Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Unifundishe Kufanya Mapenzi Yako”

“Unifundishe Kufanya Mapenzi Yako”

“Unifundishe Kufanya Mapenzi Yako”

“Unifundishe kufanya mapenzi yako, kwa maana wewe ni Mungu wangu.”​—ZAB. 143:10.

MAMBO YA KUKUMBUKA

Ni mambo gani yaliyomupata Daudi yanayoonyesha kama alihangaikia kufanya mambo kulingana na maoni ya Mungu?

Ni nini iliyomusaidia Daudi kujua mapenzi ya Mungu?

Ni nini itatusaidia tuendelee kukubaliwa na Yehova?

1, 2. Kuona mambo kama vile Mungu anavyoyaona kunaweza kutusaidia namna gani, na tutajifunza nini kutokana na mufano wa Mufalme Daudi?

 WAZIA unatembea katika eneo lenye milima ukielekea mahali fulani. Kisha unajikuta mbele ya njia mbili. Utapitia njia gani? Ili uone vizuri mahali ambako kila njia inaelekea, unaweza kupanda juu ya jiwe kubwa lililo karibu. Tunaweza kufanya hivyo tunapochukua maamuzi mazito maishani. Kuona mambo kama vile Mungu anavyoyaona kunaweza kutusaidia ‘kutembea katika njia’ ambayo Yehova anakubali.​—Isa. 30:21.

2 Katika miaka mingi ya maisha yake, Mufalme Daudi alituachia mufano muzuri kwa kufanya mambo kulingana na mapenzi ya Mungu. Acheni tuzungumuzie mambo yaliyomupata Daudi aliyemutumikia Yehova kwa moyo usiogawanyika na yale tunayoweza kujifunza kutokana na mwenendo wake.​—1 Fal. 11:4.

DAUDI ALIHESHIMU SANA JINA LA YEHOVA

3, 4. (a) Ni nini iliyomuchochea Daudi kupigana na Goliathi? (b) Daudi aliona namna gani jina la Mungu?

3 Fikiria wakati Daudi alipigana na Goliathi. Ni nini iliyomuchochea kijana Daudi kupigana na askari huyo aliyezoea sana mambo ya vita na aliyekuwa na urefu wa metre 2.9? (1 Sam. 17:4, maelezo ya chini katika Rbi8 ya Kifaransa.) Je, ni uhodari wake? Je, ni sababu alimutumaini Mungu? Mambo yote hayo mawili yalimuchochea kufanya tendo hilo la ujasiri. Hata hivyo, kumuheshimu Yehova na jina lake ndilo jambo lililomuchochea zaidi kupigana na askari huyo mwenye kuogopesha. Daudi alikasirika, kwa hiyo aliuliza hivi: ‘Kwani huyu Mufilisti asiyetahiriwa ni nani hata avitukane vikosi vya Mungu aliye hai?’​—1 Sam. 17:26.

4 Alipokuwa mbele ya Goliathi, kijana Daudi alisema hivi: ‘Unakuja kwangu ukiwa na upanga na mukuki na fumo, lakini mimi nakuja kwako nikiwa na jina la Yehova wa majeshi, Mungu wa vikosi vya Israeli, ambaye umemutukana.’ (1 Sam. 17:45) Kwa sababu ya kumutegemea Yehova, Daudi alimuua Mufilisti huyo kupitia jiwe moja tu. Siku hiyo na katika maishani yake yote, Daudi alimutumaini Yehova na aliheshimu sana jina lake. Kwa hiyo, Daudi aliwatia moyo Waisraeli wenzake ‘wajisifu katika jina takatifu la Yehova.’​—Soma 1 Mambo ya Nyakati 16:8-10.

5. Unaweza kujikuta katika hali gani inayofanana na uchokozi wa Goliathi?

5 Je, unajivunia kuwa mutumishi wa Yehova Mungu? (Yer. 9:24) Unafanya nini wakati majirani, wafanyakazi wenzako, wanafunzi wenzako, ao watu wa jamaa yako wanasema vibaya kumuhusu Yehova na kuwachekelea Mashahidi wake? Watu wanaposema vibaya kumuhusu Yehova, je, unalitetea jina lake, ukitumaini kama atakupa uhodari wa kufanya hivyo? Ni kweli kwamba, kuna “wakati wa kukaa kimya,” lakini hatupaswe kusikia haya kuitwa Mashahidi wa Yehova na wafuasi wa Yesu. (Mhu. 3:1, 7; Mk. 8:38) Ijapokuwa tunapaswa kuwa na busara na adabu tunaposhugulika na watu wasiopendezwa na ujumbe, acheni tusiwe kama Waisraeli ‘walioingiwa na hofu na kuogopa sana’ wakati walisikia maneno ya uchokozi ya Goliathi. (1 Sam. 17:11) Kuliko kuogopa, acheni tutende kwa uhodari ili kulitakasa jina la Yehova Mungu. Kusudi letu ni kuwasaidia wengine wajue ukweli kumuhusu Yehova. Ili kufanya hivyo, tunatumia Neno lake ili kuwasaidia waone faida ya kumukaribia Mungu.​—Yak. 4:8.

6. Kusudi la Daudi lilikuwa nini alipopigana na Goliathi, na sisi pia, kusudi letu kubwa linapaswa kuwa nini?

6 Pigano kati ya Daudi na Goliathi linatufundisha jambo lingine la maana. Wakati Daudi alifika kwenye uwanja wa mapigano, aliuliza hivi: ‘Atafanyiwa nini mutu atakayemupiga yule Mufilisti pale na kuondolea mbali shutuma kutoka juu ya Israeli?’ Watu waliokuwa hapo walimuambia maneno yaleyale, wakisema: ‘Mutu yule atakayemupiga [Goliathi], mufalme atamutajirisha kwa utajiri mwingi sana, naye atamupa binti yake.’ (1 Sam. 17:25-27) Lakini kusudi kubwa la Daudi halikuwa kupata zawadi. Kusudi lake kubwa lilikuwa kumutukuza Mungu wa kweli. (Soma 1 Samweli 17:46, 47.) Hilo linatufundisha nini? Je, kusudi letu kubwa maishani ni kujifanyia jina kwa kujirundikia vitu vya kimwili na kutafuta tujulikane sana? Kwa kweli tunataka kumuiga Daudi, aliyeimba hivi: ‘Mutukuzeni Yehova pamoja nami, na tulikweze jina lake pamoja.’ (Zab. 34:3) Acheni basi tumutumaini Mungu, tukihangaikia kwanza kutakaswa kwa jina lake.​—Mt. 6:9.

7. Namna gani tunaweza kuwa na imani yenye nguvu tunapokutana na watu wasiopendezwa?

7 Ili kupigana kwa ujasiri na Goliathi, Daudi alihitaji kumutumaini Yehova kwa moyo wake wote. Kijana Daudi alikuwa na imani yenye nguvu. Kumutegemea Yehova kila siku alipokuwa muchungaji, ni kati ya mambo yaliyomusaidia Daudi kuwa na imani yenye nguvu. (1 Sam. 17:34-37) Sisi pia tunahitaji imani yenye nguvu ili kuendelea kuhubiri, zaidi sana tunapokutana na watu wasiopendezwa. Tunaweza kuwa na imani kama hiyo kwa kumutegemea Mungu katika shuguli zetu za kila siku. Kwa mufano, tunaweza kuanzisha mazungumuzo ya Biblia na watu wanaokaa pembeni yetu katika motokari. Kwa nini tusiwahubirie pia watu tunaokutana nao barabarani wakati tunafanya mahubiri ya nyumba kwa nyumba?​—Mdo. 20:20, 21.

DAUDI ALIMUNGOJEA YEHOVA

8, 9. Nafasi zilipojitokeza za kumuua Mufalme Sauli, namna gani Daudi alionyesha kama aliendelea kufikiria mapenzi ya Mungu?

8 Maoni ya Daudi kumuhusu Sauli, mufalme wa kwanza wa Israeli, ni jambo lingine linaloonyesha namna Daudi alivyofurahia kumutumainia Yehova. Mara tatu Sauli alijaribu kumupigilia Daudi kwenye ukuta akitumia mukuki, lakini Daudi alikwepa kila mara, hakulipisha kisasi. Mwishowe, Daudi alimukimbia Sauli. (1 Sam. 18:7-11; 19:10) Kisha Sauli alichagua wanaume 3 000 katika Israeli na kuenda kumutafuta Daudi katika jangwa. (1 Sam. 24:2) Kisha, bila kujua, Sauli alienda katika pango ambamo Daudi alikuwa pamoja na watu wake. Daudi angetumia nafasi hiyo ili kumuua mufalme aliyekuwa akimuwinda. Zaidi ya hayo, mapenzi ya Mungu ilikuwa kwamba Daudi achukue nafasi ya Sauli. (1 Sam. 16:1, 13) Kwa kweli, ikiwa Daudi angesikiliza shauri la watu wake, angemuua mufalme Sauli. Lakini Daudi alisema hivi: ‘Ni jambo lisilowaziwa kwangu, kwa maoni ya Yehova, kwamba nimufanyie bwana wangu jambo hili, mutiwa​-mafuta wa Yehova, kwa kunyoosha mukono wangu juu yake, kwa kuwa yeye ni mutiwa​-mafuta wa Yehova.’ (Soma 1 Samweli 24:4-7.) Sauli alikuwa angali mufalme mutiwa​-mafuta wa Mungu. Daudi hakutaka kumunyanganya Sauli ufalme, kwa sababu Yehova alikuwa bado hajamuondoa kwenye mamlaka. Kwa kukata tu upindo wa koti la Sauli lisilo na mikono, Daudi alionyesha kama hakuwa na nia ya kumuumiza Sauli.​—1 Sam. 24:11.

9 Daudi alionyesha tena kwamba alimuheshimu mutiwa-mafuta wa Mungu alipomuona Sauli kwa mara ya mwisho. Wakati huo, Daudi na Abishai, walifika mahali alipokuwa Sauli na kumukuta amelala. Ijapokuwa Abishai alimuambia Daudi kama Mungu amemutia Sauli katika mikono yake na sasa anaweza kumupigilia chini kwa mukuki, Daudi hakufanya hivyo. (1 Sam. 26:8-11) Daudi aliendelea kutafuta uongozi wa Mungu. Kwa hiyo, kuliko kufuata maneno ya Abishai, Daudi aliendelea kutenda kulingana na mapenzi ya Mungu.

10. Tunaweza kujikuta katika hali gani, ni nini inayoweza kutusaidia kubaki waaminifu?

10 Sisi pia tunaweza kujikuta katika hali kama hiyo. Kwa mufano, marafiki wetu wanaweza kutuchochea tufuate mawazo yao kuliko kututia moyo tufanye mapenzi ya Mungu. Kama Abishai, watu fulani wanaweza kututia moyo tufanye mambo fulani bila kufikiria maoni ya Mungu. Ili kubaki waaminifu, tunapaswa kuelewa waziwazi maoni ya Yehova kuhusu mambo hayo na kuazimia kushikamana na njia zake.

11. Namna gani mufano wa Daudi unatusaidia kuendelea kufikiria sana mapenzi ya Mungu?

11 Daudi alimuomba Yehova hivi: “Unifundishe kufanya mapenzi yako.” (Soma Zaburi 143:5, 8, 10.) Kuliko kufuata mawazo yake ao mawazo ya wengine, Daudi alifurahia kufundishwa na Mungu. Daudi ‘alitafakari juu ya utendaji wote wa Yehova na kwa kupenda aliendelea kuhangaika kazi ya Mungu mwenyewe.’ Tunaweza sisi wenyewe kutambua mapenzi ya Mungu kwa kuzama katika Maandiko na kufikiri sana juu ya masimulizi mengi ya Biblia yanayoonyesha namna Yehova alivyotendea wanadamu.

DAUDI ALIFURAHIA KANUNI ZA MUNGU

12, 13. Sababu gani Daudi alikataa kunywa maji ambayo wanaumume wake watatu walimuletea?

12 Daudi alifurahia kanuni za Mungu na alipenda kuishi kulingana na kanuni hizo; mufano wake unastahili kuigwa. Fikiria mambo yaliyotokea wakati Daudi alitamani sana kunywa “maji kutoka katika tangi la Bethlehemu.” Wanaume watatu wa Daudi waliingia kwa nguvu katika muji uliokuwa mikononi mwa Wafilisti na kumuletea maji. Hata hivyo, ‘Daudi hakukubali kuyanywa, bali akayamwanga mbele za Yehova.’ Kwa sababu gani? Daudi alisema hivi: “Ni jambo lisiloweza kuwaziwa kwangu, kwa habari ya Mungu wangu, nifanye hivi! Je, ninywe damu ya watu hawa kwa kuhatarisha nafsi zao? Kwa maana waliyaleta kwa kuhatarisha nafsi zao.”​—1 Nya. 11:15-19.

13 Daudi alijua kama kulingana na Sheria, damu ilipaswa kumwangwa mbele za Yehova wala haikupaswa kukuliwa, na alijua kwa nini. Daudi alijua kama “nafsi ya mwili iko katika damu.” Lakini, maji waliyomuletea haikuwa damu. Kwa nini basi Daudi alikataa kunywa maji hayo? Kwa sababu aliheshimu kanuni zinazotegemeza sheria za Mungu. Kwa maoni ya Daudi, maji hayo yalikuwa na bei kama damu ya wanaume hao watatu. Kwa hiyo, Daudi alifikiri kama haikufaa kunywa maji hayo. Kuliko kuyanywa, aliamua kuyamwanga chini.​—Law. 17:11; Kum. 12:23, 24.

14. Ni nini iliyomusaidia Daudi kuona mambo kama Yehova anavyoyaona?

14 Daudi alifurahia sana sheria ya Mungu. Aliimba hivi: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.” (Zab. 40:8) Daudi alijifunza sheria ya Mungu na kufikiri sana juu yake. Alitumainia hekima ya sheria za Mungu. Kwa hiyo, Daudi alielewa maana ya sheria kuliko tu kushika sheria namna ilivyoandikwa. Tunapojifunza Biblia, ni jambo la hekima tufikiri sana kuhusu mambo tunayosoma na kuyaweka katika moyo wetu ili tujue mambo yanayomufurahisha Yehova katika hali fulani.

15. Namna gani Sulemani hakuheshimu Sheria ya Mungu?

15 Sulemani, mwana wa Daudi, alipendwa sana na Yehova Mungu. Lakini, baadaye, Sulemani hakuheshimu Sheria ya Mungu. Sulemani hakutii sheria iliyosema kama mufalme wa Israeli “asizidishe wake kwa ajili yake.” (Kum. 17:17) Tofauti na hilo, Sulemani alioa wanawake wengi wageni. Alipokuwa muzee, ‘wake zake waligeuza moyo wake ili ufuate miungu mingine.’ Hatujue akili ya Sulemani ilikuwa imeenda wapi, ‘alianza kufanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova, naye hakumufuata Yehova kikamilifu kama Daudi baba yake.’ (1 Fal. 11:1-6) Ni jambo la maana sana kwetu kutii sheria na kanuni zinazopatikana katika Neno la Mungu! Kwa mufano, kufanya hivyo ni kwa lazima tunapofikiria kuoa ao kuolewa.

16. Kuelewa maana ya kanuni ya kuoa ao kuolewa “katika Bwana tu” kunaweza kuwasaidia namna gani wale wanaofikiria kufunga ndoa?

16 Ikiwa mutu asiye Shahidi anataka kuanzisha urafiki wa kimapenzi pamoja nawe, je, jibu lako linaonyesha kwamba una maoni kama ya Daudi ao ya Sulemani? Waabudu wa kweli wanapaswa kuoa ao kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Kor. 7:39) Shahidi wa Yehova anapofikiria kufunga ndoa, anapaswa kuoa ao kuolewa na mwamini mwenzake. Ikiwa tunaelewa maana ya kanuni hiyo ya Neno la Mungu, tutakataa kuoa ao kuolewa na watu wasio Mashahidi, lakini pia, tutaepuka pia kufanya nao urafiki wa kimapenzi.

17. Ni nini itatusaidia kuepuka mutego wa kutazama ponografia?

17 Daudi alitafuta kwa bidii uongozi wa Mungu. Mufano wake unaweza kutusaidia kuepuka kutazama ponografia, ni kusema, picha ao habari za ngono. Soma maandiko yanayofuata, kisha ufikirie kanuni zinazozungumuziwa katika maandiko hayo na ujaribu kuona maoni ya Mungu ni nini kuhusu ponografia. (Soma Zaburi 119:37; Mathayo 5:28, 29; Wakolosai 3:5.) Kufikiri sana kuhusu kanuni za Mungu kutatusaidia kuepuka mutego wa kutazama ponografia.

FIKIRIA MAONI YA MUNGU KILA WAKATI

18, 19. (a) Ijapokuwa Daudi alikuwa mutu asiye mukamilifu, ni nini iliyomusaidia aendelee kukubaliwa na Mungu? (b) Unaazimia kufanya nini?

18 Daudi alikuwa mufano wa kuiga katika njia nyingi, lakini alifanya makosa mengi mazito. (2 Sam. 11:2-4, 14, 15, 22-27; 1 Nya. 21:1, 7) Hata hivyo, muda wa maisha yake yote, Daudi alikuwa akitubu kila mara alipofanya zambi. Alitembea kwa “utimilifu wa moyo” mbele za Mungu. (1 Fal. 9:4) Sababu gani tunasema hivyo? Kwa sababu Daudi alijikaza kutenda kulingana na mapenzi ya Yehova.

19 Ijapokuwa sisi ni watu wasio wakamilifu, Yehova anaweza kuendelea kutukubali. Ili aendelee kutukubali, acheni tujifunze Neno Lake kwa bidii, tufikiri sana juu ya yale tunayojifunza, na tutende kulingana na mambo ambayo tumejifunza. Tukifanya hivyo, sala yetu itafanana na ile ya mutunga​-zaburi aliyemuomba Yehova hivi kwa unyenyekevu: “Unifundishe kufanya mapenzi yako.”

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 5]

Ni nini iliyomuzuia Daudi kumuua Sauli alipokuwa na nafasi ya kufanya hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Daudi alikataa kunywa maji ambayo watu wake walimuletea. Hilo linatufundisha nini?