Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Mutumaini Yehova Mungu wa “Nyakati na Majira”

Mutumaini Yehova Mungu wa “Nyakati na Majira”

Mutumaini Yehova Mungu wa “Nyakati na Majira”

“Anabadili nyakati na majira, akiondoa wafalme na kuwasimamisha wafalme.”​—DAN. 2:21.

JE, UNAKUMBUKA?

Vitu ambavyo Mungu aliumba na unabii mbalimbali uliotimia vinaonyesha namna gani kama Yehova ni Muheshimu-Wakati Mukubwa?

Kujua kama Yehova ni Mungu wa “nyakati na majira” kunapaswa kutuchochea kufanya nini?

Kwa nini kusudi la Yehova halitegemee mambo yanayotokea ulimwenguni na mipango ya wanadamu?

1, 2. Ni nini inayoonyesha kama Yehova anaelewa vizuri sana wakati?

 YEHOVA MUNGU alifanya mupango kuwe vitu vya kupima wakati mbele hata ya kumuumba mwanadamu. Siku ya ine ya uumbaji, Mungu alisema hivi: ‘Kuwe na mianga katika anga la mbingu ili kutenganisha muchana na usiku; nayo iwe ishara na kwa ajili ya majira na kwa ajili ya siku na miaka.’ (Mwa. 1:14, 19, 26) Na kulingana na mapenzi yake, mambo yakawa hivyo.

2 Hata hivyo, mupaka sasa wanasayansi wameshindwa kueleza kama wakati ni nini. Kitabu kimoja kinasema hivi: ‘Wakati ni kati ya mambo ambayo ni vigumu sana kuelewa. Hakuna mutu anayeweza kueleza kama wakati ni nini.’ Lakini, Yehova yeye anaelewa vizuri sana wakati. Hilo halishangazi, kwa kuwa yeye ni ‘Muumba wa mbingu, Mufanyizaji wa dunia na Mutengenezaji wake.’ Yehova tu ndiye “anayetangaza tangu mwanzo ule mwisho, na kutoka zamani za kale mambo ambayo hayajafanywa.” (Isa. 45:18; 46:10) Acheni tujifunze namna vitu alivyoumba na kutimizwa kwa unabii kunaonyesha namna Yehova anavyoheshimu sana wakati. Hilo litafanya tumutumaini sana Mungu na Neno lake.

VITU ALIVYOUMBA VINATUSAIDIA KUWA NA IMANI YENYE NGUVU

3. Namna gani vitu ambavyo Yehova aliumba vinaheshimu wakati?

3 Vitu vingi ambavyo Yehova aliumba, viwe vikubwa ao vidogo, vinaheshimu sana wakati. Chembe ndogo sana inayoitwa atome inayopatikana katika kila kitu inatingizika​-tingizika kwa mwendo uleule bila kukosea ao kubadilika​-badilika. Kuna saa zinazotumia atome ili kupima wakati; saa hizo haziwezi kuchelewa hata segonde moja katika kipindi cha miaka milioni 80. Vitu kama vile dunia na nyota vinazunguka angani kwa kuheshimu wakati hivi kwamba tunaweza kujua mahali vitakuwa pa saa ao siku fulani. Kujua mahali ambapo nyota zinaweza kuwa angani kumewasaidia watu kujua majira, na kumewasaidia wale wanaosafiri watambue mahali wanapokwenda. Kwa kweli, Yehova aliyefanya vitu hivyo vyenye kutegemeka vya kupima wakati ni “hodari katika nguvu” na anastahili kupewa sifa.​—Soma Isaya 40:26.

4. Vitu vilivyo na uzima, kama vile watu, wanyama na mimea, vinaonyesha namna gani hekima ya Mungu?

4 Vitu vilivyo na uzima, kama vile watu, wanyama ao mimea, vinaongozwa na wakati. Mimea na wanyama wana namna fulani ya saa iliyo ndani yao inayowaongoza. Ndenge nyingi zina uwezo wa kujua wakati wa kuhama ili kwenda kuishi mahali pengine. (Yer. 8:7) Wanadamu pia wanaongozwa na namna fulani ya saa iliyo katika miili yao. Saa hiyo inawasaidia kutambua kama ni usiku ao ni muchana. Tunapofika katika eneo fulani kisha safari ndefu, inachukua wakati fulani ili mwili wetu uzoee saa ya mahali hapo. Kwa kweli, kuna mifano ya vitu vingi katika uumbaji inayoonyesha kama Yehova ni Mungu wa “nyakati na majira.” (Soma Zaburi 104:24.) Na kwa kuwa Yehova ni mwenye hekima na nguvu zisizo na mipaka, tunaweza kuwa na imani kama ana uwezo wa kutimiza chochote anachotaka!

KUTIMIA KWA UNABII KWA WAKATI KUNATUSAIDIA KUWA NA IMANI YENYE NGUVU

5. (a) Ni njia gani moja tu inayoweza kutusaidia kujua namna gani wakati ujao utakuwa? (b) Sababu gani ni Yehova tu anayeweza kutabiri mambo na wakati yatatimia?

5 Vitu ambavyo Yehova aliumba vinatufundisha juu ya “sifa zake ambazo hazionekani,” lakini haviwezi kujibu ulizo hili la maana: Wakati ujao utakuwa namna gani? (Rom. 1:20) Jibu linapatikana tu katika Biblia. Tunapojifunza Biblia, tutapata unabii mbalimbali uliotimizwa kwa wakati kabisa. Yehova anaweza kutufunulia mambo yatakayotokea kesho kwa sababu ana uwezo wa kuona bila kudanganyika mambo yatakayotokea wakati ujao. Tena, unabii wa Biblia unatimia kwa wakati kabisa kwa sababu Yehova Mungu anaweza kufanya mambo yatokee kulingana na kusudi lake na programu yake.

6. Ni nini inayoonyesha kama Yehova anataka tuelewe vizuri utimizo wa unabii mbalimbali wa Biblia?

6 Yehova anataka waabudu wake waelewe vizuri unabii mbalimbali wa Biblia na wafaidike kutokana na unabii huo. Ijapokuwa Mungu haoni wakati kama sisi, yeye anatumia maneno tunayoweza kuelewa anaposema kama jambo fulani litatokea kwa wakati fulani. (Soma Zaburi 90:4.) Kwa mufano, kitabu cha Ufunuo kinazungumuzia “malaika wanne” ambao “wametayarishwa kwa ajili ya ile saa na siku na mwezi na mwaka.” Maneno: saa, siku, mwezi na mwaka yanaeleweka kabisa. (Ufu. 9:14, 15) Kuona namna unabii mbalimbali ulivyotimia kwa wakati kamili kunatusaidia tutumainie sana Mungu wa “nyakati na majira” na Neno lake. Acheni tuzungumuzie mifano fulani.

7. Kutimia kwa unabii wa Yeremia juu ya Yerusalemu na Yuda kunaonyesha namna gani kwamba Yehova ni Muheshimu-Wakati Mukubwa?

7 Kwanza, tuzungumuzie mambo yaliyotokea kuanzia mwaka wa mia sita mbele ya Kristo. Biblia inasema hivi: ‘Katika mwaka wa ine wa Yehoyakimu mwana wa Yosia, mufalme wa Yuda,’ neno la Muheshimu-Wakati Mukubwa ‘lilimujia Yeremia kuhusu watu wote wa Yuda.’ (Yer. 25:1) Wakati huo, Yehova alitabiri kama Yerusalemu itaharibiwa, na Wayuda watahamishwa kutoka Yuda ili kuenda Babiloni na ‘kumutumikia mufalme wa Babiloni miaka 70.’ Mwaka wa 607 mbele ya Kristo, majeshi ya Babiloni yaliharibu Yerusalemu, na Wayahudi waliokuwa Yuda wakapelekwa Babiloni. Lakini jambo gani lingetokea kisha miaka 70? Yeremia alitabiri hivi: “Kwa maana Yehova amesema hivi, ‘Kupatana na kutimia kwa miaka 70 katika Babiloni nitawakazia ninyi fikira, nami nitawatimizia neno langu jema kwa kuwarudisha tena mahali hapa.’” (Yer. 25:11, 12; 29:10) Unabii huo ulitimia kwa wakati kabisa. Katika mwaka wa 537, Wayahudi walirudi katika inchi yao kutoka Babiloni kisha kuachiliwa huru na Wamede na Waperse.

8, 9. Namna gani unabii wa Danieli juu ya kutokea kwa Masiya na kuwekwa kwa Ufalme wa Mungu, unaonyesha kama Yehova ndiye Mungu wa “nyakati na majira”?

8 Tuzungumuzie unabii mwingine unaohusu watumishi wa Mungu wa zamani. Miaka miwili hivi mbele ya Wayahudi kuondoka Babiloni, Mungu alitabiri kupitia nabii Danieli kama Masiya angetokea miaka 483 kisha kutolewa kwa lile neno la kujenga upya Yerusalemu. Mufalme wa Wamede na Waperse alitoa ruhusa ya kujenga Yerusalemu mwaka wa 455 mbele ya Kristo. Tukihesabu miaka 483 kuanzia mwaka wa 455, tunafika kwenye mwaka wa 29. Katika mwaka huo, Yesu wa Nazareti alitiwa mafuta kwa roho takatifu alipobatizwa, na hivyo akawa Masiya. *​—Neh. 2:1, 5-8; Dan. 9:24, 25; Lu. 3:1, 2, 21, 22.

9 Tuchunguze sasa yale ambayo Maandiko yalitabiri juu ya Ufalme wa Mungu. Unabii wa Biblia ulionyesha kama Ufalme wa Masiya ungewekwa mbinguni katika mwaka wa 1914. Tena, Biblia ikaonyesha “ishara” ya kuwapo kwa Yesu na ukaonyesha kama wakati huo, Shetani atafukuzwa mbinguni na kwa hiyo mateso makubwa yangetokea duniani. (Mt. 24:3-14; Ufu. 12:9, 12) Tena, unabii wa Biblia ulionyesha waziwazi kama “nyakati zilizowekwa za mataifa” zingemalizika katika mwaka wa 1914 na kuanzia mwaka huo, Ufalme ungeanza kutawala mbinguni.​—Lu. 21:24; Dan. 4:10-17. *

10. Ni mambo gani ambayo yatatokea bila shaka kwa wakati?

10 Mbele yetu ‘Ziki kubwa’ iliyotabiriwa na Yesu inatungojea. Kisha ziki hiyo, Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu utaanza. Hakuna shaka lolote, mambo hayo yatatokea kwa wakati kama ilivyopangwa. Yesu alipokuwa duniani, Yehova alikuwa amekwisha kupanga “siku na saa” ya mambo hayo.—Mt. 24:21, 36; Ufu. 20:6.

‘TUJINUNULIE WAKATI UNAOFAA’

11. Kujua kama tunaishi siku za mwisho kunapaswa kutuchochea kufanya nini?

11 Kujua kama Ufalme wa Mungu umeanza kutawala na kama tunaishi katika “wakati wa mwisho” kunapaswa kutuchochea kufanya nini? (Dan. 12:4) Watu wengi wanajionea kila siku namna hali za dunia zinavyoharibika, lakini hawaitike kama hali hizo zinatimiza unabii wa Biblia kuhusu siku za mwisho. Wengine wanafikiri kama siku moja ulimwengu huu utaangamizwa ao wanaweza kufikiri kama wanadamu watajikaza kuleta “amani na usalama.” (1 Th. 5:3) Lakini, sisi tuna mawazo gani? Ikiwa tunaamini kabisa kama tunaishi mwisho wa siku za mwisho za ulimwengu huu wa Shetani, tunapaswa kujikaza kutumia wakati unaobaki ili kumutumikia Mungu wa “nyakati na majira” na kuwasaidia wengine wamujue, sivyo? (2 Tim. 3:1) Kwa hiyo, tunapaswa kutumia wakati wetu kwa hekima.​—Soma Waefeso 5:15-17.

12. Maneno ya Yesu juu ya siku za Noa yanatufundisha nini?

12 Si rahisi “kujinunulia wakati unaofaa” katika ulimwengu huu unaojaa mambo yanayokengeusha akili. Yesu alionya hivi: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” Siku za Noa zilikuwa namna gani? Ilitabiriwa kwamba dunia ya wakati huo itaharibiwa. Uharibifu huo ungefanya watu wabaya wazamishwe na maji ya garika ambayo yangeifunika dunia yote. Noa, ‘muhubiri wa uadilifu,’ aliwatangazia watu wa siku zake ujumbe wa Mungu kwa uaminifu. (Mt. 24:37; 2 Pet. 2:5) Lakini, wao walikuwa ‘wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, nao hawakujali mupaka garika ikaja na kuwafagilia mbali wote.’ Kwa hiyo, Yesu aliwaonya wanafunzi wake hivi: ‘Ninyi pia iweni tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa musiyofikiria.’ (Mt. 24:38, 39, 44) Tunapaswa kumuiga Noa wala si watu wa siku zake. Lakini, ni nini itatusaidia kuendelea kuwa tayari?

13, 14. Tunapongojea kuja kwa Mwana wa binadamu hatupaswi kusahau jambo gani linaloweza kutusaidia kumutumikia Mungu kwa uaminifu?

13 Ijapokuwa Mwana wa binadamu atakuja katika saa tusiyofikiria, hatupaswi kusahau kama Yehova ndiye Muheshimu​-Wakati Mukubwa. Programu yake haitegemei mambo fulani yatakayotokea ulimwenguni wala mipango ya wanadamu. Yeye anapanga wakati wake na kufanya mambo yatokee kama anavyopenda (Soma Danieli 2:21.) Andiko la Methali 21:1 linasema hivi: ‘Moyo wa mufalme ni kama vijito vya maji mukononi mwa Yehova. Huugeuza kuelekea popote anapopenda.’

14 Yehova ana uwezo wa kufanya mambo yatendeke ili kutimiza kusudi lake na kulifanya litimizwe bila kuchelewa. Mabadiliko mengi makubwa yanayotokea duniani yametimiza unabii wa Biblia, zaidi sana unabii unaohusu kuhubiriwa kwa habari njema ya Ufalme wa Mungu katika dunia yote. Kwa mufano, kuanguka kwa Muungano wa Kisovieti na matokeo yake. Watu wengi hawakuwazia kama badiliko kama hilo lingeweza kutukia kwa gafula siku fulani. Mabadiliko kama hayo yameleta matokeo mazuri, leo habari njema inahubiriwa katika inchi ambamo kazi yetu ya kuhubiri ilikatazwa hapo zamani. Kwa hiyo, acheni tununue wakati unaofaa ili kumutumikia kwa uaminifu Mungu wa “nyakati na majira.”

TUWE NA IMANI KAMA YEHOVA ATATIMIZA KUSUDI LAKE BILA KUCHELEWA

15. Tunaweza kuonyesha namna gani kama tuna imani wakati mabadiliko fulani yanapotokea katika tengenezo la Yehova?

15 Ili tuendelee kuhubiri Ufalme katika siku hizi za mwisho, tunapaswa kuwa na imani kama Yehova atatimiza kusudi lake kwa wakati. Hali za ulimwengu zinazobadilika​-badilika zinaweza kutufanya tubadilishe namna yetu ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Wakati fulani tengenezo linaweza kufanya mabadiliko fulani ili kutusaidia tupate matokeo mazuri zaidi katika kazi yetu ya kuhubiri. Tutaonyesha kama tuna imani katika Mungu wa “nyakati na majira,” ikiwa tunakubali mabadiliko hayo, na kuendelea kutumika kwa uaminifu chini ya uongozi wa Mwana wake ambaye ndiye “kichwa cha kutaniko.”​—Efe. 5:23.

16. Kwa nini tuwe na imani kama Yehova atatupatia musaada kwa wakati unaofaa?

16 Yehova anataka tusali bila woga tukiwa na tumaini kwamba atatupatia ‘musaada kwa wakati unaofaa.’ (Ebr. 4:16) Je, hilo halionyeshi kama Mungu anamupenda kila mumoja wetu? (Mt. 6:8; 10:29-31) Tunaonyesha kama tunamutumaini Yehova Mungu kwa kumuomba musaada kwa ukawaida na kwa kutenda kulingana na sala zetu na kufuata muongozo wake. Tusisahau pia kusali kwa ajili ya waamini wenzetu.

17, 18. (a) Ni jambo gani ambalo Yehova atatendea maadui wake hivi karibuni? (b) Tunapaswa kuepuka mutego gani?

17 Huu sio wakati wa ‘kusitasita kwa ukosefu wa imani’; lakini ni wakati wa kutia nguvu imani yetu. (Rom. 4:20) Adui za Mungu, yaani, Shetani na watu wanaojiacha kuongozwa naye, wanajaribu kuzuia kazi ambayo Yesu alipatia wafuasi wake, na wanajaribu kutuzuia sisi pia. (Mt. 28:19, 20) Ijapokuwa Shetani anaweza kutushambulia, tunajua kama Yehova ni “Mungu aliye hai, ambaye ni Mwokozi wa watu wa namna zote, hasa wa watu waaminifu.” Naye “anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.”​—1 Tim. 4:10; 2 Pet. 2:9.

18 Karibuni, Yehova ataharibu ulimwengu huu muovu. Hata ikiwa hatukupewa habari zote juu ya uharibifu huo na wakati gani utatokea, jambo tunalojua ni hili: Kwa wakati kamili, Kristo atawaharibu maadui wote wa Mungu, na hivyo kila mutu atalazimika kujua kama ni Yehova ndiye aliye na haki ya kutawala ulimwengu wote. Kwa hiyo, ikiwa tunakosa kutambua maana ya “nyakati na majira” ya wakati huu, huko ni kudanganyika kabisa. Basi, tunapaswa kuwa waangalifu ili tusinaswe katika mutego wa kuanza kufikiri kama “mambo yote yanaendelea sawasawa kama tangu mwanzo wa uumbaji.”​—1 Th. 5:1; 2 Pet. 3:3, 4.

TUONYESHE KAMA TUKO WENYE KUNGOJEA

19, 20. Kwa nini tuendelee kuonyesha mutazamo wa kumungojea Yehova?

19 Alipowaumba wanadamu, Yehova Mungu alitaka waishi milele ili wawe na wakati wa kujifunza juu yake na juu ya vitu vizuri alivyoumba. Andiko la Mhubiri 3:11 linasema hivi: ‘[Yehova] amefanya kila kitu kiwe chenye kupendeza kwa wakati wake. Tena wakati usio na kipimo ameuweka ndani ya moyo wao, ili mwanadamu asiweze kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mupaka mwisho.’

20 Tunafurahi sana kujua kama Yehova hajabadilisha kusudi lake juu ya wanadamu! (Mal. 3:6) Mungu yeye “habadiliki, kama kugeuka kwa kivuli.” (Yak. 1:17) Yehova hategemei njia za wanadamu za kupima wakati kama vile kuzunguka kwa dunia. Yehova ni ‘Mufalme wa umilele,’ (1 Tim. 1:17) Acheni basi tuonyeshe ‘mutazamo wa kumungojea Mungu wa wokovu [wetu].’ (Mika 7:7) Kwa hiyo, ‘tuwe hodari, nayo mioyo yetu na iwe na nguvu, sisi sote tunaomungojea Yehova.’​—Zab. 31:24.

[Maelezo ya chini]

^ Soma kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! ukurasa wa 186-195.

^ Soma kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli! ukurasa wa 94-97.

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 19]

Danieli aliamini kwamba unabii wa Mungu unatimia siku zote

[Picha katika ukurasa wa 21]

Je, unatumia vizuri wakati wako ili kufanya mapenzi ya Yehova?