Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kufanikiwa Katika Maisha Kunamaanisha Nini?

Kufanikiwa Katika Maisha Kunamaanisha Nini?

Kufanikiwa Katika Maisha Kunamaanisha Nini?

‘Utafanikisha njia yako, kisha utatenda kwa hekima.’​—YOS. 1:8.

UNGEJIBU NAMNA GANI?

Ni nini inayoonyesha kwamba Sulemani alifanikiwa?

Ni nini inayoonyesha kama mutume Paulo alifanikiwa kabisa?

Unaweza kufanya nini ili uwe mwenye kufanikiwa kabisa milele?

1, 2. (a) Watu wengi wanafikiri kufanikiwa katika maisha kunamaanisha nini? (b) Namna gani unaweza kujua mawazo ya moyo wako kuhusu kufanikiwa katika maisha?

 INAMAANISHA nini kufanikiwa ao kubarikiwa katika maisha? Watu wanatoa majibu yenye kutofautiana sana wanapoulizwa ulizo hilo. Kwa mufano, wengi wanafikiri kama kufanikiwa ao kubarikiwa katika maisha kunamaanisha kuwa na feza nyingi, kazi nzuri ao kusoma sana masomo ya juu ao université. Wengine wanafikiri kama ikiwa wana uhusiano muzuri na watu wa familia, marafiki, ao wafanyakazi wenzao basi wamefanikiwa katika maisha ao wamebarikiwa. Watumishi fulani wa Yehova wanafikiri kwamba ikiwa mutu ana madaraka fulani katika kutaniko ao ikiwa ana matokeo mazuri katika mahubiri mutu huyo amefanikiwa ao amebarikiwa.

2 Sasa wewe unafikiri kufanikiwa katika maisha ao kubarikiwa kunamaanisha nini? Ili ujue mawazo ya moyo wako kuhusu jambo hilo, andika majina ya watu wachache ambao unaheshimu ao unapendezwa nao kwa sababu unafikiri kama wamefanikiwa ao kubarikiwa katika maisha. Ni watu wa namna gani? Ni matajiri ao wenye kujulikana sana? Ni watu wenye uwezo? Majibu yako yataonyesha waziwazi mawazo ya moyo wako. Kwa sababu, kwa kawaida maamuzi yako na miradi unayofuatia katika maisha inatokana na mambo ambayo moyo wako unaona kuwa ya maana sana maishani.​—Lu. 6:45.

3. (a) Yoshua alipaswa kufanya nini ili afanikiwe katika maisha yake? (b) Tutazungumuzia nini sasa?

3 Maoni ya Yehova kuhusu kufanikiwa ao kubarikiwa katika maisha ndilo jambo la maana zaidi kwetu, na tunaweza kupata uzima wa milele ikiwa tu mawazo yake na yetu yanapatana. Wakati Yehova alimupatia Yoshua daraka la kuongoza Waisraeli kwenye Inchi ya Ahadi, alimuambia asome Sheria ya Musa ‘muchana na usiku’ na kutii kwa uangalifu mambo yaliyoandikwa ndani yake. Kisha alimuhakikishia hivi: “Ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha utatenda kwa hekima.” (Yos. 1:7, 8) Na tunajua vizuri kwamba Yoshua alifanikiwa katika maisha. Namna gani sisi? Tunaweza kujua namna gani kwamba mawazo yetu kuhusu kufanikiwa yanapatana na mawazo ya Mungu? Ili kupata majibu, acheni tuchunguze maisha ya wanaume wawili ambao Biblia inazungumuzia.

JE, SULEMANI ALIFANIKIWA KATIKA MAISHA?

4. Kwa nini tunaweza kusema kama Sulemani alifanikiwa?

4 Sulemani alibarikiwa kuliko watu wote wa wakati wake katika mambo mengi. Sababu gani? Kwa sababu kwa muda wa miaka mingi alimuogopa Yehova na kumutii, na kwa hiyo Yehova alimubariki sana. Usisahau kwamba wakati Yehova alimuambia Sulemani amuombe jambo analotaka, mufalme huyo aliomba hekima ili kuongoza watu wa Yehova. Kwa hiyo, Yehova alimubariki kwa kumupatia hekima na mali. (Soma 1 Wafalme 3:10-14.) Hekima ya Sulemani ilikuwa “pana zaidi kuliko hekima ya watu wengine wote wa Mashariki na kuliko hekima yote ya Misri.” Alijulikana sana “katika mataifa yote yanayozunguka pande zote.” (1 Fal. 4:30, 31) Alikuwa pia na mali nyingi; kila mwaka alipata kilo 25 000 ya zahabu! (2 Nya. 9:13) Alijua vizuri sana namna ya kusikilizana na wafalme wa inchi zingine, alijua kufanya biashara nao na alijenga sana. Kwa kweli, wakati Sulemani alikuwa mwaminifu kwa Mungu alifanikiwa ao kubarikiwa katika maisha yake.​—2 Nya. 9:22-24.

5. Sulemani alielewa nini kuhusu wale wanaofanikiwa kabisa katika maisha?

5 Mambo ambayo Sulemani aliandika katika kitabu cha Mhubiri yanaonyesha kama yeye alijua maana ya kufanikiwa katika maisha. Hakufikiri kwamba ni wale tu walio matajiri ao walio na uwezo ndio wanaofanikiwa ao kuwa na furaha katika maisha. Aliandika hivi: ‘Nimekuja kujua kwamba hakuna jambo lingine bora kwao kuliko mutu kufurahi na kufanya mema maishani mwake; na pia kwamba kila mutu akule, akunywe na aone mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu. Hiyo ndiyo zawadi ya Mungu.’ (Mhu. 3:12, 13) Na alielewa kwamba mambo hayo mazuri yanaweza kumuletea mutu furaha ikiwa tu ana urafiki muzuri pamoja na Mungu. Sulemani alisema kweli alipoandika hivi: ‘Huu ndio mwisho wa mambo, kila jambo limekwisha sikiwa: Muogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.’​—Mhu. 12:13.

6. Namna gani mufano wa Sulemani unatusaidia kuelewa maana ya kufanikiwa katika maisha?

6 Sulemani alimuogopa Mungu kwa muda wa miaka mingi. Biblia inasema kwamba ‘aliendelea kumupenda Yehova kwa kutembea katika sheria za Daudi baba yake.’ (1 Fal. 3:3) Sulemani alifanikiwa katika maisha yake wakati alikuwa akifanya hivyo. Mungu alimusaidia kujenga hekalu nzuri kwa ajili ya ibada ya kweli na alimuongoza kuandika vitabu vitatu vya Biblia. Kwa kweli, hata ikiwa hatuweze kufanya kama Sulemani, mufano ambao alituachia wakati alikuwa mwaminifu kwa Mungu unaweza kutuonyesha maana ya kufanikiwa katika maisha na yale tunayopaswa kufanya ikiwa tunataka pia kufanikiwa. Kwa mufano, kwa uongozi wa roho ya Mungu, Sulemani aliandika kuhusu mali, hekima, kujulikana na uwezo, mambo ambayo wengi wanafikiri ni lazima wawe nayo ili ionekane kwamba wamefanikiwa. Lakini Sulemani alisema kwamba watu wanaojisumbua ili kupata vitu hivyo ‘wanafuatilia upepo,’ ni kusema, wanajaribu kupata kitu ambacho hakitawapatia furaha ya kweli. Umejionea mwenyewe kwamba watu wanaotafuta feza hawashibe feza, sivyo? Na wanaogopa kwamba watapoteza vitu ambavyo tayari wamepata. Zaidi ya hayo, siku moja ni watu wengine ndio watabaki na mali yao.​—Soma Mhubiri 2:8-11, 17; 5:10-12.

7, 8. Namna gani Sulemani alifikia kukosa uaminifu kwa Mungu, na matokeo yalikuwa nini?

7 Kama tunavyojua, mwishowe Sulemani aliacha kumutii Yehova. Biblia inasema hivi: ‘Na ikawa kwamba wakati Sulemani alipokuwa muzee, wake zake wakawa wameugeuza moyo wake ukaifuata miungu mingine; na moyo wake haukuwa mukamilifu kwa Yehova Mungu wake, kama moyo wa Daudi baba yake. Sulemani akaanza kufanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova.’​—1 Fal. 11:4-6.

8 Mambo ambayo Sulemani alianza kufanya hayakumupendeza Yehova, naye alimuambia Sulemani yale ambayo yangemupata kwa sababu ya kukosa kutii. Mungu alimuambia hivi: ‘Kwa sababu umefanya jambo hili wala haukushika agano langu na sheria zangu nilizokuamuru, hakika nitaurarua ufalme kutoka kwako, nami nitamupa mutumishi wako.’ (1 Fal. 11:11) Jambo lenye kusikitisha kabisa, sivyo? Ijapokuwa Sulemani alikuwa amebarikiwa katika mambo mengi, mwishowe alimuhuzunisha Yehova. Ndiyo, hakuendelea kufanya jambo lililokuwa la maana sana katika maisha, ni kusema, kubaki mwaminifu kwa Yehova. Kila mumoja wetu anaweza kujiuliza: ‘Maisha ya Sulemani yananifundisha nini ili niweze kufanikiwa katika maisha?’

MUTUME PAULO ALIFANIKIWA KABISA KATIKA MAISHA

9. Kulingana na maoni ya watu wa ulimwengu, je, tunaweza kusema kama Paulo alifanikiwa katika maisha? Eleza.

9 Maisha ya mutume Paulo yalitofautiana kabisa na yale ya Mufalme Sulemani. Paulo hakuishi maisha ya kifalme. Wakati fulani alikosa chakula, kitu cha kunywa, mavazi ao kitu cha kujifunika. (2 Kor. 11:24-27) Alipomukubali Yesu kuwa Masiya, mutume Paulo hakupewa tena heshima aliyokuwa akipewa alipokuwa katika dini ya Wayahudi. Na viongozi wa dini hiyo walimuchukia. Alifungwa, alipigwa mijeledi, alipigwa fimbo, na alipigwa majiwe. Mutume Paulo alisema kwamba yeye na Wakristo wenzake walitukanwa, waliteswa, na kupatishwa haya. Yeye aliandika hivi: ‘Tumekuwa kama takataka ya ulimwengu, uchafu wa vitu vyote, mupaka sasa.’​—1 Kor. 4:11-13.

10. Sababu gani labda watu walifikiri kama Paulo alipoteza bahati yake ya kufanikiwa?

10 Paulo aliyekuwa akiitwa Saulo alipokuwa kijana, alikuwa na bahati ya kuwa mutu wa maana sana. Alizaliwa katika familia iliyoonekana kuwa yenye kufanikiwa sana na alifundishwa na Gamalieli, mwalimu aliyeheshimiwa sana. Baadaye Paulo aliandika hivi: “Nilikuwa nikifanya maendeleo makubwa zaidi katika dini ya Kiyahudi kuliko watu wengi wa umri wangu.” (Gal. 1:14) Saulo alikuwa na mapendeleo na haki ya kufanya mambo mengi sababu alijua vizuri Kiebrania na Kigiriki na alikuwa na uraia wa Roma, mambo ambayo watu wengi wangependa kupata wakati huo. Ikiwa angependa kufanikiwa katika ulimwengu, labda angepata mali nyingi na angekuwa mutu mwenye kuheshimiwa sana. Lakini, alichagua kuishi maisha ambayo watu wengine, labda hata wengine kati ya watu wa jamaa yake, waliona kuwa ya upumbavu sana. Sababu gani alifanya hivyo?

11. Mutume Paulo alisamini mambo gani na alikuwa na muradi gani? Na sababu gani?

11 Mutume Paulo alimupenda Yehova na alitaka kukubaliwa naye kuliko kuwa na mali na kujulikana sana. Kisha kujifunza kweli, yeye alianza kusamini mambo ambayo watu wengi katika ulimwengu wanazarau; mambo kama vile zabihu ya ukombozi, kazi ya kuhubiri, na tumaini la kuishi mbinguni. Alijua yale Shetani aliwahi kusema; kwamba anaweza kugeuza wanadamu ili wasimutumikie Mungu. (Ayu. 1:9-11; 2:3-5) Kwa hiyo, muradi wake ulikuwa ule wa kuendelea kumuabudu Mungu wa kweli kwa uaminifu, na kuendelea kuvumilia hata kutokee majaribu ya namna gani. Huo ni muradi ambao watu wengi katika ulimwengu wanaotaka kufanikiwa ao kubarikiwa katika maisha hawana.

12. Sababu gani umeamua kumutumainia Mungu?

12 Je, una miradi kama ile ya mutume Paulo? Si rahisi kubaki mwaminifu kila siku. Hata hivyo, tunajua kwamba tukibaki waaminifu kwa Yehova, yeye atapendezwa nasi na atatubariki, na hapo ndipo tunaweza kusema kwamba tumefanikiwa kabisa katika maisha. (Met. 10:22) Tunapata baraka nyingi sasa, na tuko hakika kwamba baraka nyingi zaidi zinatungojea wakati ujao. (Soma Marko 10:29, 30.) Kwa hiyo, tuna sababu nyingi zinazotuchochea kuweka tumaini letu si “katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa uwingi ili tuvifurahie.” Tukifanya hivyo, ‘tunajiwekea wenyewe kwa usalama hazina ya musingi muzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili tuushike imara uzima ulio wa kweli.’ (1 Tim. 6:17-19) Kwa kweli, hata kisha miaka mia moja, elfu moja na kuendelea, tutaweza kuangalia nyuma na kusema: “Nilifanikiwa kabisa katika maisha yangu!”

HAZINA YAKO IKO WAPI?

13. Ni shauri gani Yesu alitoa kuhusu kujiwekea hazina?

13 Yesu alisema hivi kuhusu hazina: “Acheni kujiwekea hazina duniani, ambako nondo na kutu hula, na ambako wezi huvunja na kuiba. Badala yake, jiwekeeni hazina mbinguni, ambako nondo na kutu havili, na ambako wezi hawavunji na kuiba. Kwa maana mahali ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.”​—Mt. 6:19-21.

14. Sababu gani si jambo la hekima kujiwekea hazina duniani?

14 Hazina ambayo mutu anaweza kujiwekea duniani inaweza kumaanisha mambo mengi kuliko tu feza. Inaweza kumaanisha moja ya mambo ambayo Sulemani aliandika na ambayo watu wanasamini sana katika ulimwengu huu, kama vile kujulikana sana, sifa ao uwezo. Maneno ya Yesu yanafanana na yale ambayo Sulemani alisema katika kitabu cha Mhubiri, ni kusema, hazina ambazo watu wanajiwekea duniani ni za muda. Labda umekwisha kujionea kwamba hazina ambazo watu wanajiwekea duniani zinaweza kuharibika na kupotea kwa urahisi. Kuhusu hazina hizo, Profesere Dale Bruner aliandika hivi: “Kujulikana sana ni jambo lisilodumu. Mutu anaweza kujulikana sana leo lakini kesho wanamusahau. Mutu fulani anaweza kupata feza nyingi leo, lakini anaweza kuzipoteza zote kesho. Kwa sababu [Yesu] anawapenda wanadamu, anawaonya kuhusu utukufu unaoweza kupotea haraka na kuwaacha bila tumaini. Haudumu! Kila siku watu wanaotumaini feza na kutafuta sifa wanavunjika moyo, na Yesu hapende wanafunzi wake wavunjike moyo.” Watu wengi watakubaliana na Profesere huyo, lakini, ni wangapi ambao wanatenda kulingana na maneno hayo? Je, wewe utayakubali na kutenda hivyo?

15. Tunapaswa kujikaza tufanikiwe katika jambo gani?

15 Viongozi fulani wa dini wamefundisha kwamba si lazima kufanya nguvu ili kufanikiwa katika maisha. Lakini, Yesu katika maneno yake hakusema kwamba hatupaswe kujikaza ili tufanikiwe. Aliyotaka kusema ni kwamba wanafunzi wake wanapaswa kujikaza wafanikiwe katika mambo yanayostahili; aliwatia moyo wajiwekee “hazina mbinguni,” hazina zitakazodumu milele. Tamaa yetu kubwa ni kujikaza ili tufanikiwe kulingana na maoni ya Yehova. Kwa kweli, maneno ya Yesu yanatukumbusha kwamba kila mutu anapaswa kuchagua jambo ambalo anapaswa kufuatilia katika maisha. Ukweli ni kwamba, kile kilicho katika moyo wetu, ao kitu tunachosamini sana, ndicho kitu tunachopaswa kujikaza kupata katika maisha.

16. Tunapaswa kuwa na uhakika gani?

16 Ikiwa katika moyo wetu tuna tamaa kabisa ya kumupendeza Yehova, tunapaswa kuwa hakika kwamba atatupatia mambo tunayohitaji. Labda wakati fulani anaweza kuruhusu tukose chakula na kinywaji kwa muda fulani, kama ilivyokuwa kwa mutume Paulo. (1 Kor. 4:11) Hata hivyo, tunapaswa kufuata shauri hili la hekima la Yesu: “Musihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ ao, ‘Tutakunywa nini?’ ao, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua munahitaji vitu hivi vyote. Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mutaongezewa hivi vitu vingine vyote.”​—Mt. 6:31-33.

KUFANIKIWA MACHONI PA MUNGU

17, 18. (a) Kufanikiwa katika maisha hakutegemee nini? (b) Kufanikiwa kwa kweli kunategemea nini?

17 Usisahau jambo hili: Kuwa mwenye kufanikiwa ao kubarikiwa kabisa katika maisha hakutegemee mambo makubwa ambayo tumefanya ao cheo tulicho nacho katika ulimwengu. Pia, hakutegemee madaraka tuliyo nayo katika kutaniko la Kikristo. Kufanikiwa kunategemea utii na uaminifu wetu kwa Mungu. Mungu anatuambia hivi: ‘Kinachoangaliwa katika wasimamizi​-nyumba ni mutu kupatwa akiwa mwaminifu.’ (1 Kor. 4:2) Kwa hiyo, tunapaswa kuendelea kuwa waaminifu. Yesu alisema hivi: ‘Yule atakayevumilia mupaka mwisho ndiye atakayeokolewa.’ (Mt. 10:22) Waaminifu watakapookolewa, hilo litaonyesha waziwazi kwamba walifanikiwa katika maisha yao, sivyo?

18 Habari hii inatufundisha kwamba kuwa mwaminifu kwa Mungu hakutegemee kujulikana sana, kusoma sana, ao kuwa na mali nyingi. Hakutegemee akili ya mutu, uwezo wake mbalimbali ao hali yake ya maisha. Kwa hiyo, kila mumoja wetu anaweza kuwa mwaminifu kwa Mungu hata ikiwa hali yake iko namna gani. Wakati wa mitume, Wakristo fulani walikuwa matajiri, wengine walikuwa maskini. Mutume Paulo aliwashauri Wakristo waliokuwa matajiri “wafanye mema, wawe matajiri katika matendo mazuri, wawe wakarimu, tayari kushiriki.” Kwa hiyo, Wakristo, iwe matajiri ao maskini wangeweza ‘kuushika imara uzima ulio wa kweli.’ (1 Tim. 6:17-19) Ni vilevile leo pia, sisi wote, tuwe matajiri ao maskini, tumepewa nafasi na daraka la kuwa waaminifu na kuwa “matajiri katika matendo mazuri.” Tukiwa hivyo, tutaonekana machoni pa Muumbaji wetu kuwa watu waliofanikiwa na tutakuwa na furaha ya kujua kwamba tunaufurahisha moyo wake.​—Met. 27:11.

19. Utafanya nini ili uwe mwenye kufanikiwa kabisa?

19 Hauweze kubadilisha kabisa namna watu wa ulimwengu wanavyokuona, lakini unaweza kubadilisha namna unavyoona hali yako. Ujikaze kuwa mwaminifu hata hali yako iwe namna gani. Si kazi ya bure. Uwe hakika kwamba Yehova atakubariki kuanzia sasa na milele. Usisahau hata kidogo maneno ambayo Yesu aliwaambia Wakristo watiwa​-mafuta: “Uwe mwaminifu hata kufikia kifo, nami nitakupa taji la uzima.” (Ufu. 2:10) Hiyo ndiyo maana ya kufanikiwa ao kubarikiwa kweli kweli!

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 6]

Watu wengi walifikiri kwamba Saulo alikuwa na bahati ya kufanikiwa katika ulimwengu

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mutume Paulo alifanikiwa kabisa