Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Nilishika Upindo wa Nguo ya Muyahudi kwa Miaka Zaidi ya 70

Nilishika Upindo wa Nguo ya Muyahudi kwa Miaka Zaidi ya 70

Masimulizi Kuhusu Maisha ya Watu

Nilishika Upindo wa Nguo ya Muyahudi kwa Miaka Zaidi ya 70

Leonard Smith anaeleza maisha yake

Nilipokuwa kijana, nilivutiwa na maandiko mawili ya Biblia. Leo, kisha zaidi ya miaka 70, ningali ninakumbuka wakati ambapo nilijua maana ya andiko la Zekaria 8:23, linalozungumuzia “wanaume kumi” wenye kushika ‘upindo wa nguo wa mutu aliye Muyahudi.’ Wanamuambia Muyahudi huyo: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.”

MUTU aliye Muyahudi anafananisha Wakristo watiwa-mafuta, na “wanaume kumi” wanafananisha “kondoo wengine,” ao “Wayonadabu,” kama walivyokuwa wakiitwa zamani. * (Yoh. 10:16) Niliposikia kweli hiyo, nilitambua kabisa kama ili nipate uzima wa milele nilipaswa niunge mukono kwa ushikamanifu Wakristo watiwa-mafuta.

Tena, mufano wa Yesu wa “kondoo” na “mbuzi,” unaopatikana katika Mathayo 25:31-46, ulinivutia sana. “Kondoo” wanafananisha wale watakaokubaliwa wakati wa mwisho kwa kuwa wametendea mema ndugu wa Kristo watiwa​-mafuta ambao wangali duniani. Kama mumoja wa vijana wa Wayonadabu, nilisema moyoni mwangu hivi, ‘Len ikiwa unapenda Kristo akuone kama kondoo, unapaswa kuunga mukono ndugu watiwa​-mafuta, unapaswa kukubali uongozi wao kwa kuwa Mungu yuko pamoja nao.’ Kuelewa jambo hilo kuliniongoza muda wa miaka zaidi ya makumi saba.

‘NAFASI YANGU NI WAPI?’

Mama yangu alibatizwa katika mwaka wa 1925 katika jumba la mikutano la Betheli. Jumba hilo liliitwa Tabernacle de Londres na lilitumiwa na ndugu waliokuwa wakiishi katika eneo hilo. Nilizaliwa tarehe 15 mwezi wa 10, 1926. Mwezi wa 3, 1940, nilibatizwa wakati wa mukusanyiko uliofanywa huko Dover, Angleterre pembeni ya bahari. Tangu utoto nilikuwa mwenye kupenda kweli ya Biblia. Kwa kuwa mama yangu alikuwa Mukristo mutiwa-mafuta, ‘upindo wa nguo ya Muyahudi’ ambao nilishika kwa mara ya kwanza ulikuwa ule wa mama yangu. Kwa wakati huo, baba yangu na dada yangu hawakuwa wakimutumikia Yehova. Tulikuwa katika Kutaniko la Gillingham katika mashariki mwa Angleterre. kutaniko lililoundwa hasa na Wakristo watiwa​-mafuta. Mama aliniachia mufano muzuri wa bidii katika mahubiri.

Mwezi wa 9, 1941, kwenye mukusanyiko uliofanywa katika muji wa Leicester, hotuba iliyokuwa na kichwa “Ushikamanifu” ulizungumuzia juu ya yule aliye na haki ya kutawala ulimwengu muzima. Hotuba hiyo ilinisaidia nielewe kwa mara ya kwanza kama sisi pia tunapaswa kujibia shitaka la kujua nani anastahili kutawala wanadamu, Yehova ao Shetani. Kwa hiyo, ni lazima kuwa upande wa Yehova na kumutetea, na tunapaswa kuendelea kuwa washikamanifu kwake, yeye ambaye ni Mutawala Mukubwa wa ulimwengu wote.

Kwenye mukusanyiko huo, mukazo ulitiliwa juu ya kazi ya upainia, na vijana walitiwa moyo wajiwekee muradi wa kuwa mapainia. Hotuba yenye kichwa “Nafasi ya Painia Katika Tengenezo” ilinifanya nijiulize, ‘Nafasi yangu ni wapi?’ Mukusanyiko huo ulinisaidia mimi, mumoja wa Wayonadabu, kuona kuwa nilipaswa kuwasaidia Wakristo watiwa-mafuta kadiri niwezavyo katika kazi ya kuhubiri. Hapo hapo tu katika muji wa Leicester, nilijaza fomu ya upainia.

KUFANYA KAZI YA UPAINIA WAKATI WA VITA

Tarehe 1 mwezi wa 12, 1941, nilipokuwa na miaka 15, nilianza kazi ya upainia wa pekee. Mama yangu ndiye aliyekuwa wa kwanza kuniunga mukono katika kazi hiyo, lakini kisha mwaka moja hivi, aliacha upainia kwa sababu ya magonjwa. Biro ya tawi ya Londres ilinitumia mutu wa kutumika naye, ndugu Ron Parkin, anayetumika sasa katika Halmashauri ya Tawi huko Porto Rico.

Tulitumwa katika miji iliyokuwa pembeni ya bahari huko Broadstairs na Ramsgate katika jimbo la Kent, ambako tulipanga katika chumba kimoja. Posho ya mapainia wa pekee ya kila mwezi ilikuwa karibu dola 8. Wakati huo tulikuwa tukilipia chumba cha kulalia, hatukuwa na vitu vingi vya kimwili, na kwa kawaida hatukujua kesho tutakula nini. Lakini bila kutazamia, kila mara Yehova alitutolea mahitaji yetu.

Tulitumia kinga sana, tulijikaza kutembeza kinga zetu zilizofungiwa mizigo na tulipambana na upepo mukali uliokuwa ukitoka katika Bahari ya Kaskazini. Tena tulipaswa kupambana na hatari ya ndege za vita zilizokuwa zikitupa mabombe na pia ya mabombe yaliyokuwa yakifyatuliwa kutoka Allemagne, kupitia juu ya muji wa Kent mupaka Londres. Siku moja niliruka toka kinga yangu na kujitupa katika mufereji wakati bombe moja ilipita juu ya kichwa changu na kulipuka katika shamba moja karibu na mahali nilipokuwa. Hata hivyo, miaka tuliyopitisha katika kazi yetu ya upainia katika Kent ilikuwa yenye furaha zaidi.

“KIJANA WA BETHELI”

Kila siku mama yangu alikuwa akiitapa Betheli. Alikuwa akisema: “Tamaa yangu kubwa ni kukuona siku moja unakuwa kijana wa Betheli.” Wazia furaha yangu na mushangao wangu mwezi wa 1, 1946, nilipopokea mwaliko wa kwenda kutumika Betheli ya Londres ili kusaidia kufanya kazi muda wa majuma matatu. Mwishoni mwa majuma hayo, Ndugu Pryce Hughes, mutumishi wa tawi, akaniomba nibaki Betheli. Mazoezi niliyopata huko yalibadili maisha yangu yote.

Betheli ya Londres ilikuwa na watu karibu 30 wakati huo, wengi wakiwa ndugu vijana wasiooa lakini kulikuwa pia ndugu wengi watiwa​-mafuta, kutia ndani Pryce Hughes, Edgar Clay, na Jack Barr, ambaye baadaye alikuja kuwa mushiriki wa Baraza Linaloongoza. Ilikuwa pendeleo kabisa kuunga mukono ndugu za Kristo kwa kutumika nikiwa bado kijana sana, chini ya uongozi wa kiroho wa “nguzo” hizo!​—Gal. 2:9.

Siku moja hapo Betheli, ndugu moja alikuja kuniambia kama kuna dada moja kwenye mulango wa mbele ambaye alipenda kuniona. Sikuwazia, ilikuwa ni mama yangu aliyekuja kuniona na alikuwa na fulushi fulani katika mukono. Aliniambia kuwa hakupenda kuingia ndani ili asinikengeushe katika kazi yangu, lakini alinipatia fulushi hiyo na akaondoka. Ni koti ya baridi iliyokuwa ndani ya fulushi hiyo. Tendo hilo la upendo lilinikumbusha Hana aliyemupelekea kijana wake Samweli vazi alipokuwa akitumika kwenye maskani.​—1 Sam. 2:18, 19.

GILEADI—SIWEZI KUSAHAU

Katika 1947, watano kati yetu waliokuwa wakitumikia Betheli walialikwa kwenye Masomo ya Gileadi katika Amerika, na mwaka uliofuata tulihuzuria darasa la 11. Tulipofika, kulikuwa baridi sana katika New York, muji ambamo masomo yaliendeshwa. Nilifurahi sana kuwa na koti hilo la baridi ambalo mama yangu aliniletea!

Siwezi kusahau miezi hiyo sita niliyopitisha katika Gileadi. Nilifaidika sana kiroho, zaidi ya hilo, kuchangana na wanafunzi wengine kutoka inchi tofauti 16 kulinifungua akili. Nilifaidika sana kurafikiana na Wakristo wenye kukomaa kiroho. Baadaye, mwanafunzi mwenzangu Lloyd Barry; mwalimu wetu, Albert Schroeder; na John Booth, mwangalizi wa Shamba la Ufalme (mahali masomo ya Gileadi yalikoendeshwa) wakawa washiriki wa Baraza Linaloongoza. Nilifurahia sana mashauri yenye upendo ambayo ndugu hao walinitolea na ushikamanifu wao kwa Yehova na kwa tengenezo lake.

KATIKA MUZUNGUKO NA KURUDI BETHELI

Kisha tu kumaliza masomo ya Gileadi, nilipewa mugawo wa kutumika katika muzunguko katika muji wa Ohio, Amerika. Nilikuwa tu na miaka 21, lakini ndugu walinipokea kwa upendo ijapokuwa moto​-moto ya ujana. Katika muzunguko huo, nilijifunza mambo mengi kutoka kwa wanaume wazee wenye kujua mambo mengi.

Kisha miezi michache, niliitwa tena kwenye Betheli ya Brooklyn, ili kupata mazoezi zaidi. Wakati huo, nikapata kujua nguzo fulani kama vile Milton Henschel, Karl Klein, Nathan Knorr, aliyeitwa kwa kutania T.J. (Bud) Sullivan, na Lyman Swingle, wote walitumika kwenye Baraza Linaloongoza wakati fulani. Yalikuwa mazoezi mazuri kabisa kuwaona wakitumika na kuona sifa zao za Kikristo. Hilo lilinifanya nitumainie tengenezo la Yehova hata zaidi. Kisha nikatumwa tena Ulaya ili kuendelea na kazi ya kuhubiri huko.

Mama yangu alikufa mwezi wa 2, 1950. Kisha mazishi, nilizungumuza sana na baba yangu pamoja na dada yangu, Dora. Nikawauliza musimamo wao juu ya kweli kwa kuwa sasa Mama ametuacha na mimi nimekwisha toka nyumbani. Walijua na kumuheshimu ndugu moja muzee mutiwa​-mafuta, Harry Browning, na wakakubali kujifunza Biblia pamoja naye. Kwa mwaka moja Baba yangu na dada yangu Dora wakabatizwa. Baadaye Baba akawa mutumishi (mutumishi wa huduma) katika Kutaniko la Gillingham. Kisha kifo cha Baba yangu, Dora akaolewa na muzee mumoja mwaminifu aliyeitwa, Roy Moreton, na akamutumikia Yehova kwa uaminifu mupaka alipokufa katika mwaka wa 2010.

KUTOA MUSAADA KATIKA FRANCE

Kwenye masomo, nilijifunza Kifaransa, Kijerumani, na Kilatini, lakini kati ya luga hizo tatu ni Kirafansa kilichonisumbua sana. Kwa hiyo nilikuwa na furaha lakini pia wasiwasi waliponiomba kwenda kusaidia kufanya kazi kwenye Betheli ya Paris, huko France. Huko, nilikuwa na pendeleo la kutumika pamoja na mutumishi wa tawi, ndugu Henri Geiger, Mukristo aliyezeeka na mutiwa​-mafuta. Haikuwa vyepesi, na kwa kweli nilifanya makosa mengi, lakini nilijifunza mengi juu ya namna mutu anapaswa kuishi na wengine.

Tena, mukusanyiko wa kwanza wa kimataifa kisha vita ulipangwa kufanywa katika Paris mwaka wa 1951, na nilikuwa kati ya wale walioutayarisha. Mwangalizi moja mwenye kusafiri kijana, ndugu Léopold Jontès, alikuja Betheli ili kunisaidia. Baadaye, ndugu Léopold alitiwa kuwa mwangalizi wa tawi. Mukasanyiko ulifanywa katika Palais des sports, pembeni ya Tour Eiffel. Wajumbe walikuja kutoka inchi 28. Siku ya mwisho, Mashahidi wa Yehova 6 000 wa France walifurahi kuona watu 10 456 kuhuzuria mukusanyiko huo!

Nilipofika France kwa mara ya kwanza, Kifaransa changu hakikuwa kizuri. Kosa kubwa nililofanya ni kujikaza kusema tu wakati nilipokuwa hakika kama sitasema makosa. Lakini nilifikia kutambua kama unapojifunza luga, ikiwa haufanye makosa, hautasaidiwa na kwa hiyo hautafanya maendeleo.

Nikaamua kujiandikisha katika masomo yaliyokuwa yakifundisha wageni Kifaransa. Nilisoma wakati wa mangaribi siku ambazo hatukuwa na mikutano. Nikaanza kupenda Kifaransa, na kadiri miaka ilivyopita niliipenda luga hiyo. Hilo lilikuwa jambo la lazima kwa kuwa liliniwezesha nitumike katika tawi la France katika kazi ya kutafsiri. Kisha nikaanza kutafsiri vichapo vya Kingereza katika Kifaransa. Ilikuwa pendeleo kubwa kusaidia kutafsiri katika Kifaransa ili ndugu wanaosema luga hiyo duniani pote wafaidike na chakula kinachotayarishwa na mutumwa mwaminifu.​—Mt. 24:45-47.

NDOA NA MAPENDELEO MENGINE

Katika mwaka wa 1956, nilimuoa dada Esther, painia kutoka Suisse ambaye nilionana naye miaka michache mbele. Hotuba ya ndoa yetu ilifanywa katika Jumba la Ufalme lililokuwa karibu na Betheli ya Londres (Tabernacle de Londres, mahali ambapo mama yangu alipata ubatizo). Ni Ndugu Hughes aliyefanya hotuba ya ndoa yetu. Mama yake na Esther alikuwa hapo, na yeye pia alikuwa na tumaini la kwenda mbinguni. Ndoa yangu ilinitolea mwanamuke niliyemupenda sana na ambaye tuliungana naye mukono kwa ushikamanifu, pia ilinisaidia niwe na mama mukwe muzuri kabisa na mwenye kukomaa kiroho, mupaka siku alipomaliza mwendo wake wa duniani katika mwaka wa 2000.

Kisha ndoa yetu, Esther nami tuliishi inje ya Betheli. Niliendelea na kazi yangu ya kutafsiri, na Esther alikuwa painia wa pekee katika vijiji vya Paris. Aliwasaidia watu wengi wafikie kuwa watumishi wa Yehova. Katika mwaka wa 1964 tuliitwa Betheli. Kisha katika 1976, wakati Halmashauri za Tawi ziliundwa, nilitiwa mushiriki wa Halmashauri ya Tawi. Muda wa miaka yote hiyo, Esther aliniunga mukono kwa upendo.

‘HAMUTAKUWA NAMI SIKUZOTE’

Nimekuwa na pendeleo la kutembelea mara kwa mara kwenye makao makuu huko New York. Nilipotembelea huko, nilipewa mashauri mazuri kutoka ndugu wa Baraza Linaloongoza. Kwa mufano, wakati fulani, wakati nilipokua na wasiwasi juu ya kumaliza kazi fulani pa wakati, Ndugu Knorr alicheka kidogo na akaniambia: “Usiogope. Fanya kazi!” Kuanzia wakati huo, ninapokuwa na kazi nyingi, kuliko kuogopa, ninatumika kazi moja baada ya nyingine na kazi inasonga mbele, mara nyingi tunamaliza pa wakati.

Mbele ya kufa, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: ‘Hamutakuwa pamoja nami sikuzote.’ (Mt. 26:11) Sisi Wakristo wa kondoo wengine hatutakuwa na ndugu za Kristo sikuzote duniani. Kwa hiyo ninaliona kuwa pendeleo kubwa kutumika pamoja na watia​-mafuta wengi kwa muda wa miaka 70​—nikishika upindo wa nguo ya Muyahudi.

[Maelezo ya chini]

^ Juu ya neno “Yonadabu,” soma kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 83, 165, 166.

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 21]

Ndugu Knorr alicheka kidogo na akaniambia: “Usiogope. Fanya kazi!”

[Picha katika ukurasa wa 19]

(Kushoto) Mama yangu na baba yangu

(Kuume) Kwenye masomo ya Gileadi katika mwaka wa 1948, nikivaa koti la baridi ambalo Mama yangu alinitolea

[Picha katika ukurasa wa 20]

Ninatafsiri hotuba ya Ndugu Lloyd Barry ya kufungua tawi la France, 1997

[Picha katika ukurasa wa 21]

(Kushoto) Nikiwa na Esther siku ya ndoa yetu

(Kuume) Pamoja katika kazi ya kuhubiri