Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Umutumikie Mungu Anayetoa Uhuru

Umutumikie Mungu Anayetoa Uhuru

Umutumikie Mungu Anayetoa Uhuru

‘Kwa maana kumupenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si muzigo muzito.’​—1 YOH. 5:3.

UNAWEZA KUJIBU NAMNA GANI?

Namna gani Shetani anawafanya watu wafikiri kama sheria za Mungu ni nzito?

Kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu marafiki wetu?

Ni nini kitakachotusaidia kubaki waaminifu kwa Mungu anayetutolea uhuru?

1. Namna gani Yehova anatumia uhuru wake, na ni nini inayoonyesha kama alipatia Adamu na Eva uhuru mwingi?

 HAKUNA mutu aliye na uhuru kama Yehova. Hata hivyo, yeye hautumie uhuru wake vibaya; wala haone kama ni yeye tu anayepaswa kuwa na uhuru. Yeye hawaamulie watumishi wake kila jambo wanalopaswa kufanya hata katika mambo madogo​-madogo. Tofauti na hilo, amewapa uhuru wa kuchagua, kwa hiyo wanaweza kuamua mambo fulani na kutosheleza tamaa zao zote nzuri. Kwa mufano, Mungu alipatia Adamu na Eva sheria moja tu; aliwakataza kula matunda ya ‘muti wa ujuzi wa mema na mabaya.’ (Mwa. 2:17) Bila shaka, Adamu na Eva wangefanya mapenzi ya Muumbaji wao bila kupoteza uhuru wao.

2. Sababu gani wazazi wetu wa kwanza walipoteza uhuru waliopewa na Mungu?

2 Sababu gani Mungu aliwapa wazazi wetu wa kwanza uhuru mwingi hivyo? Mungu aliwaumba kwa mufano wake na aliwaumba na zamiri, kwa hiyo alikuwa na haki ya kutazamia kama watamupenda yeye Muumbaji wao na kukubali awaongoze katika njia inayofaa. (Mwa. 1:27; Rom. 2:15) Lakini jambo la huzuni ni kwamba Adamu na Eva walikosa shukrani kwa Muumbaji wao aliyewapatia uzima na uhuru waliokuwa wakifurahia. Walichagua uhuru usiofaa ambao Shetani aliwaambia watapa; uhuru wa kujiamulia mazuri na mabaya. Lakini, kuliko kupata uhuru zaidi, Adamu na Eva walijiuzisha wenyewe na watoto wao katika utumwa wa zambi na hilo liliwaletea matokeo mabaya.​—Rom. 5:12.

3, 4. Shetani anaweza kutufanya tufikiri nini kuhusu sheria za Yehova?

3 Ikiwa Shetani aliweza kuwadanganya wanadamu wakamilifu wa kwanza na kuwafanya malaika wengi wakatae utawala wa Mungu, basi anaweza kutudanganya sisi pia. Shetani anatumia njia ileile ili kutudanganya. Anajaribu kutufanya tufikiri kama sheria za Mungu ni nzito na zinatufunga-funga ili tusifurahie maisha. (1 Yoh. 5:3) Ikiwa tunafanya urafiki na watu wanaowaza hivyo, sisi pia tunaweza kuanza kufikiri kama wao. Dada mumoja mwenye umri wa miaka 24, ambaye aliangukia katika uasherati, alisema hivi: “Marafiki wabaya walinifanya niangukie katika kosa hilo kwa sababu niliogopa nisionekane kuwa na mawazo tofauti na yao.” Labda wewe pia umekwisha kujionea namna mikazo ya marafiki inavyoweza kumuchochea mutu kufanya makosa.

4 Jambo lenye kuhuzunisha ni kwamba marafiki wabaya wanaweza pia kuwa katika kutaniko. Shahidi mumoja kijana alisema hivi: “Niliwajua vijana fulani ambao walifanya urafiki wa kimapenzi na watu wasio Mashahidi. Mwishowe niliona kama kadiri nilivyopitisha wakati mwingi pamoja nao ndivyo nilianza kutenda kama wao. Urafiki wangu pamoja na Yehova ulianza kuharibika. Sikuwa tena nafurahia chakula cha kiroho kwenye mikutano na nilianza kuhubiri mara mojamoja tu. Hali hiyo ilinisaidia kutambua kama ninapaswa kuachana na marafiki hao, na nilifanya hivyo.” Je, unajua kama marafiki wana uvutano wa kumufanya mutu aingie katika mwenendo usiofaa? Tutajifunza mufano moja katika Biblia.​—Rom. 15:4.

ABSALOMU ALIIBA MIOYO YAO

5, 6. Namna gani Absalomu aliwadanganya watu, na je, alifikia mipango yake ya ujanja?

5 Biblia inazungumuzia mifano ya watu ambao walikuwa na uvutano mubaya juu ya wengine. Tuchukue mufano wa Absalomu, mwana wa Mufalme Daudi. Absalomu alikuwa na sura nzuri sana. Hata hivyo, kisha muda fulani, alianza kukomalisha tamaa mbaya kama Shetani, kwa kutamani kiti cha ufalme cha baba yake, ijapokuwa hakuwa na haki ya kuwa mufalme. * Kwa njia ya ujanja Absalomu alitaka awe mufalme mahali pa baba yake, na akaanza kujionyesha kama anawahangaikia Waisraeli sana kuliko baba yake. Kama vile Shetani alivyofanya katika shamba la Edeni, Absalomu aliwafanya watu wafikiri kama yeye atawasaidia kabisa, na wakati huohuo alikuwa akisema mambo ya uongo kuhusu baba yake.​—2 Sam. 15:1-5.

6 Je, Absalomu alifikia mipango yake ya ujanja? Ndiyo, kwa kiasi fulani, kwa kuwa Biblia inasema: “Absalomu akaendelea kuiba mioyo ya watu wa Israeli.” (2 Sam. 15:6) Lakini, mwishowe kwa sababu ya kiburi alishindwa. Jambo mbaya zaidi, kiburi hicho kilimuongoza kwenye kifo, yeye na maelfu ya watu waliomuunga mukono.​—2 Sam. 18:7, 14-17.

7. Mambo ambayo Absalomu alifanya yanatufundisha nini? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 14.)

7 Kwa sababu gani Waisraeli hao walidanganywa kwa urahisi? Labda walitamani mambo ambayo Absalomu aliwaahidia. Ao labda, walidanganywa kwa sababu ya sura yake nzuri. Iwe ni jambo gani liliwavutia, jambo tunalojua ni hili: Walikosa uaminifu kwa Yehova na kwa mufalme aliyechaguliwa naye. Leo, Shetani anaendelea kutumia watu walio kama Absalomu ili kuiba mioyo ya watumishi wa Yehova. Watu hao wanaweza kusema hivi: ‘Sheria za Yehova zinafunga watu sana. Na tazama! wale wote wasiomutumikia Yehova wanafurahia maisha.’ Unaposikia maneno kama hayo, je, wewe hauone kama ni uongo na unaazimia kubaki mwaminifu kwa Mungu? Je, unatambua kama ni “sheria kamilifu” ya Yehova tu, maana yake, sheria ya Kristo ndiyo inayoweza kukuongoza kwenye uhuru wa kweli? (Yak. 1:25) Ikiwa ndivyo, onyesha kama unapendezwa na sheria hiyo, na usijaribu kuutumia vibaya uhuru wako wa Kikristo.​—Soma 1 Petro 2:16.

8. Ni mifano gani ya kisasa inayoonyesha kama kuvunja sheria za Yehova hakumuletee mutu furaha?

8 Shetani anavizia zaidi sana vijana. Akikumbuka wakati alipokuwa kijana sana, ndugu mumoja aliye sasa na miaka zaidi ya 30 anasema hivi: “Niliona kama sheria za Yehova zilikuwa zinanifunga​-funga badala ya kunilinda.” Mawazo hayo yalimufanya aangukie katika uasherati. Lakini, jambo hilo halikumuletea furaha. Alisema hivi: “Kwa miaka mingi mutu anaendelea kujuta na zamiri yake inaendelea kumusumbua.” Dada mumoja alipokuwa akikumbuka miaka yake ya ujana, aliandika hivi: “Kisha kufanya uasherati, mutu anahuzunika sana na kujiona wa bure. Kumekwisha kupita miaka 19, lakini ningali nakumbuka kwa uchungu yale niliyofanya.” Dada mwengine anaeleza hivi: “Wazo la kwamba mwenendo wangu uliwahuzunisha watu niliowapenda sana liliniumiza kiakili, kiroho na moyoni. Ni jambo mbaya sana kuishi bila kukubaliwa na Yehova. Shetani hataki ufikirie matokeo mabaya ya zambi.”

9. (a) Ni maulizo gani tunayopaswa kujiuliza wenyewe juu ya Yehova, sheria zake na kanuni zake? (b) Kwa nini ni jambo la maana kumujua Mungu vizuri?

9 Inasikitisha kuona kama vijana wengi waliokomalia katika kweli, na hata watu wakubwa, wakisha kupata matokeo mabaya ndipo wanajifunza kama furaha ya zambi kila mara ina matokeo mabaya! (Gal. 6:7, 8) Kwa hiyo, ujiulize hivi: ‘Je, ninatambua njia za ujanja ambazo Shetani anatumia ili kunidanganya na kuniumiza? Je, ninamuona Yehova kuwa Rafiki yangu wa sana, anayeniambia kila siku ukweli na anayenitakia mema? Je, ninaamini kabisa kama hawezi hata kidogo kuniima mambo mema yanayoweza kuniletea furaha ya kweli?’ (Soma Isaya 48:17, 18.) Unaweza kujibu ndiyo kwa maulizo hayo ikiwa tu unamujua Yehova vizuri. Ni lazima umujue Yehova vizuri sana na kujua kama sheria na kanuni zake zilizo katika Biblia zinaonyesha kama anatupenda; hakuzitia ili kutusonga ao kutufunga​-funga.​—Zab. 25:14.

UMUOMBE YEHOVA AKUPATIE MOYO WA HEKIMA NA MUTIIFU

10. Kwa nini tunapaswa kujikaza kumuiga Mufalme Sulemani?

10 Alipokuwa angali kijana, Sulemani aliomba Mungu hivi kwa unyenyekevu: ‘Nami ni muvulana mudogo tu. Sijui jinsi ya kutoka na jinsi ya kuingia.’ Kisha alimuomba Yehova amupatie moyo wa hekima na mutiifu. (1 Fal. 3:7-9, 12) Yehova alijibu sala hiyo ya kutoka moyoni, na anaweza pia kujibu sala yako, iwe wewe ni kijana ao mutu muzima. Bila shaka, Yehova hatakupatia ufahamu na hekima kimuujiza. Lakini, atakufanya uwe mwenye hekima ikiwa unajifunza Neno lake kwa bidii, ikiwa unamuomba roho takatifu, na ikiwa unafaidika kikamili na mipango ya kiroho anayotutolea kupitia kutaniko la Kikristo. (Yak. 1:5) Bila shaka, Yehova anatumia njia hizo ili kufanya watumishi wake, hata wale ambao ni vijana sana, wawe na hekima kuliko wale wote wanaokataa mashauri yake, kuliko hata wale wanaojiita eti ni “wenye hekima na akili” katika ulimwengu huu.​—Lu. 10:21; soma Zaburi 119:98-100.

11-13. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na Zaburi 26:4, Methali 13:20, na 1 Wakorintho 15:33? (b) Namna gani unaweza kutumia kanuni zinazopatikana katika maandiko hayo?

11 Maandiko yanayofuata yatatuonyesha faida ya kujifunza Biblia na kutafakari juu ya yale tunayosoma ili kumujua Yehova vizuri sana. Kila andiko linazungumuzia kanuni ya maana juu ya kuchagua marafiki. Andiko la Zaburi 26:4, linasema hivi: “Sikuketi na watu wasiosema kweli; wala siingii pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.” Methali 13:20 inasema hivi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” Na andiko la 1 Wakorintho 15:33 linaema: ‘Musipotoshwe. Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.’

12 Tunaweza kujifunza nini kutokana na maandiko hayo? (1) Yehova anataka tuchague marafiki wetu kwa uangalifu. Anataka kutuepusha na mambo yanayoweza kutuumiza na kuharibu urafiki wetu pamoja naye. (2) Marafiki wetu wanaweza kutuchochea kutenda mema ao mabaya; hiyo ndiyo kawaida ya maisha. Ona kwamba maneno yanayopatikana katika maandiko hayo yanaonyesha kama Yehova anajaribu kugusa moyo wetu. Namna gani hivyo? Ona kwamba maandiko hayo hayatoe amri kama vile, “haupaswe kufanya jambo hili ao haupaswe kufanya jambo lile.” Lakini, maneno yanayopatikana katika maandiko hayo ni kweli za musingi zilizo wazi ao kanuni. Kwa kweli, ni kama vile Yehova anatuambia hivi: ‘Ukweli wa mambo ndio huu. Utafanya nini? Ni mawazo gani yaliyo katika moyo wako?’

13 Mwishowe, maandiko hayo matatu yanazungumuzia kweli za musingi ao kanuni ambazo hazibadilike na ambazo zinaweza kutumiwa katika hali mbalimbali. Kwa mufano, ujiulize hivi: Namna gani ninaweza kufanya urafiki na watu “wanaoficha jinsi walivyo”? Ni hali gani zinazoweza kunifanya nishirikiane nao? (Met. 3:32; 6:12) “Watu wenye hekima” ambao Yehova anataka nifanye nao urafiki ni nani? Ni nani walio “wajinga” ambao Yehova anataka niepuke? (Zab. 111:10; 112:1; Met. 1:7) Ni “tabia nzuri” gani ambazo ninaweza kupoteza ikiwa nina marafiki wabaya? Je, marafiki wabaya wanapatikana tu inje ya kutaniko? (2 Pet. 2:1-3) Unaweza kujibu namna gani maulizo hayo?

14. Namna gani tunaweza kufanya Ibada ya Familia ya mangaribi iwe yenye kusaidia zaidi washiriki wa familia?

14 Kisha kutafakari hivyo kuhusu maandiko hayo, kwa nini usichunguze maandiko mengine ya Biblia yanayofunua mawazo ya Mungu juu ya mambo yanayokuhusu wewe ao yanayohusu familia yenu? * Wazazi, musikose kuzungumuzia habari kama hizo katika Ibada ya Familia ya mangaribi. Munapofanya hivyo, mukumbuke kama kusudi ni la kumusaidia kila mushiriki wa familia ajue kama sheria na kanuni ambazo Mungu anatutolea zinaonyesha kama anatupenda sana. (Zab. 119:72) Kwa kweli, kujifunza namna hiyo kunaweza kusaidia washiriki wa familia yetu wawe marafiki kabisa wa Yehova na kunaweza kuunganisha familia yote.

15. Unaweza kujua namna gani kama unaanza kuwa na moyo wenye hekima na mutiifu?

15 Unaweza kujua namna gani kama unaanza kuwa na moyo wenye hekima na mutiifu? Njia moja inayoweza kukusaidia ni kuona ikiwa mawazo yako yanalingana na yale ya watumishi waaminifu walioishi zamani, kama vile Daudi aliyeandika hivi: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.” (Zab. 40:8) Vivyo hivyo, muandikaji wa Zaburi 119 aliandika hivi: ‘Jinsi ninavyoipenda sheria yako! Ndiyo ninayoihangaikia muchana kutwa.’ (Zab. 119:97) Upendo kama huo hautokee kwa muujiza. Ni lazima mutu ajifunze kwa bidii, awe na zoezi ya kusali, kutafakari, na kufungua macho ili aone namna Yehova anavyomubariki sana katika maisha kwa sababu amezitii sheria zake.​—Zab. 34:8.

PIGANIA UHURU WAKO WA KIKRISTO

16. Tunapaswa kukumbuka nini ikiwa tunataka kushinda vita tunayofanya ya kupigania uhuru wa kweli?

16 Katika historia, mataifa yamefanya vita sana ili kupata uhuru. Ikiwa wao wamefanya hivyo, je, sisi pia haingetufaa tufanye vita ya kiroho ili tuendelee kulinda uhuru wetu wa Kikristo? Ni lazima tukumbuke kama hatupigane tu na Shetani, ulimwengu, na roho yenye sumu ya ulimwengu, lakini tunapigana pia na hali yetu ya kutokamilika, bila kusahau mielekeo ya moyo wetu mudanganyifu. (Yer. 17:9; Efe. 2:3) Hata hivyo, kwa musaada wa Yehova tunaweza kushinda vita hiyo. Zaidi ya hayo, ushindi wowote tutakaopata, mukubwa ao mudogo, utatimiza mambo mazuri mawili. Jambo la kwanza, tutafurahisha moyo wa Yehova. (Met. 27:11) Jambo la pili, kadiri unavyoendelea kufurahia uhuru unaotokana na nguvu ya “sheria kamilifu iliyo ya uhuru,” jambo hilo litakufanya uazimie kubaki katika ‘barabara nyembamba’ inayoongoza kwenye uzima wa milele. Katika siku zinazokuja, utafurahia uhuru mwingi zaidi ambao Yehova anawatayarishia waaminifu wake.​—Yak. 1:25; Mt. 7:13, 14.

17. Kwa nini hatupaswe kuvunjika moyo kupita kiasi juu ya makosa yetu, na Yehova anatusaidia namna gani?

17 Sisi sote tunakosea mara nyingi. (Mhu. 7:20) Unapokosea, usijione wa bure ao kuvunjika moyo kupita kiasi. Ikiwa unajikwaa, simama na endelea mbele, hata kama ni lazima kuomba musaada wa wazee wa kutaniko lako. Yakobo aliandika kama ‘sala [yao] ya imani, itamuponya huyo asiyejisikia vizuri, na Yehova atamuinua. Pia, ikiwa amefanya zambi atasamehewa.’ (Yak. 5:15) Ndiyo, usisahau hata kidogo kama Mungu ni mwenye rehema kweli kweli na alikuvuta katika kutaniko kwa sababu aliona katika moyo wako mambo fulani mazuri. (Soma Zaburi 103:8, 9.) Yehova hatakuacha hata kidogo kwa muda wote ambao utajikaza kumutumikia kwa moyo wako wote.​—1 Nya. 28:9.

18. Namna gani tunaweza kuishi kulingana na sala ya Yesu iliyo kwenye Yohana 17:15?

18 Usiku mbele ya kufa, Yesu alisali pamoja na mitume wake waaminifu 11, na katika sala hiyo alimuomba Yehova awalinde. Alisema maneno haya yasiyoweza kusahaulika juu yao: ‘Uwalinde kwa sababu ya yule muovu.’ (Yoh. 17:15) Yesu hakuwahangaikia tu mitume wake, lakini anawahangaikia pia wote wanaomufuata leo. Kwa hiyo, tunaweza kuamini kabisa kama Yehova atajibu sala ya Yesu kwa kuendelea kutulinda katika siku hizi zenye hatari. Kwa kuwa ‘yeye ni ngao kwa wale wanaotembea kwa utimilifu, atailinda njia ya washikamanifu wake.’ (Met. 2:7, 8) Kwa kweli, si rahisi kubaki mushikamanifu, lakini kufanya hivyo ndiyo njia moja tu inayoweza kukuongoza kwenye uzima wa milele na uhuru wa kweli. (Rom. 8:21) Usiache mutu yeyote akudanganye na kukupoteza!

[Maelezo ya chini]

^ Mungu alimuahidi Daudi kama “uzao” wake ungeriti kiti chake cha ufalme. Alitoa ahadi hiyo kisha Absalomu kuzaliwa. Kwa hiyo, Absalomu alipaswa kujua kama Yehova hakumuchagua ili awe mufalme mahali pa baba yake Daudi.​—2 Sam. 3:3; 7:12.

^ Maandiko mengine ambayo munaweza kuzungumuzia katika familia ni 1 Wakorintho 13:4-8, katika andiko hilo mutume Paulo anaonyesha maana ya upendo. Pia Zaburi 19:7-11, inazungumuzia baraka nyingi zinazotokana na kutii sheria za Yehova.

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 14]

Ni nani walio kama Absalomu leo na tunaweza namna gani kujilinda ili tusidanganywe nao?