Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Mufanye Angalisho na “Chachu ya Mafarisayo”

Mufanye Angalisho na “Chachu ya Mafarisayo”

Mufanye Angalisho na “Chachu ya Mafarisayo”

Yesu alionya wanafunzi wake, wafanye angalisho na “chachu ya Mafarisayo, ambayo ni unafiki.” (Lu. 12:1) Mathayo pia aliandika juu ya onyo hilo; ni yeye aliyeonyesha wazi kama wakati Yesu alipozungumuzia chachu alikuwa akilaumu “mafundisho” ya Mafarisayo.​—Mt. 16:12.

Wakati fulani Biblia inatumia neno “chachu,” ao levire, ili kumaanisha ubaya. Kwa kweli, mafundisho na matendo ya Mafarisayo yalikuwa na matokeo mabaya juu ya wasikilizaji wao. Sababu gani mafundisho ya Mafarisayo yalikuwa yenye hatari?

1 Mafarisayo walikuwa na kiburi, walijiona kuwa wenye haki kuliko watu wengine, na waliwazarau watu wa hali ya chini.

Katika mufano wake moja, Yesu alizungumuzia hali hiyo mbaya ya Mafarisayo. Yeye alisema hivi: “Yule Farisayo akasimama na kuanza kusali mambo haya akisema moyoni, ‘Ee Mungu, ninakushukuru ya kuwa mimi si kama wale watu wengine, wanyanganyi, wasio waadilifu, wazinzi, ao hata kama mukusanya​-kodi huyu. Mimi nafunga mara mbili kwa juma, mimi natoa sehemu ya kumi ya vitu vyote ninavyojipatia.’ Lakini yule mukusanya-kodi akiwa amesimama umbali fulani hakutaka hata kuinua macho yake kuelekea mbinguni, bali alikuwa akipiga-piga kifua chake, akisema, ‘Ee Mungu, unirehemu mimi mutenda-zambi.’”​—Lu. 18:11-13.

Yesu alisifu unyenyekevu wa mukusanya​-kodi, aliposema: ‘Ninawaambia ninyi, Mutu huyu alishuka kwenda nyumbani kwake akiwa amesibitishwa kuwa [mwenye haki] zaidi kuliko yule [Mufarisayo]; kwa sababu kila mutu anayejiinua atafezeheshwa, bali yule anayejinyenyekeza atainuliwa.’ (Lu. 18:14) Ijapokuwa wakusanya​-kodi walijulikana kuwa watu wenye sifa mbaya na wasioaminika, Yesu alitaka kusaidia wakusanya-kodi waliotaka kumusikiliza. Wawili kati yao, yaani, Mathayo na Zakayo, wakawa wafuasi wake.

Yehova atajisikia namna gani ikiwa tunafikiri kama sisi ni watu walio bora kuliko wengine kwa sababu ya uwezo wetu mbalimbali ao madaraka tuliopewa ao kwa sababu wengine wameshindwa ao ni wazaifu katika hali fulani? Tunapaswa kuondoa haraka mawazo kama hayo katika moyo wetu kwa sababu Biblia inasema hivi: ‘Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fazili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii juu ya ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli.’ (1 Kor. 13:4-6) Katika tafsiri The New English Bible, maneno: “Upendo . . . haushangilii juu ya ukosefu wa uadilifu,” yametafsiriwa hivi: ‘Upendo . . . haushangilii kwa sababu ya zambi za wengine.’

Tunapaswa kuwa na maoni kama yale ya mutume Paulo. Baada ya kuonyesha kama ‘Kristo Yesu alikuja ulimwenguni ili kuwaokoa watenda-zambi,’ Paulo aliongeza hivi: “Kati ya hao mimi ni wa kwanza kabisa.”​—1 Tim. 1:15.

Fikiria kwa uzito maulizo haya:

Je, ninatambua kama mimi ni mwenye zambi na kama wokovu wangu unategemea fazili zisizostahiliwa za Yehova? Ao je, ninawazarau wengine kwa sababu mimi nimemutumikia Yehova kwa miaka mingi, nina mapendeleo mengi katika tengenezo la Mungu, ao kwa sababu nimezaliwa na uwezo fulani wa pekee?

2 Mafarisayo walipenda kuwashangaza wengine kwa kujionyesha kuwa wenye haki. Walitamani ukubwa na kusifiwa na watu.

Lakini, Yesu alisema hivi juu yao: “Kazi zote wanazozifanya wao huzifanya ili watazamwe na watu; kwa maana wanapanua vibweta vyenye maandiko ambavyo wao huvaa kama ulinzi, na kuongeza ukubwa wa pindo zenye nyuzinyuzi za mavazi yao. Wao hupenda mahali penye kuonekana zaidi kwenye milo ya jioni na viti vya mbele katika masinagogi, na salamu katika masoko na kuitwa Rabi na watu.” (Mt. 23:5-7) Yesu alikuwa tofauti sana nao. Ijapokuwa alikuwa mukamilifu, yeye alikuwa munyenyekevu. Mwanaume fulani alipomuita “mwema,” Yesu alijibu hivi: ‘Kwa nini unaniita mwema? Hakuna mutu aliye mwema, ila mumoja, Mungu.’ (Mk. 10:18) Kwenye pindi nyingine, Yesu alinawisha wanafunzi wake miguu, kwa kufanya hivyo aliwaachia wafuasi wake mufano wa unyenyekevu.​—Yoh. 13:1-15.

Mukristo wa kweli anapaswa kuwatumikia waamini wenzake. (Gal. 5:13) Zaidi sana ndugu anayetaka kuwa muzee wa kutaniko anapaswa kuwatumikia wengine. Ni vizuri ikiwa “anajitahidi kufikia cheo cha mwangalizi,” lakini anapaswa kuwa na nia ya kuwatumikia wengine. Ndugu hapewi “cheo” hicho ili kujitafutia mamlaka ao kuwatawala wengine. Ni lazima wazee wawe ‘wanyenyekevu moyoni,’ kama Yesu.​—1 Tim. 3:1, 6; Mt. 11:29.

Fikiria kwa uzito maulizo haya:

Je, nina muelekeo wa kupendelea wale walio na madaraka katika kutaniko, labda nikitumaini kama watanipa mapendeleo zaidi? Je, kuhusu kazi ya Mungu, ninapenda tu kufanya ile inayoweza kuniletea sifa na kufanya nijulikane na ndugu? Je, ninafanya mambo ili wengine wanione?

3 Sheria na desturi za Mafarisayo zilifanya iwe vigumu kwa watu wa hali ya chini kushika Sheria.

Sheria ya Musa ilionyesha Waisraeli namna ya kumuabudu Yehova. Lakini haikusemea kila jambo ndogo. Kwa mufano, Sheria ilikataza kufanya kazi siku ya Sabato, lakini haikueleza waziwazi kazi ambazo walipaswa kufanya na zile ambazo hawakupaswa kufanya. (Kut. 20:10) Mafarisayo waliongeza sheria na desturi zao kwa sababu waliwaza kama Sheria ya Mungu haikuwa wazi. Yesu hakufuata sheria za Mafarisayo, lakini alishika Sheria ya Musa. (Mt. 5:17, 18; 23:23) Yesu alielewa mambo ya lazima yaliyokuwa katika Sheria ya Musa. Yesu alijua sababu zilizofanya Sheria itolewe, na alionyesha kama jambo la lazima katika Sheria ni kuonyesha rehema na huruma. Aliwaelewa wanafunzi wake, hata wakati walifanya mambo yaliyomuvunja moyo. Kwa mufano, ijapokuwa aliwasihi mitume wake watatu wabaki macho usiku huo alipokamatwa, aliwakuta mara nyingi wakiwa wenye kulala. Hata hivyo, aliwaambia hivi kwa upole: ‘Bila shaka, roho inataka, lakini mwili ni zaifu.’​—Mk. 14:34-42.

Fikiria kwa uzito maulizo haya:

Je, ninatafuta kuwekea wengine sheria kali, zisizobadilika kulingana na hali ao ninafanya mawazo yangu kuwa sheria? Je, ninataka tu wengine wafanye mambo kama ninavyopenda bila kufikiria hali?

Unapofikiria tofauti iliyo kati ya mafundisho ya Yesu na yale ya Mafarisayo, je, unaona mahali ambapo unapaswa kufanya mabadiliko? Ikiwa ni hivyo, kwa nini usiazimie kufanya hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 28]

Mafarisayo walivaa vibweta vyenye maandiko.—Mt. 23:2, 5

[Picha katika ukurasa wa 29]

Tofauti na Mafarisayo wenye kiburi, wazee wa kutaniko wanawatumikia wengine kwa unyenyekevu

[Picha katika ukurasa wa 30]

Yesu hakuwaomba wengine wafanye mambo kama vile tu anavyotaka bila kufikiria hali. Je, unamuiga?