo 4:16.) Je, hauoni kwamba kusema kuhusu Yehova na tumaini la Ufalme kumetia nguvu imani yako, kumefanya umupende Mungu zaidi na kumekusaidia kukomaza sifa za Kikristo? Hauoni kwamba kuhubiri kunakusaidia kuonyesha kwamba unashikamana na Mungu, na hivyo kuwa na furaha zaidi? Watu wengi ambao wemefundisha wengine kweli wamefurahi kuona jinsi roho ya Mungu imewasaidia wanafunzi hao kufanya mabadiliko.

TUWE WATAZAMAJI WAZURI

10, 11. (a) Namna gani Yesu na Paulo walijionyesha kuwa watazamaji wazuri na waangalifu? (b) Onyesha jinsi kuwa mutazamaji muzuri na mwangalifu kunaweza kukufanya uwasaidie watu wapendezwe na ujumbe wetu.

10 Kuna njia mbalimbali tunazoweza kutumia ili kuamusha watu na kuwafanya wapendezwe na habari njema. Kwa hiyo sisi wahubiri tunapaswa kuwa watazamaji wazuri tunapohubiri. Yesu ndiye mufano wetu wa kufuata. Kwa kuwa alikuwa mukamilifu, alitambua mawazo yasiyofaa ya Farisayo mumoja, toba ya kweli ya mwanamuke mufanya zambi, na roho ya kujinyima ya mujane. (Luka 7:37-50; 21:1-4) Kwa hiyo, Yesu angeweza kumusaidia kila mumoja wao kulingana na mahitaji yake ya kiroho. Hata hivyo, ili kuwa mutazamaji muzuri si lazima muhubiri awe mukamilifu. Mutume Paulo alituwekea mufano muzuri kuhusu jambo hilo. Aliambatanisha namna yake ya kuhubiri ili ivutie watu wa aina mbalimbali.​—Mdo. 17:22, 23, 34; 1 Kor. 9:19-23.

11 Ikiwa tunajikaza kuwa watazamaji wazuri na waangalifu kama Yesu na Paulo, tunaweza kutambua jinsi ya kuwasaidia watu wapendezwe na ujumbe wetu. Kwa mufano, unapokutana na mutu fulani, tafuta mambo yanayoweza kukusaidia kujua desturi, mapendezi, ao hali ya familia ya mutu huyo. Labda unaweza kutambua jambo analofanya wakati huo na kuonyesha kwamba unafurahia jambo hilo; kufanya hivyo kunaweza kukusaidia uanzishe mazungumuzo.

12. Tunapohubiri kwa nini tuwe waangalifu kuhusiana na mazungumuzo yetu?

12 Mutazamaji muzuri anajikaza kuepuka kukengeushwa. Tunapokuwa katika mahubiri, tunaweza kuwa na mazungumuzo yenye kujenga pamoja na ndugu tunayehubiri naye. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba tunapokuwa katika mahubiri kusudi letu ni kuhubiria wengine. (Mhu. 3:1, 7) Tunapaswa kuwa waangalifu ili mazungumuzo yetu, tunapotoka nyumba moja hadi nyingine, yasivuruge mahubiri yetu. Kuzungumuzia mawazo ambayo tunaweza kutumia ili kusaidia wale wanaopendezwa ni njia nzuri ya kukazia akili yetu juu ya kusudi letu. Pia, ijapokuwa wakati fulani tunaweza kutumia telefone ili kuhubiri, tunapaswa kuwa waangalifu ili kuitia katika hali ambayo haitavuruga mazungumuzo yetu pamoja na musikilizaji ikiwa tunaitwa.

TUPENDEZWE NA WATU TUNAOHUBIRIA

13, 14. (a) Namna gani tunaweza kutambua jambo linalopendeza musikilizaji wetu? (b) Tunaweza kufanya nini ili kumusaidia mutu apendezwe na mambo ya kiroho?

13 Wahubiri wanaokaa macho na waangalifu wanasikiliza kwa uangalifu watu wanaohubiria. Ni maulizo gani unayoweza kuuliza ili kumusaidia mutu unayekutana naye katika eneo aeleze mawazo yake? Je, ana wasiwasi kwa sababu dini zinakuwa nyingi, kwa sababu ya jeuri katika eneo anamoishi, ao kushindwa kwa serikali? Je, unaweza kumusaidia apendezwe na mambo ya kiroho kwa kuzungumuzia jinsi vitu fulani vyenye uzima viliumbwa kwa njia ya ajabu ao kwa kumuonyesha namna mashauri ya Biblia yanavyoweza kusaidia mutu katika maisha? Watu wengi wanapendezwa na sala, hata wale wasioamini kuwapo kwa Mungu. Wengi wanajiuliza ikiwa kuna mutu anayesikia sala. Wengine wanataka kupata majibu kwa maulizo yafuatayo: Je, Mungu anasikiliza sala zote? Ikiwa sivyo, tunaweza kufanya nini ili Mungu asikilize sala zetu?

14 Labda tunaweza kujifunza mengi kuhusu ufundi wa kuanzisha mazungumuzo kwa kutazama jinsi muhubiri anayezoea kazi ya kuhubiri anavyofanya. Tazama jinsi anavyoepuka kuuliza​-uliza musikilizaji maulizo yenye kusumbua ao kuingilia mambo yake ya siri. Namna gani sauti yake na sura yake vinaonyesha kwamba anapendezwa na kuelewa maoni ya musikilizaji wake?​—Met. 15:13.

WEMA NA UFUNDI WA KUFUNDISHA

15. Kwa nini tunapaswa kuonyesha wema tunapohubiri?

15 Je, wewe unafurahi unapoamushwa kwa gafula? Watu wengi hawafurahi. Kwa kawaida, watu wanapenda kuamushwa polepole. Ni hivyo pia kuhusu kuamusha watu ili watoke katika usingizi wa kiroho. Kwa mufano, ikiwa mutu fulani anakasirika unapotaka kumuhubiria, kwa kawaida inaomba kufanya nini? Umuelewe, na usikasirike, umushukuru kwa kuwa ameonyesha hali yake waziwazi, na uondoke kwa upole. (Met. 15:1; 17:14; 2 Tim. 2:24) Kwa kumutendea hivyo kwa wema, hilo linaweza kumuchochea awakaribishe Mashahidi watakaomutembelea wakati ujao.

16, 17. Namna gani unaweza kutumia busara katika mahubiri?

16 Unaweza pia kujua jambo la kusema unapokutana na mutu asiyependezwa. Mutu fulani anaweza kusema, “Nina dini yangu” ao, “Sipendezwi,” kwa sababu tu hapendi muzungumuze. Hata hivyo, kwa kutumia ufundi na kwa maneno ya upole unaweza kutokeza maulizo ambayo yatamusaidia apendezwe na mambo ya kiroho.​—Soma Wakolosai 4:6.

17 Wakati fulani tunakutana na watu walio na kazi nyingi, ni vizuri zaidi kuwaelewa na kuondoka. Lakini wakati mwingine unaweza kutambua kwamba ni vizuri kusema tu maneno machache ya lazima. Ndugu fulani wanaweza kufungua Biblia na kusoma andiko litakalomufanya musikilizaji afikiri, na kumuachia ulizo—yote hayo kwa muda usiopita dakika moja. Maneno hayo machache yanaweza kumufanya apendezwe na kukusikiliza kidogo. Kwa nini usijaribu kufanya hivyo unapokutana na hali kama hizo?

18. Tunaweza kufanya nini ili kuwa na ufundi katika kuhubiri wakati hatukupanga kufanya hivyo?

18 Tunapokutana watu katika shuguli zetu za kila siku, mara nyingi tunaweza kuwasaidia wapendezwe na habari njema ikiwa tuko tayari kuwahubiria wakati hatukupanga kufanya hivyo. Ndugu na dada wengi wanatia vichapo katika mifuko ao sakoshe zao. Pia, wanatayarisha andiko la Biblia akilini ili walizungumuzie na wengine wanapopata nafasi. Unaweza kuzungumuza na mwangalizi wa utumishi ao mapainia katika kutaniko lenu kuhusu jinsi unavyoweza kujitayarisha kwa ajili ya hilo.

TUWASAIDIE WATU WA JAMAA YETU KWA UPOLE

19. Kwa nini tusichoke kuwasaidia watu wa jamaa yetu?

19 Bila shaka, kusaidia watu wa jamaa yetu wakubali habari njema ni jambo la kawaida. (Yosh. 2:13; Mdo. 10:24, 48; 16:31, 32) Ikiwa mwanzoni wanakataa ujumbe wetu, hilo linaweza kupunguza bidii yetu. Tunaweza kufikiri kwamba yale tutakayofanya ao kusema hayatawasaidia wakubali kweli. Pia, mambo yanayotokea katika maisha yao yanaweza kuwafanya wabadili maoni yao. Ao labda umekwisha kufanya maendeleo kuhusu uwezo wako wa kufundisha, hivi kwamba unaweza kupata matokeo mazuri.

20. Kwa nini ni lazima uwe na busara unapozungumuza na watu wa jamaa?

20 Tunapaswa kuelewa watu wa familia yetu. (Rom. 2:4) Ni lazima tuzungumuze nao kwa upole kama tunavyofanya tunapokutana na watu katika mahubiri. Zungumuza nao kwa upole na kwa heshima. Kuliko kuwahubiria-hubiria, onyesha jinsi kweli imekusaidia wewe mwenyewe katika maisha yako. (Efe. 4:23, 24) Onyesha waziwazi jinsi Yehova amekubariki, kwa ‘kukufundisha ili ujifaidi mwenyewe.’ (Isa. 48:17) Acha watu wa jamaa yako waone kupitia matendo yako kwamba wewe ni Mukristo.

21, 22. Eleza jambo ambalo dada mumoja alijionea linaloonyesha faida ya kuendelea kusaidia watu wa jamaa yetu wajue ukweli.

21 Hivi karibuni, dada mumoja alisema hivi: “Nina kaka na dada zangu 13, na kila siku nimejaribu kuwahubiria kwa maneno na kwa matendo. Sipitishe mwaka bila kuwaandikia kila mumoja wao barua. Hata hivyo, kwa muda wa miaka 30, hakuna hata mumoja kati yao ambaye amekuwa Shahidi.”

22 Dada huyo anaongeza hivi: “Siku moja nilimwita kwa njia ya telefone dada yangu aliyekuwa akiishi mbali nami. Aliniambia kwamba alimwomba pasteur wake amufundishe Biblia, lakini hakukubali. Nilipomwambia kwamba niko tayari kumusaidia, yeye alisema: ‘Sawa, lakini ujue jambo hili sasa: Mimi sitakuwa kamwe Shahidi wa Yehova.’ Kisha kumutumia kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?, nilimuita kisha siku chache. Lakini alikuwa bado hajakisoma. Mwishowe, nilimwambia achukue kitabu chake, tulizungumuza kwa muda wa dakika 15 hivi kwa njia ya telefone, tulisoma na kuzungumuzia maandiko fulani kutoka katika kitabu hicho. Baada ya kuzungumuza naye mara chache kwa njia ya telefone, alipenda kujifunza kwa muda wa zaidi ya dakika 15. Kisha alianza kuniita ili tujifunze, wakati fulani asubuhi mbele niamuke na wakati mwingine mara mbili kwa siku. Mwaka uliofuata, akabatizwa, na mwaka mwingine, akaanza utumishi wa painia.”

23 Kwa nini hatupaswi kuchoka kuhusu kuamusha watu kutoka katika usingizi wa kiroho?

23 Kusaidia watu waamuke kutoka katika usingizi wa kiroho kunaomba ufundi na kutokuchoka. Wapole bado wanaendelea kukubali kweli na kufurahia jitahada zetu za kuwaamusha. Kila mwezi zaidi ya watu 20 000 wanabatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo, acheni tuchukue kwa uzito shauri la Paulo kwa ndugu Arkipo: “Endelea kuangalia huduma ambayo uliikubali katika Bwana, ili uitimize.” (Kol. 4:17) Habari inayofuata itatusaidia tuelewe kwa nini kazi yetu ya kuhubiri inahitaji kufanywa kwa haraka.

[Maulizo ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

UNAWEZA KUENDELEA KUKAA MACHO

▪ Ikiwa unaendelea kuwa na kazi nyingi katika kufanya mapenzi ya Mungu

▪ Ikiwa unaepuka matendo ya giza

▪ Ikiwa unakuwa mwangalifu ili usisinzie kiroho

▪ Ikiwa hauwazie vibaya watu wa eneo lako

▪ Ikiwa unatumia njia mupya ili kuwahubiria watu

▪ Ikiwa unakumbuka umaana wa kazi ya kuhubiri