Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Chukua Maamuzi kwa Hekima

Chukua Maamuzi kwa Hekima

‘Mutegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe.’​—MET. 3:5.

1, 2. Je, unafurahia kuchukua maamuzi, na una maoni gani kuhusu maamuzi fulani ambayo umechukua?

 MAAMUZI! Maamuzi! Kila siku tunalazimishwa kuchukua maamuzi. Unaona jambo hilo namna gani? Watu fulani wako tayari kujiamulia kila jambo. Wanafikiri kwamba wana haki ya kujiamulia kila kitu, na hawapendi mutu mwingine awaamulie. Lakini, kuna pia wale wanaoogopa kuchukua maamuzi ya maana maishani. Wengine wanatafuta mashauri katika vitabu ao kwa washauri fulani na wanatumia hata feza nyingi ili wapate mashauri yatakayowasaidia wachukue maamuzi mazuri.

2 Wengi kati yetu ni wenye kusita-sita wakati fulani. Ni kweli kwamba hatuna uwezo juu ya mambo yote, na hatuwezi kuamua kuhusu kila jambo; lakini, inapendeza kujua kwamba katika mambo mengi maishani, tunaweza kuchukua maamuzi kulingana na mapendezi yetu. (Gal. 6:5) Hata hivyo, tunakubali kwamba kila mara hatuchukue maamuzi yenye hekima wala yenye faida.

3. Yehova ametutolea nini ili kutusaidia kuchukua maamuzi mazuri, lakini tuna tatizo gani?

3 Sisi watumishi wa Yehova, tunaweza kufurahi kwa kuwa Yehova ametutolea miongozo iliyo wazi kuhusu mambo mengi ya lazima katika maisha yetu. Tunajua kwamba ikiwa tunafuata miongozo hiyo, tunaweza kuchukua maamuzi yatakayotuletea faida na kumufurahisha Yehova. Hata hivyo, wakati fulani tunajikuta katika hali ambamo tunapaswa kuchukua maamuzi kuhusu mambo fulani ambayo Biblia haizungumuzie waziwazi. Katika hali hiyo, tutaamua namna gani? Kwa mufano, tunajua kwamba hatupaswe kuiba. (Efe. 4:28) Lakini kuiba kunamaanisha nini kabisa? Je, kuiba kunategemea samani ao bei ya kitu kilichochukuliwa, nia ya mutu aliyekichukua, ao jambo lingine? Tutachukua uamuzi gani kuhusu mambo ambayo watu fulani wanafikiri kwamba hakuna muongozo ulio wazi kabisa? Ni nini itatuongoza?

TUMIA AKILI NZURI

4. Ni shauri gani ambalo labda tulipewa tulipotaka kuchukua uamuzi fulani?

4 Tunapoambia Mukristo mwenzetu kwamba tunataka kuchukua uamuzi fulani wa maana sana, anaweza kutushauri tutumie akili iliyo timamu ao akili nzuri. Bila shaka, hilo ni shauri nzuri. Biblia inatushauri tuepuke kuamua haraka​-haraka inaposema hivi: ‘Kila mutu anayetenda haraka​-haraka bila shaka anaelekea uhitaji.’ (Met. 21:5) Lakini inamaanisha nini kutumia akili nzuri? Je, inamaanisha tu kungoja muda fulani upite, kufikiri sana, kufikiria maoni ya wengine, na kuelewa mambo vizuri mbele ya kuchukua maamuzi? Mambo yote hayo yanasaidia kuchukua uamuzi muzuri, lakini kutumia akili nzuri kunatia ndani mambo mengi zaidi.​—Rom. 12:3; 1 Pet. 4:7.

5. Sababu gani hatuna akili yenye kukamilika?

5 Tunapaswa kukubali kwamba hakuna hata mumoja kati yetu anayezaliwa na akili yenye kukamilika. Sababu gani? Kwa sababu sisi wote tunazaliwa katika zambi na hatukamilike, kwa hiyo hatuzaliwe hata kidogo na mwili ao akili yenye kukamilika. (Zab. 51:5; Rom. 3:23) Tena, wakati fulani wengi kati yetu walikuwa kati ya wale ambao akili zao ‘zilipofushwa’ na Shetani; wakati fulani hatukujua Yehova na kanuni zake za haki. (2 Kor. 4:4; Tito 3:3) Kwa hiyo, hata ikiwa mutu anaweza kufikiri sana mbele ya kuchukua maamuzi fulani kulingana tu na mambo anayoona kuwa sawa, anaweza kujidanganya na kuchukua maamuzi mabaya.​—Met. 14:12.

6. Tunapaswa kufanya nini ili kuwa na akili nzuri?

6 Hata ikiwa hatukuzaliwa na mwili na akili yenye kukamilika, Baba yetu wa mbinguni, Yehova, ni mukamilifu katika kila jambo. (Kum. 32:4) Ni jambo lenye kufurahisha kujua kwamba ametusaidia kufanya upya nguvu zetu za kufikiri na kuwa na akili nzuri. (Soma 2 Timotheo 1:7.) Sisi Wakristo, tunapaswa kufikiri kwa uzito na kutenda kwa hekima. Tunapaswa kutawala, ao kuongoza, mawazo na maoni yetu na kuiga namna Yehova anavyofikiri, anavyojisikia na anavyotenda.

7, 8. Toa mufano unaoonyesha kwamba inawezekana kuchukua uamuzi muzuri ijapokuwa mukazo wa wengine ao matatizo.

7 Fikiria mufano huu. Kwa kawaida, watu fulani waliohamia katika inchi nyingine wanapozaa watoto, wanawatuma kwa watu wa jamaa yao ili wao waendelee kutumika na kuchuma feza. Mama mumoja anayeishi katika inchi ya kigeni alizaa mutoto mwanaume mwenye sura nzuri. Kisha, alianza kujifunza Biblia na kufanya maendeleo ya kiroho. Marafiki zake na watu wa jamaa walianza kumusumbua sana yeye na bwana yake ili watume mutoto huyo nyumbani kwa wazazi wa bwana yake. * Lakini, kupitia funzo lake la Biblia, mama huyo alitambua kwamba kulea mutoto huyo, ni daraka alilopewa na Mungu. (Zab. 127:3; Efe. 6:4) Je, angefuata desturi hiyo ambayo wengi waliona kuwa sawa? Ao angefuata yale aliyokuwa akijifunza katika Biblia na kukubali kuishi na feza kidogo hata ikiwa atachekwa na watu fulani? Ingekuwa wewe, ungefanya nini?

8 Kwa kuwa alihangaishwa na jambo hilo, mama huyo alimuelezea Yehova yote yaliyokuwa katika moyo wake, ili kupata muongozo wake. Alipozungumuza na dada aliyekuwa akijifunza naye Biblia na washiriki wengine wa kutaniko kuhusu tatizo lake, alianza kutambua maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo. Alifikiria pia namna watoto wanavyoumia moyoni wanapotenganishwa na wazazi wao wakati wangali wachanga. Kisha kufikiria yale ambayo Maandiko yanasema kuhusu jambo hilo, aliona kwamba kutuma mutoto wake si uamuzi muzuri. Bwana yake aliona namna washiriki wa kutaniko walivyomutegemeza na namna mutoto wao alivyokuwa mwenye furaha na afya nzuri. Kwa hiyo, alikubali kujifunza Biblia na akaanza kuhuzuria mikutano pamoja na bibi yake.

9, 10. Kutumia akili nzuri kunamaanisha nini, na namna gani tunaweza kufanya hivyo?

9 Huo ni mufano mumoja unaoonyesha kwamba kutumia akili nzuri hakumaanishe tu kwamba tunapaswa kufuata yale ambayo wengine wanaona kuwa sawa ao rahisi. Akili na moyo wetu usiokamilika vinaweza kufananishwa na saa inayotembea mbio sana ao polepole sana. Kuongozwa na saa hiyo kunaweza kuwa na matokeo mabaya sana. (Yer. 17:9) Tunapaswa kuacha akili na moyo wetu viongozwe na kanuni za Mungu.​—Soma Isaya 55:8, 9.

10 Biblia ina sababu nzuri ya kutushauri hivi: ‘Mutegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mutambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.’ (Met. 3:5, 6) Ona kwamba Biblia inasema “usitegemee uelewaji wako mwenyewe,” kisha inasema ‘Mutambue [Yehova].’ Ni Yeye aliye na akili yenye kukamilika kabisa. Kwa hiyo, tunapokuwa na uamuzi wa kuchukua, tunapaswa kutafuta maoni ya Mungu katika Biblia. Kisha, tunapaswa kuchukua uamuzi unaotegemea Biblia. Hiyo ndiyo maana ya kutumia akili nzuri, ni kusema, kutenda kulingana na maoni ya Yehova.

ZOEZA NGUVU ZAKO ZA UFAHAMU

11. Ni jambo gani linaloweza kumusaidia mutu ajifunze kuchukua maamuzi yenye hekima?

11 Si rahisi kujifunza kuchukua maamuzi yenye hekima na kutenda kulingana nayo. Hilo linaweza kuwa vigumu zaidi sana kwa wapya katika kweli ao kwa wale wanaoanza kujikaza kufanya maendeleo ya kiroho. Lakini, wapya hao, ambao Biblia inaita watoto wachanga kiroho, wanaweza kufanya maendeleo mazuri. Fikiria namna mutoto muchanga anavyojifunza kutembea bila kuanguka. Mara nyingi, jambo linalomusaidia ni kufanya hatua fupi-fupi na kufanya hivyo tena na tena. Ni hivyo pia kuhusu mutoto muchanga kiroho anapotaka kuchukua maamuzi ya hekima. Kumbuka kwamba mutume Paulo alionyesha kwamba watu wenye kukomaa kiroho ni “wale ambao kwa kutumia, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” Maneno “kwa kutumia” na “zimezoezwa” yanaonyesha kwamba inaomba kuendelea kujikaza na kufanya hivyo tena na tena; na hilo ndilo jambo ambalo wapya wanahitaji kufanya.​—Soma Waebrania 5:13, 14.

Tunazoeza uwezo wetu wa ufahamu kwa kuchukua maamuzi mazuri katika mambo tunayofanya kila siku (Ona fungu la 11)

12. Namna gani tunaweza kuzoeza uwezo wetu wa kuchukua maamuzi yenye hekima?

12 Kama tulivyoona hapo mbele, kila siku tunapaswa kuchukua maamuzi mengi, makubwa na madogo. Kulingana na utafiti fulani, matendo 40 kati ya 100 tunayofanya yanategemea mambo ambayo tumezoea sana kufanya wala si mambo tunayofikiria kimbele. Kwa mufano, labda kila asubuhi unapaswa kuamua ni mavazi gani utakayovaa. Unaweza kufikiri kwamba hilo ni jambo ndogo, na kuamua bila kufikiri sana, zaidi sana ikiwa umechelewa. Lakini ni jambo la maana kujua ikiwa mavazi hayo yanakustahili wewe mutumishi wa Yehova. (2 Kor. 6:3, 4) Unaponunua mavazi, labda unafikiria kwanza mutindo wa mavazi, lakini je, unafikiria pia ikiwa ni mavazi yenye kiasi na ikiwa una feza za kutosha ili kuyanunua? Kuchukua maamuzi mazuri katika mambo kama hayo kutatusaidia kuzoeza nguvu zetu za ufahamu, jambo ambalo litatuwezesha tuchukue maamuzi mazuri katika mambo makubwa.​—Lu. 16:10; 1 Kor. 10:31.

KOMALISHA NIA YA KUFANYA MEMA

13. Tunahitaji nini ili kutenda kulingana na maamuzi yetu?

13 Sisi wote tunajua kwamba haitoshe tu kuchukua maamuzi mazuri, lakini tunapaswa pia kutenda kulingana nayo. Kwa mufano, watu fulani wanaotaka kuacha kuvuta tumbako wanashindwa kwa sababu hawana kabisa nia ya kufanya hivyo. Jambo tunalopaswa kufanya ni kuazimia kutenda kulingana na uamuzi wetu. Watu fulani wanaamini kwamba nia inaweza kufananishwa kabisa na mwili wetu. Tunapoendelea kufanya mazoezi, mwili wetu unakuwa nguvu hata zaidi. Ikiwa tunafanya mazoezi mara chache, mwili wetu utakuwa zaifu. Kwa hiyo basi, ni nini inayoweza kutusaidia tuwe na nia ya kushikamana na maamuzi yetu na kutenda kulingana nayo? Kutafuta musaada wa Yehova kunaweza kutusaidia.​—Soma Wafilipi 2:13.

14. Ni nani aliyemutolea mutume Paulo nguvu ya kufanya yale aliyojua kwamba alipaswa kufanya?

14 Mutume Paulo alijua ukweli huo kupitia mambo aliyojionea. Wakati fulani aliomboleza hivi: “Nina uwezo wa kutaka, bali uwezo wa kufanya yaliyo mazuri haupo.” Alijua lile alilopenda kufanya ao lile ambalo alipaswa kufanya, lakini mara kwa mara jambo fulani lilimuzuia. Alisema waziwazi hivi: ‘Kwa kweli naipenda sheria ya Mungu kulingana na mutu niliye kwa ndani, lakini mimi naona ndani ya viungo vyangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya zambi iliyo ndani ya viungo vyangu.’ Je, alikata tamaa? Hapana kabisa. Alisema hivi: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Rom. 7:18, 22-25) Katika barua nyingine, aliandika hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”​—Flp. 4:13.

15. Kutenda kulingana na maamuzi yaliyochukuliwa ao kusita-sita kunaweza kuwa na matokeo gani?

15 Bila shaka, ili kumupendeza Mungu, tunapaswa kutenda bila kusita-sita. Kumbuka maneno ambayo nabii Eliya aliwaambia waabudu wa Baali na Waisraeli waasi​-imani kwenye Mulima Karmeli: ‘Mutayumba​-yumba juu ya maoni mawili tofauti mupaka wakati gani? Ikiwa Yehova ndiye Mungu wa kweli, mufuateni yeye; lakini ikiwa ni Baali, mufuateni yeye.’ (1 Fal. 18:21) Wana wa Israeli walijua yale waliyopaswa kufanya, lakini ‘waliyumba​-yumba’ na kukosa musimamo. Lakini, miaka mingi baadaye, Yoshua alituachia mufano muzuri kabisa alipoambia Waisraeli hivi: ‘Ikiwa munaona ni vibaya machoni penu kumutumikia Yehova, jichagulieni leo yule mutakayemutumikia. Lakini mimi na nyumba yangu, tutamutumikia Yehova.’ (Yos. 24:15) Azimio lake lilikuwa na matokeo gani? Yoshua na wale walioshikamana naye walibarikiwa na kuingia katika Inchi ya Ahadi, ‘inchi iliyotiririka maziwa na asali.’​—Yos. 5:6.

CHUKUA MAAMUZI KWA HEKIMA ILI UPATE BARAKA

16, 17. Toa mufano unaoonyesha namna kuchukua maamuzi kulingana na mapenzi ya Mungu kunavyoleta faida nyingi.

16 Tufikirie mufano fulani wa siku hizi. Ndugu mumoja aliyebatizwa hivi karibuni ameoa na ana watoto wadogo watatu. Siku moja, mufanyakazi mwenzake alimuambia wahamie katika kompanyi ingine ambako watalipwa mushahara muzuri na kupata faida nyingi. Ndugu yetu alifikiri na kusali kuhusu jambo hilo. Kazi aliyokuwa nayo ilikuwa na mushahara mudogo, lakini aliichagua kwa sababu katika kompanyi hiyo hawatumike Siku ya Posho na Siku ya Yenga, kwa hiyo alikuwa na wakati wa kukusanyika na kuhubiri pamoja na familia yake. Alitambua kwamba ikiwa anakubali kazi hiyo mupya, hatapata hata kidogo wakati wa kukusanyika na kuhubiri pamoja na familia yake. Ingekuwa wewe, ungefanya nini?

17 Alipolinganisha faida za kiroho na mushahara muzuri, ndugu huyo alikataa kazi hiyo. Je, unafikiri kwamba baadaye alisikitikia uamuzi wake? Hata kidogo. Alitambua kwamba faida za kiroho ambazo yeye na familia yake wangepata ni za maana sana kuliko mushahara muzuri ambao angepewa. Yeye na bibi yake walifurahi sana wakati binti wao mukubwa, mwenye miaka 10, aliwaambia kwamba anawapenda, anapenda ndugu na dada na anapenda Yehova sana. Aliwaambia kwamba alitaka kujitoa kwa Yehova na kubatizwa. Bila shaka, alipendezwa sana na mufano muzuri wa baba yake wa kutia ibada ya Yehova pa nafasi ya kwanza katika maisha yake!

Chukua maamuzi yenye hekima ili upate furaha kati ya watu wa Mungu (Ona fungu la 18)

18. Sababu gani ni jambo la maana tuchukue maamuzi kwa hekima kila siku?

18 Kwa miaka mingi, Musa Mukubwa, ni kusema, Yesu Kristo, amekuwa akiwaongoza waabudu wa kweli wa Yehova katika ulimwengu huu wa Shetani ulio kama jangwa. Yesu, ambaye pia ni Yoshua Mukubwa, iko tayari kuharibu ulimwengu huu muovu na kuongoza wafuasi wake kwenye ulimwengu mupya na wenye haki ulioahidiwa. (2 Pet. 3:13) Kwa hiyo, huu si wakati wa kurudilia namna yetu ya kufikiri ya zamani, tabia, mwenendo na miradi yetu ya zamani. Huu ni wakati wa kutafuta kujua vizuri zaidi yale ambayo Mungu anataka tufanye. (Rom. 12:2; 2 Kor. 13:5) Acheni basi, maamuzi yetu ya kila siku yaonyeshe kwamba sisi ni aina ya watu wanaostahili kupokea baraka za milele.​—Soma Waebrania 10:38, 39.

^ Watu wengine wanatuma watoto wao wachanga nyumbani ili nkambo ao tate yao awaonyeshe kwa marafiki ao watu wa jamaa.