Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Furahia Vikumbusho vya Yehova

Furahia Vikumbusho vya Yehova

‘Nimevichukua vikumbusho vyako kuwa ni uriti mupaka wakati usio na kipimo.’​—ZAB. 119:111.

1. (a) Wanadamu wanatenda namna gani wanapotolewa vikumbusho ao mashauri, na sababu gani? (b) Kiburi kinaweza kumufanya mutu atende namna gani anaposhauriwa?

 WANADAMU wanaitikia kwa njia tofauti wanapopewa mashauri. Mutu anaweza kuwa tayari kukubali kikumbusho ao shauri linalotolewa na mutu mwenye mamlaka, lakini anaweza kuzarau shauri la mutu wa hali kama yake ao wa hali ya chini. Pia namna watu wanavyojisikia wanapopewa nizamu ao shauri inatofautiana sana. Mutu anaweza kuhuzunika, kujisikia kwamba haheshimiwe, kujisikia ametiwa moyo, anaweza kufikiri kwamba anachukiwa, ao anaweza kufikiri kwamba shauri ao nizamu hiyo inamufaa. Sababu gani wengine hawakubali shauri? Sababu moja ni kiburi. Kwa kweli, kiburi kinaweza kupotosha namna mutu anavyoona mambo, na kumufanya atupilie mbali shauri fulani la lazima.​—Met. 16:18.

2. Sababu gani Wakristo wa kweli wanasamini mashauri ya Neno la Mungu?

2 Kwa upande mwingine, Wakristo wa kweli, wanasamini mashauri mazuri, zaidi sana ikiwa mashauri hayo yanatoka katika Neno la Mungu. Vikumbusho vya Yehova vinatutolea hekima, vinatufundisha na kutusaidia tuepuke mitego kama vile kufuatia vitu vya kimwili, uasherati, dawa za kulewesha ao kunywa pombe kupita kiasi. (Met. 20:1; 2 Kor. 7:1; 1 Thes. 4:3-5; 1 Tim. 6:6-11) Zaidi ya hilo, tunafurahia “hali nzuri ya moyo” inayotokana na kutii vikumbusho vya Mungu.​—Isa. 65:14.

3. Ni maoni gani ya mutunga​-zaburi ambayo tunapaswa kuiga?

3 Ili tulinde uhusiano wetu wa maana sana pamoja na Baba yetu wa mbinguni, tunapaswa kuendelea kutumia mashauri yake yenye hekima katika maisha yetu. Ni vizuri sana ikiwa tutakuwa na maoni kama ya mutunga​-zaburi aliyeandika hivi: ‘Nimevichukua vikumbusho vyako kuwa ni uriti mupaka wakati usio na kipimo, kwa maana hivyo ni furaha ya moyo wangu’! (Zab. 119:111) Je, sisi pia tunafurahia amri za Yehova, ao nyakati fulani tunaziona kuwa muzigo muzito? Hata kama wakati fulani mashauri ambayo tunapewa yanaweza kutuumiza, tusivunjike moyo. Tunaweza kutegemea bila kuyumba​-yumba hekima ya Mungu iliyo juu sana! Acheni tuzungumuzie njia tatu zitakazotusaidia tutegemee vikumbusho vya Yehova bila kuyumba​-yumba.

SALA

4. Ni jambo gani ambalo Daudi aliendelea kufanya katika maisha yake?

4 Mufalme Daudi alipata furaha na magumu katika maisha yake, lakini kuna jambo ambalo hakuacha kufanya: Aliendelea kumutegemea Muumba wake. Alisema hivi: “Kwako wewe, Ee Yehova, naiinua nafsi yangu. Ee Mungu wangu, nimekutegemea wewe.” (Zab. 25:1, 2) Ni nini kilichomusaidia Daudi aendelee kumutumainia hivyo Baba yake wa mbinguni?

5, 6. Neno la Mungu linatuambia nini kuhusu uhusiano ambao Daudi alikuwa nao pamoja na Yehova?

5 Watu wengi wanasali tu wakati wa shida. Unawaza nini ikiwa una rafiki ao jirani anayekutafuta tu wakati anahitaji feza ao mambo mengine? Kila mara utakapomuona, unaweza kuanza kufikiri kwamba labda anakutafuta tu kwa sababu ya feza. Lakini, Daudi hakuwa hivyo. Katika maisha yake yote, iwe wakati wa furaha ao wakati wa magumu, alikuwa na uhusiano muzuri pamoja na Mungu kwa sababu ya imani na upendo wake kwa Mungu.​—Zab. 40:8.

6 Ona maneno ambayo Daudi alitumia ili kumusifu na kumushukuru Yehova: “Ee Yehova Bwana wetu, jina lako ni lenye utukufu kama nini katika dunia yote, wewe ambaye utukufu wako unasimuliwa juu ya mbingu!” (Zab. 8:1) Je, maneno hayo hayakuonyeshe kwamba Daudi alikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Baba yake wa mbinguni? Daudi alisamini ukubwa na utukufu wa Mungu, na hilo lilimuchochea amusifu Yehova ‘muchana kutwa.’​—Zab. 35:28.

7. Tunafaidika namna gani tunapomukaribia Mungu kupitia sala?

7 Kama Daudi, sisi pia tunahitaji kuzungumuza na Yehova kwa ukawaida ili tuendelee kumutegemea. Biblia inasema hivi: ‘Mukaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.’ (Yak. 4:8) Kumukaribia Mungu kupitia sala ni njia ya maana inayotusaidia kupata roho takatifu.​—Soma 1 Yohana 3:22.

8. Sababu gani tunapaswa kuepuka kutumia maneno yaleyale tunaposali?

8 Unaposali, je una muelekeo wa kutumia maneno yaleyale mara kwa mara? Ikiwa ndiyo, jaribu kufikiri kidogo kuhusu yale unayotaka kusema mbele ya kusali. Ikiwa unatumia maneno yaleyale unapozungumuza na rafiki ao mushiriki wa jamaa yako, je, atafurahia jambo hilo? Bila shaka, ataacha kukusikiliza. Ni kweli kwamba, Yehova hawezi kukataa kusikiliza sala inayotoka moyoni ya mutumishi wake mwaminifu. Lakini, tunapaswa kuepuka kutumia maneno yaleyale tunapozungumuza naye.

9, 10. (a) Tunaweza kusali kuhusu nini? (b) Ni nini inayoweza kutusaidia tumutolee Yehova sala za kutoka moyoni?

9 Bila shaka, hatuwezi kusali kijuu-juu tu ikiwa tunataka kumukaribia Mungu. Ikiwa tunaendelea kumufunulia Yehova mambo yaliyo katika moyo wetu, tutamukaribia na kumutumainia zaidi. Kwa hiyo basi, tunapaswa kusali kuhusu nini? Neno la Mungu linajibu hivi: “Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.” (Flp. 4:6) Kwa hiyo, tunapaswa kusali kuhusu jambo lolote linalohusu maisha yetu ao uhusiano wetu na Mungu.

10 Tunaweza kujifunza mambo mengi kutokana na maneno ambayo wanaume na wanawake waaminifu wa zamani walisema katika sala zao zinazopatikana katika Biblia. (1 Sam. 1:10, 11; Mdo. 4:24-31) Kitabu cha Zaburi kinajaa sala za kutoka moyoni na nyimbo za kumusifu Yehova. Sala na nyimbo hizo zinaonyesha namna mbalimbali ambavyo wanadamu wanajisikia moyoni, kama vile huzuni na furaha. Kuchunguza maneno hayo ya watumishi waaminifu kunaweza kutusaidia tumutolee Yehova sala za kutoka moyoni.

KUTAFAKARI

11. Sababu gani tunapaswa kutafakari juu ya mashauri ya Mungu?

11 Daudi alisema hivi: ‘Kikumbusho cha Yehova ni chenye kutegemeka, kinamufanya asiye na uzoefu awe na hekima.’ (Zab. 19:7) Bila shaka, hata ikiwa hatuna uzoefu, tunaweza kuwa wenye hekima ikiwa tunatii amri za Mungu. Hata hivyo, tunapaswa kutafakari ili tufaidike vizuri kabisa na mashauri fulani ya Maandiko. Tunapaswa kutafakari kuhusu namna tunavyoweza kulinda uaminifu wetu tunapochochewa kufanya mabaya na wanafunzi ao wafanyakazi wenzetu, namna ya kutii amri ya Mungu kuhusu damu, kutojiingiza katika siasa, na kutumia mashauri ya Biblia kuhusu mavazi na kujipamba. Kuwa na maoni ya Mungu juu ya mambo hayo kutatusaidia tujitayarishe kupambana na majaribu yanayoweza kutokea. Kisha tunaweza kuamua katika moyo wetu jambo ambalo tunapaswa kufanya ikiwa jaribu fulani linajitokeza. Kufikiria na kuamua jambo la kufanya mbele ya wakati kunaweza kutuepusha na matatizo mengi.​—Met. 15:28.

12. Ni maulizo gani yanayoweza kutusaidia tuendelee kushikamana na vikumbusho vya Mungu?

12 Kwa kuwa tunangojea utimizo wa ahadi za Mungu, je, maisha yetu yanaonyesha kwamba tunaendelea kuwa macho kiroho? Kwa mufano, je, tunaamini kabisa kwamba Babiloni Mukubwa ataharibiwa hivi karibuni? Je, baraka ambazo tunangojea, kama vile uzima wa milele katika paradiso, zingali zinatuvutia kama vile tulipozisikia kwa mara ya kwanza? Je, tunaendelea kuhubiri kwa bidii ao tumeacha mambo ya kimwili yachukue nafasi ya kwanza katika maisha yetu? Tuseme nini kuhusu tumaini la ufufuo, kutakaswa kwa jina la Yehova, na kutetewa kwa haki yake ya kutawala? Je, mambo hayo yangali ya maana kwetu? Kutafakari juu ya maulizo hayo kunaweza kutusaidia tuchukue ‘vikumbusho vya Mungu kuwa uriti mupaka wakati usio na kipimo’ kama vile mutunga​-zaburi alivyosema.​—Zab. 119:111.

13. Sababu gani Wakristo wa kwanza​-kwanza hawakuelewa mambo fulani? Toa mufano.

13 Labda kwa sasa hatuelewe vizuri mambo fulani yanayozungumuziwa katika Biblia kwa sababu wakati haujafika ili Yehova atusaidie kuyaelewa. Yesu aliwaambia mitume wake mara kwa mara kwamba lilikuwa jambo la lazima ateseke na kufa. (Soma Mathayo 12:40; 16:21.) Lakini mitume wake hawakuelewa maana ya maneno hayo. Walielewa maana ya maneno hayo kisha kufa na kufufuliwa kwake wakati alivaa mwili wa kibinadamu na kuwatokea wanafunzi wengi, na ‘kufungua akili zao ili kuifahamu maana ya Maandiko.’ (Lu. 24:44-46; Mdo. 1:3) Vivyo hivyo, mbele ya roho takatifu kumwangwa juu yao kwenye Pentekoste ya 33, wafuasi wa Kristo hawakuelewa kwamba Ufalme wa Mungu ungesimamishwa huko mbinguni.​—Mdo. 1:6-8.

14. Mwanzoni mwa miaka ya 1900, ni mufano gani muzuri ambao ndugu zetu walituachia ijapokuwa hawakuelewa mambo vizuri kuhusu siku za mwisho?

14 Vivyo hivyo, mwanzoni mwa miaka ya 1900, Wakristo wa kweli walikuwa na matazamio mengi yasiyo ya kweli kuhusu “siku za mwisho.” (2 Tim. 3:1) Kwa mufano, katika mwaka wa 1914, Wakristo fulani walifikiri kwamba walikuwa karibu kuchukuliwa ili kwenda mbinguni. Kwa kuwa matumaini yao hayakutimizwa wakati huo, walichunguza tena Maandiko na kuvumbua kwamba kazi kubwa ya kuhubiri ilikuwa inawangojea. (Mk. 13:10) Kwa hiyo, katika mwaka wa 1922, Ndugu Rutherford, aliyekuwa akiongoza kazi ya kuhubiri wakati huo, aliwaambia wale waliokusanyika kwenye mukusanyiko wa kimataifa huko Cedar Point, Ohio, Amerika: “Tazameni, Mufalme anatawala! Ninyi ndio mawakili wake. Kwa hiyo tangazeni, tangazeni, tangazeni, Mufalme na ufalme wake.” Tangu wakati huo na kuendelea, kazi ya kutangaza “habari njema ya ufalme” imekuwa alama inayowatambulisha watumishi wa Yehova leo.​—Mt. 4:23; 24:14.

15. Namna gani tunaweza kufaidika tunapotafakari kuhusu namna ambavyo Mungu ameshugulika na watumishi wake?

15 Kutafakari kuhusu namna ambavyo Yehova ameshugulikia kwa njia nzuri watumishi wake, wa zamani na wa leo, kunatusaidia tuwe hakika kabisa kwamba Yehova ana uwezo wa kutimiza mapenzi na makusudi yake wakati unaokuja. Tena, vikumbusho vya Mungu vinatusaidia tuendelee kukumbuka na kungojea utimizo wa unabii mbalimbali ambao haujatimizwa. Tunaweza kuwa hakika kwamba kufanya hivyo kutatusaidia tuamini ahadi za Mungu.

MATENDO YA IMANI

16. Kuendelea kumutumikia Mungu kwa bidii kunatuletea faida gani?

16 Mungu wetu Yehova, ni Mungu mwenye nguvu anayetenda mambo ya ajabu. Mutunga​-zaburi aliuliza hivi: “Ni nani aliye na nguvu kama wewe, Ee Yah?” Na akaongeza hivi: ‘Mukono wako una nguvu, mukono wako wa kuume umeinuliwa.’ (Zab. 89:8, 13) Kupatana na hilo, Yehova anapendezwa sana na jitihada tunazofanya ili kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza na anabariki jitihada hizo. Anaona kwamba watumishi wake​—wanaume ao wanawake, vijana ao wazee​—hawakae bila kufanya jambo lolote na hawale ‘mukate wa uvivu.’ (Met. 31:27) Tunamuiga Muumbaji wetu kwa kuendelea kuwa na mengi ya kufanya katika kazi yake. Mungu anafurahia sana utumishi tunaomutolea kwa moyo wetu wote, kwa hiyo anatubariki na kubariki utumishi wetu.​—Soma Zaburi 62:12.

17, 18. Sababu gani tunaweza kusema kwamba matendo ya imani yanatusaidia kutegemea muongozo wa Yehova? Toa mufano.

17 Namna gani matendo ya imani yanatusaidia tumutegemee Yehova? Fikiria simulizi la Biblia kuhusu namna Waisraeli walivyoingia katika Inchi ya Ahadi. Yehova alikuwa amewaagiza makuhani wachukue sanduku la agano na kuingia katika Muto Yordani. Lakini, Waisraeli wengine walipokuwa wakikaribia muto huo, waliona kwamba mvua ya majira ya kuchipua ilikuwa imeufanya muto ujae sana. Waisraeli wangefanya nini? Je, wangebaki pembeni ya muto na kungojea majuma fulani ao muda murefu zaidi mupaka wakati maji yangepunguka? Sivyo, walimutegemea kabisa Yehova na kufuata muongozo wake. Matokeo yalikuwa nini? Biblia inasema: ‘Mara tu miguu ya makuhani waliolichukua Sanduku ilipotumbukizwa katika maji ya ukingoni, ndipo maji yanayoshuka kutoka juu yakaanza kusimama, . . . wakati huohuo wale makuhani wakaendelea kusimama bila kusonga kwenye inchi kavu na watu wakavuka mbele ya Yeriko.’ (Yos. 3:12-17) Wazia namna gani walitiwa moyo walipoona maji hayo mengi yakisimama! Bila shaka, imani ya Waisraeli katika Yehova ilitiwa nguvu kwa sababu walitegemea uongozi wake.

Je, utaonyesha kwamba unamutegemea Yehova kama vile Waisraeli wa siku za Yoshua? (Ona fungu la 17 na 18)

18 Ni kweli kwamba leo Yehova hafanye miujiza kama hiyo kwa ajili ya watu wake, lakini anabariki matendo yao ya imani. Roho yake inawapa nguvu ya kutimiza kazi aliyowatolea ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme ulimwenguni pote. Tena, kisha ufufuo wake, Shahidi wa kwanza wa Yehova, ambaye ni Kristo Yesu, aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba atawategemeza katika kazi hiyo ya maana sana alipowaambia hivi: ‘Kwa hiyo nendeni mukafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote . . . mimi nipo pamoja nanyi siku zote mupaka umalizio wa mufumo wa mambo.’ (Mt. 28:19, 20) Mashahidi wengi ambao hapo zamani walikuwa wenye kusikia haya ao kuwaogopa watu wamejionea namna roho takatifu imewatolea ujasiri wa kuzungumuza na watu wasiowajua katika mahubiri.​—Soma Zaburi 119:46; 2 Wakorintho 4:7.

19. Ijapokuwa uzaifu wetu wa kimwili, tuna uhakikisho gani?

19 Ndugu na dada fulani ni wazaifu sana kimwili kwa sababu ya ugonjwa ao uzee. Hata hivyo, wanaweza kuwa hakika kwamba “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote” anaelewa hali ya kila Mukristo wa kweli. (2 Kor. 1:3) Anapendezwa sana na yote tunayofanya ili kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza. Sisi wote hatupaswe kusahau kwamba ni imani yetu kwanza katika zabihu ya Kristo ndiyo inalinda hai nafsi yetu tunapofanya yote kulingana na hali zetu.​—Ebr. 10:39.

20, 21. Ni katika njia gani mbalimbali tunaonyesha kwamba tunamutegemea Yehova?

20 Ibada yetu inatia ndani kutumia wakati, nguvu, na mali yetu kadiri inavyowezekana katika kazi ya Yehova. Bila shaka, tunataka ‘kufanya kazi ya mweneza-injili’ kwa moyo wetu wote. (2 Tim. 4:5) Kwa kweli, tunafurahia kufanya kazi hiyo, kwa kuwa inawasaidia wengine ‘wapate ujuzi sahihi wa kweli.’ (1 Tim. 2:4) Ni wazi kwamba, kumuheshimu na kumusifu Yehova, kunatuletea baraka nyingi za kiroho. (Met. 10:22) Na jambo hilo linatusaidia tumutegemee Muumbaji wetu bila kuyumba​-yumba.​—Rom. 8:35-39.

21 Mambo ambayo tumezungumuzia yanaonyesha kwamba, ni lazima tujikaze ili kutegemea mashauri yenye hekima ya Yehova. Kwa hiyo, ni jambo la maana sana umutegemee Yehova katika sala. Tafakari kuhusu namna ambavyo Yehova ametimiza mapenzi yake hapo zamani na namna atakavyofanya hivyo wakati ujao. Endelea kumutegemea Yehova kupitia matendo ya imani. Bila shaka, vikumbusho vya Yehova vitadumu milele. Na wewe pia utaishi milele!