Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Linda Uriti Wako wa Kiroho kwa Kuchukua Maamuzi Mazuri

Linda Uriti Wako wa Kiroho kwa Kuchukua Maamuzi Mazuri

“Chukieni maovu, shikamaneni na mema.”​—ROM. 12:9.

1, 2. (a) Namna gani ulichukua uamuzi wa kumutumikia Mungu? (b) Tunaweza kujiuliza maulizo gani kuhusu uriti wetu wa kiroho?

 MAMILIONI ya watu wamechukua uamuzi muzuri wa kumutumikia Yehova Mungu na kufuata kwa ukaribu hatua za Yesu Kristo. (Mt. 16:24; 1 Pet. 2:21) Tunachukua kwa uzito ahadi tuliyomutolea Mungu ili kumutumikia. Hatukuchukua uamuzi huo kisha kujifunza Biblia kijuu-juu tu, lakini tulifanya hivyo kisha kujifunza Biblia kwa uangalifu. Tulijifunza mambo mengi yenye kuimarisha imani kuhusu uriti ambao Yehova amewatolea wale ‘wanaoendelea kupata ujuzi juu yake na juu ya yule aliyemutuma, Yesu Kristo.’​—Yoh. 17:3; Rom. 12:2.

2 Ili kuendelea kuwa na uhusiano muzuri pamoja na Yehova, tunapaswa kuchukua maamuzi yanayomupendeza. Kwa hiyo, tutazungumuzia maulizo haya ya maana katika habari hii: Uriti wetu wa kiroho ni nini? Tunapaswa kuuona namna gani? Tunapaswa kufanya nini ili tusipoteze uriti huo? Ni nini kitakachotusaidia kuchukua maamuzi mazuri?

URITI WETU WA KIROHO—NI NINI?

3. (a) Wakristo watiwa mafuta wanangojea uriti gani? (b) Na “kondoo wengine” watapokea uriti gani?

3 Ni hesabu ndogo tu ya Wakristo ndio inangojea kupata ‘uriti usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia,’ ni kusema, pendeleo la pekee la kutawala na Kristo mbinguni. (1 Pet. 1:3, 4) Ili kupata uriti huo, kila mumoja wao anapaswa ‘kuzaliwa tena.’ (Yoh. 3:1-3) Lakini, mamilioni ya “kondoo wengine” wa Yesu, ambao wanawasaidia watiwa-mafuta wake kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, watapokea uriti gani? (Yoh. 10:16) Kondoo wengine watapokea uriti ambao Adamu na Eva hawakupokea hata kidogo kwa sababu ya zambi, ni kusema, uzima wa milele katika dunia itakayokuwa paradiso, bila mateso, kifo, wala kilio. (Ufu. 21:1-4) Yesu alikuwa akifikiria Paradiso hiyo alipomuambia mutenda mabaya aliyetundikwa karibu naye hivi: “Kwa kweli ninakuambia leo, Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”​—Lu. 23:43.

4. Ni baraka gani tunazofurahia sasa?

4 Tunaweza hata sasa kufurahia baraka fulani zinazotokana na uriti wetu wa kiroho. Kuonyesha imani katika “fidia [zabihu ya ukombozi] ambayo Kristo alilipa,” kunatusaidia kuwa na amani ya akili na uhusiano muzuri pamoja na Mungu. (Rom. 3:23-25) Tunaelewa vizuri zaidi ahadi nzuri zinazozungumuziwa katika Neno la Mungu. Zaidi ya hayo, tunafurahia sana kuwa katika familia ya ulimwenguni pote ya ndugu na dada. Pia, ni pendeleo kubwa kuwa Shahidi wa Yehova. Kwa hiyo, tunaufurahia sana uriti wetu wa kiroho!

5. Shetani anaendelea kujikaza kufanya nini, na ni nini inayoweza kutusaidia kupinga hila zake?

5 Hata hivyo, ili tusipoteze uriti wetu muzuri tunapaswa kuendelea kutambua mitego ya Shetani. Siku zote Shetani anafanya yote anayoweza ili kuwachochea watumishi wa Mungu wachukue maamuzi yanayoweza kuwafanya wapoteze uriti wao. (Hes. 25:1-3, 9) Kwa kuwa anajua kwamba mwisho wake unakaribia, Shetani anafanya yote anayoweza ili kutudanganya. (Soma Ufunuo 12:12, 17.) Ikiwa tunataka kuendelea ‘kusimama imara kupinga hila za Ibilisi,’ tunapaswa kuendelea kuuona uriti wetu kuwa wa maana sana. (Efe. 6:11) Mufano wa muzaliwa wa kwanza wa Isaka unatufundisha mambo fulani ambayo hatupaswe kusahau.

USIWE KAMA ESAU

6, 7. Esau alikuwa nani, na alikuwa na uriti gani?

6 Miaka 4000 hivi iliyopita, Isaka na Rebeka walizaa mapasa, walioitwa Esau na Yakobo. Walipoendelea kukomaa, mapasa hao walionyesha sifa tofauti na walichagua kazi tofauti. ‘Esau alikuwa mwanamume anayejua jinsi ya kuwinda, mwanamume wa mbugani,’ lakini ‘Yakobo [alikuwa] asiye na lawama, aliyekaa katika mahema.’ (Mwa. 25:27) Mutafsiri mumoja wa Biblia anayeitwa Robert Alter, alionyesha kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa “asiye na lawama,” “linamaanisha utimilifu ao kutokuwa na kosa.”

7 Wakati Esau na Yakobo walikuwa na miaka 15, Abrahamu aliyekuwa nkambo ao tate yao, alikufa, lakini Yehova hakusahau ahadi aliyomutolea Abrahamu. Baadaye, Yehova alimuambia Isaka kuhusu ahadi hiyo, alimuonyesha kwamba mataifa yote ya dunia yatajibariki kupitia uzao wa Abrahamu. (Soma Mwanzo 26:3-5.) Ahadi hiyo ilionyesha kwamba Masiya, ambaye ndiye “uzao” unaotajwa katika Mwanzo 3:15—​angetokea katika kizazi cha Abrahamu. Kwa kuwa Esau ndiye aliyekuwa muzaliwa wa kwanza wa Isaka, uzao ulioahidiwa ungetokea katika kizazi chake. Esau alikuwa na uriti muzuri kabisa! Je, aliusamini?

Usitie uriti wako wa kiroho katika hatari

8, 9. (a) Esau alichukua uamuzi gani kuhusiana na uriti wake? (b) Miaka fulani baadaye, Esau alitambua nini kuhusiana na uamuzi wake, na alijisikia namna gani?

8 Siku moja alipotoka katika mawindo, Esau alimuona Yakobo ‘akitokosa [akipika] muchuzi.’ Esau alimuambia hivi: ‘Haraka, tafazali, nipe nimeze chekundu​—chekundu hicho, kwa maana nimechoka!’ Yakobo alimujibu hivi Esau: ‘Niuzie [niuzishe], kwanza kabisa, haki yako ya muzaliwa wa kwanza!’ Esau aliamua namna gani? Jambo la kushangaza ni kwamba alimuambia hivi Yakobo: “Haki ya kuzaliwa ina faida gani kwangu?” Bila shaka, Esau alibadilisha haki yake ya muzaliwa wa kwanza na bakuli la muchuzi! Ili Esau amuhakikishie kwamba amemuuzisha haki yake ya kuwa muzaliwa wa kwanza, Yakobo alimuambia hivi: “Niapie kwanza kabisa!” Bila kusita, Esau aliuzisha haki yake ya kuzaliwa. Kisha, ‘Yakobo akamupa Esau mukate na muchuzi wa dengu, naye akala na kunywa. Kisha akaondoka kwenda zake. Kwa kufanya hivyo Esau aliizarau haki yake ya kuzaliwa.’​—Mwa. 25:29-34.

9 Miaka fulani baadaye, wakati Isaka alifikiri kwamba alikuwa karibu kufa, Rebeka alifanya mipango ili Yakobo apewe haki ya kuzaliwa aliyonunua kwa Esau. Alipotambua baadaye kwamba alikuwa amechukua uamuzi wa upumbavu, Esau alimulilia Isaka hivi: ‘Je, hauna hata baraka moja tu, baba yangu? Nibariki mimi pia, hata mimi pia, baba yangu?’ Isaka aliposema kwamba hawezi kubadili baraka ambayo alikuwa tayari amemutolea Yakobo, ‘Esau alipaza sauti yake na kuanza kulia machozi.’​—Mwa. 27:30-38.

10. Namna gani Yehova aliwaona Esau na Yakobo, na sababu gani?

10 Mufano wa Esau unatufundisha nini? Esau alifikiri kwamba kutosheleza kwanza tamaa za mwili ni jambo la maana kuliko kupata baraka za wakati ujao ambazo zingetokana na uriti wake. Esau hakusamini haki yake ya kuzaliwa na hilo linaonyesha kwamba hakumupenda Mungu kabisa. Zaidi ya hayo, Esau alisahau kwamba matendo yake yangekuwa na matokeo mabaya juu ya uzao wake. Lakini, Yakobo alisamini sana uriti wake. Kwa mufano, Yakobo alifuata muongozo wa wazazi wake alipochagua bibi. (Mwa. 27:46–28:3) Kwa kuwa Yakobo alichukua uamuzi ambao ulimuomba avumilie na ajinyime, Masiya alitokea katika kizazi chake. Mungu aliwaona namna gani Esau na Yakobo? Kupitia nabii Malaki, Yehova alisema hivi: ‘Nilimupenda Yakobo, naye Esau nikamuchukia.’​—Mal. 1:2, 3.

11. (a) Sababu gani mufano wa Esau unatuhusu sisi Wakristo? (b) Sababu gani Paulo anataja uasherati anapozungumuzia matendo ya Esau?

11 Je, mambo ambayo Biblia inasema kuhusu Esau yanahusu Wakristo leo? Bila shaka. Mutume Paulo aliwaonya Wakristo wenzake wawe waangalifu ili ‘kusiwe na mwasherati wala yeyote asiyesamini mambo matakatifu, kama Esau, ambaye alitoa haki zake za kuwa muzaliwa wa kwanza kwa kubadilishana na mulo mumoja.’ (Ebr. 12:16) Hilo ni onyo kwa Wakristo wote. Tunapaswa kuendelea kusamini mambo matakatifu ili tamaa za mwili zisitutawale na kutufanya tupoteze uriti wetu. Lakini, sababu gani Paulo anataja uasherati anapozungumuzia matendo ya Esau? Kwa sababu kuwa na maoni ya kimwili kama Esau kunaweza kumufanya mutu auzishe mambo matakatifu kwa kujifurahisha kupitia mambo mabaya, kama vile uasherati.

TAYARISHA MOYO WAKO SASA

12. (a) Shetani anafanya nini ili kujaribu kila mumoja wetu? (b) Ni mifano gani ya Maandiko inayoweza kutusaidia tunapojaribiwa?

12 Sisi watumishi wa Yehova, hatutafute kujitia katika hali zinazoweza kutuongoza kwenye uasherati. Lakini, tunamuomba Yehova Mungu atusaidie kushinda majaribu. (Mt. 6:13) Tunapojikaza kubaki waaminifu katika ulimwengu huu muovu, Shetani anaendelea kufanya yote anayoweza ili aharibu hali yetu ya kiroho. (Efe. 6:12) Kwa kuwa yeye ni mungu wa ulimwengu huu muovu, Ibilisi anajua namna anavyoweza kuamusha tamaa zetu za zambi kwa kutuletea majaribu. (1 Kor. 10:8, 13) Kwa mufano, wazia unajikuta katika hali fulani ambayo inafanya iwe rahisi kwako kutosheleza tamaa fulani katika njia isiyofaa. Utachukua uamuzi gani? Je, utasema hivi kama Esau: ‘Haraka! Nipatie!’ Ao, je, utashinda jaribu hilo na kukimbia, kama alivyofanya Yosefu mwana wa Yakobo alipojaribiwa na bibi ya Potifa?​—Soma Mwanzo 39:10-12.

13. (a) Namna gani wengi wametenda kama Yosefu leo, lakini namna gani wengine wametenda kama Esau? (b) Mifano ya wale ambao wametenda kama Esau inatufundisha jambo gani la maana?

13 Ndugu na dada zetu wengi wamejikuta katika hali ambamo wanapaswa kuchagua ikiwa watatenda kama Esau ao Yosefu. Wengi wametenda kwa hekima na wamefurahisha moyo wa Yehova. (Met. 27:11) Hata hivyo, wengine kati ya waamini wenzetu wametenda kama Esau wanapojaribiwa; wameuzisha uriti wao wa kiroho. Kwa kuongezea, ndugu na dada wengi wanakaripiwa ao kutengwa na kutaniko kila mwaka kwa sababu ya uasherati. Kwa hiyo, ni jambo la maana sana kutayarisha moyo wetu sasa, zaidi sana mbele hatujajikuta katika majaribu! (Zab. 78:8) Acheni tuzungumuzie mambo mawili yanayoweza kutusaidia kutayarisha moyo wetu na kuchukua maamuzi mazuri baadaye.

FIKIRI NA UTIE NGUVU HALI YAKO YA KIROHO

Tunatia nguvu hali yetu ya kiroho kwa kutafuta hekima ya Yehova

14. Ni maulizo gani ambayo tunapaswa kufikiria ili ‘tuchukie maovu’ na “kushikamana na mema”?

14 Jambo la kwanza ni kufikiri juu ya matokeo ya mwenendo wetu. Ikiwa tunamupenda Yehova, Mutoaji wa uriti huo, kwa moyo wetu wote, tutasamini sana uriti wetu wa kiroho. Ikiwa tunamupenda mutu fulani, tutaepuka kumuumiza, sivyo? Lakini, tutajikaza kufanya mambo yanayomupendeza. Kwa hiyo, tunapaswa kutafuta wakati ili kufikiri ikiwa matokeo yatakuwa nini juu yetu na juu ya wengine ikiwa tunafanya mambo mabaya. Tunapaswa kujiuliza: ‘Matendo yangu mabaya yatakuwa na matokeo gani juu ya uhusiano wangu na Yehova? Matendo yangu mabaya yatakuwa na matokeo gani juu ya familia yangu? Ndugu na dada katika kutaniko wataona matendo yangu namna gani? Je, yatawakwaza wengine?’ (Flp. 1:10) Tunapaswa pia kujiuliza hivi: ‘Je, ni jambo la maana kabisa nijifurahishe kwa dakika chache katika zambi ili tu nivune maumivu ya moyo baadaye? Je, ninataka kabisa kuwa kama Esau, aliyelia sana kisha kutambua kwamba alikuwa amedanganyika?’ (Ebr. 12:17) Kufikiria sana maulizo hayo kutatusaidia ‘tuchukie maovu’ na “kushikamana na mema.” (Rom. 12:9) Upendo wetu kwa Yehova ndio utakaotusaidia tushikamane na uriti wetu wa kiroho.​—Zab. 73:28.

15. Ni mipango gani inayoweza kutia nguvu hali yetu ya kiroho?

15 Jambo la pili ni kutia nguvu hali yetu ya kiroho. Yehova amefanya mipango mingi inayotia nguvu hali yetu ya kiroho ili tusiangukie katika hatari mbalimbali za kiroho. Mipango hiyo inatia ndani kujifunza Biblia, mikutano ya Kikristo, kazi ya kuhubiri, na sala. (1 Kor. 15:58) Tunatia nguvu hali yetu ya kiroho kila mara tunapomumwangia Yehova moyo wetu katika sala na kila mara tunapotumia wakati mwingi katika kazi ya kuhubiri. (Soma 1 Timotheo 6:12, 19.) Kuwa nguvu kiroho kunategemea sana namna tunavyojikaza ili kutia nguvu hali yetu ya kiroho. (Gal. 6:7) Jambo hilo linakaziwa sana katika sura ya pili ya kitabu cha Methali.

‘ENDELEA KUTAFUTA’

16, 17. Namna gani tunaweza kupata uwezo wa kufikiri utakaotusaidia kuchukua maamuzi mazuri?

16 Sura ya pili ya kitabu cha Methali inatutia moyo tutafute hekima na uwezo wa kufikiri. Sifa hizo zinatusaidia kuchagua kati ya mema na mabaya, zinatusaidia tujizuie kuliko kujifurahisha tu katika zambi. Lakini, hilo linawezekana ikiwa tu tunajikaza. Biblia inakazia ukweli huo inaposema hivi: ‘Mwanangu, ikiwa utapokea maneno yangu na kujiwekea amri zangu kama hazina, ili kwa sikio lako usikilize hekima kwa makini, ili uelekeze moyo wako kwenye utambuzi, ikiwa utaita uelewaji na kupaaza sauti yako uite utambuzi, ikiwa utaendelea kuutafuta kama feza, na kuendelea kuutafuta kama hazina zilizofichika, ndipo utakapoelewa kumwogopa Yehova, nawe utapata kumujua Mungu. Kwa maana Yehova mwenyewe anatoa hekima; kinywani mwake hutoka ujuzi na utambuzi.’​—Met. 2:1-6.

17 Tunaweza kupata uwezo wa kufikiri utakaotusaidia kuchukua maamuzi mazuri ikiwa tu tunafanya mambo yanayoonyeshwa katika kitabu cha Methali. Tunaweza kushinda majaribu ikiwa tunaacha maneno ya Yehova yafinyange moyo wetu, ikiwa tunamuomba Yehova kwa bidii atuongoze, na ikiwa tunaendelea kutafuta ujuzi wa Mungu kama hazina zilizofichwa.

18. Umeazimia kuendelea kufanya nini, na sababu gani?

18 Yehova anawapa ujuzi, uelewaji, utambuzi, na hekima wale wanaofanya yote wanayoweza ili kutafuta sifa hizo. Tunapojikaza kutafuta na kutumia sifa hizo, urafiki wetu pamoja na Yehova, aliye Mutoaji wa sifa hizo, utakuwa wa karibu zaidi. Pia, uhusiano wetu wa karibu pamoja na Yehova utatusaidia kuchukua maamuzi mazuri tunapopambana na majaribu. Kumukaribia Yehova na kuogopa kumuhuzunisha kutatuzuia kufanya zambi. (Zab. 25:14; Yak. 4:8) Kwa kuwa tunafurahia urafiki wetu na Yehova na tunafurahia kutumia hekima ya Mungu, acheni sisi wote tuazimie kuendelea kuchukua maamuzi mazuri yatakayofurahisha moyo wa Yehova na kutusaidia kulinda uriti wetu wa kiroho.