Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yehova Anatulinda Ili Tupate Wokovu

Yehova Anatulinda Ili Tupate Wokovu

Yehova Anatulinda Ili Tupate Wokovu

‘Munalindwa kwa nguvu za Mungu kupitia imani kwa ajili ya wokovu ulio tayari kufunuliwa katika kipindi cha mwisho cha wakati.’​—1 PET. 1:4, 5.

UTAJIBU NAMNA GANI?

Namna gani Yehova alituvuta kwenye ibada ya kweli?

Namna gani tunaweza kumuacha Yehova atuongoze kupitia shauri lake?

Namna gani Yehova anatutolea vitia-moyo?

1, 2. (a) Sababu gani tunaweza kuamini kabisa kama Mungu atatusaidia tuendelee kuwa waaminifu? (b) Sababu gani tunaweza kusema kama Yehova anajua vizuri sana kila mumoja wetu?

 ‘YULE ambaye atavumilia mupaka mwisho ndiye atakayeokolewa.’ (Mt. 24:13) Aliposema maneno hayo, Yesu alipenda kuonyesha waziwazi kama ili kulindwa na kuokoka wakati Mungu atauharibu ulimwengu wa Shetani, tunapaswa kuendelea kuwa waaminifu mupaka mwisho. Lakini hilo halimaanishi kama Yehova atatuachilia tutumie hekima yetu na nguvu zetu wenyewe ili kuvumilia. Biblia inatuhakikishia hivi: ‘Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mujaribiwe kupita munavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi muweze kulivumilia.’ (1 Kor. 10:13) Maneno hayo yanamaanisha nini?

2 Yehova atatulinda ili tusijaribiwe kupita kipimo kwa kuwa yeye anatujua vizuri sana; anajua majaribu tunayopata, anajua nguvu zetu na uzaifu wetu, na mambo tunayoweza kuvumilia. Je, Mungu anatujua vizuri hivyo? Ndiyo. Maandiko yanasema kama Yehova anamujua kila mumoja wetu vizuri sana. Anajua mambo tunayofanya kila siku na tabia zetu. Anaweza hata kuelewa mawazo yetu na makusudi ya moyo wetu.​—Soma Zaburi 139:1-6.

3, 4. (a) Namna gani mambo yaliyomupata Daudi yanaonyesha kama Yehova anapendezwa na kila mumoja wetu leo? (b) Ni kazi gani ya ajabu sana ambayo Yehova anatimiza leo?

3 Je, Mungu anaweza kabisa kuhangaikia mwanadamu hivyo, mwanadamu ambaye ni kitu kidogo sana? Mutunga​-zaburi Daudi alifikiri sana juu ya jambo hilo, na alisema hivi juu ya Yehova: ‘Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba umuweke akilini, na mwana wa mutu wa udongo hivi kwamba umutunze?’ (Zab. 8:3, 4) Labda Daudi aliuliza ulizo hili kwa sababu ya mambo aliyokutana nayo. Yehova aliona kuwa Daudi kijana wa Yese, alikuwa mutu ‘aliyekubalika kwa moyo wake’ na kwa hiyo, alimuchukua ‘kutoka katika viwanja vya malisho ili awe kiongozi’ juu ya Israeli. (1 Sam. 13:14; 2 Sam. 7:8) Wazia namna Daudi alivyojisikia alipotambua kama ijapokuwa alikuwa kijana muchungaji wa kondoo, Muumbaji wa vitu vyote alipendezwa na mawazo yake ya siri alipokuwa akitafakari!

4 Ni jambo la ajabu pia kuona namna Yehova anavyopendezwa na kila mumoja wetu leo. Anaendelea kukusanya katika ibada safi “vitu vyenye kutamanika vya mataifa,” na anasaidia watumishi wake waendelee kubaki waaminifu. (Hag. 2:7) Ili kuelewa vizuri namna Yehova anavyotusaidia tubaki waaminifu, acheni tuzungumuzie kwanza namna anavyowavuta watu kwenye ibada yake ya kweli.

NI MUNGU NDIYE AMETUVUTA

5. Namna gani Yehova anavuta watu kwa Mwana wake? Toa mufano.

5 Yesu alisema: ‘Hakuna mutu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amuvute.’ (Yoh. 6:44) Maneno hayo yanaonyesha kama haiwezekani kuwa mwanafunzi wa Kristo bila kusaidiwa na Mungu. Namna gani Yehova anavuta watu walio mufano wa kondoo kwa Mwana wake? Anafanya hivyo kupitia mahubiri ya habari njema na nguvu ya roho takatifu. Kwa mufano, wakati Paulo na wamisionari wenzake walikuwa katika inchi ya Filipi, walikutana na mwanamuke mumoja aliyeitwa Lidia na wakaanza kumuhubiria habari njema. Biblia inasema hivi: “Yehova akafungua wazi moyo wake asikilize kwa makini mambo yaliyokuwa yakisemwa na Paulo.” Ndiyo, Mungu alitumia roho yake ili imusaidie Lidia aelewe mambo ambayo Paulo alikuwa akimuhubiria; matokeo yalikuwa mazuri, kwa kuwa yeye na watu wa nyumba yake walibatizwa.​—Mdo. 16:13-15.

6. Namna gani Mungu ametuvuta sisi wote kwenye ibada yake ya kweli?

6 Je, tuna mufano tu wa Lidia? Hapana. Kwa kuwa wewe ni Mukristo aliyejitoa kwa Mungu, wewe pia ulivutwa na Mungu kwenye ibada yake safi. Baba yetu wa mbinguni aliona jambo fulani nzuri katika moyo wa Lidia, vilevile aliona jambo fulani nzuri katika moyo wako. Ulipoanza kusikiliza habari njema, Yehova alikusaidia kupitia roho takatifu yake ili uelewe vizuri habari njema hiyo. (1 Kor. 2:11, 12) Ulipojikaza kutumia katika maisha yako mambo uliyokuwa unajifunza, yeye alibariki nguvu zako ili ufanye mapenzi yake. Ulipojitoa kwake, moyo wake ulifurahi sana. Kwa kweli, tangu wakati ulipoanza kutembea kwenye barabara inayoongoza kwenye uzima, Yehova amekuwa pamoja nawe katika kila hatua unayofanya.

7. Namna gani tunajua kama Mungu ataendelea kutusaidia ili tubaki waaminifu?

7 Yehova ametusaidia tangu tulipoanza kutembea pamoja naye na tunajua kama ataendelea kutusaidia ili tubaki waaminifu. Anajua kama hatukuja katika kweli kwa nguvu zetu, na hatuwezi kubaki katika kweli kwa nguvu zetu wenyewe. Alipowaandikia Wakristo watiwa​-mafuta, mutume Petro alisema hivi: ‘Munalindwa kwa nguvu za Mungu kupitia imani kwa ajili ya wokovu ulio tayari kufunuliwa katika kipindi cha mwisho cha wakati.’ (1 Pet. 1:4, 5) Kwa kawaida, maneno hayo ya Petro yanawatia moyo Wakristo wote na yanapaswa kumupendeza kila mumoja wetu. Sababu gani? Kwa sababu sisi wote tuna lazima ya musaada wa Mungu ili kuendelea kuwa waaminifu kwake.

MUNGU ANAWEZA KUTUZUIA ILI TUSIFANYE KOSA

8. Sababu gani inawezekana tuingie katika hatari ya kufanya kosa fulani bila sisi kujua?

8 Maisha magumu na hali yetu ya kukosa ukamilifu vinaweza kufanya tusione mambo kama Yehova na kutuingiza katika hatari ya kufanya kosa fulani bila sisi kujua. (Soma Wagalatia 6:1.) Jambo fulani lililotokea katika maisha ya Daudi litatusaidia kuelewa hilo.

9, 10. Namna gani Yehova alimuzuia Daudi asifanye kosa, na anafanya namna gani hivyo kwa ajili yetu leo?

9 Daudi alipowindwa na Mufalme Sauli mwenye wivu, alijizuia sana ili asimulipishe kisasi hata ikiwa alikuwa na nafasi ya kumuua. (1 Sam. 24:2-7) Lakini muda kidogo kisha hapo, kwa sababu ya kukosa ukamilifu, Daudi alishindwa kujizuia. Siku fulani, alikuwa na lazima ya chakula kwa ajili ya wanaume wake, kwa hiyo akatuma watu ili kumuomba Nabali chakula, Nabali alikuwa pia Mwisraeli. Nabali alipomujibu kwa matusi, Daudi alikasirika sana na akaondoka ili kwenda kulipiza kisasi. Alikusudia kumuangamiza Nabali na watu wa nyumba yake, alisahau kama kwa kufanya hivyo angewaua pia watu wasio na kosa na hilo lingemufanya awe na deni ya damu mbele ya Mungu. Ni Abigaili, muke wa Nabali, ndiye aliyemuzuia Daudi kutenda kitendo hicho kibaya. Daudi alitambua kama ni Yehova aliyemuzuia, ndio sababu alimuambia Abigaili hivi: ‘Abarikiwe Yehova Mungu wa Israeli, aliyekutuma leo unipokee! Busara yako na ibarikiwe, nawe ubarikiwe, ambaye umenizuia leo nisiingie katika hatia ya damu na kuacha mukono wangu mwenyewe uniokoe.’​—1 Sam. 25:9-13, 21, 22, 32, 33.

10 Tunaweza kujifunza nini kutokana na habari hiyo? Yehova alimutumia Abigaili ili amuzuie Daudi kufanya kosa. Mara nyingi anafanya hivyo pia kwa ajili yetu leo. Hakika, hatupaswi kutumainia kama kila mara Mungu atatuma mutu fulani ili kutuzuia kila wakati tunapotaka kufanya kosa. Tena, hatuwezi kujua vizuri kabisa namna Mungu atatenda katika hali fulani ao namna gani ataachilia jambo fulani litendeke ili makusudi yake yatimizwe. (Mhu. 11:5) Hata hivyo, tunaweza kutumainia kabisa kama kila wakati Yehova anajua hali zetu na atatusaidia ili tuendelee kubaki waaminifu kwake. Anatuhakikishia hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.” (Zab. 32:8) Namna gani Yehova anatushauria? Namna gani tunaweza kufaidika na shauri lake? Na kwa nini tunaweza kuwa hakika kama Yehova anaongoza watu wake leo? Ona namna kitabu cha Ufunuo kinajibu maulizo hayo.

KUSIKILIZA SHAURI KUNATULINDA

11. Ni nini inayoonyesha kama Yehova anajua vizuri sana mambo yanayofanyika katika makutaniko ya watu wake?

11 Katika maono yaliyoandikwa katika Ufunuo sura ya 2 na ya 3, Yesu Kristo aliyetukuzwa anachunguza makutaniko saba ya Asia Ndogo. Maono hayo yanaonyesha kama Kristo anaona sifa za kila kutaniko lakini pia anaona hali moja moja katika kila kutaniko. Kwa mufano, anataja majina fulani, anataja kila jambo linalofanyika, na anapongeza na kutoa shauri kulingana na hali. Hilo linaonyesha nini? Makutaniko hayo saba yanafananisha Wakristo watiwa​-mafuta kisha mwaka wa 1914, na mashauri aliyotolea makutaniko hayo saba ni kwa faida ya makutaniko yote ya watu wa Mungu duniani leo. Jambo hilo linaonyesha wazi kabisa kama Yehova anaongoza watu wake kupitia Mwana wake. Namna gani tunaweza kufaidika na mwongozo huo?

12. Namna gani tunaweza kumuacha Yehova aongoze hatua zetu?

12 Kufanya funzo la pekee ni njia moja inayoweza kutusaidia tufaidike na mwongozo wenye upendo wa Yehova. Kupitia vitabu vya mutumwa mwaminifu na mwenye busara, Yehova anatutolea mashauri yenye kutujenga. (Mt. 24:45) Lakini ili tufaidike na mashauri hayo, tunapaswa kuchukua wakati wa kujifunza vitabu hivyo na kutumia katika maisha mambo tunayojifunza. Funzo la pekee ni njia moja ambayo kupitia hiyo Yehova anaweza ‘kutulinda ili tusijikwae.’ (Yuda 24) Je, umekwisha kusoma jambo fulani katika vitabu vyetu na kisha ulijisikia kuwa jambo hilo liliandikwa kwa ajili yako? Ulione jambo hilo kuwa ni shauri kutoka kwa Yehova. Rafiki yako anaweza kukupiga​-piga kwenye bega ili akukumbushe kufanya jambo fulani, vilevile Yehova anaweza kutumia roho yake ili akukumbushe jambo fulani juu ya mwenendo wako fulani ao tabia yako fulani unayopaswa kubadilisha. Kama unakubali uongozi huo ambao roho inakutolea, kwa kufanya hivyo unamuacha Yehova aongoze hatua zako. (Soma Zaburi 139:23, 24.) Kwa hiyo ni vizuri tuchunguze mazoea yetu ya funzo letu la pekee.

13. Sababu gani ni jambo la hekima tuchunguze programu yetu ya funzo?

13 Kujiburudisha wakati mwingi kunaweza kutuiba wakati wetu wa kufanya funzo la pekee. Ndugu mumoja alisema hivi: “Ni kwepesi sana kuacha funzo la pekee. Leo kuna viburudisho vingi sana kuliko zamani na vinapatikana kwa wepesi sana kwenye televizyo, kwenye ordinateur, na kwenye telefone. Vinajaa mahali pote.” Ikiwa hatufanyi angalisho, wakati ambao tungetumia ili kufanya funzo la pekee kwa undani unaweza kupunguka polepole mupaka wakati hatutakuwa tena na funzo la pekee. (Efe. 5:15-17) Kila mumoja wetu anapaswa kujiuliza: ‘Mara ngapi ninachukua wakati wa kujifunza kwa undani Neno la Mungu? Je, ni wakati tu nina hotuba ao sehemu kwenye mikutano?’ Ikiwa ni hivyo, labda tunaweza kutumia inavyofaa mangaribi inayopangwa kwa ajili ya funzo la familia ao funzo la pekee ili kupata hekima ambayo Yehova anatoa ili kutulinda kwa ajili ya wokovu.​—Met. 2:1-5.

VITIA-MOYO VINATUSAIDIA KUVUMILIA

14. Namna gani Maandiko yanaonyesha kwamba Yehova anahangaikia namna tunavyojisikia?

14 Katika maisha yake, Daudi alipatwa na taabu nyingi sana ambazo zingeweza kumuvunja moyo. (1 Sam. 30:3-6) Maneno yake yanayopatikana katika Biblia yanaonyesha kama Yehova alijua namna alivyokuwa anajisikia. (Soma Zaburi 34:18; 56:8.) Mungu anajua pia namna sisi tunavyojisikia. ‘Tunapovunjika moyo’ ao ‘tunapopondwa roho,’ anatukaribia. Kujua hilo tu kunaweza kutufariji, kama kulivyomufariji Daudi aliyeimba hivi: ‘Nitakuwa na shangwe na kushangilia katika fazili zako zenye upendo, kwa kuwa umeona mateso yangu; umejua juu ya taabu za nafsi yangu.’ (Zab. 31:7) Yehova anajua kabisa mateso yetu lakini anatusaidia pia kuyavumilia. Anatutia nguvu kwa kututolea faraja na vitia​-moyo. Njia moja ambayo anatumia ni mikutano ya Kikristo.

15. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mambo yaliyomupata Asafu?

15 Mambo yaliyomupata mutunga​-zaburi Asafu yanaonyesha faida za kuhuzuria mikutano. Asafu alipowaza sana juu ya ukosefu wa haki, hakuona tena faida ya kumutumikia Mungu, na alivunjika moyo. Alizungumuzia hali yake hivi: “Moyo wangu ulikuwa umetiwa uchungu nami nilikuwa na maumivu makali kwenye figo zangu.” Basi, akaanza kupoteza furaha yake ya kumutumikia Yehova. Ni nini iliyomusaidia Asafu abadilishe tena mawazo yake? Yeye alisema: ‘Nikaingia katika patakatifu pakuu pa Mungu.’ Alipokusanyika pamoja na waabudu wengine wa Yehova, alibadilisha mawazo yake. Aliona kama ijapokuwa watu wabaya walifanikiwa ilikuwa kwa muda tu, na aliona pia kama Yehova atatengeneza mambo kwa wakati wake. (Zab. 73:2, 13-22) Hilo linaweza kutufikia pia. Mambo ya ukosefu wa haki katika dunia hii ya Shetani yanaweza kutuvunja moyo. Tunapokusanyika pamoja na ndugu zetu tunapata nguvu mupya na kunatusaidia tulinde furaha yetu ya kumutumikia Yehova.

16. Namna gani mufano wa Hana unaweza kutusaidia?

16 Kwa hiyo basi, utafanya nini ikiwa unakutana na hali fulani katika kutaniko ambayo inakuondoa furaha ya kuhuzuria mikutano? Labda iliomba uache pendeleo fulani la utumishi katika kutaniko na jambo hilo linakusumbua sana, ao labda hausikilizani na ndugu fulani ao dada fulani. Ikiwa ni hivyo, mufano wa Hana unaweza kukusaidia. (Soma 1 Samweli 1:4-8.) Kumbuka kama mbanda yake Penina alikuwa anamusumbua sana kwa sababu yeye Hana hakuwa anazaa. Kila mwaka wakati familia ilipokuwa ikienda huko Shilo kumutolea Yehova zabihu ndipo hali ilikuwa mbaya zaidi. Hali hiyo ilimusumbua sana Hana, naye ‘alikuwa akilia na kukataa kula.’ Hata hivyo, Hana hakuacha hali hiyo imuzuie kwenda mahali ambapo angepaswa kumuabudu Yehova. Yehova aliona imani yake na akamubariki.​—1 Sam. 1:11, 20.

17, 18. (a) Namna gani tunapokea vitia-moyo kwenye mikutano ya kutaniko? (b) Unajisikia namna gani unapoona namna Yehova anavyotuhangaikia ili kutusaidia tuokolewe?

17 Leo, Wakristo wanapaswa kumuiga Hana. Ni lazima tuhuzurie mikutano kwa ukawaida. Sisi wote tumekwisha kujionea kama tunapohuzuria mikutano tunapata vitia​-moyo tunavyohitaji. (Ebr. 10:24, 25) Kwenye mikutano tunakuta ndugu na dada wenye kuchangamuka na hilo linatufariji. Kwenye mikutaniko tunaweza kusikia hotuba fulani ao maelezo fulani na hilo linaweza kugusa moyo wetu. Kuzungumuza na ndugu fulani ao dada fulani mbele ao kisha mikutano kunaweza kufanya atusikilize tunapomuelezea magumu yetu ao atuambie jambo fulani linaloweza kutufariji. (Met. 15:23; 17:17) Tunapomuimbia Yehova pamoja na wengine, tunajisikia kuwa wenye kutiwa moyo na furaha. Zaidi sana tunapolemewa na ‘fikira zinazofazaisha’ tunahitaji vitia​-moyo ambavyo tunapokea kwenye mikutano, ambako Yehova anatutia nguvu kupitia ‘faraja zake’ na kutegemeza azimio letu la kuendelea kubaki waaminifu kwake.​—Zab. 94:18, 19.

18 Kwa kuwa Mungu anatuhangaikia kwa upendo, tunajisikia kama mutunga​-zaburi Asafu, aliyemuimbia Yehova hivi: ‘Umeushika mukono wangu wa kuume. Utaniongoza kwa shauri lako, na baadaye utanipeleka kwenye utukufu.’ (Zab. 73:23, 24) Sisi ni wenye shukrani sana kwa sababu Yehova anatulinda ili tupate wokovu!

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Yehova amekuvuta wewe pia

[Picha katika ukurasa wa 30]

Kutumia shauri la Mungu kunatulinda

[Picha katika ukurasa wa 31]

Vitia-moyo tunavyopokea vinatutia nguvu