Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Siku Hii Itakuwa Ukumbusho Kwenu”

“Siku Hii Itakuwa Ukumbusho Kwenu”

‘Siku hii itakuwa ukumbusho kwenu, nanyi mutaisherehekea ikiwa sherehe kwa Yehova.’​—KUT. 12:14.

1, 2. Ni tukio gani la kila mwaka ambalo Wakristo wote wanahitaji kuona kuwa la maana, na sababu gani?

 KATI ya siku ambazo watu wanakumbuka kila mwaka, ni siku gani ambayo hauwezi kusahau? Mutu mwenye kuoa ao kuolewa anaweza kutaja siku ambayo alifunga ndoa. Wengine wanaweza kutaja siku ambayo watu wengi wanakumbuka tukio fulani la kihistoria, kama vile siku ambayo inchi yao ilipata uhuru. Lakini, je, unajua tukio fulani ambalo limekumbukwa kwa miaka zaidi ya 3 500?

2 Tukio hilo ni Pasaka. Pasaka inakumbusha wakati ambapo Waisraeli walikombolewa katika utumwa wa Misri. Unapaswa kuona tukio hilo kuwa la maana. Sababu gani? Kwa sababu linahusiana na sehemu fulani za maana sana za maisha yako. Lakini, pengine unaweza kufikiri hivi: ‘Hata ikiwa Wayahudi wanasherehekea Pasaka, mimi si muamini wa dini ya Wayahudi. Je, siku hiyo ina maana fulani kwangu?’ Jibu linapatikana katika maneno haya yenye maana sana: ‘Kristo pasaka yetu ametolewa zabihu.’ (1 Kor. 5:7) Ili kuelewa vizuri umaana wa jambo hilo, tunahitaji kujifunza kuhusu Pasaka ya Wayahudi na kuchunguza uhusiano ulio kati ya Pasaka hiyo na amri moja iliyotolewa kwa Wakristo wote.

SABABU GANI PASAKA ILIFANYWA?

3, 4. Ni mambo gani yaliyotokea mbele ya Pasaka ya kwanza?

3 Mamilioni ya watu ulimwenguni wasiokuwa Wayahudi wanajua mambo fulani yalitokea mbele ya Pasaka ya kwanza. Pengine wamesoma mambo fulani kuhusu tukio hilo katika kitabu cha Kutoka, wameelezwa mambo fulani, ao wametazama filme fulani kuhusu tukio hilo.

4 Kisha Waisraeli kupitisha miaka mingi huko Misri, Yehova alimutuma Musa na ndugu yake, Haruni, ili wamuombe Farao awaachilie watu Wake. Mutawala huyo mwenye kiburi wa Misri hakuacha Waisraeli waende, kwa hiyo Yehova alileta mapigo fulani juu ya inchi ya Misri. Mwishowe, Mungu alituma pigo la kumi, ambalo liliua kila muzaliwa wa kwanza wa Wamisri. Pigo hilo lilimufanya Farao awaachilie Waisraeli.​—Kut. 1:11; 3:9, 10; 5:1, 2; 11:1, 5.

5. Waisraeli walipaswa kufanya nini mbele waachiliwe huru? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

5 Lakini Waisraeli walipaswa kufanya nini mbele waachiliwe huru? Karibu na tarehe 21 ao 22 Mwezi wa 3, 1513, katika Abibu, * Mungu aliwaambia Waisraeli kwamba siku kumi ya mwezi huo, walipaswa kuanza kujitayarisha kwa ajili ya tukio fulani ambalo lingefanywa siku 14 Nisani. Siku hiyo ilianza wakati jua lilishuka kwa sababu siku ya Wayahudi ilianza wakati jua lilishuka na kumalizika wakati jua lilishuka siku iliyofuata. Siku 14 Nisani, kila familia ilipaswa kuchinja kondoo dume (ao beberu) na kupakaa sehemu ya damu yake juu ya nguzo na sehemu ya juu ya mulango. (Kut. 12:3-7, 22, 23) Familia ilipaswa kula mwana​-kondoo aliyechomwa na mukate usiotiwa chachu na mboga za majani. Malaika wa Mungu alipita katika inchi na kuua kila muzaliwa wa kwanza wa Wamisri, lakini Waisraeli ambao walitii walipona, na kisha waliachiliwa huru.​—Kut. 12:8-13, 29-32.

6. Namna gani watu wa Mungu walipaswa kuiona Pasaka baadaye?

6 Waisraeli walipaswa kuendelea kukumbuka namna walivyokombolewa. Mungu aliwaambia hivi: ‘Siku hii itakuwa ukumbusho kwenu, nanyi mutaisherehekea ikiwa sherehe kwa Yehova katika vizazi vyenu vyote. Nanyi mutaisherehekea kama sheria mupaka wakati usio na kipimo.’ Kisha kusherehekea Pasaka siku 14 Nisani, Waisraeli walisherehekea pia Sikukuu ya Keki Zisizotiwa Chachu iliyofanya siku saba. Siku hizo munane zinaweza pia kuitwa Pasaka. (Kut. 12:14-17; Lu. 22:1; Yoh. 18:28; 19:14) Pasaka ilikuwa moja ya sherehe rasmi (‘sikukuu,’ Biblia Habari Njema) ambazo Wayahudi walipaswa kusherehekea kila mwaka.​—2 Nya. 8:13.

7. Yesu alianzisha nini aliposherehekea Pasaka mara ya mwisho?

7 Kwa kuwa walikuwa Wayahudi waliokuwa chini ya Sheria ya Musa, Yesu na mitume wake walisherehekea Pasaka ya kila mwaka. (Mt. 26:17-19) Waliposherehekea Pasaka mara ya mwisho, Yesu alianzisha tukio mupya ambalo wafuasi wake walipaswa kuendelea kusherehekea kila mwaka. Tukio hilo ni Chakula cha Mangaribi cha Bwana. Lakini walipaswa kufanya hivyo siku gani?

CHAKULA CHA MANGARIBI CHA BWANA KINAPASWA KUFANYWA SIKU GANI?

8. Tunaweza kujiuliza ulizo gani tunapolinganisha tarehe ya Pasaka na ya Ukumbusho?

8 Kwa kuwa Yesu alianzisha Ukumbusho wa kifo chake kisha tu Pasaka, tukio hilo jipya lilipaswa kufanywa siku hiyohiyo ambayo Pasaka ilifanywa. Lakini, pengine umetambua kwamba kwenye kalendari fulani za sasa, kuna tofauti ya siku moja ao siku nyingi kati ya tarehe ya Ukumbusho wa Kifo cha Yesu na tarehe ya Pasaka ya Wayahudi. Sababu gani kuna tofauti hiyo? Jibu linapatikana katika amri ambayo Mungu aliwatolea Waisraeli. Kisha kusema kwamba ‘kutaniko nzima la kusanyiko la Israeli litamuchinja’ mwana​-kondoo, Musa alionyesha ni wakati gani kabisa katika siku 14 Nisani ambapo walipaswa kufanya hivyo.​—Soma Kutoka 12:5, 6.

9. Kulingana na andiko la Kutoka 12:6, mwana-kondoo wa Pasaka alipaswa kuchinjwa wakati gani? (Soma pia kisanduku  “Ilikuwa Wakati Gani?”)

9 Kitabu kimoja kinasema kwamba andiko la Kutoka 12:6 linaonyesha kwamba mwana​-kondoo alipaswa kuchinjwa “katikati ya zile jioni mbili.” (The Pentateuch and Haftorahs) Tafsiri fulani za Biblia zinatumia maneno yaleyale. Tafsiri zingine kama vile, Tanakh ya Wayahudi, inaonyesha kwamba ilikuwa wakati ambapo jua lilikuwa limeshuka lakini mwangaza mudogo ulikuwa ungali. Tafsiri zingine pia zinasema kwamba ilikuwa mangaribi wakati ambapo jua lilikuwa limeshuka lakini mwangaza kidogo ulikuwa ungali ao karibu na wakati ambapo giza linaanza. Kwa hiyo mwana​-kondoo alipaswa kuchinjwa mwanzoni mwa siku 14 Nisani kisha jua kushuka, lakini mwangaza kidogo ulikuwa ungali.

10. Kulingana na watu fulani, mwana-kondoo alichinjwa wakati gani, lakini hilo linatokeza ulizo gani?

10 Baadaye, Wayahudi fulani walifikiri kwamba kuchinja kondoo zote zilizoletwa kwenye hekalu kungechukua wakati mwingi. Kwa hiyo, walianza kufikiri kwamba maneno “katikati ya zile jioni mbili” yanayopatikana kwenye Kutoka 12:6 yanahusu kipindi cha mwisho cha siku 14 Nisani, kati ya wakati ambapo jua lilianza kushuka (kisha​-muchana) na wakati ambapo giza linaanza. Lakini ikiwa ni hivyo, Wayahudi walikula chakula cha Pasaka wakati gani? Profesa Jonathan Klawans, anayejua sana historia ya Wayahudi, alisema hivi: “Siku inaanza wakati jua linashuka, kwa hiyo kondoo wanachinjwa siku 14 Nisani lakini Pasaka inaanza siku 15 Nisani na Wayahudi wanakula chakula cha Pasaka tarehe hiyo, hata ikiwa tofauti hiyo haionyeshwe waziwazi katika kitabu cha Kutoka.” Pia, aliandika hivi: “Maandishi ya Marabi. . . hayajaribu hata kutuambia namna ambavyo Pasaka ilifanywa mbele ya kuharibiwa kwa hekalu” katika mwaka wa 70 kisha kuzaliwa kwa Yesu.

11. (a) Yesu alipatwa na nini katika siku ya Pasaka ya mwaka wa 33? (b) Sababu gani siku 15 Nisani ya mwaka wa 33 iliitwa Sabato ‘kubwa’? (Soma maelezo ya chini.)

11 Kwa hiyo, tunaweza kujiuliza, Namna gani kuhusu Pasaka ya mwaka wa 33? Bila shaka, siku 13 Nisani, mbele ya siku ‘ambapo munyama wa pasaka lazima atolewe zabihu,’ Kristo aliambia Petro na Yohana hivi: ‘Nendeni mukatutayarishie pasaka ili tule.’ (Lu. 22:7, 8) “Mwishowe. . . saa ilifika” ili kula chakula cha Pasaka, siku 14 Nisani kisha jua kushuka, ilikuwa Siku ya Ine mangaribi. Yesu alikula Pasaka pamoja na mitume wake, na kisha alianzisha Chakula cha Bwana cha Mangaribi. (Lu. 22:14, 15) Usiku huo alikamatwa na kuhukumiwa. Ilipokaribia kuwa saa sita ya muchana ya siku 14 Nisani, Yesu alitundikwa, na kisha muchana alikata roho. (Yoh. 19:14) Hivyo ndivyo, ‘Kristo pasaka yetu alivyotolewa’ katika siku ileile ambayo mwana​-kondoo wa Pasaka alichinjwa. (1 Kor. 5:7; 11:23; Mt. 26:2) Siku hiyo ya Wayahudi ilipokaribia kumalizika, Yesu alizikwa​—mbele ya siku 15 Nisani kuanza. *​—Law 23:5-7; Lu. 23:54.

UKUMBUSHO NI WA MAANA KWAKO

12, 13. Namna gani watoto wa Waisraeli walishiriki katika sherehe ya Pasaka?

12 Tuzungumuzie tena mambo yaliyotokea huko Misri. Musa alisema kwamba wakati ujao, watu wa Mungu wangeendelea kushika Pasaka; walipaswa kuifanya ‘mupaka wakati usio na kipimo.’ Kila mwaka wakati wa Pasaka, watoto wangewauliza wazazi wao sababu gani walisherehekea Pasaka. (Soma Kutoka 12:24-27; Kum. 6:20-23) Kwa njia hiyo, Pasaka ingekuwa “ukumbusho” wa maana hata kwa watoto.​—Kut. 12:14.

13 Toka kizazi hata kizazi, Waisraeli walifundisha watoto wao mambo ya maana sana kuhusu Pasaka. Jambo moja walilojifunza ni kwamba Yehova anaweza kuwalinda watumishi wake. Watoto walijifunza kwamba Yehova si Mungu wa kuwazia​-wazia tu. Yehova iko, na anapendezwa na watu wake na anawalinda. Alionyesha hilo alipowalinda wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli “alipowaletea Wamisri pigo.”

14. Wazazi Wakristo wanaweza kutumia Pasaka ili kuwasaidia watoto wao wajue nini?

14 Wazazi Wakristo hawawaelezee watoto wao kila mwaka maana ya Pasaka hiyo. Lakini je, wewe pia unawafundisha watoto kwamba Mungu analinda watu wake? Je, unawasaidia wasadiki kama wewe kwamba Yehova angali anawalinda watu wake? (Zab. 27:11; Isa. 12:2) Je, unafanya hivyo kwa njia ya mazungumuzo yenye kupendeza kati yako nao, ao unafanya hivyo kama mutu anayewatolea hotuba? Ujikaze kuwafundisha mambo hayo ili kuchochea familia yako ikomae kiroho.

Unapozungumuzia Pasaka, ni mambo gani unayoweza kuwafundisha watoto wako? (Ona fungu la 14)

15, 16. Pasaka na habari zilizo katika kitabu cha Kutoka zinatufundisha nini kumuhusu Yehova?

15 Pasaka inaweza kutufundisha mambo mengine pia. Yehova aliwakomboa pia watu wake, na ‘kuwatoa katika Misri.’ Fikiria sana jambo hilo. Aliwaongoza kupitia nguzo ya wingu na nguzo ya moto. Walipita katikati ya Bahari Nyekundu ambayo ilikuwa imegawanyika na kufanya nguzo mbili upande wa kuume na upande wa kushoto. Walipofika upande mwingine, waliona nguzo mbili hizo za maji zikifunika jeshi la Wamisri. Kisha Waisraeli waliokombolewa walipaza sauti hivi: ‘Acheni nimwimbie Yehova. Farasi na mupandaji wake amewatupa baharini. Nguvu zangu na uwezo wangu ni Yah, kwa maana yeye ndiye wokovu wangu.’​—Kut. 13:14, 21, 22; 15:1, 2; Zab. 136:11-15.

16 Ikiwa wewe una watoto, je, unawasaidia wamutegemee Yehova, wamuone kuwa Mukombozi wao? Je, wanaweza kuona kwamba unaamini hivyo katika maneno na maamuzi yako? Bila shaka unaweza kupanga muzungumuzie katika Ibada ya Familia habari tuliyosoma katika kitabu cha Kutoka sura ya 12-15 na ukazie namna Yehova alivyowakomboa watu wake. Wakati mwengine munaweza kuzungumuzia jambo hilo kwa kusoma Matendo 7:30-36 ao Danieli 3:16-18, 26-28. Kwa kweli, vijana na wazee wanapaswa kujua kwamba Yehova anaweza kuwakomboa watumishi wake kama alivyofanya hapo zamani. Kama alivyowakomboa watu wake katika siku za Musa, atatukomboa katika siku zinazokuja.​—Soma 1 Wathesalonike 1:9, 10.

SIKU YA KUKUMBUKA

17, 18. Sababu gani damu ya Yesu ni yenye samani zaidi kuliko damu ya mwana​-kondoo aliyechinjwa wakati wa Pasaka?

17 Wakristo wa kweli hawasherehekee Pasaka ya Wayahudi. Pasaka ilikuwa sehemu ya Sheria ya Musa, na sisi hatuko chini ya sheria hiyo. (Rom. 10:4; Kol. 2:13-16) Tofauti na hilo, tunasherehekea tukio lingine, ni kusema, kifo cha Mwana wa Mungu. Lakini, tunaweza kujifunza mambo mengi kutokana na Pasaka iliyoanzishwa huko Misri.

18 Damu ya mwana​-kondoo iliyopakwa kwenye nguzo na sehemu ya juu ya mulango iliokoa uzima wa wazaliwa wa kwanza. Leo, hatutoe zabihu za wanyama wakati wa Pasaka ao wakati mwingine. Lakini damu ya zabihu ya Yesu ni yenye samani kubwa zaidi, damu hiyo itatuwezesha kupata uzima wa milele. Mutume Paulo aliandika kwamba Wakristo watiwa​-mafuta wanaokolewa kupitia “damu ya kunyunyiza,” ni kusema, damu ya Yesu. Wakristo hao ni “kutaniko la wazaliwa wa kwanza ambao wameandikishwa mbinguni.” (Ebr. 12:23, 24) Wakristo walio na tumaini la kuishi milele hapa duniani wataokolewa pia kupitia damu hiyo. Kwa hiyo, sisi wote tunapaswa kuendelea kufikiria uhakikisho huu: ‘Kwa njia yake tuna kuachiliwa huru kwa njia ya fidia kupitia damu ya huyo, ndiyo, musamaha wa makosa yetu, kulingana na utajiri wa fazili zake zisizostahiliwa.’​—Efe. 1:7.

19. Sababu gani namna mwana​-kondoo wa Pasaka alivyochinjwa inatufanya tutumainie kabisa unabii wa Biblia?

19 Waisraeli walipochinja mwana​-kondoo wa Pasaka, hawakupaswa kuvunja hata mufupa wake mumoja. (Kut. 12:46; Hes. 9:11, 12) Tuseme nini basi kuhusu “Mwana​-kondoo wa Mungu” aliyekuja kutukomboa? (Yoh. 1:29) Alitundikwa katikati ya watenda-mabaya wawili. Wayahudi walimuomba Pilato atoe ruhusa ya kuvunja mifupa ya wanaume hao waliokuwa wametundikwa ili wafe haraka. Kwa hiyo, miili yao ingeondolewa kwenye miti mbele ya siku 15 Nisani, ambayo ilikuwa Sabato kubwa. Askari walivunja miguu ya watenda​-mabaya wawili, “lakini walipokuja kwa Yesu, kwa kuwa waliona kwamba tayari alikuwa amekufa, hawakuivunja miguu yake.” (Yoh. 19:31-34) Kama vile mifupa ya mwana​-kondoo wa Pasaka haikupaswa kuvunjwa, mifupa ya Yesu haikuvunjwa pia. Kwa hiyo mwana​-kondoo wa Pasaka alikuwa “kivuli” cha mambo ambayo yangetendeka siku 14 Nisani, mwaka wa 33. (Ebr. 10:1) Hilo lilitimiza maneno yanayopatikana kwenye Zaburi 34:20. Kwa hiyo, tunapaswa kutumainia kabisa unabii wa Biblia.

20. Ni tofauti gani kubwa iliyo kati ya Pasaka na Chakula cha Mangaribi cha Bwana?

20 Lakini, kuna tofauti fulani kati ya Pasaka na Chakula cha Mangaribi cha Bwana. Hilo linaonyesha kwamba Pasaka ambayo Wayahudi walikuwa wakisherehekea haikuwa kivuli cha yale ambayo Kristo aliwaambia wafuasi wafanye ili kukumbuka kifo chake. Walipofanya Pasaka huko Misri, Waisraeli walikula nyama ya mwana​-kondoo lakini hawakula damu yake. Jambo hilo linatofautiana na maagizo ambayo Yesu aliwatolea wanafunzi wake. Alisema kwamba wale watakaotawala “katika Ufalme wa Mungu” wanapaswa kula mukate na kunywa divai ambayo ni mifano ya mwili wake na damu yake. Tutazungumuzia kwa urefu jambo hilo katika habari inayofuata.​—Mk. 14:22-25.

21. Sababu gani ni jambo la maana kujifunza kuhusu Pasaka?

21 Bila shaka, Pasaka ilikuwa tukio la maana sana katika historia ya watu wa Mungu, na kila mumoja wetu anapaswa kujifunza mambo mengi kutokana na tukio hilo. Kwa hiyo, hata ikiwa Pasaka ‘ilikuwa ukumbusho kwa’ Wayahudi, wala si kwa Wakristo, sisi Wakristo tunapaswa kujifunza mambo mengi kuihusu na kupata somo kutokana nayo kwa sababu “andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu”.​—2 Tim. 3:16.

^ Mwezi wa Abibu uliitwa Nisani kisha Waisraeli kutoka uhamishoni Babiloni, lakini, ili kurahisisha mambo, tutatumia Nisani ili kutaja mwezi wa kwanza wa kalendari ya Wayahudi.

^ Siku 15 Nisani ilianza jua liliposhuka. Sabato (Siku ya Posho) ya kila juma ya mwaka huo ilitokea kwa wakati mumoja na siku ya kwanza ya Sikukuu ya Keki Zisizotiwa Chachu ambayo mara nyingi ilikuwa Sabato. Kwa kuwa Sabato hizo mbili zilitokea wakati mumoja, zilikuwa Sabato ‘kubwa.’​—Soma Yohana 19:31, 42.