Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Wewe Ni Musimamizi- Nyumba Mwenye Kutumainika?

Je, Wewe Ni Musimamizi- Nyumba Mwenye Kutumainika?

Je, Wewe Ni Musimamizi- Nyumba Mwenye Kutumainika?

“Ninyi si mali yenu wenyewe.”​—1 KOR. 6:19.

UNGEJIBU NAMNA GANI?

Wasimamizi​-nyumba wa nyakati za zamani walikuwa na madaraka gani?

Wasimamizi​-nyumba wote wa Mungu wamepewa madaraka gani?

Tunapaswa kuliona namna gani daraka la usimamizi​-nyumba ambalo tumepewa?

1. Watu wana maoni gani kuhusu kuwa mutumwa?

 MIAKA karibu 2 500 iliyopita, mwandikaji mumoja Mugiriki aliandika hivi: ‘Hakuna mutu anayependa kuwa mutumwa.’ Watu wengi leo wanakubali maneno hayo. Neno “mutumwa” linawafanya watu wengi wafikiri juu ya wanaume na wanawake wanaotendewa kinyama na kulazimishwa kuwatumikia wengine, watu wanaotumika sana ili kuwatajirisha mabwana wao na wale wanaowagandamiza.

2, 3. (a) Watumwa ao watumishi wa Kristo wana pendeleo gani? (b) Tutazungumuzia maulizo gani kuhusu kazi ya usimamizi​-nyumba?

2 Hata hivyo, Yesu alionyesha kwamba wanafunzi wake wanapaswa kuwa watumishi wanyenyekevu ao watumwa. Lakini, utumwa wa Wakristo haumaanishe kuteswa ao kuzarauliwa. Wakristo wanafurahia utumwa wao kwa sababu Bwana wao Yesu Kristo anawasamini, anawaheshimu na kuwatumainia. Kwa mufano, fikiria maneno ambayo alisema muda kidogo mbele ya kifo chake kuhusu ‘mutumwa’ mumoja. Alisema kwamba angemupatia ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara’ madaraka mengi.​—Mt. 24:45-47.

3 Inapendeza kujua kwamba mutumwa huyohuyo katika andiko la Luka, anaitwa ‘musimamizi​-nyumba.’ (Soma Luka 12:42-44.) Wakristo wengi waaminifu wanaoishi leo hawako katika kikundi cha musimamizi​-nyumba mwaminifu. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba, kwa njia fulani, kila mutu anayemutumikia Mungu anafanya kazi ya musimamizi​-nyumba. Musimamizi​-nyumba ana madaraka gani? Namna gani anapaswa kuchukua madaraka yake? Ili kupata majibu ya maulizo hayo, acheni tuzungumuzie madaraka ya wasimamizi​-nyumba wa zamani.

KAZI YA WASIMAMIZI-NYUMBA

4, 5. Wasimamizi-nyumba wa zamani walikuwa na madaraka gani? Toa mifano.

4 Zamani, musimamizi​-nyumba alikuwa kila mara mutumwa mwenye kutumainika aliyepewa kazi ya kusimamia nyumba na kazi mbalimbali za bwana wake. Kwa kawaida, wasimamizi​-nyumba walikuwa na mamlaka makubwa na walipewa kazi ya kusimamia vitu vya nyumbani, kama vile feza, na watumwa wengine. Mufano wa Eliezeri unaonyesha jambo hili; alikuwa na daraka la kusimamia mali nyingi ya Abrahamu. Labda Eliezeri ndiye aliyetumwa na Abrahamu Mesopotamia ili amutafutie Isaka bibi. Hilo lilikuwa daraka nzito kabisa!​—Mwa. 13:2; 15:2; 24:2-4.

5 Yosefu, mwana wa mujukuu wa Abrahamu, alisimamia nyumba ya Potifa. (Mwa. 39:1, 2) Baadaye, Yosefu pia alikuwa na musimamizi-nyumba, aliyesimamia ‘nyumba yake.’ Musimamizi-nyumba huyo aliwakaribisha ndugu kumi wa Yosefu na kuwatimizia mahitaji yao. Yosefu alimutumia ili kuwajaribu ndugu zake kwa kutia kikombe cha feza cha Yosefu katika mifuko yao na kisha akawaambia kama wameiba kikombe hicho. Kwa kweli, wasimamizi​-nyumba walitumainiwa sana.​—Mwa. 43:19-25; 44:1-12.

6. Kwa kuwa wazee ni wasimamizi​-nyumba, je, wanatimiza wote madaraka yaleyale?

6 Miaka mingi baadaye, mutume Paulo aliandika kwamba wazee katika makutaniko walipaswa kuwa ‘wazimamizi​-nyumba wa Mungu.’ (Tito 1:7) Kwa kuwa wamewekwa ili kuchunga “kundi la Mungu,” wazee wanaongoza na kusimamia makutaniko. (1 Pet. 5:1, 2) Lakini, madaraka yao yanatofautiana. Kwa mufano, leo wazee fulani wanatumikia kutaniko moja. Waangalizi wenye kusafiri wanatumikia makutaniko mengi. Na washiriki wa Halmashauri ya tawi wanashugulikia makutaniko ya inchi nzima. Hata hivyo, wote wanaombwa kutimiza migawo yao kwa uaminifu; wote ‘watatoa hesabu’ mbele za Mungu.​—Ebr. 13:17.

7. Tunajua namna gani kwamba, kwa njia fulani, Wakristo wote ni wasimamizi​-nyumba?

7 Lakini, tuseme nini juu ya Wakristo wengine ambao si waangalizi ao wazee? Katika barua aliyoandikia Wakristo wote, mutume Petro alisema hivi: ‘Kwa kadiri ambayo kila mumoja amepokea zawadi, itumieni katika kuhudumiana kama wasimamizi-nyumba wazuri wa fazili zisizostahiliwa za Mungu zinazoonyeshwa kwa njia mbalimbali.’ (1 Pet. 1:1; 4:10) Kwa neema yake, Mungu ametupatia sisi wote zawadi ao uwezo mbalimbali tunaoweza kutumia ili kuwasaidia ndugu na dada zetu. Kwa hiyo, wote wanaomutumikia Mungu ni wasimamizi​-nyumba, na kwa sababu ya kazi yao, Mungu anawaheshimu, anawatumainia na anataka watumie vizuri zawadi na uwezo aliowapa.

SISI NI MALI YA MUNGU

8. Ni kanuni gani moja ya maana ambayo tunapaswa kukumbuka?

8 Acheni tuzungumuzie kanuni tatu ambazo sisi wasimamizi​-nyumba tunapaswa kufikiria. Kanuni ya kwanza: Sisi ni mali ya Mungu na tutatoa hesabu kwake. Paulo aliandika hivi: ‘Ninyi si mali yenu wenyewe, kwa maana mulinunuliwa kwa bei,’ ni kusema, damu iliyomwangwa ya Kristo. (1 Kor. 6:19, 20) Kwa sababu sisi ni mali ya Yehova, tunapaswa kutii amri zake, na amri hizo si muzigo muzito. (Rom. 14:8; 1 Yoh. 5:3) Sisi pia ni watumwa wa Kristo. Tumepewa uhuru mwingi kama vile wasimamizi-nyumba wa zamani, lakini si uhuru wa kufanya kila jambo tunalotaka. Tunapaswa kutimiza madaraka yetu kulingana na maagizo ambayo tumepewa. Hata tuwe na mapendeleo ya utumishi ya namna gani, sisi ni watumwa wa Mungu na Kristo.

9. Yesu alitumia mufano gani ili kuonyesha daraka la mutumwa kwa bwana wake?

9 Yesu anatusaidia kuelewa daraka la mutumwa kwa bwana wake. Siku moja aliwaambia wanafunzi wake kuhusu mutumwa aliyerudi nyumbani kisha kufanya kazi siku nzima. Je, bwana wake alimuambia: “‘Njoo hapa mara moja uketi mezani’? Hapana. Lakini alimuambia, ‘Nitayarishie kitu ili nipate mulo wangu wa jioni, nawe jifunge unihudumie mupaka niwe nimemaliza kula na kunywa, kisha unaweza kula na kunywa.’ Je, alimushukuru mutumwa huyo kwa sababu alifanya mambo aliyoagizwa? Yesu alifasiria jambo hilo hivi: ‘Ndivyo na ninyi, pia, wakati mumefanya mambo yote muliyoagizwa, semeni, sisi ni watumwa wasiofaa kitu. Jambo ambalo tumefanya ndilo tulilopaswa kufanya.’”​—Lu. 17:7-10.

10. Ni nini inayoonyesha kwamba Yehova anapendezwa sana na namna tunavyojikaza ili kumutumikia?

10 Kwa kweli, Yehova anapendezwa sana na namna tunavyojikaza ili kumutumikia. Biblia inatuhakikishia hivi: ‘Mungu hakose kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mulioonyesha kwa ajili ya jina lake.’ (Ebr. 6:10) Yehova haweze hata kidogo kutuomba mambo yanayopita uwezo wetu. Zaidi ya hayo, kila jambo analotuomba ni kwa faida yetu na si muzigo muzito kabisa. Vilevile, kulingana na mufano wa Yesu, mutumwa hatafute faida zake kwa kufanya mambo yanayomupendeza. Mufano huo unatufundisha kwamba tulipojitoa kwa Yehova katika sala, tulichagua kutia faida zake pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu, sivyo?

MAMBO AMBAYO YEHOVA ANAOMBA SISI SOTE TUFANYE

11, 12. Ni sifa gani ambayo sisi wasimamizi​-nyumba tunapaswa kuonyesha na tunapaswa kuepuka nini?

11 Kanuni ya pili: Sisi wasimamizi-nyumba tunafuata sisi wote kanuni zilezile. Ni kweli kwamba kuna madaraka fulani yanayopewa tu Wakristo fulani katika kutaniko. Hata hivyo, Wakristo wote wamepewa madaraka mengi. Kwa mufano, sisi Mashahidi wa Yehova na wanafunzi wa Yesu, tunaamuriwa kupendana. Yesu alisema kwamba upendo ndio alama ya kuwatambulisha Wakristo wa kweli. (Yoh. 13:35) Lakini hatuwapende tu wale walio ndugu na dada zetu. Tunajikaza kuwaonyesha upendo hata wale wasiokuwa Mashahidi. Hilo ni jambo ambalo kila mumoja wetu anaweza na anapaswa kufanya.

12 Tunaombwa pia kuwa na mwenendo muzuri. Tunataka kabisa kuepuka mwenendo na namna ya kuishi isiyopatana na Neno la Mungu. Mutume Paulo aliandika: ‘Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume wanaowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume wanaolala na wanaume, wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyanganyi hawatauriti ufalme wa Mungu.’ (1 Kor. 6:9, 10) Bila shaka, tunapaswa kujikaza ili kupatanisha maisha yetu na sheria za Mungu. Kufanya hivyo kunaleta faida nyingi, kama vile afya nzuri, uhusiano muzuri pamoja na wengine, na maisha yanayokubaliwa machoni pa Mungu.​—Soma Isaya 48:17, 18.

13, 14. Wakristo wote wamepewa kazi gani, na tunapaswa kuiona namna gani?

13 Usisahau pia kwamba musimamizi-nyumba alikuwa na kazi ya kufanya. Sisi pia tuna kazi ya kufanya. Tumepewa zawadi nzuri, ni kusema, ujuzi wa ile kweli. Mungu anataka tuwaelezee wengine kweli hiyo. (Mt. 28:19, 20) Mutume Paulo aliandika: ‘Acheni mutu atukadirie sisi hivyo kuwa tuko chini ya Kristo nasi ni wasimamizi​-nyumba wa siri takatifu za Mungu.’ (1 Kor. 4:1) Paulo alijua kwamba kuwa musimamizi-nyumba kunamaanisha kujua vizuri “siri takatifu” na kuzielezea wengine kwa uaminifu kama vile Bwana wetu Yesu Kristo alivyoamuru.​—1 Kor. 9:16.

14 Kuwaelezea wengine ile kweli ni alama inayoonyesha kama tunawapenda. Bila shaka hali za Wakristo zinatofautiana. Sisi wote hatuweze kuhubiri sawasawa. Yehova anaelewa jambo hilo. Jambo la maana ni kufanya yote tunayoweza kufanya kulingana na uwezo wetu. Hilo litaonyesha kwamba tunapenda kabisa Mungu na majirani wetu.

TUNAPASWA KUWA WAAMINIFU

15-17. (a) Sababu gani musimamizi​-nyumba anapaswa kuwa mwaminifu? (b) Yesu alitumia mufano gani ili kuonyesha matokeo ya kukosa uaminifu?

15 Kanuni ya tatu inayohusiana sana na kanuni mbili ambazo tumezungumuzia ni hii: Tunapaswa kuwa waaminifu, wenye kutumainika. Kuwa na sifa nzuri na uwezo mbalimbali hakutamuletea musimamizi​-nyumba faida yoyote ikiwa anashindwa kutimiza mambo anayoombwa kufanya ao ikiwa anakosa uaminifu kwa bwana wake. Uaminifu ni wa lazima ili kuwa musimamizi​-nyumba muzuri. Kumbuka kwamba Paulo aliandika hivi: ‘Kinachoangaliwa katika wasimamizi​-nyumba ni mutu kupatwa akiwa mwaminifu.’​—1 Kor. 4:2.

16 Tuwe hakika kwamba ikiwa sisi ni waaminifu tutapata zawadi. Ikiwa sisi si waaminifu, tutapoteza yote. Tunajifunza jambo hilo kutokana na mufano wa Yesu wa talanta. Watumwa ‘waliofanya biashara’ kwa uaminifu na feza za bwana wao walipongezwa na kubarikiwa sana. Mutumwa ambaye alishindwa kutumia talanta ambayo bwana wake alimukabizi, aliitwa mutumwa ‘muovu,’ “goigoi,” na “asiyefaa kitu.” Na alinyanganywa talanta aliyopewa, na kutupwa inje.​—Soma Mathayo 25:14-18, 23, 26, 28-30.

17 Siku ingine fulani, Yesu alizungumuzia matokeo ya kukosa uaminifu. Yeye alisema hivi: “Mutu fulani alikuwa tajiri naye alikuwa na musimamizi​-nyumba, na huyo akashtakiwa kwake kuwa anapoteza mali zake. Kwa hiyo akamuita na kumuambia, ‘Ni nini hili ninalosikia juu yako? Toa hesabu ya usimamizi wako, kwa maana hauweze tena kuisimamia nyumba.’” (Lu. 16:1, 2) Kwa kuwa mutumwa huyo alitumia vibaya mali ya bwana wake, bwana wake alimufukuza. Mufano huo unatupatia somo nzuri kabisa! Tunapaswa kutimiza kazi tuliyopewa kwa uaminifu.

JE, NI JAMBO LA HEKIMA KUJILINGANISHA NA WENGINE?

18. Sababu gani hatupaswe kujilinganisha na wengine?

18 Kila mumoja wetu anaweza kujiuliza, ‘Ninaona kazi yangu ya usimamizi-nyumba namna gani?’ Si jambo la hekima kujilinganisha na wengine. Biblia inatushauri hivi: ‘Kila mumoja na asibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mutu yule mwengine.’ (Gal. 6:4) Kuliko kujilinganisha na wengine, tunapaswa kukaza akili yetu juu ya mambo ambayo sisi tunaweza kufanya. Hilo litatuepusha kuwa na kiburi na litatusaidia tusivunjike moyo. Tunapochunguza mambo tunayoweza kufanya, tunapaswa kujua kwamba hali yetu ya jana si ya leo. Labda hatuweze kufanya tena yote tuliyokuwa tukifanya hapo zamani kwa sababu ya magonjwa, uzee, ao madaraka mbalimbali. Kwa upande mwengine, labda tuna uwezo wa kufanya mambo mengi kuliko yale tunayofanya sasa. Ikiwa ndivyo, sababu gani basi tusiongeze utendaji wetu?

19. Ikiwa hatupewe pendeleo fulani, sababu gani hatupaswe kuvunjika moyo?

19 Jambo lingine tunalopaswa kufikiria ni madaraka tuliyo nayo ao yale tunayojikaza kupata. Kwa mufano, labda ndugu anataka kuwa muzee katika kutaniko ao anataka kupewa hotuba kwenye mikusanyiko. Ni vizuri kujikaza kutimiza sifa zinazoombwa ili kupata mapendeleo hayo, lakini hatupaswe kuvunjika moyo ikiwa tunafikiri kwamba mapendeleo hayo yanachelewa. Tunaweza kupewa mapendeleo fulani kisha muda murefu, labda kwa sababu ambazo hatuelewe sasa. Kumbuka kwamba labda Musa alifikiri kama alikuwa tayari kuongoza Waisraeli kutoka Misri, lakini alipaswa kungojea miaka 40 mbele ya kupata pendeleo hilo. Kwa hiyo alikuwa na muda wa kutosha ili kuonyesha sifa alizohitaji ili kuongoza watu hao wenye shingo ngumu na waasi.​—Mdo. 7:22-25, 30-34.

20. Mambo yaliyomupata Yonathani yanatufundisha nini?

20 Wakati fulani labda hatutapewa pendeleo tulilotazamia. Yonathani alijikuta katika hali hiyo. Kwa kuwa alikuwa mwana wa Sauli, ni yeye ndiye angekuwa mufalme juu ya Israeli yote. Lakini, Mungu alimuchagua Daudi, kijana mudogo zaidi, ili awe mufalme. Je, Yonathani alivunjika moyo ao kukasirika? Hapana. Alikubali hali hiyo na kumutegemeza Daudi hata ikiwa kufanya hivyo kulihatarisha maisha yake. Yonathani alimuambia Daudi hivi: ‘Wewe utakuwa mufalme juu ya Israeli, na mimi nitakuwa wa pili kwako.’ (1 Sam. 23:17) Hilo linatufundisha nini? Tofauti na baba yake, Yonathani alikubali uamuzi wa Yehova, naye hakumusikilia Daudi wivu. Kuliko kuwasikilia wengine wivu kwa sababu ya mapendeleo waliyopewa, sisi wote tunapaswa kujikaza kutimiza madaraka yetu. Tuwe hakika kwamba katika ulimwengu mupya, Yehova atawatimizia watumishi wake wote tamaa ya moyo wao.

21. Tunapaswa kuona namna gani pendeleo tulilopewa?

21 Acheni tukumbuke kwamba sisi ni wasimamizi-nyumba wenye kutumainika; sisi si watumwa wanaoteswa na kugandamizwa. Mungu anatusamini sana kwa kutupatia kazi ya kuhubiri habari njema katika siku hizi za mwisho, kazi ambayo haitarudiliwa tena. Tunapofanya kazi hiyo, Mungu anatuachia uhuru wa kuchagua namna ya kutimiza madaraka mbalimbali aliyotutolea. Acheni basi tuwe wasimamizi​-nyumba waaminifu. Na tufurahie pendeleo tulilopewa la kumutumikia Mutawala mukubwa zaidi wa ulimwengu wote.

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Acheni tutimize kwa uaminifu madaraka yetu