Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yehova Alinifundisha Kufanya Mapenzi Yake

Yehova Alinifundisha Kufanya Mapenzi Yake

Masimulizi Kuhusu Maisha ya Watu

Yehova Alinifundisha Kufanya Mapenzi Yake

Max Lloyd anaeleza maisha yake

Ilikuwa usiku sana katika mwaka wa 1955. Mimi na misionere mwengine tulikuwa katika eneo letu huko Paraguay, Amerique du sud, wakati nyumba tulimokuwa ilizunguukwa na watu wenye jeuri waliokuwa wakilalamika hivi: “Mungu wetu anasikia kiu ya kunywa damu, na anapenda damu ya wageni.” Basi, namna gani sisi wageni tulifika katika inchi hiyo?

MAMBO yalianzia Australie, kumepita miaka mingi, mahali ambapo nilikomalia na ambapo Yehova alianza kunifundisha kufanya mapenzi yake. Katika mwaka wa 1938, dada mumoja alimutolea baba yangu kitabu Ennemis. Tayari baba na mama hawakuwa wanapendezwa tena na viongozi wao wa dini, kwa sababu walikuwa wakisema kama sehemu fulani za Biblia ni hadisi za kutunga tu. Kisha mwaka mumoja hivi, wazazi wangu walibatizwa ili kuonyesha kama walijitoa kwa Yehova. Kuanzia wakati huo, jambo la maana sana katika familia yetu lilikuwa ni kufanya mapenzi ya Yehova. Kisha, dada yangu, Lesley, aliyenipita miaka mitano, alibatizwa, mimi pia nikabatizwa mwaka wa 1940 nilipokuwa na umri wa miaka kenda.

Kisha tu Vita ya Pili ya Ulimwengu kuanza, serikali ya Australie ilikataza Mashahidi wa Yehova kuchapa na kutolea watu vitabu vyao. Kwa hiyo, nilipokuwa ningali kijana mudogo, nilijifunza kuelezea wengine mambo niliyoamini kwa kutumia Biblia tu. Kila siku nilikuwa na Biblia yangu nilipoenda kwenye masomo, ili niweze kufasiria wenzangu sababu gani ninakataa kuisalimu bendera ao kuunga mukono vita.​—Kut. 20:4, 5; Mt. 4:10; Yoh. 17:16; 1 Yoh. 5:21.

Wanafunzi wengi hawakupenda kurafikiana nami kwa sababu waliniita “mupelelezi wa Allemagne.” Katika siku hizo, filme zilikuwa zikionyeshwa kwenye masomo. Mbele filme ianze, kila mutu alipaswa kusimama na kuimba wimbo wa taifa. Nilipobaki mwenye kukaa, wanafunzi wawili ao watatu walijaribu kunisimamisha kwa nguvu wakinikokota nywele. Mwishowe nilifukuzwa kwenye masomo kwa sababu ya kushikamana na mambo niliyoamini kutoka katika Biblia. Hata hivyo, niliendelea kusoma kwa njia ya barua nikiwa nyumbani.

MWISHOWE NINAFIKIA MURADI WANGU

Nilikuwa na muradi wa kuanza utumishi wa painia wakati ningekuwa na miaka 14. Lakini, nilivunjika moyo wakati wazazi wangu waliniambia kama nilipaswa kwanza kutafuta kazi ya kimwili. Walikazia kama ni lazima nilijipie chumba na kubaki nyumbani, lakini waliahidi kama wataniruhusu kuanza kazi ya upainia nitakapokuwa na miaka 18. Hilo lilifanya tuendelee kubishana nao kwa ukawaida juu ya feza nilizokuwa nikipata. Niliwaonyesha kama nilipenda kuchunga feza hizo ili zinisaidie nitakapokuwa painia, lakini walikuwa wakizichukua.

Wakati wa kuanza kazi ya upainia ulipofika, wazazi wangu waliniikalisha na kuniambia kama walikuwa wananiwekea katika banke pesa nilizokuwa nikiwapa. Kisha walinirudishia pesa hizo zote ili ninunue manguo na mambo mengine niliyohitaji ili nifanye kazi ya upainia. Hivyo, walikuwa wakinifundisha ili nijue namna ya kujitimizia mahitaji yangu kuliko kungojea wengine wanifanyie hivyo. Ninapokumbuka hilo, ninatambua kama mazoezi hayo yalikuwa ya lazima.

Mimi na Lesley tulipokuwa tukikomaa, mapainia walikuja kila mara kubaki kwetu, na tulifurahia kuhubiri pamoja nao. Kila Siku ya Posho na Siku ya Yenga, tulihubiri nyumba kwa nyumba, katika barabara, na tuliongoza mafunzo ya Biblia. Wakati huo kila muhubiri aliombwa kuhubiri saa 60 kwa mwezi. Mama alijikaza siku zote ili kueneza saa hizo, na kwa kufanya hivyo alituwekea, mimi na Lesley, mufano muzuri.

KUFANYA KAZI YA UPAINIA KATIKA TASMANIE

Mugao wangu wa kwanza ulikuwa kisiwa cha Tasmanie huko Australie, ambako dada yangu na bwana yake walikuwa wakihubiri. Lakini, kisha muda fulani walialikwa ili kuhuzuria darasa la 15 la Masomo ya Gileadi. Nilikuwa mwenye haya na ilikuwa mara yangu ya kwanza kuishi mbali na nyumbani. Watu fulani waliwazia kama nitafanya miezi mitatu tu huko Tasmanie na kurudi nyumbani. Hata hivyo, kisha mwaka mumoja, katika 1950, niliwekwa kuwa mutumishi wa kutaniko (leo anaitwa muratibu wa baraza la wazee). Kisha, nikakubaliwa kuwa painia wa pekee, na nilitumika pamoja na ndugu mwengine kijana.

Tulipewa mugao katika muji wa mbali ambako watu walikuwa wakichimba shaba (cuivre), na ni sisi tu tuliokuwa Mashahidi katika muji huo. Tulisafiri kwa bus na tukafika katika muji huo mangaribi. Usiku wa kwanza, tulilala katika hoteli moja ya zamani. Tulipokuwa tukihubiri nyumba kwa nyumba siku iliyofuata, tuliwauliza watu ikiwa kunaweza kupatikana chumba cha kupangia. Karibu na saa za mangaribi, mutu mumoja alituambia kama nyumba ya kiongozi fulani wa dini iliyopatikana karibu na Kanisa la Presbiteri haikuwa na mutu na alituambia tuende kuzungumuza na kiongozi wa dini juu ya jambo hilo. Kiongozi huyo alikuwa mutu muzuri na akatupangisha katika nyumba hiyo. Kila siku tulitoka katika nyumba ya kiongozi wa dini na kuenda katika kazi ya kuhubiri; hilo lilishangaza sana.

Katika eneo hilo watu wengi walipendezwa. Tulikuwa na mazungumuzo mazuri pamoja na watu na tuliongoza mafunzo mengi ya Biblia. Viongozi wa dini walioishi katika muji mukubwa wa inchi hiyo walipoambiwa kama Mashahidi wa Yehova walikuwa wakiishi katika makao ya kiongozi wa dini, walimuambia atuondoe mara moja katika nyumba hiyo. Kwa mara nyingine tena hatukuwa na mahali pa kulala.

Siku iliyofuata tulihubiri mupaka saa za kisha midi, kisha tukaanza kutafuta mahali ambapo tungelala. Tulikosa makao, tukaenda katika tribine ya uwanja wa kabumbu. Tulificha valize zetu katika tribine hiyo na kuendelea na kazi ya kuhubiri. Usiku ulianza kuingia, lakini tuliamua kuhubiri nyumba chache zilizobaki ili kumaliza barabara hiyo. Kwenye nyumba moja, mwanaume fulani alitutolea nyumba ndogo yenye vyumba viwili iliyopatikana nyuma ya nyumba yake.

MUZUNGUKO NA GILEADI

Kisha kuhubiri miezi karibu munane katika mugao huo, biro ya tawi ya Australie iliniomba niwe mwangalizi wa muzunguko. Jambo hilo lilinishangaza sana kwa sababu nilikuwa na miaka 20 tu. Baada ya kupata mazoezi kwa majuma mawili, nilianza kuyatembelea makutaniko kwa ukawaida ili kuyatia moyo. Watu wengi waliokuwa wakubwa hawakuzarau ujana wangu lakini waliniheshimu kwa sababu ya kazi ambayo nilikuwa nikifanya.

Kuyatembelea makutaniko kulinifanya nizoee hali mbali mbali. Juma moja nilisafiri kwa bus, juma lingine kwa gari-moshi, kisha motokari ao moto, nikibeba valize yangu ya manguo na sakoshe ya mahubiri. Kupitisha wakati pamoja na Mashahidi wenzangu kuliniletea furaha nyingi. Mutumishi mumoja wa kutaniko alifurahia kunikaribisha kwake hata ikiwa sehemu moja tu ya nyumba yake ndiyo iliyokuwa imekwisha jengwa. Juma hilo kitanda changu kiliwekwa katika nafasi ya kuogea, lakini sote tulifurahia kupitisha juma hilo pamoja.

Jambo lingine la kushangaza lilitokea katika mwaka wa 1953 nilipopokea fomu kwa ajili ya darasa la 22 la Masomo ya Gileadi. Nilifurahi lakini nilikuwa pia mwenye wasiwasi. Kwa sababu nilikumbuka namna dada yangu na bwana yake walitumwa katika inchi ya Pakistan kisha kupata diplome ya Masomo ya Gileadi tarehe 30, mwezi wa 7, 1950. Haikufanya mwaka mumoja, Lesley akagonjwa na akafa huko. Nilikuwa ninajiuliza namna wazazi wangu watajisikia ikiwa ningetumwa katika inchi nyingine baada tu ya mambo hayo kutokea? Hata hivyo, waliniambia hivi: “Uende kumutumikia Yehova mahali popote ambapo anakutuma.” Sikuwahi tena kumuona baba yangu. Baba yangu alikufa katika mwaka wa 1957.

Muda mufupi tu baadaye, tulisafiri kwa mashua kwa kipindi cha majuma sita pamoja na mashahidi wengine watano kutoka Australie mupaka muji wa New York. Tulipokuwa njiani, tulisoma na kujifunza Biblia pamoja, na tuliwahubiria wale tuliosafiri nao. Mbele ya kuenda mahali ambapo masomo yalifanywa huko South Lansing, New York, tulihuzuria mukusanyiko wa kimataifa uliofanywa mwezi wa 7, 1953 katika uwanja wa Yankee Stadium. Hesabu kubwa sana ya watu 165 829 walihuzuria mukusanyiko huo.

Wanafunzi 120 wa darasa letu walitoka kila sehemu ya dunia. Kisha kupata diplome ya Gileadi, ndipo kila mutu alijua mahali ambako ametumwa. Mara moja tulienda haraka katika maktaba ya masomo ili kujua inchi tulikotumwa. Nilitumwa katika Paraguay, inchi ambamo muvurugo kuhusu mambo ya politike ilikuwa jambo la kawaida. Muda mufupi tu kisha kufika huko, niliuliza wamisionere wengine juu ya fujo kama ya sherehe fulani ambayo nilisikia usiku. Walicheka kidogo na kuniambia: “Hayo ni mabadiliko ya kwanza ya politike ambayo umejionea. Tazama inje.” Askari walikuwa kila mahali!

TUMEPONEA CHUPUCHUPU

Siku moja, nilimusindikiza mwangalizi wa muzunguko alipoenda kutembelea kutaniko la mbali na kuonyesha watu filme La Société du Monde Nouveau en action. Tulisafiri kwa muda wa saa munane ao kenda kwa kutumia gari-moshi, motokari ya kukokotwa na farasi, na motokari ya kukokotwa na ngombe. Tulibeba groupe électrogène kubwa na tala kubwa inayotumiwa ili kuonyesha filme. Kisha kufika mahali tulipoenda, siku iliyofuata tulihubiri watu waliopatikana katika mashamba na kuwaalika waje kutazama filme wakati wa usiku. Watu karibu 15 walikuja.

Kisha kuonyesha watu filme kwa dakika karibu 20, tuliambiwa kama tunapaswa kujificha haraka katika nyumba. Tulichukua tala hiyo kubwa na tukajificha. Ni wakati huo ndio wanaume fulani walianza kuleta fujo, kupiga bunduki, na kuimba: “Mungu wetu anasikia kiu ya kunywa damu, na anapenda damu ya wageni.” Kulikuwa wageni wawili tu, mimi na mwangalizi wa muzunguko! Wale waliokuja kutazama filme waliwazuia wanaume hao wasivunje nyumba. Lakini, karibu saa kenda ya usiku, wapinzani hao walirudi mahali hapo wakipiga bunduki zao na kusema kama watatushambulia wakati tutarudi katika muji.

Ndugu walimujulisha mukubwa wa muji jambo hilo, na akaja pamoja na farasi wawili ili kuturudisha katika muji. Kila mara tulipofika mahali palipo na miti mingi, mukubwa huyo alichukua bunduki yake na kututangulia ili kuona ikiwa kuna adui wanaotuvizia. Nilitambua kama farasi ilikuwa njia nzuri ya kusafiri, kwa hiyo nilinunua moja.

WAMISIONERE WENGINE WANAKUJA

Ijapokuwa upinzani wa viongozi wa kidini, tuliendelea kupata matokeo mazuri katika kazi ya kuhubiri. Katika 1955, wamisionere watano walikuja kutusaidia. Mumoja wao alikuwa Elsie Swanson, dada kutoka inchi ya Canada aliyekuwa mumoja wa wanafunzi wa darasa la 25 la Gileadi. Tulikuwa naye kwa muda mufupi kwenye Beteli mbele atumwe katika muji mwengine. Aliamua kumutumikia Yehova maisha yake yote hata ikiwa hakutegemezwa kabisa na wazazi wake ambao hawakuikubali kweli. Tarehe 31 mwezi wa 12, 1957, nilimuoa Elsie, na tuliishi peke yetu katika nyumba ya wamisionere iliyopatikana sehemu ya kusini ya Paraguay.

Hatukuwa na maji katika nyumba yetu, kwa hiyo tulitumia maji ya kisima kilichopatikana katika uwanja nyuma ya nyumba yetu. Tena, hatukuwa na choo ao mahali pa kunawia katika nyumba, hatukuwa na mashini ya kufua manguo, hatukuwa hata na frigo. Tulinunua chakula kila siku kwa sababu hatukuwa na frigo ya kulinda chakula. Lakini, maisha hayo rahisi na uhusiano wenye upendo pamoja na ndugu na dada katika kutaniko vilifanya tuwe wenye furaha katika ndoa yetu wakati huo.

Katika 1963, muda mufupi kisha kufika Australie ili kumuona mama yangu, alipatwa na mushituko wa moyo, labda kwa sababu ya kufurahia sana kuniona kisha miaka kumi. Tulipokaribia kurudi katika mugao wetu huko Paraguay, tulipaswa kuchukua uamuzi fulani muzito katika maisha yetu. Je, ingefaa kumuacha mama katika hospitali, na kurudi katika mugao wetu tuliopenda huko Paraguay, tukitazamia mutu mwengine amutunze? Kisha kusali, mimi na Elsie tuliamua kubaki na kumutunza mama. Tuliendelea kumutunza na kufanya utumishi wetu wa wakati wote mupaka kifo chake katika mwaka wa 1966.

Katika Australie nilifurahia kwa miaka mingi pendeleo la kuwa mwangalizi wa muzunguko na wa wilaya na kufundisha Masomo ya Huduma ya Ufalme kwa ajili ya wazee. Kisha badiliko lingine likatokea katika maisha yetu. Niliwekwa kuwa mushiriki wa Halmashauri ya Tawi la Australie. Baadaye, wakati ulipofika ili kujenga Beteli mupya, niliombwa kusimamia halmashauri ya ujenzi. Kwa musaada wa wafanyakazi wengi wenye hekima na wanaotumika kwa umoja, Beteli yenye kupendeza ilijengwa.

Siku zilizofuata, niliombwa kutumika katika Biro ya Utumishi inayosimamia kazi ya kuhubiri katika inchi. Nilipata pia pendeleo la kutembelea Beteli zingine kama mwangalizi wa eneo la dunia ili kuwasaidia Wanabeteli na kuwatia moyo. Imani yangu ilitiwa nguvu nilipokutana na ndugu na dada katika inchi nyingi waliopitisha miaka mingi katika vifungo na kambi za mateso kwa sababu ya uaminifu wao kwa Yehova.

MUGAO WETU WA SASA

Kisha kutoka katika safari ndefu ya kutembelea Wanabeteli katika 2001, nilipokea mualiko wa kuenda Brooklyn, New York, kutumika katika Halmashauri mupya ya Beteli ya Amerika. Baada ya kusali kuhusu mualiko huo, mimi na Elsie tulikubali kwa furaha mugao huo. Sasa kumepita miaka zaidi ya 11, na tungali hapa Brooklyn.

Ninafurahi sana kuwa na bibi anayefurahia kufanya jambo lolote ambalo Yehova anamuomba. Sasa mimi na Elsie tuna miaka zaidi ya 80 na afya yetu si mbaya. Tunangojea kwa hamu kufurahia milele mafundisho na baraka nyingi ambazo Yehova atatolea wale wanaoendelea kufanya mapenzi yake.

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 19]

Juma moja nilisafiri kwa bus, juma lingine kwa gari-moshi, kisha motokari ao moto, nikibeba valize yangu ya manguo na sakoshe ya mahubiri

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 21]

Tunangojea kwa hamu kufurahia milele mafundisho ya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kushoto: Katika muzunguko huko Australie Kuume: Mimi pamoja na wazazi wangu

[Picha katika ukurasa wa 20]

Siku tuliyofunga ndoa, tarehe 31 mwezi wa 12, 1957