Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Maneno Yenye Kutia Moyo “Kutoka Katika Kinywa cha Watoto”

Maneno Yenye Kutia Moyo “Kutoka Katika Kinywa cha Watoto”

Maneno Yenye Kutia Moyo “Kutoka Katika Kinywa cha Watoto”

Katika Mwezi wa 12, 2009, Tribinali Kubwa ya Russie iliamua kufunga dini ya Mashahidi wa Yehova katika muji wa Taganrog na kuwanyanganya Jumba lao la Ufalme. Tribinali hiyo ilitangaza pia kwamba vichapo vyetu 34 ni vichapo hatari vya watu wenye musimamo mukali wa kidini. Uamuzi huo wenye kushangaza uliwekwa kwenye adresi yetu ya Internete pamoja na picha za Mashahidi walioteswa kwa sababu ya uamuzi huo, kutia ndani watoto.

Miezi michache baadaye, Biro ya Usimamizi ya Mashahidi wa Yehova Katika Russie ilipokea furushi na barua kutoka familia moja ya Mashahidi wanaoishi Queensland, Australie. Familia hiyo iliona uamuzi huo wa Tribinali Kubwa ya Russie. Katika barua yao waliandika hivi: “Ndugu Wapendwa, watoto wetu, Cody na Larissa, walihuzunika sana kwa sababu ya majaribu ambayo rafiki zetu katika Russie walipata na waliguswa moyo sana na imani waliyoonyesha. Kwa hiyo wameandika barua na kutuma karte fulani, na tumetuma furushi ndogo iliyo na zawadi ambazo tulipenda kutumia watoto katika Taganrog, ili wajue kama kuna watoto wengine wanaoishi mbali sana ambao pia wanamutumikia Yehova na wanaoendelea kuwafikiria. Watoto wetu wanawakumbatia kwa furaha na wanawatumia salamu zenye upendo.”

Watoto wa Taganrog walipopokea zawadi hizo, waliandikia familia hiyo ya Australie barua za shukrani. Ndugu mumoja wa Beteli ya Russie alivutiwa na maneno yenye kutia moyo “kutoka katika kinywa cha watoto,” kwa hiyo, aliandikia Cody na Larissa hivi: “Munajua kama watoto na watu wazima hawawezi kufurahi ikiwa wanapewa malipizi kwa sababu ya jambo fulani ambalo hawakufanya. Ndugu na dada zetu katika Taganrog hawakufanya jambo lolote mbaya, lakini wamenyanganywa Jumba lao la Ufalme. Hilo limewahuzunisha sana. Watatiwa moyo sana kujua kwamba ndugu zao wanaoishi katika inchi za mbali wanawafikiria. Asante sana kwa ukarimu wenu na roho yenu yenye upendo!”​—Zab. 8:2.

Bila shaka, tuko katika familia ya ulimwenguni pote ya ndugu na dada, na upendo tunaoonyeshana unatusaidia tupambane na majaribu na magumu ya maisha. Wakati ambapo mabishano yanaendelea katika vyumba vya tribinali ya Russie kuhusu vichapo vya Mashahidi wa Yehova, watoto wetu wanaendelea kuhangaikiana bila kujali luga, kabila, rangi ao inchi. Kwa kufanya hivyo, wanaonyesha kama maneno haya ya Yesu ni ya kweli: ‘Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mukiwa na upendo kati yenu wenyewe.’​—Yoh. 13:35.

[Picha katika ukurasa wa 32]

Watoto katika Russie (kushoto) waliopokea zawadi kutoka kwa watoto wa Australie (kuume)