Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Mukutano Ulioonyesha Umoja na Mipango Yenye Kufurahisha

Mukutano Ulioonyesha Umoja na Mipango Yenye Kufurahisha

Ripoti ya Mukutano wa Kila Mwaka

Mukutano Ulioonyesha Umoja na Mipango Yenye Kufurahisha

MIKUTANO ya kila mwaka ya Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania inafurahisha sana. Jambo hilo lilionekana wazi wakati wa mukutano wa 127, uliofanywa Siku ya Posho, tarehe  1 mwezi wa 10, 2011. Wageni walioalikwa kutoka sehemu mbalimbali za dunia walikusanyika katika Jumba la Mukusanyiko la Mashahidi wa Yehova katika Jersey City, New Jersey, Amerika.

Ndugu Gerrit Lösch, mushiriki wa Baraza Linaloongoza, aliwakaribisha wahuzuriaji hao wenye furaha. Aliwaambia wageni kutoka inchi 85 kwamba Mashahidi wa Yehova wanafurahia umoja wa pekee duniani pote. Umoja huo unatoa ushahidi muzuri na unamutukuza Yehova. Kwa kweli, umoja ndio uliokuwa habari kuu ya mukutano huu.

RIPOTI NZURI KUTOKA MEXIQUE

Sehemu ya kwanza ya mukutano huo ilizungumuzia umoja wa watu wa Yehova. Ndugu Baltasar Perla aliwauliza ndugu watatu kutoka Familia ya Beteli ya Mexique kuhusu mupango uliochukuliwa wa kufunga biro sita za tawi za Amerika ya Kati ili biro ya tawi ya Mexique isimamie utendaji katika inchi hizo. Ndugu na dada fulani wa tawi hizo wamehamia kwenye Beteli ya Mexique, hilo limefanya Beteli hiyo iwe na watu kutoka mataifa mbali mbali. Ndugu na dada hao waliotoka katika inchi mbalimbali wamefanya kuwe na ubadilishanaji wa kitia-moyo. Ni kama vile Yehova alichukua kitambaa kikubwa na kuvuta mipaka inayogawanya watu wa mataifa mbalimbali.

Tatizo ambalo iliomba sasa kushindana nalo ni lile la kuwasaidia wahubiri wa inchi hizo wasifikiri kama wamekuwa mbali na tengenezo la Yehova hata ikiwa biro za tawi hazifanye tena kazi katika inchi zao. Tatizo hilo limetatuliwa kwa sababu kila kutaniko, hata makutaniko yaliyo katika maeneo ya mbali, yanapashana habari moja kwa moja na biro ya tawi kupitia Internete.

HABARI KUTOKA JAPON

Ndugu James Linton, kutoka tawi ya Japon, alieleza namna ndugu zetu walivyoteswa na matetemeko ya udongo na tsunami vilivyotokea katika inchi hiyo katika mwezi wa 3, 2011. Mashahidi wengi walipoteza ndugu na rafiki zao na vitu vyao. Mashahidi wa inchi zingine walisaidia kujenga nyumba zaidi ya 3100 na waliwatolea mamia ya motokari. Ndugu wenye kujitolea walitumika pamoja na Halmashauri za Ujenzi na walitumika sana ili kutengeneza nyumba zilizoharibika za ndugu zao. Zaidi ya ndugu 1700 walijitoa ili kutumika kila mahali palipokuwa lazima. Kikundi cha ndugu wenye kujitolea waliotoka États-Unis walisaidia kutengeneza Jumba la Ufalme na ndugu 575 walifanya kazi hiyo.

Mahitaji ya kiroho ya wale waliopata musiba yalifikiriwa sana na walipewa vitia-moyo ili kuwafariji. Zaidi ya wazee 400 wamejitolea kutumikia katika makutaniko yanayohitaji wachungaji. Baraza Linaloongoza lilionyesha kama linahangaikia ndugu na dada zao wa Japon lilipowatuma waangalizi wawili wa eneo la dunia kutoka makao makuu ili kutia ndugu na dada moyo katika mahali palipopatwa na musiba. Maneno ya upendo ambayo Mashahidi wa Yehova walitumia ndugu zao kutoka duniani pote yalifariji sana.

USHINDI MBALIMBALI WA KISHERIA

Wahuzuriaji walimusikiliza kwa uangalifu sana ndugu Stephen Hardy, kutoka biro ya tawi ya Grande-Bretagne, alipozungumuzia ushindi mbalimbali wa kisheria wa hivi karibuni. Kwa mufano, serikali ya France ilikuwa ikiomba Mashahidi wa Yehova katika inchi hiyo walipe takse ao kodi ya dolare milioni 82. Jambo hilo lilitatuliwa wakati Mahakama ya Ulaya ya Haki za Wanadamu ilituunga mukono na kusema kama serikali ya France imevunja nukta ya 9 ya Makubaliano ya Ulaya, inayolinda uhuru wa kidini. Maneno ya uamuzi huo yanaonyesha kama kwa kweli serikali ya France haikuwa ikitafuta feza, lakini kulikuwa jambo lingine kwa sababu uamuzi huo unasema hivi: “Kukataa kutambua kisheria shirika la kidini, kutafuta kuvunja shirika hilo, kutumia maneno ya kutukana chama cha kidini, ni kuvunja haki yao inayotajwa katika nukta ya 9 ya Makubaliano ya Ulaya.”

Pia, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Wanadamu ilituunga mukono katika kesi inayohusu Arménie. Tangu 1965, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Wanadamu imesema kama Makubaliano ya Ulaya hayakuwalinda watu kutokana na kazi ya jeshi ya kulazimishwa. Baraza Kuu ya Mahakama ya Ulaya liliamua kwamba “kukataa kazi ya kijeshi kwa kuchochewa na sababu nzuri na zisizoweza kubadilishwa,” kunapaswa kukubaliwa na Makubaliano ya Ulaya. Uamuzi huo ulilazimisha Arménie na inchi kama vile Azerbaïdjan na Turquie kutambua haki hiyo.

MIPANGO YA UJENZI

Musemaji aliyefuata alikuwa Ndugu Guy Pierce, mushiriki wa Baraza Linaloongoza. Yeye alijua kama wahuzuriaji wote walikuwa na hamu ya kusikia kuhusu mipango ya ujenzi katika muji wa New York. Kwa hiyo, kupitia video alionyesha namna ujenzi unavyoendelea huko Wallkill, Patterson, na kwenye viwanja vilivyonunuliwa hivi karibuni vinavyopatikana katika miji ya Warwick na Tuxedo, New York. Ujenzi wa makao mapya huko Wallkill unaweza kumalizika katika mwaka wa 2014 na makao hayo yatakuwa na vyumba zaidi ya 300.

Kuna mipango ya kujenga makao mengine katika uwanja wa hektare 100 huko Warwick. Ndugu Pierce alisema hivi: “Ijapokuwa hatuyajua mapenzi ya Mungu kuhusu Warwick, tumeanza kutayarisha uwanja huo ili kuhamishia makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko.” Tuna mipango ya kutumia hektare 20 ya uwanja wetu unaopatikana kilometre 10 kusini mwa Warwick ili kuweka mashine na vifaa vya ujenzi. Aliongeza hivi: “Kisha kupata ruhusa ya kujenga, tunatumaini kumaliza ujenzi kwa kipindi cha miaka ine.” “Kisha makao yetu ya Brooklyn inaweza kuuzishwa.”

Ndugu Pierce aliuliza hivi: “Je, Baraza Linaloongoza limesahau kama ziki kubwa inakaribia sana?” “Sivyo kabisa,” akajibu. “Ikiwa ziki kubwa inakatiza mipango yetu, hilo litakuwa jambo nzuri, jambo nzuri kabisa!”

MUFANYE ANGALISHO NA SIMBA ANAYENGURUMA

Ndugu Stephen Lett, mushiriki wa Baraza Linaloongoza, alizungumuzia andiko la 1 Petro 5:8, linalosema hivi: ‘Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kumumeza mutu.’ Ndugu Lett alisema kama mufano ambao Petro alitumia kumulinganisha Shetani na simba unafaa kabisa.

Kwa kuwa simba zina nguvu na zinakimbia kwa uharaka kuliko watu, hatupaswe kupigana ao kumukimbia Shetani kwa nguvu zetu wenyewe. Tunahitaji musaada wa Yehova. (Isa. 40:31) Simba inajificha na kurarua munyama kimyakimya; kwa hiyo tunapaswa kuepuka giza la kiroho ambamo Shetani anatafutia munyama wa kunasa. Kama tu simba anavyoua wanyama wasio na hatari kama vile antilope ao kitoto cha zebre, Shetani pia hana huruma na angetaka kutuua. Mara nyingi, simba inaposhiba, nyama inayoacha inakuwa isiyotambuliwa tena, vilevile “hali ya mwisho” ya wale wanaonaswa kiroho na Shetani ‘inakuwa mbaya zaidi kuliko ile ya kwanza.’ (2 Pet. 2:20) Kwa hiyo, lazima tumupinge Shetani na kushikamana na kanuni za Biblia ambazo tumejifunza.​—1 Pet. 5:9.

FURAHIA NAFASI YAKO KATIKA NYUMBA YA YEHOVA

Kisha kukaja Ndugu Samuel Herd, mushiriki mwengine wa Baraza Linaoongoza. Yeye alisema kama “kila mumoja wetu ana nafasi yake katika nyumba ya Yehova.” Wakristo wote wana nafasi katika “nyumba” ya Mungu, ni kusema, katika hekalu lake la kiroho ao mupango unaotuwezesha kumuabudu Mungu kupitia zabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo. Tunapaswa kupendezwa na pendeleo hilo nzuri. Kama Daudi, tunatamani “kukaa katika nyumba ya Yehova siku zote za maisha [yetu].”​—Zab. 27:4.

Ndugu Herd alizungumuzia Zaburi 92:12-14 na kuuliza, “Namna gani Yehova anatusaidia kuwa na hali nzuri ya kiroho?” Akajibu hivi: “Katika paradiso ya kiroho, Mungu anatupatia joto, anatulinda, na kutupa maji ya kweli yanayoburudisha. Kwa hiyo, tunapaswa kumushukuru Yehova kwa mambo hayo.” Ndugu Herd aliwatia moyo wasikilizaji hivi: “Acheni tufurahie kubaki katika nyumba ya Yehova si kwa muda mufupi lakini milele.”

WAKRISTO WANAHESHIMU NENO LA MUNGU

Ndugu David Splane, yeye pia mushiriki wa Baraza Linaloongoza, alieleza katika hotuba iliyofuata kama siku zote Wakristo wameheshimu Neno la Mungu. Katika siku za mitume, Wakristo walitegemea Neno la Mungu ili kutatua tatizo la kutahiriwa. (Mdo. 15:16, 17) Lakini, Wakristo fulani walioishi katika kipindi kilichoanza mwaka wa 101, ambao walifundishwa filozofia ya Kigiriki, walianza kutanguliza ujuzi wao kuliko Maandiko. Baadaye, wengine walifanya maoni ya wale walioitwa eti Mababa wa Kanisa na watawala wa Roma yachukue nafasi ya Maandiko, hilo lilitokeza mafundisho mengi ya uongo.

Ndugu Splane alisema kama katika mufano mumoja, Yesu alionyesha kama sikuzote kungekuwa na Wakristo watiwa​-mafuta wa kweli ili kuitetea kweli. (Mt. 13:24-30) Hatuwezi kusema kwa uhakika kama Wakristo hao walikuwa nani. Hata hivyo, kwa miaka mingi, watu wengi wamefunua mafundisho na matendo yasiyopatana na Maandiko. Kati yao kulikuwa: Askofu mukuu Agobard wa Lyons katika miaka ya 800, Peter wa Bruys, Henry wa Lausanne na Valdès (ao Waldo) katika miaka ya 1100, John Wycliffe katika miaka ya 1300, William Tyndale katika miaka ya 1500, na Henry Grew na George Storrs katika miaka ya 1800. Leo, Mashahidi wa Yehova wanaendelea kushikamana na kanuni za Kimaandiko na wanaiona Biblia kuwa musingi wa mafundisho ya kweli. Kwa sababu hiyo, Baraza Linaoongoza limechagua andiko la mwaka wa 2012 kuwa Yohana 17:17: “Neno lako ni kweli.”

MABADILIKO YENYE KUFURAHISHA KUHUSU MASOMO NA UTUMISHI

Tangazo lililofanywa na Anthony Morris, mushiriki wa Baraza Linaloongoza, lilionyesha mabadiliko kuhusu utumishi wa wamisionere na mapainia wa pekee. Kuanzia mwezi wa 9, 2012, Masomo ya Biblia kwa Ajili ya Ndugu na Bibi Zao itaanza kufanywa katika inchi fulani zitakazochaguliwa. Kusudi la Masomo ya Gileadi limebadilika. Kuanzia mwezi wa 10, 2011, Masomo ya Gileadi ilianza kuzoeza watu ambao wamekuwa katika aina fulani ya pekee ya utumishi wa wakati wote kama vile wamisionere ambao hawajafanya masomo ya Gileadi, mapainia wa pekee, waangalizi wanaosafiri, ao Wanabeteli. Wale watakaofundishwa kwenye masomo hayo watasaidia kutia nguvu watu wa Mungu katika biro za tawi, katika kazi ya kusafiri, ao katika maeneo yaliyo na watu wengi ambako wanaweza kuyatia moyo makutaniko katika kazi ya kuhubiri.

Mapainia wa pekee wengine watatumwa ili kuhubiria maeneo ya mbali na maeneo ambayo hayajafikiwa. Kuanzia mwezi wa 1, 2012, ndugu fulani waliosoma Masomo ya Biblia kwa Ajili ya Ndugu Wasiooa na Masomo ya Biblia kwa Ajili ya Ndugu na Bibi Zao walitumwa kama mapainia wa pekee wa muda ili kuhubiri maeneo mapya na kupanua kazi ya kuhubiri katika maeneo ya mbali. Watatumika kama mapainia wa pekee kwa mwaka mumoja mupaka miaka mitatu. Wale watakaotumika vizuri watapata migawo ya kudumu.

Mukutano huu ulikuwa kipindi cha furaha. Tunatumaini kama Yehova atabariki mipango hiyo mipya ya kuongeza utendaji wetu katika kazi ya kuhubiri na kuendeleza umoja wetu duniani pote ili kumuletea utukufu na sifa.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa was 18, 19]

WALITAKA KUWAJUA VIZURI

Programu ilitia ndani kipindi cha kuuliza watu maulizo. Dada watano wajane, ambao bwana zao walikuwa washiriki wa Baraza Linaloongoza waliulizwa maulizo. Dada Marina Sydlik, Edith Suiter, Melita Jaracz, Melba Barry, na Sydney Barber walieleza namna walivyojifunza kweli na namna walivyoingia katika utumishi wa wakati wote. Kila mumoja wao alieleza mambo mazuri, mawazo ambayo anakumbuka kuhusu bwana yake na baraka walizofurahia pamoja. Kisha kipindi hicho cha kumalizia chenye kutia moyo, wahuzuriaji waliimba wimbo namba 86, wenye kichwa “Wanawake Waaminifu, Dada Wakristo.”

[Picha]

(Juu) Daniel na Marina Sydlik; Grant na Edith Suiter; Theodore na Melita Jaracz

(Chini) Lloyd na Melba Barry; Carey na Sydney Barber

[Karte kwenye ukurasa wa 16]

(Ili kuona maelezo hayo, ona kitabu)

Biro sita za tawi zilizofungwa ili biro ya tawi ya Mexique isimamie utendaji katika inchi hizo

MEXIQUE

GUATEMALA

HONDURAS

SALVADOR

NICARAGUA

COSTA RICA

PANAMA

[Picha katika ukurasa wa 17]

Namna makao makubwa ya Mashahidi wa Yehova yatakavyojengwa katika muji wa Warwick, New York