Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Umekwisha ‘Kumujua Mungu’—Utafanya Nini Sasa?

Umekwisha ‘Kumujua Mungu’—Utafanya Nini Sasa?

‘Mumemujua Mungu.’​—GAL. 4:9.

1. Sababu gani pilote anapaswa kuchunguza mambo yote yaliyo kwenye liste yake mbele ya kuanza safari?

 PILOTE wanaoendesha avion za ajabu wana mambo zaidi ya 30 ya kuchunguza mbele ya kuanza safari. Ikiwa hawachunguze mambo hayo kwa uangalifu kila wakati mbele ya kuanza safari, wanaongeza uwezekano wa kufanya aksida. Unajua ni pilote gani hasa ambaye anaombwa kufanya uchunguzi huo kila wakati? Ni yule ambaye amezoea kazi hiyo! Ijapokuwa yeye ni mwenye uzoefu, anaweza kwa urahisi kupuuza uchunguzi huo ao kuufanya kijuu​-juu tu.

2. Wakristo wanaombwa kufanya uchunguzi gani?

2 Kama pilote mwenye kuhangaikia usalama wa watu, unaweza kutumia liste ya mambo yanayokusaidia kuchunguza hali yako ya kiroho ili uhakikishe kwamba imani yako itabaki yenye nguvu wakati wa majaribu. Iwe umebatizwa hivi karibuni ao umekwisha kumutumikia Yehova muda wa miaka mingi, ni jambo la lazima kuendelea kuchunguza kwa ukawaida imani yako na kuona ikiwa ungali mushikamanifu kwa Yehova Mungu. Kupuuza kufanya hivyo kwa ukawaida na kwa bidii kunaweza kuhatarisha hali yako ya kiroho. Biblia inatushauri hivi: ‘Yeye anayefikiri kuwa amesimama na ajihazari kwamba asianguke.’​—1 Kor. 10:12.

3. Wakristo wa Galatia walihitaji kufanya nini?

3 Wakristo wa huko Galatia walihitaji kuchunguza ikiwa imani yao ilikua yenye nguvu na kufurahia uhuru wao wa kiroho. Kupitia zabihu ya ukombozi ambayo Yesu alitoa, wote wanaomuamini wanaweza kuwa na pendeleo la kumujua Mungu katika njia ya pekee sana, ni kusema, kuwa watoto wake. (Gal. 4:9) Ili kuwa na pendeleo hilo, Wagalatia walipaswa kutupilia mbali mafundisho ya wafuasi wa dini ya Kiyahudi waliokaza watu washike Sheria ya Musa. Walipaswa kufanya hivyo, kwa sababu Wakristo Wasio Wayahudi ambao hawakutahiriwa waliokuwa katika makutaniko hawakuwahi hata siku moja kuwa chini ya Sheria hiyo. Kwa hiyo, Wayahudi na Wakristo Wasio Wayahudi, wote walihitaji kufanya maendeleo ya kiroho. Wakristo Wayahudi walipaswa kuelewa kwamba hawakupaswa kujiwekea haki yao wenyewe kupitia mupango wa Sheria ya Musa.

HATUA ZA KWANZA-KWANZA ILI KUMUJUA MUNGU

4, 5. Ni shauri gani mutume Paulo aliwatolea Wakristo wa Galatia, na kwa nini linatuhusu leo?

4 Shauri ambalo mutume Paulo aliwatolea Wagalatia liliandikwa katika Biblia kwa kusudi fulani: Kuzuia Wakristo wa kweli wasipuuze wakati wowote utajiri mwingi wa kweli ya Biblia na kurudilia mambo waliyoacha nyuma. Yehova alimuongoza mutume Paulo awatie moyo wale waliokuwa katika kutaniko la Galatia na pia waabudu wake wote ili wabaki imara.

5 Ni vizuri kila mumoja wetu akumbuke namna alivyokombolewa kutoka katika utumwa wa kiroho na kuwa Shahidi wa Yehova. Kwa hiyo, tunapaswa kujiuliza maulizo haya mawili: “Je, ninakumbuka hatua nilizofanya ili nistahili kubatizwa? Je, ninakumbuka namna nilivyofikia kumujua Mungu na kujulikana naye na hivyo kufurahia uhuru wa kweli wa kiroho?”

6. Tutazungumuzia nini?

6 Sisi wote tulifanya hatua kenda. Hatua hizo ambazo tunaweza kufananisha na liste ya mambo yanayotusaidia kuchunguza hali yetu ya kiroho, zinapatikana ndani ya kisanduku  “Hatua Zinazoongoza Kwenye Ubatizo na Zinazomusaidia Mukristo Aendelee Kukomaa.” Tunapojikumbusha kwa ukawaida hatua hizo kenda, hilo litatusaidia tuwe na nguvu ya kuepuka kurudilia tena mambo ya ulimwengu huu. Kama vile pilote ambaye amezoea sana kazi yake anavyoendelea kuchunguza mambo yaliyo kwenye liste yake mbele ya kuanza safari ili kuepuka aksida, wewe pia unapaswa kuendelea kuchunguza liste yako ya kiroho ili uendelee kumutumikia Mungu kwa uvumilivu.

WALE WANAOJULIKANA NA MUNGU WANAENDELEA KUKOMAA KIROHO

7. Tunapaswa kufuata kielelezo gani, na sababu gani?

7 Liste ya pilote inamukumbusha kama kuna mambo ya kuchunguza kwa ukawaida na kwa uangalifu mbele ya kuanza safari. Sisi pia tunapaswa kujichunguza kwa ukawaida na kuchunguza programe yetu ya kiroho tunayofuata tangu kubatizwa. Mutume Paulo alimuandikia Timotheo hivi: “Endelea kushika kielelezo cha maneno yenye afya uliyosikia kutoka kwangu pamoja na imani na upendo vinavyohusiana na Kristo Yesu.” (2 Tim. 1:13) “Maneno yenye afya” yanayopatikana katika Neno la Mungu. (1 Tim. 6:3) Kama vile mutu anayechonga sanamu anapaswa kufuata muchoro fulani, ‘kielelezo cha ile kweli’ kinatusaidia kuwa na maoni ya ujumla kuhusu namna tunavyoweza kufanya yale yanayomupendeza Yehova. Acheni tuzungumuzie sasa hatua zinazoongoza kwenye ubatizo na kuona namna tunavyofuata kwa ukaribu kielelezo cha ile kweli.

8, 9. (a) Sababu gani tunapaswa kuendelea kukomaa katika ujuzi na imani? (b) Toa mufano unaoonyesha kwamba ni jambo la lazima sana kukomaa kiroho na kwamba hilo ni jambo lenye kuendelea.

8 Jambo la kwanza kwenye liste yetu ni kuwa na ujuzi. Kisha tunaweza kukomalisha imani. Lakini tunapaswa kuendelea kukomaa katika mambo hayo mawili, ni kusema, kuendelea kujifunza na kukomalisha imani yetu. (2 Thes. 1:3) Kukomaa kunamaanisha kuendelea kufanya mabadiliko katika mambo mbalimbali; kunamaanisha kuongeza urefu ao ukubwa wa kitu. Kwa hiyo, kisha ubatizo tunapaswa kujikaza ili hali yetu ya kiroho iendelee kuongezeka wala si kupunguka.

Muti unaendelea kukomaa. Wakristo pia wanapaswa kuendelea kukomaa

9 Tunaweza kulinganisha ukomavu wetu wa kiroho na namna muti unavyokomaa. Muti unaweza kukomaa na kuwa na urefu wenye kushangaza, zaidi sana ikiwa mizizi yake inaingia sana katika udongo. Kwa mufano, miti fulani ya mierezi ya Lebanoni inaweza kufikia urefu wa metre 37 na kuwa na mizizi yenye kuingia sana katika udongo na shina lenye metre 12 muviringo. (Wim. 5:15) Kisha kufikia hatua hiyo muti huo unaendelea kukomaa lakini bila kuonekana waziwazi. Mwaka baada ya mwaka, shina la muti huo linaendelea kuwa kubwa na mizizi yake inaendelea kuingia ndani sana katika udongo na kufanya muti huo ukaze sana. Ni hivyo pia kuhusu ukomavu wa kiroho wa Mukristo. Tunaweza kukomaa haraka kiroho wakati tunaanza kujifunza Biblia mupaka tutakapofikia ubatizo. Ndugu na dada katika kutaniko wanafurahi kuona jinsi tunavyofanya maendeleo. Tunaweza hata kufikia kuwa mapainia na hata kufikia mapendeleo mengine. Katika miaka inayofuata, labda ukomavu wetu wa kiroho hautaonekana tena waziwazi. Hata hivyo, bado tunapaswa kuendelea kukomaa katika imani na ujuzi ‘kufikia kuwa watu waliokomaa, kufikia kipimo cha kimo ambacho ni cha ujazo wa Kristo.’ (Efe. 4:13) Kwa hiyo, kama vile muti unavyoanza kuota mupaka kufikia kuwa muti mukubwa, sisi pia tunapaswa kufanya maendeleo mupaka kufikia kuwa Wakristo wenye kukomaa kiroho.

10. Sababu gani hata Wakristo wenye kukomaa kiroho wanahitaji kufanya maendeleo?

10 Lakini kukomaa kwetu kiroho hakusimamie hapo. Ni lazima tuwe na ujuzi mwingi na imani iwe na mizizi. Tukifanya hivyo tutakuwa kama muti unaoingiza sana mizizi yake katika udongo, ni kusema, Neno la Mungu. (Met. 12:3) Katika kutaniko la Kikristo, kuna ndugu na dada wengi ambao wamefanya hivyo. Kwa mufano, ndugu mumoja ambaye amekuwa muzee wa kutaniko kwa miaka zaidi ya makumi tatu anatambua kama angali anafanya maendeleo ya kiroho. Anasema hivi: “Furaha yangu juu ya Biblia inaendelea kuongezeka sana. Ninaendelea kupata nafasi mupya ya kutumia kanuni na sheria za Biblia katika njia mbalimbali. Furaha yangu juu ya mahubiri inaendelea kuongezeka.”

KOMALISHA URAFIKI WAKO PAMOJA NA MUNGU

11. Inatuomba tufanye nini ili tufikie kumujua Yehova?

11 Kukomaa kunamaanisha pia kumukaribia Baba yetu na Rafiki yetu, Yehova. Anataka tujisikie kwamba anatukubali. Anataka tujue kwamba anatupenda na kutulinda kama vile mutoto anavyojisikia anapokumbatiwa na muzazi anayemupenda ao tunavyojisikia tunapokuwa pembeni ya rafiki wa kweli na mwaminifu. Kama unavyojua, urafiki wa namna hiyo pamoja na Yehova haufanyike kwa siku moja. Inachukua wakati ili kumujua na kumupenda Yehova. Kwa hiyo, ili kufikia kumujua Yehova vizuri, fanya yako yote ili uwe na wakati wa kusoma Neno lake kila siku. Na usome kila habari ya Munara wa Mulinzi na Amkeni! na vichapo vingine vyenye kutegemea Biblia.

12. Tunapaswa kufanya nini ili tujulikane na Yehova?

12 Sala zinazotoka moyoni zinaweza kusaidia marafiki wa Mungu wakomae kiroho, pia kuwa na marafiki wazuri kunaweza kutusaidia. (Soma Malaki 3:16.) ‘Masikio ya Yehova yanaelekea dua [ao kilio] yao.’ (1 Pet. 3:12) Kama muzazi mwenye upendo, Yehova anasikiliza kwa uangalifu tunapomulilia atusaidie. Kwa hiyo, tunapaswa ‘kudumu katika sala.’ (Rom. 12:12) Hatuweze kuwa Wakristo wenye kukomaa kiroho bila musaada kutoka kwa Yehova. Matatizo ya dunia hii ni mengi sana hivi kwamba si rahisi kuyashinda kwa nguvu zetu wenyewe. Ikiwa tunaacha kudumu katika sala, tunazuia ile nguvu ya Mungu isitufikie; nguvu ambayo Mungu anaweza kututolea, na iko tayari kufanya hivyo. Je, unatosheka na namna unavyosali, ao unaona kama unahitaji kufanya maendeleo ili kutoa sala zenye kutoka moyoni?​—Yer. 16:19.

13. Sababu gani kukusanyika na ndugu na dada wengine ni jambo la maana sana ili kukomaa kiroho?

13 Yehova anapendezwa na wale wote “wanaotafuta kimbilio kwake”; kwa hiyo, hata kisha kumujua Mungu, ni lazima tuendelee kwa ukawaida kujiunga na wale wengine wanaomujua Mungu katika kutaniko. (Nah. 1:7) Katika dunia hii inayojaa mambo mengi yenye kuvunja moyo, ni jambo la hekima kuwa kila mara pamoja na ndugu na dada zetu wanaotutia moyo. Tutapata faida gani? Katika kutaniko, utapata watu watakaokuchochea “katika upendo na matendo mazuri.” (Ebr. 10:24, 25) Upendo huo ambao mutume Paulo anazungumuzia katika barua yake kwa Waebrania ni upendo kati ya ndugu na dada wanaomuabudu Yehova kwa nia moja katika makutaniko. Ili kuonyesha upendo kama huo ni vizuri kushirikiana ao kufanya mambo pamoja na Wakristo wengine. Chunguza liste yako ya kiroho ili kuona ikiwa unahuzuria na kushiriki kwa ukawaida kwenye mikutano.

14. Sababu gani kutubu na kugeuka ni mambo yenye kuendelea?

14 Ili kuwa Wakristo ilituomba kutubu zambi na kugeuka. Hata hivyo, kutubu na kugeuka ni mambo yenye kuendelea. Zambi inajificha ndani yetu sisi wanadamu wasio wakamilifu kama vile nyoka anavyojificha na kuwa tayari kumuuma mutu. (Rom. 3:9, 10; 6:12-14) Basi tubaki waangalifu, tusisahau makosa yetu. Jambo lenye kufurahisha ni kwamba Yehova anatuvumilia tunapojikaza kupiganisha uzaifu wetu na kufanya mabadiliko yanayohitajiwa. (Flp. 2:12; 2 Pet. 3:9) Mambo yanayoweza kutusaidia sana ni kuwa waangalifu kuhusu namna tunavyotumia wakati wetu, mali yetu, na kuacha kufuatilia vitu vya kimwili. Dada mumoja aliandika hivi: “Nililelewa katika kweli, hata hivyo, nilikomaa nikiwa na maoni mengine kuhusu Yehova. Nilikuwa nikimuogopa sana, na nilifikiri kwamba singeweza kumupendeza hata kidogo.” Baadaye, dada huyo alipata “matatizo mengi ya kiroho” kwa sababu ya vizuizi vyake mwenyewe. Anaendelea kusema hivi: “Haikuwa sababu sikumupenda Yehova, lakini ni kwa sababu sikumujua vizuri kabisa. Hata hivyo kisha kusali mara nyingi, nilianza kubadilika. Nilitambua kwamba Yehova aliniongoza kama mutoto mudogo, alinisaidia kuepuka tatizo moja moja, na kwa upole alinionyesha yale niliyopaswa kufanya.”

15. Yesu na Baba yake wanajua nini?

15 Endelea ‘kusema na watu’ kuhusu habari njema. Malaika wa Mungu aliambia mutume Petro na mitume wengine maneno hayo kisha wao kuwekwa huru kimuujiza kutoka gereza. (Mdo. 5:19-21) Ndiyo, jambo lingine lililo kwenye liste yetu ya kiroho ni kuhubiri kila juma. Yesu na Baba yake wanachunguza jinsi imani yetu iko na kazi yetu ya kuhubiri. (Ufu. 2:19) Mahubiri ni sehemu kubwa ya maisha yetu.

16. Sababu gani ni vizuri kukumbuka namna ulivyojitoa kwa Yehova katika sala?

16 Kumbuka namna ulivyojitoa kwa Yehova katika sala. Kitu cha bei sana tulicho nacho ni urafiki wetu pamoja na Yehova. Anajua wale walio wake. (Soma Isaya 44:5.) Chunguza katika sala ikiwa urafiki wako pamoja na Yehova ni muzuri na wenye nguvu. Kuhusiana na hilo, kumbuka ile tarehe ya maana sana, ni kusema, tarehe ya ubatizo wako. Kufanya hivyo pia kutakusaidia ukumbuke kwamba ubatizo wako ni alama ya uamuzi wa maana sana ambao umefanya.

BAKI KARIBU NA YEHOVA KWA UVUMILIVU

17. Sababu gani tunahitaji kuvumilia ili tubaki karibu na Yehova?

17 Mutume Paulo alipowaandikia Wagalatia, alikazia ulazima wa kuvumilia. (Gal. 6:9) Hilo ni jambo la maana sana kwa Wakristo wa leo pia. Utapambana na majaribu, lakini Yehova atakusaidia. Endelea kumuomba Yehova roho takatifu. Utasikia kuwa unatulizana wakati atabadili huzuni yako kuwa furaha, na mahangaiko yako kuwa amani. (Mt. 7:7-11) Fikiria jambo hili: Ikiwa Yehova anahangaikia ndege, hauone kwamba atakuhangaikia hata zaidi kwa sababu wewe unamupenda na umejitoa kwake? (Mt. 10:29-31) Hata ikiwa unapambana na matatizo gani, usirudi nyuma, usiache. Ni baraka kubwa kabisa kujulikana na Yehova.

18. Kwa kuwa ‘umekwisha kumujua Mungu,’ utafanya nini sasa?

18 Kwa hiyo, ikiwa umemujua Mungu hivi karibuni na umebatizwa, utafanya nini sasa? Endelea kumujua Yehova vizuri zaidi, endelea kukomaa kiroho. Na ikiwa umebatizwa tangu miaka mingi, utafanya nini sasa? Wewe pia endelea kufanya ujuzi wako kumuhusu Yehova uingize kabisa mizizi na uwe mwingi. Tusipuuze hata kidogo urafiki wetu pamoja na Yehova. Kwa hiyo, tunapaswa kufanya uchunguzi wa liste yetu ya kiroho kila wakati ili kuwa hakika kwamba tunaendelea kukomaa kiroho na kutengeneza zaidi urafiki wetu pamoja na Baba yetu mwenye upendo, Rafiki yetu na Mungu wetu, Yehova.​—Soma 2 Wakorintho 13:5, 6.