Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Mufanye Hivi kwa Kunikumbuka Mimi’

‘Mufanye Hivi kwa Kunikumbuka Mimi’

“Baada ya kutoa shukrani, akaumega [mukate] na kusema: ‘Huu unamaanisha mwili wangu ambao ni kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.’”​—1 KOR. 11:24.

1, 2. Pengine mitume walikuwa na mawazo gani mbele Yesu aende Yerusalemu?

 ‘ANGA limengaa, na mwezi umetokea kwa mara ya kwanza. Jana usiku, walinzi wa usiku huko Yerusalemu waliona mwezi huo pia. Washiriki wa Sanhedrini wanaposikia jambo hilo, mara moja wanatangaza kwamba mwezi mupya, ni kusema, Nisani, umeanza. Kisha watu wanawasha moto na wajumbe wanaeneza haraka habari hiyo. Hata watu wanaoishi hapa wamesikia habari hiyo. Bila shaka, Yesu anapaswa kufanya haraka ili afike Yerusalemu mbele ya Pasaka.’

2 Pengine mitume fulani waliokuwa na Yesu mbele aende Yerusalemu kwa mara ya mwisho walikuwa na mawazo hayo. Wakati huo, walikuwa huko Perea, upande mwingine wa Yordani. (Mt. 19:1; 20:17, 29; Mk. 10:1, 32, 46) Kisha tu Wayahudi kujua siku ambayo mwezi wa kwanza wa Kiyahudi unaoitwa Nisani utaanza, Pasaka ilipaswa kufanywa siku 13 baadaye, ni kusema, siku 14 Nisani kisha jua kushuka.

3. Sababu gani Wakristo wanapendezwa kabisa na tarehe ya Pasaka?

3 Tarehe ya Chakula cha Mangaribi cha Bwana, ambayo inalingana na tarehe ya Pasaka, itakuwa tarehe 14 Mwezi wa 4, 2014 kisha jua kushuka. Hiyo itakuwa siku ya maana sana kwa Wakristo wa kweli na wale wanaopendezwa na ujumbe wa Biblia. Sababu gani? Kwa sababu ya yale tunayosoma kwenye 1 Wakorintho 11:23-25: “Yesu katika ule usiku aliokuwa akienda kutolewa alichukua mukate na, baada ya kutoa shukrani, akaumega na kusema: ‘Huu unamaanisha mwili wangu ambao ni kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.’ Akafanya vivyo hivyo kuhusu kile kikombe pia.”

4. (a) Tunaweza kujiuliza maulizo gani kuhusu Ukumbusho? (b) Namna gani tunafikia kujua tarehe ya Ukumbusho wa kila mwaka? (Soma kisanduku  “Ukumbusho wa 2014.”)

4 Bila shaka utahuzuria tukio moja tu ambalo Yesu aliwaambia wafuasi wake wakumbuke kila mwaka. Lakini, tunaweza kuanza kujiuliza hivi: ‘Namna gani ninaweza kujitayarisha kwa ajili ya Ukumbusho? Ni mifano gani itakayotumiwa? Ukumbusho huo utafanywa namna gani? Tukio hilo na mifano itakayotumiwa inapaswa kuwa na maana gani kwangu?’

MIFANO ITAKAYOTUMIWA

5. Yesu aliagiza matayarisho gani yafanywe kwa ajili ya Pasaka ya mwisho pamoja na mitume wake?

5 Yesu alipowaambia mitume wake watayarishe chumba ambamo wangekula Pasaka, hakuwaambia wapambe sana chumba hicho; lakini, inaonekana alitaka tu chumba kinachofaa, kilicho safi na kilicho na nafasi ya kutosha kwa ajili yake na mitume wake. (Soma Marko 14:12-16.) Walipaswa kutayarisha kila kitu kilichohitajiwa, kutia ndani mukate usiotiwa chachu na divai nyekundu. Walipomaliza kula Pasaka, Yesu alizungumuzia mifano hiyo miwili, ni kusema, mukate na divai.

6. (a) Kisha kula Pasaka, Yesu alisema nini kuhusu mukate? (b) Ni mukate wa namna gani unaotumiwa kwenye Ukumbusho?

6 Mutume Mathayo aliyekuwa hapo aliandika hivi baadaye: “Yesu alichukua mukate na, baada ya kutoa baraka, akaumega, akawapa wanafunzi, akasema: ‘Muchukue, mukule.’” (Mt. 26:26) ‘Mukate’ huo haukuwa na chachu, kama ule uliotumiwa wakati wa Pasaka. (Kut. 12:8; Kum. 16:3) Mukate huo ulitengenezwa kwa unga wa ngano na maji tu, haukutiwa chachu ao vikolezo vyovyote, kama vile chumvi. Kwa kuwa haukutiwa chachu, mukate huo haungevimba. Ilikuwa rahisi kuuvunja vipande​-vipande kwa sababu ulikuwa wenye kukauka kama biskwiti. Leo, mbele ya Ukumbusho, wazee wa kutaniko wanaweza kumuomba mutu fulani atengeneze mukate. Mutu huyo atatumia unga wa ngano na maji, atapakaa mafuta kidogo kwenye chombo atakachotumia ili kupika mukate huo. (Ikiwa haiwezekane kupata unga wa ngano, tunaweza kutumia unga wa muchele, shayiri, mahindi ao mbegu zingine kama hizo.) Matzoth, ambao ni mukate wa Kiyahudi usiotiwa chachu, mayai ao vitunguu, unaweza kutumiwa pia.

7. Yesu alitumia divai gani, na ni aina gani ya divai inayopaswa kutumiwa kwenye Ukumbusho?

7 Mutume Mathayo anaendelea kusema hivi: “[Yesu] akachukua kikombe na, akiisha kushukuru, akawapa, akisema: ‘Mukunywe, ninyi nyote.’” (Mt. 26:27, 28) Divai nyekundu ndio ilikuwa katika kikombe ambacho Yesu alitumia. (Haikuwa maji yaliyokamuliwa karibuni katika mizabibu, kwa sababu wakati wa kuvuna mizabibu ulikuwa umepita sana.) Waisraeli hawakutumia divai walipokula Pasaka ya kwanza huko Misri, lakini Yesu hakusema kwamba ni vibaya kunywa divai kwenye Pasaka hiyo. Hata alitumia sehemu ya divai hiyo kwenye Chakula cha Mangaribi cha Bwana. Kwa hiyo, Wakristo wanatumia divai kwenye Ukumbusho. Kwa kuwa hakukuwa ulazima wa kuongeza jambo fulani katika damu ya Yesu ili iwe na samani zaidi, divai iliyotumiwa haikuongezwa kitu ili iwe makali sana. Divai nyekundu isiyochanganywa na kitu ndio inapaswa kutumiwa. Inaweza kuwa divai iliyotengenezwa nyumbani ao divai nyekundu, kama vile Beaujolais, Bourgogne ao Chianti ambayo mutu anaweza kununua.

MUKATE NA DIVAI VINAMAANISHA NINI?

8. Sababu gani Wakristo wanapendezwa na maana ya mukate na divai?

8 Mutume Paulo alionyesha waziwazi kwamba Wakristo wote wanapaswa kuendelea kusherehekea Chakula cha Mangaribi cha Bwana. Aliandikia waamini wenzake huko Korintho hivi: “Nilipokea kutoka kwa Bwana kile nilichowapa ninyi pia, kwamba Bwana Yesu . . . alichukua mukate na baada ya kutoa shukrani, aliumega na kusema: ‘Huu unamaanisha mwili wangu ambao ni kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.’” (1 Kor. 11:23, 24) Kwa hiyo, Wakristo leo wanasherehekea tukio hilo kila mwaka na wanapendezwa na maana ya mukate na divai.

9. Watu fulani wana maoni gani yasiyo ya kweli kuhusu mukate ambao Yesu alitumia?

9 Waamini fulani wanaonyesha kwamba Yesu alisema hivi: ‘Huu ni mwili wangu,’ kwa hiyo wanaamini kwamba mukate aliotumia uligeuka kimuujiza kuwa mwili halisi wa Yesu. Lakini, hiyo si kweli. * Yesu alikuwa mbele ya mitume wake waaminifu, na mukate usiotiwa chachu ambao wangekula ulikuwa vilevile mbele yao. Kwa kweli, Yesu alikuwa akizungumuza kwa njia ya mufano, kama vile alivyokuwa akifanya nyakati zingine.​—Yoh. 2:19-21; 4:13, 14; 10:7; 15:1.

10. Mukate unaotumiwa kwenye Ukumbusho unafananisha nini?

10 Mukate ambao mitume waliona na ambao wangekula ulimaanisha mwili wa Yesu. Mwili gani? Wakati fulani, watumishi wa Yehova walifikiri kwamba kwa sababu Yesu alivunja mukate lakini hata mufupa wake mumoja haukuvunjwa, mukate ulimaanisha “mwili wa Kristo,” ni kusema, kutaniko la watiwa​-mafuta. (Efe. 4:12; Rom. 12:4, 5; 1 Kor. 10:16, 17; 12:27) Lakini, baadaye, ilionekana kwamba ikiwa tunafikiri vizuri na kuchunguza Maandiko, tutaona kwamba mukate unamaanisha mwili wa kibinadamu wa Yesu. Yesu “aliteseka katika mwili,” hata kufikia kutundikwa. Kwa hiyo, mukate unaotumiwa kwenye Ukumbusho unafananisha mwili wa kibinadamu wa Yesu ambamo ‘alichukua zambi’ zetu.​—1 Pet. 2:21-24; 4:1; Yoh. 19:33-36; Ebr. 10:5-7.

11, 12. (a) Yesu alisema nini kuhusu divai? (b) Divai inayotumiwa kwenye Ukumbusho inamaanisha nini?

11 Mafasiriyo hayo yanatusaidia kuelewa yale ambayo Yesu alisema baadaye kuhusu divai. Tunasoma hivi: ‘Akafanya vivyo hivyo kuhusu kile kikombe pia, baada ya yeye kula mulo wa jioni [chakula cha mangaribi], akisema: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa musingi wa damu yangu.’” (1 Kor. 11:25) Biblia nyingi zinatafsiri maneno hayo kama tafsiri ya neno kwa neno ya Robert Young inayosema hivi: ‘Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu.’ Je, hicho kikombe ambacho Yesu alitumia kilikuwa agano jipya? Hapana. Neno “kikombe” lilitumiwa ili kumaanisha divai iliyokuwa ndani yake. Yesu alisema kwamba divai hiyo ilimaanisha ao ilifananisha nini? Divai hiyo ilifananisha damu yake iliyomwangwa.

12 Katika Injili ya Marko, tunakuta maneno haya ya Yesu: “Hii inamaanisha ‘damu yangu ya agano,’ ambayo itamwangwa kwa ajili ya wengi.” (Mk. 14:24) Bila shaka, damu ya Yesu ‘ilimwangwa kwa ajili ya wengi kwa musamaha wa zambi.’ (Mt. 26:28) Kwa hiyo, divai nyekundu inafananisha kabisa damu ya Yesu. Kupitia damu ya Yesu tunaweza kupata ‘musamaha wa makosa yetu.’​—Soma Waefeso 1:7.

Mitume walikunywa divai iliyofananisha damu ya Yesu ya agano (Ona fungu la 11 na 12)

UKUMBUSHO WA KIFO CHA KRISTO UNAFANYWA NAMNA GANI?

13. Ukumbusho wa kifo cha Kristo unafanywa namna gani?

13 Ikiwa utahuzuria Ukumbusho pamoja na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza, unafikiri mambo yatafanyika namna gani? Ukumbusho utafanywa mahali safi na pa kawaida, ambapo kila mutu atakuwa na nafasi ya kufurahia mukutano huo. Maua yanaweza kutumiwa ili kupamba mahali hapo, lakini hautaona mapambo mengi yenye kukengeusha, hapatakuwa kama mahali pa karamu. Muzee anayestahili atatoa hotuba itakayozungumuzia waziwazi na kwa njia yenye kuheshimika yale ambayo Biblia inasema kuhusu Ukumbusho. Atawasaidia wote wapendezwe na yale ambayo Kristo alifanya kwa ajili yetu. Kristo alikufa ili tuweze kuishi milele. (Soma Waroma 5:8-10.) Musemaji atazungumuzia tumaini mbili zinazotajwa katika Biblia.

14. Hotuba ya Ukumbusho itazungumuzia tumaini gani mbili?

14 Tumaini moja ni kutawala pamoja na Yesu mbinguni. Ni wafuasi wachache wa Kristo tu, kama vile mitume wake waaminifu, ndio walio na tumaini hilo. (Lu. 12:32; 22:19, 20; Ufu. 14:1) Tumaini lingine ni lile la Wakristo wengi wanaomutumikia Mungu kwa uaminifu leo. Wakristo hao wana tumaini la kuishi milele katika Paradiso duniani. Mwishowe, mapenzi ya Mungu yatatendeka duniani kama ilivyo mbinguni, jambo ambalo Wakristo wamekuwa wakiomba kwa miaka mingi. (Mt. 6:10) Biblia inazungumuzia hali nzuri watakazofurahia milele.​—Isa. 11:6-9; 35:5, 6; 65:21-23.

15, 16. Mukate unatumiwa namna gani wakati wa Ukumbusho?

15 Wakati hotuba itakuwa karibu kumalizika, musemaji ataonyesha kwamba wakati umefika ili kufanya kama Yesu alivyofanya. Kama tulivyozungumuzia hapo juu, mifano miwili itatumiwa, ni kusema, mukate usiotiwa chachu na divai nyekundu. Mifano hiyo itakuwa kwenye meza karibu na musemaji. Musemaji atasoma katika Biblia mambo ambayo Yesu alisema na kufanya alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake. Kwa mufano, tunasoma hivi katika kitabu cha Mathayo: “Yesu alichukua mukate na, baada ya kutoa baraka, akaumega, akawapa wanafunzi, akasema: ‘Muchukue, mukule. Huu unamaanisha mwili wangu.’” (Mt. 26:26) Yesu alivunja mukate usiotiwa chachu vipande​-vipande ili kupitishia vipande hivyo mitume wake waliokuwa kila upande. Utaona kwenye Ukumbusho tutakaofanya tarehe 14 Mwezi wa 4 vipande fulani vya mukate kwenye masahani.

16 Kutakuwa masahani ya kutosha ili mifano ipitishwe kwa wote kwa wakati muchache. Sherehe hiyo haitakuwa yenye kutia ndani mambo mengi. Kisha sala fupi, masahani yatapitishwa kwa utaratibu, kulingana na hali ya kwenu. Ni wachache tu ndio watakula mukate, pengine hakuna hata mutu atakayekula, kama ilivyokuwa katika makutaniko mengi wakati wa Ukumbusho wa 2013.

17. Namna gani maagizo ya Yesu kuhusu divai yanafuatwa kwenye Ukumbusho?

17 Kisha, musemaji atasoma tena maneno ya Yesu katika Mathayo: “[Yesu] akachukua kikombe na, akiisha kushukuru, akawapa, akisema: ‘Mukunywe, ninyi nyote; kwa maana hii inamaanisha “damu yangu ya agano,” ambayo itamwangwa kwa ajili ya wengi kwa musamaha wa zambi.’” (Mt. 26:27, 28) Kwa kufuata namna Yesu alivyofanya, sala nyingine itatolewa na kisha ‘vikombe’ vya divai nyekundu vitapitishwa kwa wahuzuriaji wote.

18. Hata ikiwa ni wachache tu ndio watakula mukate na kunywa divai, ao pengine kusiwe hata mutu mumoja atakayetumia mifano, sababu gani ni jambo la maana kuwa kwenye Ukumbusho?

18 Wahuzuriaji wengi hawakule mukate na kunywa divai wakati mifano hiyo inapitishwa kwa sababu Yesu alionyesha kwamba ni wale tu watakaotawala pamoja naye katika Ufalme wa mbinguni ndio wanastahili kula mukate na kunywa divai. (Soma Luka 22:28-30; 2 Tim. 4:18) Wahuzuriaji wengi watatazama tu kwa heshima namna mifano itakavyopitishwa. Hata hivyo, kuwa kwenye Ukumbusho ni jambo la maana sana kwao, kwa kuwa hilo linaonyesha kwamba wanasamini sana zabihu ya Yesu. Wakati wa Ukumbusho, wanaweza kutafakari kuhusu baraka ambazo zabihu ya ukombozi ya Yesu inaweza kuwaletea. Wana tumaini la kuwa kati ya ‘mukutano mukubwa’ utakaookoka ‘ziki kubwa’ inayokuja. Hao ni waabudu ambao ‘watakuwa wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana​-Kondoo.’​—Ufu. 7:9, 14-17.

19. Unaweza kujitayarisha namna gani ili ufaidike na Ukumbusho?

19 Mashahidi wa Yehova duniani pote wanajitayarisha kwa ajili ya mukutano huo wa pekee. Majuma fulani mbele, tutawaalika watu wengi iwezekanavyo ili waje kuhuzuria Ukumbusho. Tena, katika siku hizo mbele ya Ukumbusho, wengi wetu watasoma mambo ambayo Yesu alifanya na yale yaliyotokea tarehe hiyo ya mwaka wa 33. Tutafanya mipango ili mambo yetu ya kipekee yasitufanye tukose kuhuzuria Ukumbusho. Ni vizuri kufika mbele ya wimbo na sala ya mwanzo ili tuwakaribishe wageni na kisha tufaidike na programu yote. Sisi wote, washiriki wa kutaniko na wageni, tutafaidika sana ikiwa tutafuatana na musemaji anaposoma maandiko katika Biblia. Jambo la maana hata zaidi ni kwamba, kuhuzuria Ukumbusho kutaonyesha kwamba tunapendezwa sana na zabihu ya Yesu na tunatii amri hii aliyotuachia: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.”​—1 Kor. 11:24.

^ Heinrich Meyer, Mujerumani mwenye elimu ya mambo ya Biblia anasema hivi: “Kuona . . . kwamba mwili wa Yesu ulikuwa haujavunjwa (ulikuwa ungali muzima), na vilevile, damu Yake ilikuwa haijamwangwa, hakuna hata mumoja wale walioalikwa [mitume] ambaye angeweza kufikiri . . . kwamba walikuwa wanakula na kunywa kabisa-kabisa mwili na damu ya Bwana, [kwa hiyo] Yesu Mwenyewe hakufikiria kwamba maneno Yake yangeeleweka katika maana ambayo wao [mitume wake] hawangekubaliana nayo baadaye.”