Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Utajitoa kwa Ajili ya Ufalme?

Je, Utajitoa kwa Ajili ya Ufalme?

‘Mungu anapenda mutoaji muchangamufu.’​—2 KOR. 9:7.

1. Watu wengi wanajitoa kwa ajili ya mambo gani, na sababu gani?

 WATU wako tayari kujitoa kwa ajili ya mambo ambayo wanaona kuwa ya maana. Wazazi wanatoa wakati, feza, na nguvu zao ili kutunza watoto wao. Wakimbiaji vijana wanaotaka kuwakilisha inchi yao kwenye michezo ya Olimpike wanapitisha saa nyingi kila siku ili kufanya mazoezi kwa bidii wakati ambapo marafiki wao wanacheza na kujifurahisha. Yesu pia alijitoa kwa ajili ya mambo aliyoona kuwa ya lazima. Hakutafuta raha, na hakuwa na watoto. Lakini, alitia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza. (Mt. 4:17; Lu. 9:58) Wafuasi wake pia waliacha mambo mengi ili kutegemeza kazi ya Ufalme. Waliona kuwa jambo la lazima kuendeleza kwanza kazi ya Ufalme, na walijitoa ili kufanya mengi kadiri walivyoweza ili kutegemeza kazi hiyo. (Mt. 4:18-22; 19:27) Kwa hiyo tunaweza kujiuliza hivi: ‘Ni jambo gani lililo la maana katika maisha yangu?’

2. (a) Ni zabihu gani ambazo ni za maana kwa Wakristo wote wa kweli? (b) Wakristo fulani wanaweza kujitoa ili kufanya mambo gani ya ziada?

2 Zabihu fulani ni za maana kwetu na zinatusaidia kuendelea kuwa na uhusiano muzuri pamoja na Yehova. Wakati na nguvu tunazotumia ili kusali, kusoma Biblia, kufanya ibada ya familia, kuhuzuria mikutano na kuhubiri, mambo yote hayo ni zabihu za maana tunazomutolea Yehova. * (Yos. 1:8; Mt. 28:19, 20; Ebr. 10:24, 25) Kazi ya kuhubiri inasonga mbele, na watu wengi wanaendelea kumiminika kwenye ‘mulima wa nyumba ya Yehova’ kwa sababu Yehova anabariki jitihada zetu. (Isa. 2:2) Ili kutegemeza kazi za Ufalme, wengi wanajitoa ili kutumikia kwenye Beteli, kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme na ya Mikusanyiko, kutayarisha mikusanyiko, ao kusaidia wale waliopigwa na misiba ya asili. Yehova hatuombe tufanye mambo hayo ya ziada ili kupata uzima wa milele, lakini yanasaidia kutegemeza faida za Ufalme.

3. (a) Kujitoa kwa ajili ya kazi ya Ufalme kunatuletea faida gani? (b) Ni maulizo gani tunayopaswa kufikiria?

3 Leo, kuna uhitaji mukubwa wa kutegemeza kazi ya Ufalme kuliko wakati mwingine wowote. Inafurahisha kuona namna wengi wanavyojitoa kwa kupenda kwa ajili ya kazi ya Yehova! (Soma Zaburi 54:6.) Roho hiyo ya kujitoa inatuletea furaha nyingi tunapoendelea kungojea Ufalme wa Mungu. (Kum. 16:15; Mdo. 20:35) Lakini, ni lazima sisi wote tujichunguze vizuri. Je, kuna njia ambamo tunaweza kujitoa ili kufanya mengi zaidi katika kazi ya Ufalme? Namna gani tunapaswa kutumia wakati, feza, nguvu na uwezo wetu mbalimbali? Tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu mambo gani tunapotoa zabihu? Acheni tuzungumuzie mambo tunayoweza kujifunza kutokana na zabihu za kujipendea zilizofanywa zamani. Kufanya hivyo kutaongeza furaha yetu.

ZABIHU KATIKA ISRAELI

4. Waisraeli walifaidika namna gani kwa kutoa zabihu?

4 Katika Israeli, ilifaa kutoa zabihu ili kusamehewa zambi. Watu walipaswa kutoa zabihu ili wakubaliwe na Yehova. Sheria iliomba watu kutoa zabihu fulani, lakini zingine zilitolewa kwa kujipendea. (Law. 23:37, 38) Zabihu zote za kuteketezwa zingetolewa kama zabihu za kujipendea, ao zawadi kwa Yehova. Zabihu kama hizo zilitolewa wakati wa sherehe ya kumutolea Yehova hekalu katika siku za Sulemani.​—2 Nya. 7:4-6.

5. Yehova alifanya mupango gani kwa ajili ya wale wasiojiweza?

5 Yehova alielewa kwamba kila mutu hakuwa na uwezo wa kutoa zabihu yenye kulingana na ile ya mwingine, kwa hiyo aliomba kila mutu atoe kulingana na uwezo wake. Sheria ya Yehova ilisema kwamba damu ya munyama ilipaswa kumwangwa chini, hilo lilikuwa ‘kivuli cha mambo mema [ambayo] yangekuja’ kupitia Mwana wake, Yesu. (Ebr. 10:1-4) Lakini, Yehova aliomba kila mutu atoe kulingana na uwezo wake. Kwa mufano, Mungu angekubali mutu ambaye hangepata ngombe, kondoo ao mbuzi atoe njiwa-tetere. Kwa hiyo, hata mutu asiyejiweza angefurahia kumutolea Yehova zabihu. (Law. 1:3, 10, 14; 5:7) Hata ikiwa wanyama waliotolewa kama zabihu walitofautiana, kulikuwa mambo mawili ambayo kila mutu aliyetoa zabihu za kujipendea alipaswa kufikiria.

6. Ni mambo gani mawili ambayo kila mutu aliyetaka kutoa zabihu alipaswa kufikiria, na sababu gani mambo hayo yalikuwa ya maana?

6 Kwanza, mutu alipaswa kumutolea Yehova kilicho bora zaidi. Yehova aliwaambia Waisraeli kwamba ili ‘zabihu iwaletee kibali’ chake, ilipaswa kuwa bila kasoro. (Law. 22:18-20) Ikiwa munyama alikuwa na kasoro, haingefaa kumutoa kama zabihu kwa Yehova. Pili, mutu anayetoa zabihu alipaswa kuwa safi. Ikiwa mutu hakuwa safi mbele atoe zabihu ya kujipendea, alipaswa kufanya toleo la zambi ao toleo la hatia ili kufanya uhusiano wake na Yehova uwe muzuri. (Law. 5:5, 6, 15) Hilo lilikuwa jambo la lazima sana. Sheria ya Yehova ilisema kwamba ikiwa mutu fulani asiye safi anakula zabihu ya ushirika, iliyotia ndani zabihu ya kujipendea, alipaswa kuondolewa kati ya watu wa Mungu. (Law. 7:20, 21) Kwa upande mwingine, wakati mutu anayetoa zabihu alikuwa na uhusiano muzuri na Yehova na wakati zabihu yake ilikuwa bila kasoro, mutoaji huyo alipaswa kutoa zabihu yake kwa furaha na zamiri njema.​—Soma 1 Mambo ya Nyakati 29:9.

NAMNA YA KUTOA ZABIHU LEO

7, 8. (a) Wengi wanapata baraka gani wanapojitoa kwa ajili ya kazi ya Ufalme? (b) Tunaweza kutoa nini?

7 Leo pia, wengi wako tayari kujitoa katika kazi ya Ufalme, na hilo linamufurahisha sana Yehova. Kutumikia ndugu na dada zetu kunaleta baraka nyingi. Ndugu mumoja anayetumika katika ujenzi wa majumba ya Ufalme na kusaidia wale waliopigwa na misiba ya asili anaeleza kwamba anashindwa kueleza furaha kubwa anayopata anapowasaidia ndugu na dada. Anasema hivi: “Kuona namna ndugu na dada wanavyofurahi na kushukuru wanapokuwa katika Jumba jipya la Ufalme ao wanapopokea musaada kisha kupigwa na musiba wa asili kunatufanya tuone kwamba kazi na jitihada zilizofanywa hazikuwa za bure.”

Matoleo mengi yalikuwa ya kujipendea, kama zabihu tunazotoa leo (Ona fungu la 7-13)

8 Leo, tengenezo la Yehova limeendelea kutumia njia mbalimbali ili kutegemeza kazi ya Yehova. Katika mwaka wa 1904, Ndugu C. T. Russell aliandika hivi: “Kila mumoja ajione kuwa amewekwa na Bwana kuwa musimamizi wa wakati wake mwenyewe, mamlaka yake, feza, na mambo mengine, na kila mumoja anapaswa kutumia talanta hizo kwa kadiri anavyoweza, kwa utukufu wa Bwana-Mukubwa.” Tunatoa mambo fulani ili kutegemeza kazi ya Yehova, lakini hilo linatuletea baraka nyingi. (2 Sam. 24:21-24) Je, tunaweza kutoa mali yetu ili kutegemeza kazi ya Ufalme?

Wafanyakazi fulani wa Beteli ya Australia

9. Ni kanuni gani ya Yesu inayopatikana kwenye Luka 10:2-4 inayoweza kutusaidia tutumie vizuri wakati wetu?

9 Wakati wetu. Inaomba wakati na nguvu nyingi ili kutafsiri na kuchapisha vichapo vyetu, kujenga mahali pa ibada, kutayarisha mikusanyiko, kusaidia wale waliopigwa na misiba, na kufanya mambo mengine ya lazima. Kila mutu iko na saa 24 tu kwa siku. Hata hivyo, Yesu alitoa kanuni inayoweza kutusaidia tutumie wakati wetu vizuri. Alipowatuma wanafunzi wake katika mahubiri, Yesu aliwaambia ‘wasimukumbatie mutu yeyote wakimusalimu barabarani.’ (Lu. 10:2-4) Sababu gani ilifaa Yesu atoe maagizo hayo? Mutu mumoja mwenye elimu ya Biblia anasema hivi: “Watu wa Mashariki hawakuwa wanasalimiana kama sisi tunavyofanya kwa kuinama kidogo, ao kupatia mutu mukono, lakini walisalimiana kwa kukumbatiana mara nyingi, kuinamisha kichwa, na hata kuinamisha uso mupaka chini. Yote hayo yaliomba wakati mwingi.” Yesu hakusema hivyo ili kuwatia moyo wafuasi wake wasiwachangamukie watu. Lakini, alitaka tu kuwaonyesha kwamba walikuwa na wakati muchache na walipaswa kutumia sehemu kubwa ya wakati huo ili kushugulikia mambo ya maana zaidi. (Efe. 5:16) Je, tunaweza kutumia kanuni hiyo ili kuwa na wakati mwingi zaidi wa kushiriki katika kazi ya Ufalme?

Wahubiri wa Ufalme kwenye Jumba la Ufalme huko Kenya, Afrika

10, 11. (a) Michango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote inatumiwa namna gani? (b) Ni kanuni gani inayopatikana katika 1 Wakorintho 16:1, 2 inayoweza kutusaidia?

10 Feza zetu. Feza nyingi zinahitajiwa ili kutegemeza kazi ya Ufalme. Dola nyingi zinatumiwa kila mwaka ili kutosheleza mahitaji ya waangalizi wanaosafiri, mapainia wa pekee na wamisionere. Kuanzia mwaka wa 1999, Majumba ya Ufalme zaidi ya 24 500 yamejengwa katika inchi maskini. Lakini, Majumba ya Ufalme karibu 6 400 yangali yanahitajiwa. Magazeti milioni 100 hivi ya Munara wa Mulinzi na Amuka! yanachapishwa kila mwezi. Yote hayo yanafanywa kupitia michango ya kujipendea.

11 Mutume Paulo alitoa kanuni ya kufuata tunapofikiria kutoa michango. (Soma 1 Wakorintho 16:1, 2.) Akiongozwa na roho ya Mungu, aliwatia moyo ndugu katika Korintho wasingojee mupaka mwisho wa juma ili kuona ikiwa walibaki na kiasi gani cha feza, lakini walipaswa kuweka pembeni kiasi fulani mwanzoni mwa juma kulingana na uwezo wao. Kama ilivyokuwa wakati wa mitume, leo ndugu na dada wanafanya mipango mbele ya wakati ili kutoa michango kulingana na uwezo wao. (Lu. 21:1-4; Mdo. 4:32-35) Yehova anapendezwa sana na roho hiyo ya kutoa.

Ndugu anayejitolea katika Ujenzi huko Tuxedo, New York, Amerika.

12, 13. Sababu gani Wakristo fulani wanafikiri kwamba hawawezi kumutolea Yehova nguvu na uwezo wao mbalimbali, lakini namna gani Yehova anaweza kuwasaidia?

12 Nguvu na uwezo wetu mbalimbali. Yehova anabariki jitihada tunazofanya ili kutumia nguvu na uwezo wetu mbalimbali kwa ajili ya kazi ya Ufalme. Anaahidi kutusaidia ikiwa tunachoka. (Isa. 40:29-31) Je, tunafikiri kwamba hatuna uwezo wa kutosha ili kutegemeza kazi ya Ufalme? Je, tunafikiri kwamba wengine ndio wana uwezo muzuri kuliko sisi? Kumbuka kwamba Mungu anaweza kufanya uwezo wako uwe muzuri, kama alivyotendea Bezaleli na Oholiabu.​—Kut. 31:1-6; ona picha mwanzoni mwa habari hii.

13 Yehova anatutia moyo tusijizuie kumutolea kilicho bora zaidi. (Met. 3:27) Hekalu lilipokuwa likijengwa upya, Yehova aliwaambia Wayahudi huko Yerusalemu wachunguze mambo waliyokuwa wakifanya kuliko kutegemeza ujenzi. (Hag. 1:2-5) Walikuwa wamekengeushwa na mambo mengine na walikuwa hawafikirie tena kazi ya ujenzi. Sisi pia tunapaswa kuchunguza ikiwa shuguli zetu hazituzuie kutia kazi ya Yehova pa nafasi ya kwanza. Je, tunaweza ‘kuweka moyo wetu juu ya njia zetu’ ili tufanye mengi katika kazi ya Ufalme inayofanywa katika siku hizi za mwisho?

TUJITOE KULINGANA NA UWEZO WETU

14, 15. (a) Namna gani mufano wa ndugu na dada zetu wasiojiweza unatutia moyo? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

14 Wengi wanaishi katika inchi ambamo matatizo na umaskini ni mambo ya kawaida. Tengenezo la Yehova linajikaza kusaidia ndugu na dada wanaoishi katika inchi hizo. (2 Kor. 8:14) Lakini, hata ndugu na dada wasiojiweza wanafurahia kutoa. Yehova anafurahi sana kuona wale wasiojiweza wakitoa kwa furaha.​—2 Kor. 9:7.

15 Katika inchi moja ya Afrika iliyo maskini sana, ndugu fulani wanalima sehemu fulani ya shamba yao na wanatumia feza wanazopata kisha kuuzisha mazao waliyovuna katika sehemu hiyo ili kutegemeza kazi ya Ufalme. Katika inchi hiyohiyo, mupango ulifanywa ili kujenga Jumba moja la Ufalme ambalo ndugu na dada walihitaji sana. Ndugu na dada wa mahali hapo walitaka kusaidia kujenga. Lakini, kazi ya ujenzi ilipaswa kuanza wakati wa kupanda mbegu. Kwa kuwa walitamani sana kushiriki katika kazi hiyo, muchana walisaidia katika ujenzi wa Jumba la Ufalme na mangaribi walienda katika mashamba yao ili kupanda mbegu zao. Walionyesha roho ya kujitoa kabisa! Mufano wao unatukumbusha ndugu wa Makedonia. Walikuwa katika ‘umaskini mukubwa,’ lakini waliomba kwa kusihi sana ili wapewe pendeleo la kutoa. (2 Kor. 8:1-4) Acheni sisi pia tuazimie ‘kutoa kulingana na baraka za Yehova Mungu ambazo ametupatia.’​—Soma Kumbukumbu la Torati 16:17.

16. Tunapaswa kufanya nini ili zabihu tunazotoa zikubaliwe na Yehova?

16 Hata hivyo, tunapaswa kufikiria jambo fulani. Kama ilivyokuwa kwa Waisraeli wa zamani, tunapaswa kuhakikisha kwamba zabihu za kujipendea tunazotoa ni zenye kukubalika kwa Mungu. Tunapaswa kuendelea kuwa na usawaziko ili tushugulikie madaraka ya kuitunza familia yetu na ya kumuabudu Yehova. Kutumia wakati na mali yetu ili kuwasaidia wengine hakupaswe kutufanya tuzarau mahitaji ya kiroho na ya kimwili ya familia yetu. Ikiwa tunazarau mahitaji hayo, tutakuwa tukitoa mambo tusiyokuwa nayo. (Soma 2 Wakorintho 8:12.) Zaidi ya hilo, tunapaswa kuendelea kutunza hali yetu ya kiroho. (1 Kor. 9:26, 27) Hata hivyo, tuwe hakika kwamba tunapoishi kulingana na kanuni za Biblia, zabihu tunazotoa zinatuletea furaha nyingi na ‘zinakubaliwa zaidi’ na Yehova.

ZABIHU ZETU NI ZA MAANA SANA

17, 18. Tunawaona namna gani wale wote wanaojitoa kwa ajili ya kazi ya Ufalme, na kila mumoja wetu anapaswa kufikiria nini?

17 Ndugu na dada zetu wengi ‘wanajimimina [wanajimwanga] kama toleo la kinywaji’ kupitia mambo wanayofanya ili kutegemeza kazi mbalimbali za Ufalme. (Flp. 2:17) Tunawashukuru sana wale ambao wameonyesha roho hiyo ya kujitoa. Tunawashukuru pia bibi na watoto wa ndugu zetu wanaosimamia kazi ya Ufalme kwa roho yao ya ukarimu na kujitoa.

18 Kazi nyingi inaombwa kufanywa ili kutegemeza faida za Ufalme. Acheni kila mumoja wetu afikirie sana namna anavyoweza kutegemeza kazi hiyo kulingana na uwezo wake. Unaweza kuwa hakika kwamba utapata baraka nyingi sasa na hata zaidi, katika ‘mufumo wa mambo unaokuja.’​—Mk. 10:28-30.

^ Soma habari ‘Tumutolee Yehova Zabihu Zetu kwa Nafsi Yote’ katika Munara wa Mulinzi wa 15/01/2012, ukurasa wa 21-25.