Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tuendelee Kuishi Kama “Wakaaji wa Muda”

Tuendelee Kuishi Kama “Wakaaji wa Muda”

Tuendelee Kuishi Kama “Wakaaji wa Muda”

‘Nawahimiza ninyi kama wageni na wakaaji wa muda kwamba muendelee kujiepusha na tamaa za kimwili.’​—1 PET. 2:11.

UNGEJIBU NAMNA GANI?

Sababu gani Wakristo watiwa-mafuta wanaweza kuitwa wakaaji wa muda?

Ni katika maana gani “kondoo wengine” ni wakaaji wa muda?

Ni jambo gani unalongojea kwa hamu wakati ujao?

1, 2. “Wale waliochaguliwa” ambao mutume Petro alizungumuzia ni watu gani na sababu gani alisema wao ni “wakaaji wa muda”?

 MIAKA 30 hivi kisha Yesu kupanda mbinguni, mutume Petro aliandikia ‘wakaaji wa muda waliotawanyika huku na huku katika Ponto, Galatia, Kapadokia, Asia, na Bithinia, wale waliochaguliwa.’ (1 Pet. 1:1) Kwa kweli, kwa kutumia maneno “wale waliochaguliwa,” Petro alizungumuzia wale waliokuwa wametiwa mafuta kwa roho takatifu kama yeye na waliokuwa ‘wamezaliwa upya’ ili kutawala na Kristo mbinguni. (Soma 1 Petro 1:3, 4.) Lakini sababu gani aliwaita wachaguliwa hao “wageni na wakaaji wa muda”? (1 Pet. 2:11) Leo duniani pote kati ya Mashahidi 650, utakuta mumoja tu ndiye anayejidai kuwa mutiwa​-mafuta, kwa hiyo, je, maneno hayo yana maana yoyote kwetu leo?

2 Wakristo wa siku za mitume walistahili kabisa kuitwa “wakaaji wa muda” kwa sababu hawangeendelea kuishi duniani. Ni vilevile kuhusu Wakristo watiwa​-mafuta leo. Mutume Paulo, aliye wa “kundi dogo” la watiwa​-mafuta alieleza hivi: ‘Lakini sisi, uraia wetu uko mbinguni, ambako kutoka huko pia tunamungojea mwokozi kwa hamu, Bwana Yesu Kristo.’ (Lu. 12:32; Flp. 3:20) Kwa kuwa ‘uraia [wao] uko mbinguni,’ watiwa-mafuta wanapokufa wanaacha maisha ya duniani ili kupata kitu kizuri sana, ni kusema, maisha ya kutoweza kufa huko mbinguni. (Soma Wafilipi 1:21-23.) Kwa hiyo, wanastahili kabisa kuitwa ‘wakaaji wa muda’ katika dunia hii inayoongozwa na Shetani.

3. Tunaweza kujiuliza ulizo gani kuhusu “kondoo wengine”?

3 Lakini namna gani “kondoo wengine”? (Yoh. 10:16) Kulingana na Biblia wana tumaini nzuri la kuwa wakaaji wa milele wa dunia hii. Hakuna shaka, dunia hii itakuwa makao yao milele! Hata hivyo, katika maana fulani wao pia wanaweza kuonwa kuwa wakaaji wa muda. Namna gani?

“UUMBAJI WOTE UNAENDELEA KUUGUA”

4. Viongozi wa dunia hawaweze kumaliza nini?

4 Kadiri Yehova atakavyoruhusu ulimwengu huu wa Shetani kuendelea kuwa, kila mutu, kutia na Wakristo wataendelea kuteseka kwa sababu ya uasi ambao Shetani alitokeza juu ya Yehova. Andiko la Waroma 8:22 linasema hivi: ‘Tunajua kwamba uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja mupaka sasa.’ Hata ikiwa viongozi wa dunia, wanasayansi, na wale wanaotolea watu wanaoteseka misaada wana nia nzuri, hawaweze kumaliza matatizo ya wanadamu.

5. Kuanzia mwaka wa 1914, mamilioni ya watu wamechukua hatua gani, na sababu gani?

5 Kwa hiyo, kuanzia mwaka wa 1914, mamilioni ya watu wamechagua kwa kujipendea kuwa raia wa mufalme aliyesimamishwa na Mungu, Kristo Yesu. Hawatake hata kidogo kuwa sehemu ya ulimwengu wa Shetani na wanakataa kuutegemeza. Lakini, wanatumia maisha yao na uwezo wao mbalimbali ili kuunga mukono Ufalme wa Mungu, na kutumikia faida za Ufalme huo.​—Rom. 14:7, 8.

6. Mashahidi wa Yehova ni wakaaji wageni katika maana gani?

6 Kwa kweli, katika inchi zaidi ya 200 wanamoishi, Mashahidi wa Yehova wanajulikana kuwa wanainchi wazuri kabisa, wanaotii sheria. Hata hivyo, wanaishi kama wageni mahali popote ambako wanapatikana. Mashahidi hawajiingize hata kidogo katika mambo ya politike ao kujiunga na watu wanaotetea haki za raia. Kuanzia sasa, wanajua kwamba wao ni raia wa ulimwengu mupya utakaoletwa na Mungu. Wanafurahi kujua kwamba karibuni siku zao za kuishi kama wakaaji wa muda katika ulimwengu huu muovu zitakwisha.

7. Ni nini itafanyika ili watumishi wa Mungu wawe wakaaji wa kudumu, na watakaa wapi?

7 Karibuni Yesu atatumia mamlaka yake ili kuharibu ulimwengu huu muovu wa Shetani. Serikali kamilifu ya Yesu itaondoa zambi na mateso katika dunia. Serikali hiyo itaharibu wote, viumbe vyenye kuonekana ao visivyoonekana, vinavyopinga haki ya Yehova ya kuwa Mutawala Mukubwa wa Ulimwengu. Ndipo watumishi wa Mungu waaminifu watakuwa wakaaji wa kudumu wa dunia itakayokuwa Paradiso. (Soma Ufunuo 21:1-5.) Sasa katika maana kamili, uumbaji ‘utawekwa huru kabisa kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.’​—Rom. 8:21.

WAKRISTO WA KWELI WANAPASWA KUFANYA NINI?

8, 9. Petro alimaanisha nini aliposema kama tunapaswa “kujiepusha na tamaa za mwili”?

8 Mutume Petro alieleza mambo ambayo Wakristo wanapaswa kufanya aliposema hivi: ‘Wapendwa, nawahimiza ninyi kama wageni na wakaaji wa muda kwamba muendelee kujiepusha na tamaa za mwili, ambazo ndizo huendelea kupambana na nafsi.’ (1 Pet. 2:11) Wakati Petro aliandika mashauri hayo, aliwaandikia kwanza Wakristo watiwa-mafuta, lakini yanafaa pia kwa kondoo wengine wa Yesu.

9 Si vibaya kutosheleza tamaa fulani za mwili ikiwa tunafanya namna Muumbaji wetu alivyokusudia. Kwa kweli, tamaa hizo zinafanya tufurahie maisha zaidi. Kwa mufano, kula chakula kizuri na kunywa kinywaji kizuri, kujiburudisha na kufurahia kupitisha wakati muzuri pamoja na marafiki ni tamaa za kimwili za kawaida ambazo mutu anaweza kufurahia. Vilevile ni jambo la kawaida na si zambi kwa bibi na bwana kufurahia kitendo cha ndoa. (1 Kor. 7:3-5) Lakini, tamaa za mwili ambazo Petro alizungumuzia ni zile ‘tamaa za mwili zinazoendelea kupambana na nafsi.’ Tafsiri fulani ya Biblia inaziita “tamaa mbaya” (Verbum Bible). Kwa hiyo, tunapaswa kuzuia tamaa yoyote ya mwili isiyopatana na mapenzi ya Yehova na inayoweza kuharibu urafiki wetu pamoja na Yehova. Mukristo asipofanya hivyo anaweza kupoteza tumaini lake la uzima wa milele.

10. Ni mitego gani fulani ambayo Shetani anatumia ili kufanya Wakristo wawe sehemu ya ulimwengu?

10 Kusudi la Shetani ni kuregeza musimamo wa Wakristo wa kweli wa kuendelea kuishi kama “wakaaji wa muda.” Shetani anatumia mitego kama vile uvutio wa vitu vya kimwili, kushawishiwa kufanya uasherati, tamaa ya kutaka kujulikana na kuwa mutu wa maana katika ulimwengu, kutaka kuwa wa kwanza katika kila jambo, na mutu kuchochewa kupenda sana inchi yake. Tunapoamua kujiepusha na tamaa hizo mbaya za mwili, tunaonyesha wazi kwamba hatutake kuwa sehemu ya ulimwengu huu muovu wa Shetani. Kwa kufanya hivyo, tunaonyesha wazi kwamba sisi ni wakaaji wa muda wa ulimwengu huu. Kuwa wakaaji wa kudumu katika ulimwengu mupya na wenye haki wa Mungu ndilo jambo tunalotamani sana na tunafanya yote ili kulifikia.

MWENENDO MUZURI

11, 12. Kwa kawaida watu wanawaona wageni namna gani, na watu wanaweza kufikiri nini juu ya Mashahidi wa Yehova?

11 Mutume Petro anaendelea kuzungumuzia jambo ambalo Wakristo walio “wakaaji wa muda,” wanaombwa kufanya. Kwenye mustari wa 12 anasema hivi: ‘Dumisheni mwenendo wenu ukiwa muzuri katikati ya mataifa, ili, katika jambo ambalo wanasema juu yenu ya kuwa ninyi ni watenda​-maovu, waweze, likiwa tokeo la matendo yenu mazuri ambayo wameshuhudia kwa macho, kumutukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.’ Kwa kawaida, watu wanawachambua wageni ao watu wanaoishi kwa muda katika inchi isiyokuwa yao. Kwa kwa sababu tu wageni wanaishi kwa njia iliyo tofauti, wenyeji wanaweza kuanza kusema kama wageni hao ni watu wabaya. Usemi wao, matendo yao, namna wanavyovalia na labda hata namna wanavyoonekana vinaweza labda kuachana kwa njia fulani na hali ya wenyeji. Lakini wakati wanafanya kazi nzuri, ni kusema, wakati mwenendo wao ni muzuri, kuwasema vibaya huko hakutakuwa na musingi wowote.

12 Vilevile Wakristo wanatofautiana na majirani wao katika njia fulani kama vile katika usemi ao namna yao ya kijifurahisha. Kila mara wanavalia na kujipamba kwa njia iliyo tofauti na ile ya majirani wao. Kwa sababu ya tofauti hizo, watu fulani wasiowajua vizuri wanaweza kusema kama wao ni watu wabaya. Lakini, wengine wanaweza kuwasifu kwa sababu ya namna yao ya kuishi.

13, 14. “Hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake” namna gani? Toa mifano.

13 Kwa kweli, mwenendo wetu muzuri unaweza kufanya wengine waache kutuchambua bila sababu. Lakini usisahau kwamba hata Yesu, aliyekuwa mwaminifu kwa Mungu kuliko wanadamu wote, alisemwa vibaya. Watu fulani walimuita ‘mulafi na mwenye mazoea ya kunywa divai, rafiki ya wakusanya-kodi na watenda-zambi.’ Hata hivyo, mwenendo wake muzuri ulionyesha kama yale waliyokuwa wakisema yalikuwa uongo. Yesu alisema kwamba “hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake.” (Mt. 11:19) Ndivyo ilivyo leo. Kwa mufano, watu wanaoishi karibu na Beteli ya Selters, huko Alemanye, wanawaona ndugu na dada wanaotumika kwenye Beteli kuwa watu tofauti, ni kusema hawawaelewe. Lakini kiongozi wa muji huo aliwatetea aliposema hivi: “Mashahidi wanaotumika hapo wana namna yao ya kuishi, lakini hawavuruge amani ya wengine.”

14 Maneno ya namna hiyo yalisemwa pia kuhusu Mashahidi wa Yehova wanaoishi Moscow, katika inchi ya Russie. Watu waliwasingizia mambo mengi. Lakini Mwezi wa 6, 2010, Tribinale Kubwa ya Ulaya ya Haki za Wanadamu ya huko Strasbourg, France, iliamua hivi: “Tribinale inaona kwamba wakubwa wa muji wa Moscow walivunja haki ya kidini na ya kukusanyika ya Mashahidi wa Yehova. Tribinale za Moscow hazikutoa sababu za ‘kweli na za kutosha’ zinazoonyesha kwamba Mashahidi” walivunja ndoa za watu, waliwatia moyo mashahidi wenzao wajiue, ao walikataa matunzo ya waganga. Kwa hiyo, “uamuzi wa tribinale zao ulikuwa mukali sana, usiobadilika kulingana na hali na usiolingana na kusudi ambalo tribinale ilikuwa ikifuatia.”

KUJITIISHA KWA NJIA INAYOFAA

15. Wakristo wa kweli ulimwenguni pote wanafuata kanuni gani ya Biblia?

15 Mashahidi wa Yehova katika Moscow na duniani pote wanatii amri ingine ambayo Petro alizungumuzia. Yeye aliandika hivi: ‘Kwa ajili ya Bwana, jitiisheni wenyewe kwa kila kitu kilichofanywa na binadamu: iwe ni kwa mufalme akiwa mukubwa ao ni kwa magavana.’ (1 Pet. 2:13, 14) Wakristo wa kweli si sehemu ya ulimwengu, hata hivyo wako tayari kutii mamlaka zilizo “katika vyeo vyao vya kadiri,” kama vile mutume Paulo alivyowaagiza.​—Soma Waroma 13:1, 5-7.

16, 17. (a) Ni mambo gani yanayoonyesha kwamba hatupinge serikali ao guvernema ya inchi tunamoishi? (b) Viongozi fulani wa serikali wametambua nini kuhusu Mashahidi wa Yehova?

16 Mashahidi wa Yehova wanajiendesha kama “wakaaji wa muda” katika ulimwengu huu, hata hivyo hawafanye hivyo ili kuipinga serikali ao guvernema fulani kisirisiri; wala hawawakataze wengine kuamua kujiingiza katika mambo yao ya politike na namna yao ya kutatua matatizo ya maisha. Tofauti na dini zingine, Mashahidi wa Yehova hawajiingize katika mambo ya politike. Hawajaribu hata kidogo kuwasukuma viongozi wa serikali watawale hivi ao hivi. Kwa hiyo, kusema kwamba Mashahidi wa Yehova wanajaribu kuwavuruga watu ao kwamba wanachochea watu waipinge serikali ao guvernema ni wazo lisilo la kweli!

17 Mutume Petro aliwashauri Wakristo ‘waheshimu wafalme.’ Wakristo wanapotii shauri hilo wanaonyesha kwamba wanawaheshimu wakubwa wa serikali kulingana na cheo chao. (1 Pet. 2:17) Wakati fulani, viongozi wa serikali wametambua kama hawana sababu yoyote ya kuwashakia Mashahidi wa Yehova. Kwa mufano, Steffen Reiche, aliyekuwa ministre katika serikali ya muji wa Brandenburg na aliyekuwa katika parlema ya Alemanye alisema hivi: “Mashahidi wa Yehova katika kambi za mateso na magereza walionyesha sifa ambazo ni za lazima sana leo na wakati uliopita, ili inchi iwe kabisa ya kidemokrasia: kwa mufano, hawakubadili maoni yao walipoteswa na maaskari wa SS na waliwasaidia wafungwa wenzao. Sifa hizo ni za maana sana kwa kila mwanainchi wa inchi yetu kwa sababu watu wengi wameanza kuwatesa wageni na wale walio na imani ao mawazo ya politike yaliyo tofauti na yao.”

KUONYESHA UPENDO

18. (a) Sababu gani si jambo la kushangaza ikiwa tunapenda ushirika wote wa ndugu na dada? (b) Watu wasiokuwa Mashahidi wamejionea nini?

18 Mutume Petro aliandika hivi: ‘Upendeni ushirika muzima wa akina ndugu, muogopeni Mungu.’ (1 Pet. 2:17) Mashahidi wa Yehova wanaogopa kumuchukiza Mungu, na jambo hilo linawachochea kufanya mapenzi yake. Wanafurahi kuwa na umoja na ndugu na dada zao duniani pote walio na tamaa ile ile ya kumutumikia Mungu. Kwa hiyo, si jambo la kushangaza ikiwa ‘wanapenda ushirika muzima wa akina ndugu.’ Kwa sababu upendo wa kindugu unakosekana sana katika dunia hii inayojaa watu wenye kujipenda wenyewe, watu wanashangaa sana kuona namna Mashahidi wa Yehova wanavyopendana. Kwa mufano, kwenye mukusanyiko wa kimataifa wa mwaka wa 2009 huko Alemanye, mufanyakazi mumoja mwanamuke anayewatembeza wageni na anayetumika katika Kompanyi moja ya Amerika ya kusafirisha watu alishangaa kuona namna Mashahidi wa Alemanye walionyesha Mashahidi waliotoka katika inchi mbalimbali upendo na namna walivyowatolea musaada. Yeye alisema kwamba tangu wakati alipoanza kuwatembeza watu hajaona jambo kama hilo. Baadaye, Shahidi mwengine alisema hivi: “Kila jambo alilokuwa akisema juu yetu, alikuwa akilisema kwa furaha na mushangao.” Je, umekwisha kusikia watu wakisema hivyo kuhusu mukusanyiko fulani ambao umehuzuria?

19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini, na sababu gani?

19 Mambo ambayo tumezungumuzia na mengine yanaonyesha kwelikweli kwamba Mashahidi wa Yehova ni “wakaaji wa muda” katika ulimwengu huu wa Shetani. Na wanaazimia kwa furaha kuendelea kuishi kama wakaaji wa muda. Wana tumaini lenye nguvu na pia wana sababu nyingi za kutumaini kwamba karibuni watakuwa wakaaji wa kudumu wa ulimwengu mupya wa Mungu wenye uadilifu. Je, unangojea kwa hamu ulimwengu huo mupya?

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 20]

Hatutafute kuuokoa ulimwengu wa Shetani

[Picha katika ukurasa wa 20]

Tunatetea ulimwengu mupya wa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 22]

Ukweli wa Biblia umesaidia kuunganisha familia hii ya Russie