Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Watu Wanaona Utukufu wa Yehova Wanapokutazama?

Je, Watu Wanaona Utukufu wa Yehova Wanapokutazama?

Je, Watu Wanaona Utukufu wa Yehova Wanapokutazama?

‘Tunatoa kama vioo murudisho wa utukufu wa Yehova.’​—2 KOR. 3:18.

JE, UNAKUMBUKA?

Ijapokuwa sisi tumezaliwa wenye zambi, tunaweza kumutukuza Yehova namna gani?

Kusali na kuhuzuria mikutano ya kutaniko kunatusaidia namna gani kuonyesha katika maisha yetu utukufu wa Mungu?

Ni nini kitatusaidia tuendelee kumutukuza Yehova?

1, 2. Sababu gani inawezekana kuiga sifa za Yehova?

 KILA mumoja wetu anafanana wazazi wake katika jambo fulani. Kwa hiyo, haishangaze kusikia mutu akimuambia kijana fulani: ‘Unamufanana baba yako.’ Tena mutu anaweza kumuambia binti fulani: ‘Nikikuona, ninamukumbuka mama yako.’ Mara nyingi watoto wanaiga wazazi wao. Je, sisi pia tunaweza kumuiga Baba yetu wa mbinguni, Yehova? Hata ikiwa hatujawahi kumuona, tunaweza kujua sifa zake nzuri kwa kujifunza Neno lake, kwa kutazama vitu alivyoumba, na kwa kutafakari juu ya Maandiko, zaidi sana juu ya maneno na matendo ya Mwana wake, Yesu Kristo. (Yoh. 1:18; Rom. 1:20) Kwa hiyo, tunaweza kuonyesha utukufu wa Yehova.

2 Mbele ya kuumba Adamu na Eva, Mungu alitumaini kama wanadamu wataweza kutimiza mapenzi yake; kuonyesha sifa zake, na kumutukuza. (Soma Mwanzo 1:26, 27.) Tukionyesha sifa za Yule aliyetuumba tutaonyesha kama tunashikamana naye. Tukifanya hivyo, tutakuwa na pendeleo la kuonyesha utukufu wa Mungu hata ikiwa mazoea yetu, elimu yetu, ao kabila zetu zinatofautiana. Sababu gani? Kwa sababu ‘Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mutu ambaye anamuogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.’​—Mdo. 10:34, 35.

3. Tunaweza kujisikia namna gani tunapoendelea kumutumikia Yehova?

3 Wakristo watiwa-mafuta wanaonyesha utukufu wa Yehova katika maisha yao. Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Sisi sote, wakati tunapotoa kama vioo murudisho wa utukufu wa Yehova tukiwa na nyuso zisizo na utaji, tunageuzwa na kuwa katika mufano uleule kutoka utukufu mupaka utukufu.’ (2 Kor. 3:18) Nabii Musa alipokuwa akishuka kutoka Mulima Sinai akibeba mbao zilizokuwa na Amri Kumi, uso wake ulingaa sana, ao ulikuwa ukitosha miale, kwa sababu Musa alikuwa amezungumuza na Yehova. (Kut. 34:29, 30) Ijapokuwa Wakristo hawajazungumuza na Mungu uso kwa uso, wala nyuso zao hazitoi miale, watu wanaweza kuona kama wana furaha wanapozungumuza juu ya Yehova, sifa zake, na kusudi lake nzuri kuelekea wanadamu. Nyakati za zamani kioo kilikuwa cha chuma, na ili kingae zaidi watu walikuwa wakikinoa. Vilevile leo, Wakristo watiwa-mafuta na kondoo wengine wanaangarisha utukufu wa Yehova katika maisha yao na kazi yao ya kuhubiri. (2 Kor. 4:1) Je, watu wanaona utukufu wa Yehova kupitia mwenendo wako na kushiriki kwako kwa ukawaida katika mahubiri?

TUNATAMANI KUMUTUKUZA YEHOVA

4, 5. (a) Kama mutume Paulo, tunapigana vita gani? (b) Zambi imetutia katika hali gani?

4 Sisi watumishi wa Yehova, tunatamani kabisa kumuheshimu na kumutukuza Muumbaji wetu katika kila kitu tunachofanya. Lakini, mara nyingi yale tunayotamani kufanya si yale tunayofanya. Mutume Paulo alipambana na tatizo hilo. (Soma Waroma 7:21-25.) Basi, sababu gani vita hiyo iko ndani ya miili yetu? Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Wote wamefanya zambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.’ (Rom. 3:23) Ni wazi kabisa, wanadamu wameriti zambi kutoka kwa Adamu, kwa hiyo zambi imewatawala ‘kama Mufalme’ mwenye kuwagandamiza.​—Rom. 5:12; 6:12.

5 Zambi ni nini? Ni jambo lolote lisilopatana na sifa za Yehova, njia zake, kanuni zake, na mapenzi yake. Zambi inaharibu urafiki wetu na Mungu. Zambi inatufanya tukose shabaha ao kusudi fulani. Ni kama vile mupiga​-mishale anayetupa mushale lakini haufikie kitu alichovizia. Tunaweza kufanya zambi kwa kukusudia ao bila kukusudia. (Hes. 15:27-31) Zambi imetia mizizi ndani ya wanadamu na inawatenganisha na Muumbaji wao. (Zab. 51:5; Isa. 59:2; Kol. 1:21) Wanadamu wengi hawafanye mapenzi ya Yehova, kwa hiyo wamepoteza pendeleo la kufanya wengine waone utukufu wa Mungu. Kwa kweli, zambi ni ugonjwa mubaya sana unaowatesa wanadamu.

6. Ijapokuwa sisi ni watu wenye zambi, ni mupango gani unaotuwezesha kumutukuza Mungu?

6 Ijapokuwa sisi ni watu wenye zambi, Yehova amejionyesha kuwa “Mungu anayetoa tumaini.” (Rom. 15:13) Amefanya mupango wa kumaliza zambi, yaani, zabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo. Tukionyesha imani katika zabihu hiyo, hatutakuwa tena ‘watumwa wa zambi,’ lakini tutakuwa na nafasi ya kuonyesha utukufu wa Yehova. (Rom. 5:19; 6:6; Yoh. 3:16) Kufanya hivyo kutatusaidia tuwe marafiki sana wa Mungu, na hilo litatuletea baraka sasa na uzima wa milele wakati ujao. Ijapokuwa tungali wanadamu wenye zambi, tunafurahi sana kujua kama Mungu anaona kila mumoja wetu kuwa mutu wa lazima kwa sababu anatupatia pendeleo la kutuwezesha tuonyeshe utukufu wake.

NAMNA YA KUMUTUKUZA MUNGU

7. Kila mutu anapaswa kutambua nini ili aweze kuonyesha utukufu wa Yehova?

7 Ili kuonyesha utukufu wa Mungu kama inavyofaa, tunapaswa kutambua kama sisi ni watenda​-zambi. (2 Nya. 6:36) Tunapaswa kutambua uzaifu wetu na kujikaza kuushinda, kwa kufanya hivyo, tunaweza kusonga mbele ili kuwa katika hali ya kumutukuza Mungu kama inavyofaa. Kwa mufano, ikiwa tumeangukia katika zambi ya kutazama pornografia, yaani, kutazama watu wanaofanya mambo machafu, kama vile kwenye Internet, tunapaswa kukubali kwanza kama tumefanya zambi na kama tunahitaji musaada wa wazee, na kisha tunapaswa kuchukua hatua ya kwenda kuwaona wazee ili watusaidie. (Yak. 5:14, 15) Hilo ni jambo la lazima sana ambalo mutu aliyefanya zambi anapaswa kufanya ili maisha yake yamutukuze Mungu kabisa. Sisi waabudu wa Yehova, tunapaswa kujichunguza kila mara ili kuona kama tungali tunaendelea kuishi kulingana na kanuni za Yehova. (Met. 28:18; 1 Kor. 10:12) Hata ikiwa uzaifu wetu ni wa namna gani, tusijiachilie, tunapaswa kuendelea kushindana na uzaifu huo ili tuweze kuonyesha utukufu wa Yehova katika maisha yetu.

8. Ijapokuwa sisi hatukamilike, tunapaswa kufanya nini?

8 Yesu pekee ndiye aliyeishi na kufa bila kumukosea Mungu, na kila mara watu waliona utukufu wa Mungu kupitia yeye. Yesu alikuwa mutu mukamilifu, lakini, sisi hatukamilike. Hata hivyo, tunaweza kufuata mufano wake ikiwa tunajikaza. (1 Pet. 2:21) Yehova anaona nguvu tunazofanya ili kumutukuza na anapendezwa na maendeleo tunayofanya kuhusu jambo hilo, na kwa hiyo yeye hatakosa kubariki jitihada zetu.

9. Biblia inaweza kutusaidia namna gani ikiwa tunataka kuishi kama vile Mungu anavyopenda?

9 Neno la Yehova linaweza kutusaidia ili tujue namna gani tunaweza kuonyesha vizuri zaidi utukufu wa Mungu katika maisha yetu. Tunapaswa kujifunza sana Biblia na kutafakari juu ya yale tunayosoma. (Zab. 1:1-3) Kusoma Biblia kila siku kutatusaidia tuonyeshe katika maisha yetu utukufu wa Mungu vizuri zaidi. (Soma Yakobo 1:22-25.) Mutu asipojifunza Biblia hawezi kuwa na imani yenye nguvu, itakuwa vyepesi kwake kuangukia katika zambi nzito, na hawezi kuwa na tamaa ya kumupendeza Yehova.​—Zab. 119:11, 47, 48.

10. Sala inaweza kutusaidia namna gani ili tumutumikie Yehova vizuri zaidi?

10 Ili utukufu wa Mungu uonekane katika maisha yetu, tunapaswa pia ‘kudumu katika sala.’ (Rom. 12:12) Ni jambo la lazima sana kumuomba Yehova atusaidie tumutumikie kwa njia anayokubali. Kwa hiyo, kupitia sala tunaweza kumuomba atupatie roho takatifu, imani zaidi, na nguvu za kupambana na vishawishi. Tunaweza pia kumuomba atusaidie ili tujue ‘kutumia sawasawa neno la kweli.’ (2 Tim. 2:15; Mt. 6:13; Lu. 11:13; 17:5) Ni jambo la lazima tumutegemee Baba yetu wa mbinguni Yehova, kama vile mutoto anavyomutegemea baba yake. Tukimuomba atusaidie ili tumutumikie kwa moyo wote, bila shaka atasikia sala hiyo na atatusaidia. Tusifikiri hata kidogo kama sala zetu zitamuuzi. Katika sala tumusifu Mungu, tumushukuru, tumuombe musaada wa kupambana na majaribu, na tumuombe atusaidie ili tumutumikie kwa njia inayotukuza jina lake takatifu.​—Zab. 86:12; Yak. 1:5-7.

11. Namna gani mikutano ya kutaniko inatusaidia tuonyeshe utukufu wa Mungu katika maisha yetu?

11 Mungu amemupatia ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara’ kazi ya kuwatunza kondoo wake anaowapenda. (Mt. 24:45-47; Zab. 100:3) Mutumwa mwaminifu anapenda kutusaidia ili tuonyeshe utukufu wa Yehova katika maisha yetu. Kupitia mikutano, tunasaidiwa kubadilisha maisha yetu na kuwa na sifa nzuri za Kikristo kama vile mushonaji anavyoweza kurekebisha nguo ya mutu ili mutu huyo awe mwenye kupendeza zaidi. (Ebr. 10:24, 25) Kwa hiyo, tujikaze kufika kwa wakati. Ikiwa tuna tabia ya kuchelewa kwenye mikutano yetu, hilo litafanya tupitwe na mafundisho fulani tunayohitaji ili kutengeneza hali yetu fulani inayoweza kufanya tumupendeze Yehova zaidi.

TUMUIGE MUNGU

12. Namna gani tunaweza kumuiga Mungu?

12 Tunaweza kuonyesha utukufu wa Yehova katika maisha yetu ikiwa tu tunakuwa ‘waigaji wa Mungu.’ (Efe. 5:1) Njia moja inayoweza kutusaidia kumuiga Yehova ni kujifunza kuona mambo kama yeye. Tukijaribu kuishi kama tunavyopenda, tunamukosea Mungu heshima na mwenendo huo utatuletea magumu mengi. Kwa kuwa ulimwengu tunamoishi unaongozwa na Shetani Ibilisi, tunapaswa kujikaza kuchukia mambo ambayo Yehova anachukia na kupenda sana mambo anayopenda. (Zab. 97:10; 1 Yo. 5:19) Tunapaswa kuamini kabisa katika moyo wetu kama, ikiwa tunapenda kabisa kumutumikia Mungu kwa njia anayokubali, tunapaswa kufanya mambo yote kwa utukufu wake.​—Soma 1 Wakorintho 10:31.

13. Kwa nini tunapaswa kuchukia zambi, na hilo litatuchochea kufanya nini?

13 Yehova anachukia zambi, kwa hiyo sisi pia tunapaswa kuichukia. Ikiwa tunachukia zambi, tutafanya namna yote ili kuepuka kitu chochote kinachoweza kutuingiza katika zambi. Kwa mufano, ni lazima tuepuke uasi-imani kwa sababu hiyo ni zambi inayoweza kutufanya tuwe watu wasiostahili kumutukuza Mungu. (Kum. 13:6-9) Kwa hiyo, tuwaepuke kabisa waasi​-imani ao watu wanaojiita ndugu lakini matendo yao yanamutukanisha Mungu. Tutafanya hivyo hata ikiwa mutu huyo ni mutu wa familia yetu. (1 Kor. 5:11) Hatutapata faida yoyote kwa kujaribu kubishana na waasi-imani ao watu wanaochambua-chambua tengenezo la Yehova. Ndiyo, hali yetu ya kiroho itakuwa katika hatari ikiwa tutasoma ao kutafuta kujua habari zao katika vitabu ao kwa njia ya Internet.​—Soma Isaya 5:20; Mathayo 7:6.

14. Tunapojikaza kuonyesha utukufu wa Mungu katika maisha yetu, ni sifa gani tunayopaswa kuonyesha sana, na sababu gani?

14 Kuonyesha upendo ni njia ya pekee ya kumuiga Baba yetu wa mbinguni. Kama yeye, tunapaswa kuwa na upendo. (1 Yo. 4:16-19) Bila shaka, tunapopendana hilo linaonyesha kama sisi ni wanafunzi wa Yesu na kama sisi ni watumishi wa Yehova. (Yoh. 13:34, 35) Ijapokuwa wakati fulani​-fulani hali yetu ya kutokukamilika inaweza kutufanya tusionyeshe ndugu zetu upendo, tusijiachilie, tunapaswa kujikaza siku zote kuwapenda ndugu zetu. Kuonyesha upendo na sifa zingine za Mungu kutatusaidia tusitende zambi ao mambo mengine yanayoweza kuwakasirisha wengine.​—2 Pet. 1:5-7.

15. Upendo unatuchochea kuwatendea wengine namna gani?

15 Upendo unatuchochea tuwatendee wengine mambo mazuri. (Rom. 13:8-10) Kwa mufano, ikiwa bwana na bibi wanapendana, wataepuka uzinifu. Kuwapenda wazee wa kutaniko na kuwaheshimu kutatuchochea tukubali na tutii muongozo wao. Ikiwa watoto wanawapenda wazazi wao, watawatii na kuwaheshimu na wataepuka kuwasema-sema vibaya wazazi wao. Ikiwa tunawapenda wanadamu wenzetu, tutaepuka kuwazarau na tutazungumuza nao kwa heshima. (Yak. 3:9) Tena, upendo unawachochea wazee watendee kondoo za Mungu kwa upole.​—Mdo. 20:28, 29.

16. Upendo utatusaidia namna gani ili tutimize kazi yetu ya kuhubiri?

16 Tunapaswa pia kuonyesha upendo katika kazi yetu ya kuhubiri. Kwa kuwa tunamupenda sana Yehova, hatutavunjika moyo kwa sababu watu tunaohubiria wanaonyesha ubaridi ao hawapendezwi. Badala yake, tutaendelea kuhubiri habari njema. Upendo utatuchochea tujitayarishe vizuri kuhusu mahubiri na tujikaze kuwa walimu wazuri wa Neno la Mungu. Ikiwa kweli tunapenda Mungu na jirani yetu, hatutaona kazi ya kuhubiri kuwa yenye kuchokesha ao hatutahubiri kwa sababu tu tunaombwa kuhubiri. Badala yake, tutaona kazi ya kuhubiri kuwa pendeleo kubwa na tutaifanya kwa furaha.​—Mt. 10:7.

ENDELEA KUMUTUKUZA YEHOVA

17. Kutambua kama sisi ni wenye zambi kunatusaidia namna gani?

17 Watu wengi katika ulimwengu hawajui ubaya wa zambi, lakini sisi tunajua. Ndiyo sababu tunajua kama tunapaswa kupambana na uzaifu wetu. Kutambua kama sisi tumezaliwa na zambi kunatusaidia kuizoeza zamiri yetu kusudi itusaidie kutenda yaliyo sawa wakati tamaa ya zambi inaanza kuchochea akili na moyo wetu. (Rom. 7:22, 23) Bila shaka, tunaweza kuwa na uzaifu fulani, lakini Mungu anaweza kutupatia nguvu ya kutenda yaliyo sawa katika hali yoyote inayoweza kujitokeza.​—2 Kor. 12:10.

18, 19. (a) Nini nini kitatusaidia kupigana na Shetani na mashetani wake na kuwashinda? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

18 Ikiwa tunataka kumutukuza Yehova, tunapaswa pia kupambana na roho wabaya, yaani, Shetani na mashetani wake. Mungu ametupatia silaha za kiroho ili tuweze kupigana nao na kuwashinda. (Efe. 6:11-13) Shetani anajaribu bila kuacha kutuchochea tumupatie utukufu ambao ni Yehova tu ndiye anayestahili kupewa. Tena, Ibilisi anafanya yake yote ili aharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova. Lakini wakati sisi na mamilioni ya ndugu wasiokamilika, wanaume, wanawake na watoto, tunaendelea kuwa washikamanifu na kumutukuza Mungu, hilo ni pigo kabisa kwa Shetani. Kwa hiyo, acheni tuendelee kumusifu Yehova kama wale viumbe wa mbinguni wanaopaza sauti hivi: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.”​—Ufu. 4:11.

19 Hata kuwe nini, acheni tuazimie kuendelea kumutukuza Yehova. Yeye anafurahi kabisa anapoona watumishi wake waaminifu wakijikaza kumuiga na kuonyesha utukufu wake katika maisha yao. (Met. 27:11) Tunapaswa kujisikia kama Daudi aliyeimba hivi: ‘Ninakusifu, Ee Yehova Mungu wangu, kwa moyo wangu wote, nami nitalitukuza jina lako mupaka wakati usio na kipimo.’ (Zab. 86:12) Tunangojea kwa hamu sana siku tutaonyesha utukufu wa Yehova katika hali ya ukamilifu na tutaweza hivyo kumusifu milele. Wanadamu wote watiifu watafurahia pendeleo hilo. Je, watu wanaona utukufu wa Yehova Mungu wanapokutazama? Je, unapenda uendelee kufanya hivyo milele na milele?

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 27]

Je, unaonyesha utukufu wa Yehova katika mambo haya?