Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Walinzi wa Mufalme Wanatolewa Ushahidi

Walinzi wa Mufalme Wanatolewa Ushahidi

Tuko katika mwaka wa 59. Wafungwa wanaolindwa na askari ambao wamechoka wanaingia katika muji wa Roma kupitia mulango wa Porta Capena. Makao ya Nero, mutawala wa Roma, yanapatikana juu ya Mulima Palatine, na yanachungwa na askari walio na panga zao katika mavazi yao ya kiaskari. * Mukubwa wa kikundi cha askari 100 anayeitwa Yulio anawapitisha wafungwa wake mbele ya Baraza Kubwa la Roma kuelekea Mulima Vinimal. Wanapita katika bustani yenye mazabahu mengi kwa ajili ya miungu ya Waroma na wanapita pia mahali ambapo askari wanazoea kufanya maonyesho ya kiaskari.

Muchoro wa Walinzi ambao labda ulitoka kwenye Arc de Claude iliyojengwa katika mwaka wa 51

Mutume Paulo alikuwa mumoja wa wafungwa hao. Miezi fulani mbele ya hapo, wakati alikuwa katika mashua iliyopelekwa huku na huku na zoruba kali, malaika wa Mungu alimuambia hivi: “Utasimama mbele ya Kaisari.” (Mdo. 27:24) Je, Paulo anakaribia kufanya hivyo? Anapofika katika muji mukubwa wa Waroma, bila shaka Paulo anakumbuka maneno ambayo Bwana Yesu alimuambia kwenye Munara wa Antonia. Yesu alimuambia hivi: “Jipe moyo! Kwa maana kama vile ambavyo umekuwa ukitoa ushahidi kamili katika Yerusalemu juu ya mambo yanayonihusu, vivyo hivyo utatoa ushahidi katika Roma pia.”​—Mdo. 23:10, 11.

Labda Paulo alisimama kidogo ili kutazama Kambi ya Walinzi wa Mufalme, ngome kubwa iliyokuwa na kuta zilizojengwa kwa matofali mekundu na iliyokuwa na minara. Ngome hiyo ilikuwa makao ya Walinzi wa Mufalme na pia polisi wa muji waliokuwa wakilinda muji. Walinzi zaidi ya 12 000 wa Mufalme na polisi wengi wa muji, maelfu ya askari wengine, kama vile askari wapanda-farasi walikuwa wakiishi katika ngome hiyo. Ngome hiyo ya Walinzi wa Mufalme inaonyesha kwamba Mufalme alikuwa na uwezo mukubwa sana. Kwa kuwa Walinzi wa Mufalme ndio wanaowalinda wafungwa wanaotoka katika majimbo, ndio sababu, Yulio anapitisha kikundi cha wafungwa wake katika moja ya milango ine ya muji. Kisha kusafiri kwa shida kwa miezi mingi, mwishowe amewafikisha wafungwa wake mahali walipokuwa wakienda.​—Mdo. 27:1-3, 43, 44.

MUTUME PAULO ANAHUBIRI “BILA KIZUIZI”

Wakati wa safari, mutume Paulo aliambiwa katika maono kwamba mashua itavunjika, lakini watu wote waliokuwa katika mashua wangeokolewa. Aliumwa na nyoka mwenye sumu, lakini hakupata shida yoyote. Aliponyesha wagonjwa katika kisiwa cha Malta, na watu wa kisiwa hicho walianza kusema kwamba yeye alikuwa mungu. Labda Walinzi wa Mufalme walioamini mambo ya uchawi walisikia habari hizo.

Mutume Paulo alikuwa tayari ameonana na ndugu wa Roma ‘waliokuja kukutana naye kwenye Soko la Apio na Mikahawa Mitatu.’ (Mdo. 28:15) Hata ikiwa yeye ni mufungwa, namna gani atatimiza tamaa yake ya kuhubiri habari njema katika muji wa Roma? (Rom. 1:14, 15) Watu fulani wanafikiri kama wafungwa walitiwa katika mikono ya mukubwa wa walinzi. Ikiwa ni hivyo, labda mutume Paulo alipelekwa kwa Afranius Burrus, mukubwa wa walinzi aliyekuwa wa pili katika utawala wa Mufalme. * Kwa vyovyote, kuliko kulindwa na wakubwa wa vikundi vya askari, Paulo analindwa sasa na mulinzi wa kawaida wa Mufalme. Anaruhusiwa kuishi katika nyumba yake mwenyewe na kupokea wageni na kuwahubiria “bila kizuizi.”​—Mdo. 28:16, 30, 31.

MUTUME PAULO ANAWAHUBIRIA WADOGO NA WAKUBWA

Mutume Paulo alipokuwa katika gereza, askari walimusikia akiandikisha barua alizotumia makutaniko

Alipokuwa akiwahukumu watu, labda Burrus alimuuliza mutume Paulo maulizo, kwenye Kambi ya Walinzi ao kwenye makao ya Mufalme mbele ya kumupeleka mbele ya Mufalme Nero. Mutume Paulo alitumia nafasi hiyo ya pekee ili “kutoa ushahidi kwa wadogo na wakubwa.” (Mdo. 26:19-23) Hatujue Burrus aliona mambo namna gani, lakini Paulo hakutiwa katika gereza lililokuwa katika kambi ya Walinzi. *

Nyumba ambayo Paulo alipangia ilikuwa kubwa, kwa hiyo alikaribisha na kutolea ushahidi ‘wakubwa wa Wayahudi’ na ‘hesabu kubwa ya watu waliokuja katika makao yake.’ Askari walinzi wa Mufalme pia walimusikiliza mutume Paulo alipokuwa ‘akitoa ushahidi’ juu ya Ufalme na Yesu ‘tangu asubuhi mupaka mangaribi.’​—Mdo. 28:17, 23.

Kuta za Kambi ya Walinzi wa Mufalme namna zinavyoonekana leo

Kila siku pa saa munane ya muchana, kikundi cha askari wanaolinda makao ya Mufalme kilibadilishwa. Askari waliomulinda Paulo walibadilishwa pia kwa ukawaida. Kwa muda wa miaka miwili ambayo mutume Paulo alikuwa mufungwa, askari walimusikia akiandikisha barua (labda kupitia mutu fulani ao mwandishi). Barua hizo zilitumwa kwa makutaniko ya Efeso, Filipi, na Wakristo Waebrania. Askari hao walimuona pia akiandika yeye mwenyewe barua kwa Filemoni. Alipokuwa katika gereza, Paulo alimuhangaikia Onesimo, mutumwa aliyetoroka, ‘aliyemuzaa alipokuwa katika vifungo vyake vya gereza,’ na alimutuma kwa bwana wake. (Flm. 10) Bila shaka, mutume Paulo aliwahubiria pia askari waliomulinda. (1 Kor. 9:22) Tunaweza kuwazia namna mutume Paulo anavyouliza askari kuhusu kusudi la kila silaha ambayo askari Waroma alivalia na kisha anatumia habari alizopewa katika mufano muzuri unaopatikana katika kitabu cha Waefeso.​—Efe. 6:13-17.

“KULISEMA NENO LA MUNGU BILA WOGA”

Kufungwa kwa Paulo kulisaidia “kuendeleza mbele habari njema” katikati ya Walinzi wa Mufalme na wengine. (Flp. 1:12, 13) Vikundi vya walinzi wa Mufalme vilivyokuwa katika kambi vilipashana habari katika Utawala wote wa Roma na vilishirikiana pia na nyumba ya mufalme na jamaa yake kubwa. Nyumba ya mufalme ilitia ndani watu wa jamaa yake, watumishi, na watumwa, ambao wengine kati yao walikuwa Wakristo. (Flp. 4:22) Ujasiri wa mutume Paulo katika kuhubiri uliwatia moyo ndugu wa Roma ‘waliseme neno la Mungu bila woga.’​—Flp. 1:14.

Katika hali yoyote, tunaweza kuhubiria wale wanaotushugulikia katika njia mbalimbali

Mahubiri ya mutume Paulo katika Roma yanatutia moyo sisi pia ‘tunapohubiri neno katika wakati unaofaa na katika wakati wa taabu.’ (2 Tim. 4:2) Kati yetu kuna wale ambao hawaweze kutoka nyumbani, wengine wako katika nyumba za watu wazee, ao katika hospitali na wengine hata wamefungwa kwa sababu ya imani yao. Katika hali yoyote, tunaweza kuhubiria wale wanaokuja kututembelea, ao labda wale wanaotushugulikia katika njia mbalimbali. Tunapotumia kila nafasi ili kuhubiri bila woga, tunajionea waziwazi kwamba ‘neno la Mungu halifungwe.’​—2 Tim. 2:8, 9.

^ Ona kisanduku “Walinzi wa Mufalme katika Siku za Nero.”

^ Ona kisanduku “Sextus Afranius Burrus.”

^ Katika mwaka wa 36/37 Kaisari Tiberio alimufunga Herode Agrippa hapo, kwa sababu Herode alionyesha kwamba alitamani Caligula awe mufalme. Caligula alipokuwa mufalme alimushukuru Herode na kumufanya kuwa mutawala.​—Mdo. 12:1.