Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

VITU VYA MAANA SANA VYA HISTORIA YETU

Mufalme Alifurahi Sana!

Mufalme Alifurahi Sana!

HILO lilitokea katika Mwezi wa 8, 1936 kwenye makao ya mufalme wa Swaziland. Kwa kutumia gari lenye vikuza-sauti, ndugu Robert na George Nisbet walikuwa wamemaliza tu kupiga muziki na hotuba zilizorekodiwa za Ndugu Rutherford. Mufalme Sobhuza wa Pili alifurahi sana. Ndugu George anaeleza hivi: “Jambo ambalo lilitushangaza ni kwamba mufalme alitaka tumuuzishe gramafoni (mashine inayotumiwa ili kusikiliza muziki ao hotuba iliyorekodiwa), rekodi, na vikuza​-sauti!”

Robert alimujibu kwa heshima kwamba vitu hivyo si vya kuuzisha. Sababu gani? Sababu vilikuwa mali ya mutu mwengine. Mufalme alitaka ajue mutu huyo.

Ndugu Robert alimuambia kwamba “vilikuwa vya Mufalme mwengine.” Kisha Sobhuza alitaka ajue Mufalme huyo ni nani. Ndugu Robert alisema kwamba Mufalme huyo “ni Yesu Kristo, Mufalme wa Ufalme wa Mungu.”

Kisha kusikia hayo, Mufalme Sobhuza alisema hivi kwa heshima nyingi: “Oh, huyo ni Mufalme mukubwa sana. Sitaki kukamata kitu chochote ambacho ni mali yake.”

Ndugu Robert aliandika hivi: ‘Nilishangazwa sana na hali ya huyo Mutawala Mukubwa, Mufalme Sobhuza. Alizungumuza Kiingereza vizuri na bila kutumia maneno magumu-magumu ao bila kujivuna na alikuwa mwenye kusema mambo waziwazi kabisa na mwenye kukaribiwa kwa urahisi. Nilikaa pamoja naye kwa dakika 45 hivi katika biro yake, naye George alikuwa anapiga muziki inje.’

Robert anaendelea kusema hivi: ‘Baadaye siku hiyo, tulitembelea Masomo ya Kitaifa ya Swaziland ambako tulijionea jambo moja lenye kupendeza sana. Tulimuhubiria kiongozi wa masomo hayo, na alitusikiliza vizuri. Tuliposema kwamba tumekuja na gramafoni na kwamba tulitaka awaruhusu wanafunzi wote wasikilize hotuba zenye kurekodiwa, alifurahi sana na aliwaomba wanafunzi wote wakae kwenye majani ili wasikilize. Tuliambiwa kwamba masomo hayo inawafundisha vijana ukulima, kutunza bustani, useremala, ujenzi, Kiingereza, na hesabu; na inawafundisha binti kuwatunza wagonjwa, kazi za nyumbani, na kazi zingine za lazima. Tate ao nkambo mwanamuke wa huyo Mutawala Mukubwa ndiye aliyeanzisha masomo hayo.’

Wanafunzi wa masomo ya segondere waliosikiliza hotuba katika 1936 huko Swaziland

Kuanzia 1933, Mufalme Sobhuza alisikiliza kwa furaha mapainia waliotembelea makao yake ya kifalme. Wakati mumoja, alikuwa amewakusanya askari wake walinzi 100 ili wasikilize rekodi za ujumbe wa Ufalme. Alijiandikisha ili apokee magazeti kwa ukawaida na alikubali vichapo vyetu. Kisha tu muda muchache, maktaba yake ilijaa vichapo vya Biblia! Zaidi ya hayo, alichunga sana maktaba yake hata ikiwa serikali ya kikoloni ya Uingereza ilikuwa imekataza vichapo vyetu wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu.

Mufalme Sobhuza wa Pili aliendelea kuwakaribisha Mashahidi wa Yehova kwenye makao yake ya kifalme huko Lobamba, hata aliita viongozi wa kidini waje kusikiliza hotuba zao za Biblia. Shahidi mumoja wa mahali hapo anayeitwa Helvie Mashazi alipokuwa anazungumuzia Mathayo sura ya 23, kikundi kimoja cha viongozi wa dini kilijitokeza kikiwa na hasira na kujaribu kumulazimisha akae chini. Lakini Mufalme alimutetea, na alimuomba Ndugu Mashazi aendelee kuzungumuza. Tena, Mufalme aliwaomba wasikilizaji wote waandike maandiko yote ambayo ndugu Mashazi alizungumuzia katika hotuba yake!

Kisha kusikiliza hotuba moja iliyotolewa na ndugu mumoja painia, viongozi wane wa dini walificha mikufu yao ya shingoni na kusema hivi: “Hatuko tena viongozi wa dini, sasa sisi ni Mashahidi wa Yehova.” Kisha, walimuomba painia huyo vichapo kama vile walivyoona kwa Mufalme.

Kuanzia miaka ya 1930 mupaka kifo chake kilichotokea katika 1982, Mufalme huyo aliendelea kuheshimu Mashahidi wa Yehova na hakuruhusu wateswe kwa sababu ya kutoshika desturi za Waswazi. Kwa hiyo, Mashahidi walikuwa na sababu nzuri ya kumushukuru, na walihuzunika kabisa alipokufa.

Mwanzoni mwa 2013, kulikuwa wahubiri wa Ufalme zaidi ya 3000 katika Swaziland. Inchi hiyo ina wakaaji zaidi ya milioni moja, na kila muhubiri anapaswa kuhubiria watu 384 tu. Mapainia zaidi ya 260 walikuwa wanatumikia katika makutaniko 90, na watu 7496 walihuzuria Ukumbusho katika 2012. Ni wazi kwamba kutakuwa na ongezeko kubwa wakati ujao. Mashahidi waliotembelea Swaziland katika miaka ya 1930 waliweka musingi muzuri kabisa.​—Imechukuliwa kutoka vitu vya maana sana vya historia yetu huko Afrika Kusini.