Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Acheni Ndiyo Yenu Imaanishe Ndiyo

Acheni Ndiyo Yenu Imaanishe Ndiyo

Acheni Ndiyo Yenu Imaanishe Ndiyo

“Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo.”​—MT. 5:37.

UNAWEZA KUJIBU?

Yesu alitoa amri gani kuhusu viapo?

Namna gani Yesu alituwekea mufano muzuri kwa kuacha Ndiyo yake imaanishe Ndiyo?

Ni katika mambo gani tunapaswa kuacha Ndiyo yetu imaanishe Ndiyo?

1. Yesu alitoa amri gani kuhusu viapo, na sababu gani?

 KWA kawaida, si lazima Wakristo wafanye viapo, kwa kuwa wanatii amri hii ya Yesu inayosema: “Acheni Ndiyo yenu imaanishe Ndiyo.” Yesu alimaanisha kama mutu anapaswa kutimiza maneno yake. Mbele ya kutoa amri hiyo, Yesu alisema hivi: ‘Musiape hata kidogo.’ Alisema hivi ili kulaumu tabia ya watu wengi ya kuapa mara kwa mara katika mazungumuzo yao bila kuwa na nia ya kutimiza mambo wanayosema. Wale wanaoapa kuliko tu kusema Ndiyo ao hapana, wanaweza kuonyesha hivyo kama wao ni watu walio na tabia ya kusema uongo na kama wao ni watu wanaoongozwa na ‘yule muovu.’​—Soma Mathayo 5:33-37.

2. Je, ni vibaya kuapa katika kila hali? Eleza.

2 Je, maneno ya Yesu yanamaanisha kama ni vibaya kabisa kuapa? Hapana. Kama tulivyojifunza katika habari iliyotangulia, Yehova Mungu na mutumishi wake Abrahamu walitoa viapo kuhusu mambo fulani ya lazima sana. Pia, Sheria ya Mungu iliomba watu wafanye viapo ili kumaliza matatizo fulani. (Kut. 22:10, 11; Hes. 5:21, 22) Kwa hiyo, Mukristo anaweza kuapa kwenye tribinali ili kuonyesha kama mambo atakayosema ni kweli. Ao, katika hali fulani za pekee Mukristo anaweza kuapa ili kuwahakikishia wengine nia yake ao ili kuwasaidia wengine kutatua matatizo fulani. Kwa mufano, kuhani mukubwa alipomuomba afanye kiapo, Yesu hakukataa, lakini alisema kweli mbele ya Sanhedrini ya Wayahudi. (Mt. 26:63, 64) Hata hivyo, haikuwa lazima Yesu afanye kiapo kila wakati alikuwa akisema. Lakini, ili kukazia ukweli wa ujumbe wake, mara nyingi Yesu alitanguliza maneno yake na usemi huu wa pekee: “Kwa kweli kabisa [ao kweli, kweli] ninawaambia ninyi.” (Yoh. 1:51, 13:16, 20, 21, 38) Acheni tuzungumuzie mambo mengine tunayoweza kujifunza kutokana na mifano ya Yesu, Paulo, na wengine walioacha Ndiyo yao imaanishe Ndiyo.

YESU ALIACHA NDIYO YAKE IMAANISHE NDIYO

3. Yesu alimuahidi Mungu nini katika sala, na namna gani Baba yake alionyesha kama alikubali sala yake?

3 “Tazama! Nimekuja . . . ili kufanya mapenzi yako, Ee Mungu.” (Ebr. 10:7) Maneno hayo yanaonyesha kama Yesu alikubali mbele ya Mungu kutimiza mambo yote yaliyotabiriwa kuhusu Uzao ulioahidiwa, pia alikubali ‘kutiwa jeraha kwenye kisigino’ na Shetani (Mwa. 3:15) Hakuna mwanadamu ambaye alikuwa amekwisha kujitoa hivyo ili kuchukua daraka hilo nzito. Sauti ya Yehova ilisikika kutoka mbinguni, alionyesha kama anamutumainia kabisa Mwana wake. Lakini hakumuomba Yesu atoe kiapo ili kuonyesha kama atatimiza maneno yake.​—Lu. 3:21, 22.

4. Namna gani Yesu aliacha Ndiyo yake imaanishe Ndiyo?

4 Sikuzote Yesu alikuwa anatenda kulingana na yale alikuwa anafundisha, ni kusema, aliacha Ndiyo yake imaanishe Ndiyo. Yeye hakuruhusu jambo lolote limukengeushe, aliendelea kutimiza kazi ambayo Baba yake alimupatia ya kuhubri habari njema ya Ufalme wa Mungu na kufanya wanafunzi. (Yoh. 6:44) Biblia inahakikisha kama Yesu alitimiza ahadi aliyomutolea Mungu ya kufanya mapenzi yake, inaposema hivi: “Hata ahadi za Mungu ziwe nyingi kadiri gani, zimekuwa Ndiyo kwa njia yake.” (2 Kor. 1:20) Bila shaka, Yesu alituachia mufano muzuri sana, alitimiza kabisa yale aliyomuahidia Baba yake. Acheni tuzungumuzie sasa mutu aliyejikaza kumuiga Yesu.

PAULO ALIACHA NDIYO YAKE IMAANISHE NDIYO

5. Mutume Paulo alituwekea mufano gani?

5 “Nitafanya nini, Bwana?” (Mdo. 22:10) Paulo, aliyejulikana kwa jina la Saulo, alisema maneno hayo yenye kutoka moyoni, ili kuonyesha kwamba alikubali muongozo wa Bwana Yesu aliyetukuzwa, aliyemutokea katika maono ili kumuambia aache kuwatesa wanafunzi wake. Kisha tukio hilo, Paulo alitubu kwa unyenyekevu makosa yake ya zamani, alibatizwa, na alikubali kazi ya pekee aliyopewa ili kutolea watu wa mataifa ushahidi kumuhusu Yesu. Kuanzia wakati huo, Paulo aliendelea kumuita Yesu “Bwana,” na aliendelea kumuheshimu Bwana wake mupaka mwisho wa maisha yake. (Mdo. 22:6-16; 2 Kor. 4:5; 2 Tim. 4:8) Paulo alikuwa tofauti na watu wengine ambao Yesu alizungumuzia aliposema hivi: “Kwa nini, basi, munaniita ‘Bwana! Bwana!’ lakini hamufanye mambo ninayosema?” (Lu. 6:46) Kwa kweli, Yesu alitazamia wote wanaomukubali kuwa Bwana waache ndiyo yao imaanishe ndiyo kama mutume Paulo.

6, 7. (a) Sababu gani mutume Paulo alibadilisha programu yake ya kutembelea kutaniko la Korintho, na sababu gani wale waliomuchambua juu ya hilo hawakuwa na sababu ya kufanya hivyo? (b) Tunapaswa kuwaona namna gani wale wanaotuongoza?

6 Paulo alieneza ujumbe wa Ufalme, alianzisha na kutembelea makutaniko mengi katika Asia Ndogo na Ulaya. Wakati mumoja, Paulo aliona kuwa jambo la lazima kuapa kwamba mambo aliyoandika yalikuwa kweli. (Gal. 1:20) Watu fulani katika Korintho waliposema kama maneno ya Paulo hayaweze kutumainiwa, yeye alijitetea hivi: “Mungu anaweza kutegemewa ili neno letu kwenu lisiwe ni Ndiyo na pia Siyo.” (2 Kor. 1:18) Alipoandika maneno hayo, Paulo alikuwa ameacha muji wa Efeso, alikuwa Makedonia akijielekeza huko Korintho. Mwanzoni, alikuwa amepanga kutembelea kutaniko la Korintho mbele aende Makedonia. (2 Kor. 1:15, 16) Lakini, Paulo alibadilisha programu yake kama vile waangalizi wenye kusafiri leo wanavyoweza kubadilisha tarehe za kutembelea makutaniko. Waangalizi wenye kusafiri hawafanye mabadiliko hayo bila sababu, ao kwa kutafuta faida zao; lakini wanaweza kufanya hivyo kwa sababu ya mambo fulani yanayoomba kushugulikiwa haraka. Tunaweza kusema ikiwa mutume Paulo alibadilisha programu ya kutembelea kutaniko la Korintho ilikuwa ni kwa faida ya kutaniko hilo. Kwa nini tunasema hivyo?

7 Muda fulani tu kisha kupanga safari yake, mutume Paulo alipata habari yenye kuhuzunisha kwamba kulikuwa mugawanyiko katika kutaniko la Korintho na kwamba uasherati uliendelea kuachiliwa. (1 Kor. 1:11; 5:1) Ili kurekebisha hali hiyo, mutume Paulo alitoa mashauri fulani mazito katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho. Kisha, kuliko kuondoka Efeso na kuenda mara moja Korintho, Paulo aliamua kuwaachia ndugu zake wakati wa kutosha ili kutumia mashauri aliyowatolea hivi kwamba wakati angefika kuwatembelea, ziara yake ingekuwa yenye kujenga zaidi. Katika barua yake ya pili aliyowaandikia, aliwaonyesha kama hiyo ndio iliyokuwa sababu ya kweli iliyomufanya abadili programu yake. Aliwaandikia hivi: ‘Namuita Mungu awe shahidi juu ya nafsi yangu mwenyewe ya kuwa ni kwa kuwahurumia ninyi kwamba bado sijaja Korintho.’ (2 Kor. 1:23) Tusiwe kama wale waliomuchambua mutume Paulo; lakini acheni tuwaheshimu sana wale wanaotuongoza. Mutume Paulo aliacha Ndiyo yake imaanishe Ndiyo. Kwa hiyo tunapaswa kumuiga, kama vile yeye alivyomuiga Kristo.​—1 Kor. 11:1; Ebr. 13:7.

MIFANO MINGINE YA KUIGA

8. Rebeka alituachia mufano gani?

8 ‘Mimi niko tayari kuenda.’ (Mwa. 24:58) Rebeka aliwaambia mama yake na kaka yake maneno hayo kwa sababu alikuwa tayari kuacha familia yao siku hiyohiyo na kusafiri kilometre 800 pamoja na mutu ambaye hakumujua ili kuwa bibi ya Isaka. (Mwa. 24:50-58) Rebeka aliacha Ndiyo yake imaanishe Ndiyo. Na katika maisha yake alionyesha kama yeye ni mwanamuke mwaminifu aliyemuogopa Mungu; alikubali kukaa kama mugeni katika mahema katika Inchi ya Ahadi. Rebeka alipata pendeleo la kuwa mumoja wa kambo za Yesu Kristo, Uzao ulioahidiwa.​—Ebr. 11:9, 13.

9. Namna gani Ruthu aliacha Siyo yake imaanishe Siyo?

9 “Hapana, bali tutarudi pamoja nawe kwa watu wako.” (Rut. 1:10) Hayo ni maneno ambayo wajane wa Moabu, Ruthu na Orpa, walimuambia mama-mukwe wao mujane, Naomi, alipokuwa akirudi Bethlehemu. Mwishowe, Naomi aliwakaza warudi kwao, Orpa yeye akarudi. Lakini, Ruthu aliacha Siyo yake imaanishe Siyo. (Soma Ruthu 1:16, 17.) Alishikamana na Naomi, aliacha watu wa jamaa yake bila kuwa na tumaini la kuwaona tena na aliachana na dini ya uongo ya Moabu. Aliendelea kumuabudu Yehova kwa uaminifu na alipata pendeleo la kuwa mumoja wa wanawake watano tu ambao Mathayo anataja katika ukoo wa Kristo.​—Mt. 1:1, 3, 5, 6, 16.

10. Sababu gani Isaya ni mufano muzuri kwetu?

10 “Mimi hapa! Nitume mimi.” (Isa. 6:8) Mbele ya kusema maneno hayo, Isaya aliona maono ya utukufu wa Yehova akiwa ameketi juu ya kiti Chake cha ufalme juu ya hekalu la Israeli. Alipokuwa akitazama kwa mushangao utukufu huo, Isaya alimusikia Yehova akisema hivi: ‘Nitamutuma nani, na ni nani atakayeenda kwa ajili yetu?’ Kupitia maneno hayo Yehova alikuwa anatafuta mutu wa kuenda kuwatolea watu Wake wasiotii ujumbe wake. Isaya alikubali mualiko huo wa Yehova na aliacha Ndiyo yake imaanishe Ndiyo. Kwa miaka zaidi ya 46, alikuwa nabii aliyemutumikia Yehova kwa uaminifu; alitolea watu ujumbe wenye nguvu ili kuwaonyesha makosa yao na ujumbe muzuri wa kurudishwa kwa ibada ya kweli.

11. (a) Sababu gani ni jambo la maana kutimiza mambo tunayosema? (b) Mifano ya watu ambao hawakutimiza maneno yao inatutolea onyo gani?

11 Sababu gani Yehova aliandikisha mifano hiyo katika Neno lake? Na kwa nini kuacha Ndiyo yetu imaanishe Ndiyo ni jambo la kuchukua kwa uzito? Biblia inaonya waziwazi kama mutu asiyetimiza mapatano anastahili kifo. (Rom. 1:31, 32) Biblia inazungumuzia mifano mibaya ya watu kama vile Farao wa Misri, mufalme Zedekia wa Yuda, na Anania na Safira, ambao hawakuacha Ndiyo yao imaanishe Ndiyo. Wote walipatwa na matokeo mabaya na mifano yao ni onyo kwetu.​—Kut. 9:27, 28, 34, 35; Eze. 17:13-15, 19, 20; Mdo. 5:1-10.

12. Ni nini itatusaidia ili tuwe watu wanaotimiza yale wanayosema?

12 Tunaishi “katika siku za mwisho,” na tunazungukwa na watu “wasio washikamanifu,” watu ‘walio na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wanazikana nguvu zake.’ (2 Tim. 3:1-5) Tunapaswa kuepuka marafiki hao wabaya kadiri iwezekanavyo. Tunapaswa kukusanyika kwa ukawaida na wale wanaojikaza kuacha Ndiyo yao imaanishe Ndiyo.​—Ebr. 10:24, 25.

NDIYO YA MAANA SANA ULIYOSEMA

13. Mwanafunzi wa Yesu Kristo ana nafasi gani tatu za kusema Ndiyo ya maana sana?

13 Kujitoa kwa Mungu katika sala ndiyo ahadi ya maana sana ambayo mutu anaweza kutoa. Wale wanaotaka kujikana wenyewe ili kuwa wanafunzi wa Yesu wana nafasi tatu za pekee za kusema Ndiyo ili kuonyesha kama watatimiza ahadi waliyotoa. (Mt. 16:24) Nafasi ya kwanza: Wazee wawili wanapozungumuza na mutu anayetaka kuwa muhubiri asiyebatizwa, wanamuuliza hivi: “Je, kwa kweli unataka kuwa mumoja wa Mashahidi wa Yehova?” Nafasi ya pili: Mutu huyo akisha kufanya maendeleo ya kiroho na kuomba abatizwe, wazee watakutana naye na kumuuliza hivi: “Je, umekwisha kujiweka wakfu (kujitoa) kwa Yehova katika sala?” Na nafasi ya tatu: Siku ya ubatizo, kila mutu atakayebatizwa anaulizwa hivi: “Kwa musingi wa zabihu ya Yesu Kristo, umetubu zambi zako na kujiweka wakfu (kujitoa katika sala) kwa Yehova ili kufanya mapenzi yake?” Wanafunzi hao wapya wanapojibu Ndiyo mbele ya watazamaji wengi, wanaonyesha kama wataheshimu ahadi yao ya kumutumikia Mungu milele.

14. Kila mara tunapaswa kujichunguza na kujiuliza maulizo gani?

14 Hata kama umebatizwa karibuni ao umemutumikia Mungu kwa miaka mingi, kila mara unapaswa kujichunguza na kujiuliza maulizo kama haya: ‘Je, ninamuiga Yesu Kristo kwa kuendelea kuheshimu Ndiyo yangu ya maana sana? Je, ninaendelea kumutii Yesu kwa kutia kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi pa nafasi ya kwanza katika maisha yangu?’​—Soma 2 Wakorintho 13:5.

15. Ni katika mambo gani tunapaswa kuacha Ndiyo yetu imaanishe Ndiyo?

15 Ili kutimiza naziri yetu tuliyofanya tulipojitoa kwa Yehova katika sala, tunapaswa pia kuwa waaminifu katika mambo mengine ya lazima. Kwa mufano: Je, wewe ni mwenye kuoa ao kuolewa? Basi endelea kuheshimu naziri ya pekee uliyofanya ya kumupenda sana bwana ao bibi yako. Je, mumeandikiana mapatano ya biashara ao umejaza fomu kwa ajili ya mapendeleo fulani ya kiteokrasi? Ikiwa ndiyo, basi usikose kutimiza mapatano hayo na kuheshimu ahadi uliyotoa. Labda ndugu fulani asiye na uwezo mwingi alikualika kwenye chakula na ulikubali. Basi unapaswa kuheshimu ahadi yako hata ikiwa ndugu mwengine mwenye maisha mazuri zaidi anakualika siku hiyohiyo. Je, umeahidi kumurudilia mutu fulani uliyekutana naye katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba ili kumutolea musaada zaidi? Basi ikiwa ni hivyo, acha Ndiyo yako imaanishe Ndiyo, na Yehova atabariki utumishi wako.​—Soma Luka 16:10.

KUHANI WETU MUKUBWA NA MUFALME ANAWEZA KUTUSAIDIA

16. Ikiwa hatukutimiza ahadi yetu, tunapaswa kufanya nini?

16 Biblia inaonyesha kama, kwa sababu sisi ni watu wasio wakamilifu, ‘tunajikwaa mara nyingi,’ zaidi sana katika kusema. (Yak. 3:2) Tunapaswa kufanya nini basi ikiwa tunatambua kama hatukutimiza ahadi yetu? Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ilionyesha jambo la kufanya ikiwa mutu ‘alisema kwa midomo yake bila kufikiri.’ (Law. 5:4-7, 11) Leo pia kuna mupango unaoweza kusaidia ikiwa Mukristo ameangukia katika zambi kama hiyo. Tukitubu zambi hiyo, Kuhani wetu Mukubwa, Yesu Kristo, atatusaidia kupata musamaha wa Yehova. (1 Yoh. 2:1, 2) Lakini, ili Mungu aendelee kutukubali, tunapaswa kuwa na matendo yanayoonyesha kama tumetubu kabisa kwa kutorudilia-rudilia zambi hiyo. Tunapaswa kufanya yote tuwezayo ili kutengeneza hali hiyo iliyomuumiza mwengine kwa sababu ya kuahidi kwetu bila kufikiri. (Met. 6:2, 3) Kwa kweli, ni jambo la maana sana kufikiri kwa uzito mbele ya kutoa ahadi ambazo hatutaweza kutimiza.​—Soma Mhubiri 5:2.

17, 18. Wale wanaojikaza kuacha Ndiyo yao imaanishe Ndiyo watapata baraka gani wakati ujao?

17 Bila shaka waabudu wa Yehova wanaoendelea kujikaza ili kuacha Ndiyo yao imaanishe Ndiyo watapata baraka nyingi wakati ujao! Wakristo watiwa-mafuta 144 000 watakuwa na uzima usioweza kufa huko mbinguni ambako watatawala pamoja na Yesu katika Ufalme wake “nao watatawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.” (Ufu. 20:6) Mamilioni ya watu wengine wataishi katika paradiso duniani itakayotawaliwa na Ufalme wa Kristo. Yesu atawasaidia watu wawe wakamilifu kimwili na kiakili.​—Ufu. 21:3-5.

18 Ikiwa tunabaki waaminifu mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu, hatutashakia tena maneno ya mutu yeyote. (Ufu. 20:7-10) Wakati huo, kila mutu atakayesema Ndiyo itamaanisha Ndiyo, na kila mutu atakayesema Siyo itamaanisha Siyo. Itakuwa hivyo kwa sababu kila mutu atamuiga kwa ukamilifu Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, Yehova, aliye “Mungu wa ukweli.”​—Zab. 31:5.

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kuanzia ubatizo wake mupaka kifo chake, Yesu alitimiza yale aliyomuahidia Baba yake

[Picha katika ukurasa wa 30]

Je, unaacha Ndiyo yako ya maana sana imaanishe Ndiyo?