Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kulisha Watu Wengi Kupitia Wachache

Kulisha Watu Wengi Kupitia Wachache

“Baada ya kuimega ile mikate, [Yesu] akawagawia wanafunzi, nao wanafunzi wakaugawia ule umati.”​—MT. 14:19.

1-3. Eleza namna gani Yesu alilisha watu wengi karibu na Bethsaida. (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

 WAZIA jambo hili. (Soma Mathayo 14:14-21.) Ni siku chache tu mbele ya Pasaka ya mwaka wa 32. Wanaume karibu 5 000 bila kuhesabu wanawake na watoto wadogo, wanamufuata Yesu na wanafunzi wake karibu na Bethsaida, kijiji kilicho upande wa kaskazini pembeni ya Bahari ya Galilaya.

2 Anapoona kikundi cha watu, Yesu anawasikilia huruma, kwa hiyo anawaponya wagonjwa waliokuwa kati yao na anawafundisha mambo mengi kuhusu Ufalme wa Mungu. Usiku unapokuwa karibu kuingia, wanafunzi wake wanamuomba awaache watu waende zao kwenye vijiji vilivyo karibu ili wajinunulie chakula. Lakini Yesu anawaambia wanafunzi wake hivi: ‘Ninyi muwape chakula.’ Labda maneno yake yanawashangaza sana wanafunzi wake, kwa sababu wana chakula kidogo sana​—mikate tano na samaki wadogo wawili.

3 Akichochewa na huruma, Yesu anafanya muujiza: Huo ndio muujiza pekee ambao waandikaji wote ine wa Injili wanazungumuzia. (Mk. 6:35-44; Lu. 9:10-17; Yoh. 6:1-13) Yesu anawaambia wafuasi wake waambie watu wakae kwenye majani mabichi na wajipange vikundi​-vikundi vya watu 50 na vya watu 100. Kisha kutoa sala ya shukrani, Yesu anaanza kugawanya mikate na samaki. Kuliko kuwapa watu chakula yeye mwenyewe, Yesu anawapatia ‘wanafunzi, nao wanafunzi wanaugawia ule umati [kikundi cha watu].’ Kwa njia ya muujiza, kuna chakula kingi zaidi kwa ajili ya kila mutu! Fikiria kidogo: Yesu analisha maelfu ya watu kupitia wachache, ni kusema, wanafunzi wake. *

4. (a) Yesu alihangaikia zaidi kuwapa watu chakula cha aina gani, na sababu gani? (b) Tutazungumuzia nini katika habari hii na ile inayofuata?

4 Yesu alihangaikia zaidi kuwapa wafuasi wake chakula cha kiroho. Alijua kwamba kutumia chakula cha kiroho, ni kusema, kweli zinazopatikana katika Neno la Mungu, kunaongoza kwenye uzima wa milele. (Yoh. 6:26, 27; 17:3) Ni huruma hiyohiyo iliyomuchochea Yesu kulisha watu wengi mukate na samaki, ndio iliyomufanya Yesu apitishe saa nyingi pamoja na wanafunzi wake akiwafundisha. (Mk. 6:34) Lakini alijua kwamba wakati wake duniani ulikuwa mufupi na kwamba angerudi mbinguni. (Mt. 16:21; Yoh. 14:12) Akiwa mbinguni, namna gani Yesu angeendelea kuwalisha vizuri kiroho wanafunzi wake walio duniani? Angefanya kama alivyofanya hapo mbele, ni kusema, angewalisha watu wengi kupitia wachache. Lakini, wachache hao wangekuwa nani? Acheni tuone namna Yesu alivyotumia wachache ili kulisha wanafunzi wake wengi waliotiwa mafuta katika siku za mitume. Kisha, katika habari inayofuata, tutazungumuzia ulizo hili la maana sana kwa kila mumoja wetu: Namna gani tunaweza kuwatambua wale wachache ambao Kristo anatumia ili kutulisha leo?

Maelfu ya watu walilishwa kupitia wachache (Ona fungu la 4)

YESU ANAWACHAGUA WALE WACHACHE

5, 6. (a) Ni uamuzi gani muzito ambao Yesu alichukua ili kuhakikisha kwamba wafuasi wake watalishwa vizuri kiroho kisha kifo chake? (b) Namna gani Yesu aliwatayarisha mitume wake ili waweze kutimiza vizuri daraka lao la maana sana ambalo wangetimiza kisha kifo chake?

5 Baba anayechukua daraka lake kwa uzito anafanya mipango ili familia yake ishugulikiwe vizuri kisha kifo chake. Vivyo hivyo, Yesu, ambaye alikuja kuwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo, alifanya mipango ili wafuasi wake washugulikiwe vizuri kiroho kisha kifo chake. (Efe. 1:22) Kwa mufano, miaka miwili hivi mbele ya kifo chake, Yesu alichukua uamuzi muzito. Alichagua wafuasi wa kwanza kati ya wale wachache ambao baadaye wangelisha wengi. Tuone namna gani alifanya hivyo.

6 Kisha kusali usiku wote, Yesu alikusanya wanafunzi wake na kati yao alichagua mitume 12. (Lu. 6:12-16) Kwa miaka miwili iliyofuata, alitumika sana na wale mitume 12, akiwafundisha kwa maneno na matendo. Alijua kwamba walikuwa na mengi ya kujifunza; kwa hiyo, waliendelea kuitwa “wanafunzi.” (Mt. 11:1; 20:17) Alitolea kila mumoja wao mashauri ya maana sana na mazoezi mengi katika kazi ya kuhubiri. (Mt. 10:1-42; 20:20-23; Lu. 8:1; 9:52-55) Bila shaka alikuwa anawatayarisha kwa ajili ya daraka la maana sana ambalo wangetimiza kisha kifo chake na kisha yeye kurudi mbinguni.

7. Namna gani Yesu alifunua jambo ambalo mitume wake wangehangaikia kwanza?

7 Mitume wangekuwa na daraka gani? Kadiri Pentekoste ya mwaka wa 33 ilivyokuwa ikikaribia, ilionekana waziwazi kwamba mitume wangetumika katika ‘cheo cha uangalizi.’ (Mdo. 1:20) Lakini, ni jambo gani ambalo wangehangaikia kwanza? Kisha ufufuo wake, Yesu alifunua jambo hilo katika mazungumuzo aliyofanya na mutume Petro. (Soma Yohana 21:1, 2, 15-17.) Mbele ya mitume fulani, Yesu alimuambia Petro hivi: “Lisha kondoo wangu wadogo.” Kwa kusema hivyo, Yesu alionyesha kwamba mitume wake wangekuwa kati ya wale wachache ambao angetumia ili kulisha wengi chakula cha kiroho. Hilo ni jambo lenye kugusa moyo kabisa na linaloonyesha namna Yesu anavyowapenda ‘kondoo wake wadogo’! *

KULISHA WENGI TANGU PENTEKOSTE NA KUENDELEA

8. Namna gani waamini wapya kwenye Pentekoste walionyesha kwamba walitambua njia ambayo Kristo alikuwa akitumia ili kulisha wengi?

8 Kuanzia Pentekoste ya mwaka wa 33, Kristo aliyefufuliwa alitumia mitume wake ili kulisha mabaki ya wanafunzi wake watiwa​-mafuta. (Soma Matendo 2:41, 42.) Wayahudi na wageuzwa​-imani walitambua kwamba mitume ndio njia ambayo Yesu alikuwa akitumia ili kulisha Wakristo watiwa​-mafuta katika siku hizo. Bila kusita, ‘waliendelea kujitoa wenyewe kwa fundisho la mitume.’ Kulingana na mutu mumoja mwenye elimu ya mambo ya Biblia, maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa ‘waliendelea kujitoa wenyewe’ yanaweza kumaanisha “kuwa imara na kuonyesha uaminifu usioyumba​-yumba kuhusu jambo fulani.” Waamini wapya walikuwa na njaa sana ya chakula cha kiroho, na walijua vizuri sana mahali pa kupata chakula hicho. Wakiwa na uaminifu usioyumba​-yumba, walitegemea mitume wawafasirie maneno na matendo ya Yesu na kuwaelezea maana ya maandiko yanayohusu Yesu. *​—Mdo. 2:22-36.

9. Namna gani mitume walionyesha kwamba walichukua kwa uzito daraka lao la kulisha kondoo wa Yesu?

9 Mitume walichukua kwa uzito daraka lao la kulisha kondoo wa Yesu. Kwa mufano, fikiria namna walivyoshugulikia jambo moja lilitokea katika kutaniko mupya; jambo ambalo halikuwa rahisi na ambalo lingeweza kuwagawanya. Inashangaza kujua kwamba jambo hilo lilihusu chakula​—chakula cha kimwili. Wajane waliosema Kigiriki walisahauliwa katika ugawaji wa kila siku wa chakula, lakini wajane waliosema Kiebrania hawakutendewa hivyo. Namna gani mitume walitatua tatizo hilo ngumu? “Wale kumi na wawili” walichagua ndugu saba wenye kustahili ili wasimamie “kazi ya lazima,” kazi ya kugawa chakula. Mitume hao, wengi kati yao walikuwa ni wale Yesu alitumia ili kugawa chakula wakati alilisha watu wengi kimuujiza, waliona kwamba ilikuwa jambo la maana zaidi kwao kushugulikia namna ambavyo watu wangelishwa kiroho. Kwa hiyo, walijitoa katika “huduma ya neno.”​—Mdo. 6:1-6.

10. Namna gani Kristo alitumia mitume na wanaume fulani wazee katika Yerusalemu?

10 Mwanzoni mwa mwaka wa 49, mitume waliokuwa wangali wazima walisaidiwa na wazee fulani wenye uzoefu. (Soma Matendo 15:1, 2.) “Mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu” walifanyiza baraza linaloongoza. Kristo, Kichwa cha kutaniko, alitumia kikundi hicho kidogo cha wanaume wenye uzoefu ili kushugulikia mambo yaliyohusiana na mafundisho na kusimamia na kuongoza kazi ya kufundisha na kuhubiri habari njema ya Ufalme.​—Mdo. 15:6-29; 21:17-19; Kol. 1:18.

11, 12. (a) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Yehova alibariki mupango ambao Mwana wake alitumia ili kulisha makutaniko wakati wa mitume? (b) Njia ambayo Kristo alitumia ili kulisha kondoo zake kiroho, ilijulikana waziwazi namna gani?

11 Je, Yehova alibariki mupango huo ambao Mwana wake alitumia ili kulisha makutaniko wakati wa mitume? Bila shaka, ndiyo! Tunajua hilo namna gani? Kitabu cha Matendo kinatoa ripoti hii: “Basi [Paulo na wenzake] walipoendelea kusafiri kupitia katika majiji walikuwa wakiwapa wale waliokuwa huko maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wanaume wazee waliokuwa katika Yerusalemu ili wayashike. Kwa hiyo, kwa kweli, makutaniko yakaendelea kufanywa imara katika imani na kuongezeka hesabu siku baada ya siku.” (Mdo. 16:4, 5) Ona kwamba makutaniko hayo yalikuwa na maendeleo kwa sababu ndugu na dada walitii kwa uaminifu uongozi wa baraza linaloongoza lililokuwa huko Yerusalemu. Bila shaka hilo linaonyesha waziwazi kwamba Yehova alibariki mupango ambao Mwana wake alitumia ili kulisha makutaniko. Tusisahau kwamba maendeleo ya kiroho yanawezekana kupitia tu baraka ya Yehova.​—Met. 10:22; 1 Kor. 3:6, 7.

12 Kama tulivyoona hapo mbele, Yesu alilisha watu wengi kupitia wachache. Njia aliyotumia ili kutoa chakula cha kiroho ilijulikana waziwazi. Zaidi ya hilo, mitume, waliokuwa washiriki wa kwanza-kwanza wa baraza linaloongoza, walikuwa na ushahidi ulio wazi ili kuonyesha kwamba walitegemezwa na Mungu. Andiko la Matendo 5:12 linasema kwamba ‘kupitia mikono ya mitume ishara nyingi na mambo ya ajabu yaliendelea kutukia kati ya watu.’ * Kwa hiyo, wale waliogeuka kuwa Wakristo hawakuwa na sababu ya kujiuliza, ‘Ni nani kweli ambao Kristo anatumia ili kulisha kondoo wake?’ Lakini, mambo yalibadilika mwishoni mwa wakati wa mitume.

Wakati wa mitume, kulikuwa na ushahidi ulio wazi uliosaidia kujua ni nani Yesu alitumia ili kulisha kutaniko (Ona fungu la 12)

MAGUGU YALIPOKUWA MENGI KULIKO NGANO

13, 14. (a) Yesu alionyesha nini kuhusu kushambuliwa kwa kutaniko la Kikristo, na maneno yake yalianza kutimia wakati gani? (b) Mashambulizi yangetokea pande gani mbili? (Ona maelezo ya kumalizia.)

13 Yesu alitabiri kwamba kutaniko la Kikristo lingeshambuliwa. Kumbuka, katika mufano wake wa kiunabii wa ngano na magugu, Yesu alionyesha kwamba katika shamba ambalo limetoka tu kupandwa ngano (Wakristo watiwa-mafuta) mungepandwa pia magugu (wale wanaojidai kuwa Wakristo). Alionyesha kwamba ngano na magugu yangeendelea kukomalia pamoja, bila kuvunwa, mupaka wakati wa mavuno, ambao ungetokea kwenye ‘umalizio wa mufumo wa mambo.’ (Mt. 13:24-30, 36-43) Kisha tu muda mufupi, maneno ya Yesu yalianza kutimia. *

14 Uasi-imani ulitokea kwa kiasi fulani wakati wa mitume, lakini mitume waaminifu wa Yesu walikuwa “kizuizi;” walizuia kutaniko la Kikristo lisichafuliwe na mafundisho ya uongo. (2 Thes. 2:3, 6, 7) Lakini, mutume wa mwisho alipokufa, uasi-imani ulitia mizizi na kuendelea kwa muda murefu. Wakati huo, magugu yalikuwa mengi kuliko ngano. Hakukuwa tena kikundi kilichopangwa kama lile baraza lililokuwa linaongoza ili kutoa chakula cha kiroho kwa ukawaida. Hata hivyo, hali hiyo ingebadilika mwishowe. Lakini hilo lingetokea wakati gani?

NI NANI ANGETOA CHAKULA WAKATI WA MAVUNO?

15, 16. Wanafunzi wa Biblia waliojifunza maandiko kwa bidii walipata matokeo gani, na hilo linatokeza ulizo gani?

15 Wakati wa kukomaa kwa mbegu ulipokuwa ukimalizika, watu fulani walianza kupendezwa sana na kweli ya Biblia. Kumbuka kwamba katika miaka ya 1870, kikundi kidogo cha watu waliotaka kujua kabisa kweli walijiunga pamoja, na walifanya madarasa ya Biblia, walijitenga na magugu, ni kusema, wale wanaopatikana katika dini zinazojidai kuwa za Kikristo. Watu hao wenye bidii, waliojiita Wanafunzi wa Biblia, walijifunza Biblia kwa unyenyekevu na maoni mazuri, walisali na kuchunguza Maandiko kwa uangalifu.​—Mt. 11:25.

16 Bidii yao ilizaa matunda. Wanaume na wanawake hao waaminifu walifunua mafundisho ya uongo na walitangaza kweli za Biblia kwa kuchapisha na kugawanya vichapo vya Biblia mahali mbalimbali. Kazi yao iligusa mioyo na kusadikisha wengi waliokuwa na njaa na kiu cha ile kweli. Lakini hilo linatokeza ulizo moja la maana sana: Je, wale Wanafunzi wa Biblia wa miaka iliyotangulia 1914 ndio waliokuwa njia ambayo Kristo angetumia ili kulisha kondoo wake? Jibu ni hapana. Wanafunzi hao walikuwa wangali katika kipindi cha kukomaa kwa mbegu, na mupango wa kuwa na kikundi cha kutoa chakula cha kiroho ulikuwa tu bado unaanza. Wakati ulikuwa haujafika ili wale wanaojidai kuwa Wakristo watenganishwe na ngano, ni kusema, Wakristo wa kweli.

17. Ni mambo gani ya maana yaliyoanza kutokea katika 1914?

17 Kama vile tulivyojifunza katika habari iliyotangulia, wakati wa mavuno ulianza katika 1914. Katika mwaka huo, mambo mengi yalianza kutokea. Yesu alitiwa kuwa Mufalme, na siku za mwisho zilianza. (Ufu. 11:15) Kuanzia 1914 mupaka mwanzoni mwa 1919, Yesu alikuja na Baba yake kufanya uchunguzi na usafishaji wa maana wa hekalu la kiroho. * (Mal. 3:1-4) Kisha, kuanzia 1919, ngano ilianza kukusanywa. Je, wakati ulikuwa umefika sasa ili Kristo aweke kikundi kilichopangwa vizuri ambacho angetumia ili kutoa chakula cha kiroho? Bila shaka, ndiyo!

18. Yesu alitabiri kwamba angefanya nini, na kadiri siku za mwisho zilivyoendelea, ni ulizo gani la maana ambalo lilitokezwa?

18 Katika unabii wake kuhusu wakati wa mwisho, Yesu alitabiri kama angeweka kikundi fulani ili kutoa chakula cha kiroho “kwa wakati unaofaa.” (Mt. 24:45-47) Angetumia njia gani? Kama vile tu alivyofanya alipolisha watu kimuujiza, Yesu angelisha tena watu wengi kupitia wachache. Lakini kadiri siku za mwisho zilivyoendelea, ulizo la maana lilitokezwa, Wachache hao watakuwa nani? Tutazungumuzia ulizo hilo na maulizo mengine kuhusu unabii wa Yesu katika habari inayofuata.

 

^ Fungu la 3: Kwenye pindi nyingine, wakati Yesu alilisha kimuujiza wanaume 4 000 bila kuhesabu wanawake na watoto, aliwapatia tena “wanafunzi [chakula], nao wanafunzi wakaugawia umati.”​—Mt. 15:32-38.

^ Fungu la 7: Katika siku za Petro, “kondoo wadogo” wote ambao wangelishwa walikuwa na lile tumaini la kuenda mbinguni.

^ Fungu la 8: Kwa kuwa waamini wapya wote ‘waliendelea kujitoa wenyewe kwa fundisho la mitume,’ hilo linaonyesha kwamba mitume walifundisha kwa ukawaida. Mafundisho fulani ambayo mitume walitolea watu yaliandikwa katika vitabu vilivyoongozwa na roho ya Mungu, ambavyo sasa ni sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

^ Fungu la 12: Hata ikiwa, wanafunzi wengine pia walipokea zawadi za roho ili kufanya miujiza, inaonekana kwamba mara nyingi walipokea zawadi hizo moja kwa moja kupitia mitume ao wakati mitume walikuwa hapo.—Mdo. 8:14-18; 10:44, 45.

^ Fungu la 13: Maneno ya mutume Paulo yanayopatikana katika andiko la Matendo 20:29, 30 yanaonyesha kwamba kutaniko lingeshambuliwa kutoka pande mbili. Kwanza, wale wanaojidai kuwa Wakristo (“magugu”) ‘wangeingia katikati ya’ Wakristo wa kweli. Pili, “kutoka katika” Wakristo wa kweli, wengine wangegeuka kuwa waasi-imani, na kusema “mambo yaliyopotoka.”

^ Fungu la 17: Soma habari “Tazama! Mimi Nipo Pamoja Nanyi Siku Zote,” katika gazeti hili, ukurasa wa 11, fungu la 6.