Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Ni Nani kwa Kweli Mutumwa Mwaminifu na Mwenye Busara?’

‘Ni Nani kwa Kweli Mutumwa Mwaminifu na Mwenye Busara?’

‘Ni nani kwa kweli mutumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimuweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani?’​—MT. 24:45.

1, 2. Yesu anatulisha kupitia njia gani leo, na sababu gani ni jambo la maana sana kutambua njia hiyo?

 “NDUGU zangu, siwezi kuhesabu ni mara ngapi mumenitolea vichapo vilivyokuwa na habari ambazo nilihitaji hasa na kwa wakati ambao nilizihitaji kabisa.” Maneno hayo yalikuwa katika barua ya shukrani ambayo dada mumoja aliandikia ndugu wanaotumika kwenye makao makubwa ya Mashahidi wa Yehova. Je, umekwisha kujisikia kama dada huyo? Wengi kati yetu wamejisikia hivyo. Je, hilo linapaswa kutushangaza? Hapana kabisa.

2 Chakula cha kiroho ambacho tunapata kwa wakati unaofaa ni uhakikisho wa kwamba Yesu, ambaye ni Kichwa cha kutaniko, anaendelea kutimiza ahadi yake ya kutulisha. Anafanya hivyo kupitia nani? Alipotoa alama ya kuwapo kwake, Yesu alisema kwamba angetumia ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara’ ili kutoa “chakula kwa wakati unaofaa” kwa watumishi wake wa nyumbani. * (Soma Mathayo 24:45-47.) Mutumwa huyo mwaminifu ndiye njia ambayo Yesu anatumia ili kulisha wafuasi wake wa kweli wakati huu wa mwisho. Ni jambo la maana sana tumutambue mutumwa huyo mwaminifu kwa sababu hatuwezi kuwa na afya nzuri ya kiroho ao uhusiano muzuri na Yehova ikiwa hatutambue njia hiyo ambayo Yehova anatumia.​—Mt. 4:4; Yoh. 17:3.

3. Tangu zamani, vichapo vyetu vimekuwa vikifasiria namna gani mufano wa mutumwa mwaminifu?

3 Kwa hiyo basi, namna gani tunapaswa kuelewa mufano wa Yesu kuhusu mutumwa mwaminifu? Tangu zamani, vichapo vyetu vimekuwa vikieleza mambo hivi: Kwenye Pentekoste ya mwaka wa 33, Yesu alimuweka mutumwa mwaminifu juu ya watumishi wake wa nyumbani. Mutumwa huyo anawakilisha Wakristo wote watiwa-mafuta walio duniani kwa wakati wowote kuanzia mwaka wa 33. Na watumishi wa nyumbani wanawakilisha Wakristo hao watiwa-mafuta wakiwa mutu mumoja-mumoja. Tena, vimeeleza kwamba katika 1919, Yesu alimuweka mutumwa mwaminifu ‘juu ya mali yake yote,’ ni kusema, faida zake zote za Ufalme duniani. Hata hivyo, kisha kuchunguza tena kwa uangalifu maneno ya Yesu na kusali, tumetambua kwamba tunapaswa kurekebisha namna tulivyoelewa maneno hayo ya Yesu kuhusu mutumwa mwaminifu na mwenye busara. (Met. 4:18) Acheni tuchunguze mufano huo na namna gani unatuhusu, iwe tuna tumaini la kuishi mbinguni ao duniani.

MUFANO HUO ULITIMIA WAKATI GANI?

4-6. Sababu gani tunaweza kusema kwamba mufano wa Yesu kuhusu mutumwa mwaminifu ulianza kutimia kisha tu 1914?

4 Mistari inayozungumuzia mufano wa mutumwa mwaminifu na mwenye busara inaonyesha kwamba mufano huo haukuanza kutimia kwenye Pentekoste ya mwaka wa 33, lakini ungetimia katika wakati huu wa mwisho. Acheni tuchunguze maandiko fulani ili kuona sababu gani tunasema hivyo.

5 Mufano wa mutumwa mwaminifu ni sehemu ya unabii wa Yesu unaozungumuzia ‘alama ya kuwapo [kwake] na ya umalizio wa mufumo wa mambo.’ (Mt. 24:3) Sehemu ya kwanza ya unabii huo, unaozungumuziwa kwenye Mathayo 24:4-22, ingetimia mara mbili—ingetimia mara ya kwanza kuanzia mwaka wa 33 mupaka mwaka wa 70, na ingetimia mara ya pili kwa njia kubwa zaidi katika siku zetu. Je, hilo linamaanisha kwamba maneno ya Yesu kuhusu mutumwa mwaminifu yangetimia pia mara mbili? Hapana.

6 Kuanzia maneno yanayopatikana katika Mathayo 24:29, Yesu alikazia kwanza mambo ambayo yangetokea katika siku zetu. (Soma Mathayo 24:30, 42, 44.) Akizungumuzia kuhusu mambo yatakayotokea wakati wa ziki kubwa, Yesu alisema kwamba watu ‘watamuona Mwana wa binadamu akija juu ya mawingu ya mbinguni.’ Kisha, kuhusu wale ambao wangeishi katika siku hizo za mwisho, Yesu alionyesha umaana wa kuendelea kukesha aliposema hivi: ‘Hamujue ni siku gani Bwana yenu atakuja’ na aliongezea hivi: ‘Mwana wa binadamu atakuja katika saa musiyofikiria.’ * Katika mistari hiyo, alipokuwa akieleza mambo ambayo yangetokea katika siku za mwisho, Yesu alizungumuzia mufano wa mutumwa mwaminifu. Kwa hiyo, tunaweza kusema kwamba maneno yake kuhusu mutumwa mwaminifu huyo yalianza kutimia kisha tu siku za mwisho kuanza katika 1914. Maelezo hayo yanaonekana kuwa wazi zaidi. Sababu gani?

7. Ni ulizo gani la maana lilitokea kipindi cha mavuno kilipoanza, na sababu gani?

7 Fikiri kidogo kuhusu ulizo hili: ‘Ni nani kwa kweli mutumwa mwaminifu na mwenye busara?’ Katika wakati wa mitume, hakukuwa na sababu ya kuuliza ulizo hilo. Kama tulivyoona katika habari iliyotangulia, mitume walifanya miujiza na hata kuwapa wengine zawadi za kufanya miujiza ili kuonyesha kwamba walitegemezwa na Mungu. (Mdo. 5:12) Kwa hiyo, hakuna mutu yeyote ambaye angeweza kuuliza ni nani kabisa aliyewekwa na Kristo ili kuongoza. Lakini, mambo yalikuwa tofauti kabisa katika 1914. Kipindi cha mavuno yalianza katika mwaka huo. Wakati wa kutenganisha magugu na ngano ulikuwa umefika sasa. (Mt. 13:36-43) Kwa wakati wa mavuno ulikuwa umeanza, ulizo la maana sana lilitokezwa: Namna gani watu wangetambua ngano, ni kusema, Wakristo watiwa​-mafuta, kwa sababu wakati huo wengi walijidai kuwa wafuasi wa kweli wa Yesu? Jibu lilipatikana katika mufano wa mutumwa mwaminifu. Wafuasi watiwa​-mafuta wa Kristo walipaswa kuwa ndio watu waliokuwa wakilishwa vizuri kiroho.

MUTUMWA MWAMINIFU NA MWENYE BUSARA NI NANI?

8. Sababu gani inafaa kabisa kwamba mutumwa mwaminifu afanyizwe na Wakristo watiwa-mafuta?

8 Mutumwa mwaminifu anapaswa kufanyizwa na Wakristo watiwa-mafuta walio duniani. Watiwa-mafuta hao wanaitwa “ukuhani wa kifalme” na wamepewa kazi ya “‘kutangaza kotekote sifa bora’ zake yeye aliyewaita kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.” (1 Pet. 2:9) Kwa hiyo, inafaa kabisa kwamba washiriki wa “ukuhani [huo] wa kifalme” washiriki moja kwa moja katika kazi ya kufundisha waamini wenzao kweli.​—Mal. 2:7; Ufu. 12:17.

9. Je, Wakristo wote watiwa​-mafuta wanafanyiza mutumwa mwaminifu? Eleza.

9 Je, watiwa-mafuta wote ambao wanaishi duniani wanafanyiza mutumwa mwaminifu? Hapana. Ukweli ni kwamba si watiwa​-mafuta wote walio na daraka la kutolea chakula cha kiroho waamini wenzao duniani pote. Kati ya ngano kuna ndugu watiwa​-mafuta ambao ni watumishi wa huduma ao wazee katika kutaniko la kwao. Wanahubiri nyumba kwa nyumba na kufundisha katika makutaniko yao, na wanategemeza kwa uaminifu uongozi kutoka kwenye makao makubwa. Lakini hawana daraka la kutolea ndugu na dada duniani pote chakula cha kiroho. Tena kati ya watiwa​-mafuta kuna dada wanyenyekevu ambao hawatazamie hata siku moja kutimiza daraka la kufundisha katika kutaniko.​—1 Kor. 11:3; 14:34.

10. Mutumwa mwaminifu na mwenye busara ni nani?

10 Kwa hiyo basi, mutumwa mwaminifu na mwenye busara ni nani? Kama vile Yesu alivyowalisha watu wengi kupitia wachache, mutumwa huyo ni kikundi kidogo cha ndugu watiwa​-mafuta ambao wana daraka la kutayarisha na kutoa chakula cha kiroho wakati wa kuwapo kwa Kristo. Katika siku hizi za mwisho, ndugu watiwa​-mafuta wanaofanyiza mutumwa mwaminifu wametumikia pamoja kwenye makao yetu makubwa. Katika miaka ya hivi karibuni, mutumwa huyo amefikiriwa sana kuwa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Ona kwamba, katika mufano wake, Yesu anamutaja ‘mutumwa’ huyo kama mutu mumoja ijapokuwa anafanyizwa na zaidi ya mutu mumoja. Kwa hiyo, maamuzi ya Baraza Linaloongoza hayachukuliwe na mutu mumoja.

NI NANI WALIO WATUMISHI WA NYUMBANI?

11, 12. (a) Ni madaraka gani mawili ambayo mutumwa mwaminifu na mwenye busara alipewa? (b) Ni wakati gani Yesu alimuweka mutumwa mwaminifu juu ya watumishi wake wa nyumbani, na alichagua nani?

11 Inapendeza kuona kwamba katika mufano wa Yesu, mutumwa mwaminifu na mwenye busara anapewa madaraka mawili tofauti. Daraka la kwanza ni kusimamia watumishi wa nyumbani, na daraka la pili ni kusimamia mali yote ya bwana wake. Kwa kuwa mufano huo unatimia tu katika wakati huu wa mwisho, ni wazi kwamba mutumwa huyo alipewa madaraka hayo mawili kisha Yesu kuanza kutawala huko mbinguni katika 1914.

12 Ni wakati gani Yesu alimuweka mutumwa mwaminifu juu ya watumishi wake wa nyumbani? Ili kujibu ulizo hilo, tuzungumuzie tena mambo yaliyotokea katika 1914, ni kusema, mwanzoni mwa wakati wa mavuno. Kama tulivyojifunza katika habari zilizotangulia, wakati huo watu wengi waliokuwa katika vikundi vingi vya kidini walijidai kuwa Wakristo. Yesu angechagua mutumwa mwaminifu kutoka katika kikundi gani? Ulizo hilo lilijibiwa kisha Yesu na Baba yake kuchunguza hekalu la kiroho. Hekalu hilo ni mupango ambao Yehova amefanya ili tumuabudu katika njia anayokubali. Uchunguzi huo ulifanywa kuanzia 1914 mupaka mwanzoni mwa 1919. * (Mal. 3:1) Walifurahia kikundi kimoja kidogo cha Wanafunzi wa Biblia waaminifu walioonyesha kwamba walishikamana kwa moyo wote na Yehova na Neno lake. Bila shaka, walihitaji kusafishwa kwa njia fulani, na walikubali kwa unyenyekevu kuchunguzwa na kusafishwa katika kipindi hicho kifupi. (Mal. 3:2-4) Wale Wanafunzi wa Biblia waaminifu walikuwa Wakristo wa kweli, ni kusema, ngano. Katika 1919, wakati Wakristo watiwa-mafuta waliamuka tena kiroho, Yesu alichagua ndugu fulani watiwa-mafuta wenye kukomaa kiroho kati ya Wakristo wa kweli ili wawe mutumwa mwaminifu na mwenye busara na aliwaweka juu ya watumishi wake wa nyumbani.

13. Ni nani pia walio sehemu ya watumishi wa nyumbani, na sababu gani?

13 Kwa hiyo basi, ni nani walio watumishi wa nyumbani? Kwa kifupi, ni wale wote wanaolishwa. Mwanzoni mwa siku za mwisho, watumishi wote wa nyumbani walikuwa watiwa​-mafuta. Baadaye, mukutano mukubwa wa kondoo wengine ukawa sehemu ya watumishi wa nyumbani. Siku hizi, wale kondoo wengine wanafanyiza sehemu kubwa ya lile “kundi moja” linaloongozwa na Kristo. (Yoh. 10:16) Vikundi hivyo viwili vinafaidika na chakula kilekile cha kiroho kinachotolewa na mutumwa mwaminifu kwa wakati unaofaa. Tuseme nini kuhusu washiriki wa Baraza Linaloongoza ambao ndio mutumwa mwaminifu na mwenye busara leo? Ndugu hao pia wanahitaji kulishwa kiroho. Kwa hiyo, wanatambua kwa unyenyekevu kwamba kila mumoja wao ni mutumishi pia wa nyumbani kama mufuasi mwengine yeyote wa kweli wa Yesu.

Iwe tumaini letu ni la kuishi mbinguni ao duniani, sisi wote ni watumishi wa nyumbani na tunahitaji chakula kile kile cha kiroho kwa wakati unaofaa

14. (a) Mutumwa mwaminifu amepewa daraka gani, na hilo linatia ndani nini? (b) Ni onyo gani ambalo Yesu alimutolea mutumwa mwaminifu na mwenye busara? (Ona kisanduku ‘Ikiwa Wakati Wowote Mutumwa Huyo Muovu . . .’)

14 Yesu alimupatia mutumwa mwaminifu na mwenye busara daraka nzito. Zamani, mutumwa mwenye kutumainiwa, ao musimamizi-nyumba, alisimamia mambo mengi ya nyumbani. (Lu. 12:42) Kwa hiyo, mutumwa mwaminifu na mwenye busara amepewa daraka la kusimamia nyumba ya imani. Daraka hilo linatia ndani kusimamia mali ya kimwili (kama vile majengo mbalimbali tunayotumia kwa ajili ya ibada), kazi ya kuhubiri, programe za mikusanyiko, na utayarishaji wa vichapo vya Biblia vya kutumia katika mahubiri, mikutano na funzo la pekee. Watumishi wa nyumbani wanategemea mipango hiyo ya kiroho inayofanywa na mutumwa mwaminifu.

NI WAKATI GANI ATAWEKWA JUU YA MALI YOTE YA BWANA WAKE?

15, 16. Ni wakati gani Yesu atamuweka mutumwa mwaminifu juu ya mali yake yote?

15 Ni wakati gani Yesu atamupatia mutumwa mwaminifu daraka la pili, ni kusema, kumuweka ‘juu ya mali yake yote’? Yesu alisema hivi: ‘Atakuwa mwenye furaha ikiwa bwana wake atakapofika [atakapokuja] atamukuta akifanya hivyo! Kwa kweli ninawaambia ninyi, Atamuweka juu ya mali yake yote.’ (Mt. 24:46, 47) Ona kwamba Yesu anamupatia daraka la pili kisha kufika na kukuta kwamba mutumwa huyo amekuwa “akifanya hivyo,” ni kusema, ameendelea kwa uaminifu kutolea watumishi wake wa nyumbani chakula cha kiroho. Kwa hiyo, hangepewa madaraka hayo mawili kwa wakati mumoja. Ili kuelewa namna gani na wakati gani Yesu atamuweka mutumwa huyo juu ya mali yake yote, tunapaswa kujua mambo mawili: Atakuja wakati gani na mali yake inatia ndani nini.

16 Yesu atakuja wakati gani? Jibu linapatikana katika maneno ya Yesu. Kumbuka kwamba katika mistari inayotangulia, neno ‘kuja’ kwa Yesu linahusu wakati ambapo atakuja ili kutangaza hukumu na kuitekeleza wakati wa mwisho wa dunia. * (Mt. 24:30, 42, 44) Kwa hiyo, ‘kufika’ ao ‘kuja’ kwa Yesu kunakozungumuziwa katika mufano wa mutumwa mwaminifu kutatokea wakati wa ziki kubwa.

17. ‘Mali ya Yesu’ inatia ndani nini?

17 ‘Mali yote ya [Yesu]’ inatia ndani nini? Yesu hakuonyesha kwamba neno ‘yote’ linahusiana tu na mali yake ya duniani. Bila shaka, Yesu ana mamlaka makubwa mbinguni. Yeye alisema hivi: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mt. 28:18; Efe. 1:20-23) Kwa sasa, mali yake inatia ndani Ufalme wa Kimesiya, ambao alipewa tangu mwaka wa 1914 na ambao atashiriki na wafuasi wake watiwa-mafuta.​—Ufu. 11:15.

18. Sababu gani Yesu atafurahia sana kumuweka mutumwa mwaminifu juu ya mali yake yote?

18 Tuseme nini basi kuhusu mambo yote ambayo tumejifunza katika habari hii? Yesu atakapokuja ili kuhukumu wakati wa ziki kubwa, atakuta kwamba mutumwa mwaminifu ameendelea kwa uaminifu kutolea watumishi wake wa nyumbani chakula kwa wakati unaofaa. Kwa hiyo, Yesu atafurahia sana kumupatia daraka la pili, ni kusema, kumuweka juu ya mali yake yote. Wale wanaofanyiza mutumwa mwaminifu watapewa pendeleo hilo watakapoanza kutawala pamoja na Kristo mbinguni.

19. Je, ndugu wanaofanyiza mutumwa mwaminifu watapokea zawadi kubwa mbinguni kuliko watiwa​-mafuta wengine? Eleza.

19 Je, ndugu wanaofanyiza mutumwa mwaminifu watapokea zawadi kubwa mbinguni kuliko watiwa-mafuta wengine? Hapana. Zawadi fulani inaweza kuahidiwa kikundi kidogo tu, lakini wengine pia wanaweza kufaidika nayo. Kwa mufano, fikiria yale ambayo Yesu aliwaambia mitume wake waaminifu 11 mbele ya kifo chake. (Soma Luka 22:28-30.) Yesu aliahidi kikundi hicho kidogo cha wanaume kwamba watapokea zawadi nzuri kwa sababu walibaki waaminifu. Watatawala pamoja naye mbinguni. Lakini, kisha miaka mingi, alionyesha kwamba wale wote 144 000 watakaa kwenye viti vya ufalme na kutawala pamoja naye. (Ufu. 1:1; 3:21) Vivyo hivyo, kulingana na andiko la Mathayo 24:47, Yesu aliahidi kikundi kidogo cha wanaume, ni kusema, ndugu watiwa​-mafuta wanaofanyiza mutumwa mwaminifu, kwamba watawekwa juu ya mali yake yote. Lakini kwa kweli, wote 144 000 watashiriki katika utawala wa Yesu mbinguni.​—Ufu. 20:4, 6.

Wote 144 000 watashiriki katika utawala wa Yesu mbinguni

20. Sababu gani Yesu alimuweka mutumwa mwaminifu, na unaazimia kufanya nini?

20 Kupitia mutumwa mwaminifu na mwenye busara, Yesu anaendelea kutumia njia ile ile aliyotumia alipolisha watu wengi kimuujiza, ni kusema, kulisha watu wengi kupitia wachache. Yesu alimuweka mutumwa mwaminifu huyo ili kuhakikisha kwamba wafuasi wake wa kweli, iwe ni watiwa​-mafuta ao wale wa kondoo wengine, wataendelea kupata chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa katika siku za mwisho. Acheni tuazimie basi kuonyesha kwamba tunapendezwa sana na mupango huo kwa kuendelea kuunga mukono kabisa ndugu watiwa​-mafuta wanaofanyiza yule mutumwa mwaminifu na mwenye busara.​—Ebr. 13:7, 17.

 

^ Fungu la 2: Kwenye pindi nyingine, Yesu alizungumuzia mufano unaofanana na huu. Katika mufano huo alimutaja ‘mutumwa’ kuwa ‘musimamizi-nyumba’ na “watumishi wake wa nyumbani” kuwa “watumishi.”​—Lu. 12:42-44.

^ Fungu la 6: ‘Kuja’ kwa Kristo (Katika Kigiriki, erʹkho·mai) ni tofauti na “kuwapo” (pa·rou·siʹa) kwake. Kuwapo kwake kusikoonekana kulianza mbele ya kuja kwake, ni kusema, kuja kuyahukumu mataifa.

^ Fungu la 12: Soma habari “Tazama! Mimi Nipo Pamoja Nanyi Siku Zote,” katika gazeti hili, ukurasa wa 10-12, fungu la 5-8.

^ Fungu la 16: Soma habari “Tuambie, Mambo Haya Yatakuwa Wakati Gani?” katika gazeti hili, kwenye ukurasa wa 7-8, fungu la 14-18.

(Ona fungu la 19)