Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Usiache Akili Yako ‘Itikiswe’ kwa Urahisi

Usiache Akili Yako ‘Itikiswe’ kwa Urahisi

‘Akina ndugu, tunawaomba ninyi musitikiswe upesi kutoka kwenye kufikiri kwenu.’​—2 THES. 2:1, 2.

1, 2. Sababu gani udanganyifu umeenea sana leo, na habari za uongo zinaenezwa namna gani? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

 UDANGANYIFU, ujanja na uongo ni mambo yenye kuenea sana leo. Hilo halipaswi kutushangaza. Biblia inaonyesha waziwazi kwamba Shetani ni fundi katika kuwadanganya watu, na yeye ndiye mutawala wa ulimwengu huu. (1 Tim. 2:14; 1 Yoh. 5:19) Kwa kuwa tunakaribia mwisho wa ulimwengu huu muovu, hasira ya Shetani inaendelea kupanda kwa sababu anajua kama ana “kipindi kifupi cha wakati” tu. (Ufu. 12:12) Kwa hiyo tunaweza kutazamia kwamba wale wanaoongozwa na Shetani wataendelea kutenda kwa udanganyifu. Watatafuta zaidi sana kuwadanganya waabudu wa kweli.

2 Wakati fulani vyombo vya habari vinawasingizia watumishi wa Yehova na kutangaza uongo wa waziwazi kuwahusu. Habari za uongo zinaenezwa kupitia vipindi vya televizyo, magazeti, na Internete. Kwa hiyo, watu fulani wanadanganywa na kuamini habari hizo bila kuzichunguza.

3. Ni nini inayoweza kutusaidia tusidanganywe?

3 Sisi ni wenye furaha kwa sababu tuna Neno la Mungu, ambalo ni “lenye faida . . . kwa kunyoosha mambo.” Neno hilo linaweza kutusaidia tusidanganywe na adui yetu, Shetani. (2 Tim. 3:16) Ni jambo la maana tujifunze kutokana na mambo ambayo mutume Paulo aliandika kuhusu Wakristo fulani wa Thesalonike ambao walikuwa wamedanganywa, kwa kukubali mambo yasiyokuwa ya kweli. Mutume Paulo aliwashauri ‘wasitikiswe upesi kutoka kwenye kufikiri kwao.’ (2 Thes. 2:1, 2) Mashauri hayo ya mutume Paulo yanatufundisha nini, na namna gani tunaweza kuyatumia leo?

MAONYO KWA WAKATI UNAOFAA

4. Namna gani Wakristo wa Thesalonike walionywa kuhusu kuja kwa “siku ya Yehova,” na sisi tunaonywa namna gani?

4 Katika barua yake ya kwanza kwa kutaniko la Thesalonike, mutume Paulo alizungumuzia kuja kwa “siku ya Yehova.” Alipenda ndugu na dada wasiwe katika giza na wawe tayari. Kwa kuwa walikuwa “wana wa nuru,” aliwatia moyo ‘wakae macho na kutunza akili zao.’ (Soma 1 Wathesalonike 5:1-6.) Leo, tunangojea uharibifu wa Babiloni Mukubwa, ni kusema, dini zote za uongo. Uharibifu huo utaonyesha kwamba siku kubwa ya Yehova imeanza. Jambo la kufurahisha ni kwamba, tumeelewa vizuri namna ambavyo kusudi la Yehova litatimizwa. Pia, kupitia kutaniko, tunapewa vikumbusho kwa ukawaida na kwa wakati unaofaa ili tutunze akili zetu. Kusikiliza maonyo hayo tunayopata kwa ukawaida kunaweza kutia nguvu azimio letu la kumutolea Mungu ‘utumishi mutakatifu pamoja na nguvu zetu za kufikiri.’​—Rom. 12:1.

Mutume Paulo aliandika barua zilizowatolea Wakristo maonyo kwa wakati unaofaa (Ona fungu la 4 na la 5)

5, 6. (a) Paulo alizungumuzia nini katika barua yake ya pili kwa Wathesalonike? (b) Mungu atafanya nini hivi karibuni kupitia Yesu, na ni vizuri kila mumoja wetu ajiulize maulizo gani?

5 Muda kidogo tu kisha kutumia Wakristo wa Thesalonike barua yake ya kwanza, mutume Paulo aliwatumia barua ya pili. Katika barua hii ya pili alizungumuzia ziki ambayo itatokea wakati ambapo Bwana wetu Yesu atawahukumu ‘wale wasiomujua Mungu na wale wasiotii habari njema.’ (2 Thes. 1:6-8) Mambo anayozungumuzia katika sura ya pili ya barua hii yanaonyesha kwamba watu fulani katika kutaniko hilo walikuwa wameanza kuvurugika katika akili na kuogopa sana waliposikia kwamba siku ya Yehova ilikuwa imekaribia. (Soma 2 Wathesalonike 2:1, 2.) Wakristo hao wa kwanza-kwanza hawakuelewa vizuri namna kusudi la Yehova lingetimizwa, kama vile mutume Paulo alivyosema kuhusu unabii: “Kwa maana tuna ujuzi wa sehemu tu nasi tunatoa unabii kwa sehemu tu; lakini wakati kile kilicho kamili kitakapofika, kile kilicho kwa sehemu tu kitaondolewa mbali.” (1 Kor. 13:9, 10) Lakini maonyo hayo yaliyoongozwa na roho ambayo Paulo, Petro na ndugu wengine watiwa mafuta waaminifu wa wakati huo waliandika, yalipaswa kuwasaidia kuendelea kulinda imani yao.

6 Ili kurekebisha mambo, roho ya Mungu ilimuongoza mutume Paulo kuonyesha waziwazi kwamba mbele siku ya Yehova ifike kungetokea uasi-imani mukubwa na ‘mutu wa uasi-sheria.’ * Kisha, kwa wakati unaofaa, Bwana Yesu ‘angewafanya kuwa si kitu’ wale wote waliokuwa wamedanganywa. Mutume Paulo alionyesha kwamba wangepewa hukumu hiyo kwa sababu “hawakukubali kuipenda ile kweli.” (2 Thes. 2:3, 8-10) Kwa hiyo, ni jambo la maana kila mumoja wetu ajiulize hivi: ‘Ninaipenda kweli kwa kadiri gani? Je, ninajua mafasiriyo mapya yanayochapishwa katika gazeti Munara wa Mulinzi na vichapo vyetu vingine vinavyotegemea Biblia?’

CHAGUA MARAFIKI WAKO KWA HEKIMA

7, 8. (a) Wakristo wa kwanza​-kwanza walipaswa kupambana na hatari gani? (b) Wakristo wanapaswa kupambana na hatari gani ya pekee leo?

7 Bila shaka, zaidi ya waasi​-imani na mafundisho yao, Wakristo wangepambana na hatari zingine. Mutume Paulo alimuandikia Timotheo kwamba “kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote.” Alionyesha pia kwamba “kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Tim. 6:10) Zaidi ya hayo, walipaswa pia kupambana kila mara na “matendo ya mwili.”​—Gal. 5:19-21.

8 Lakini, inapendeza kujua sababu gani mutume Paulo aliwatolea Wathesalonike maonyo mazito kuhusu wale ambao aliita “mitume wa uongo.” Kati yao kulikuwa watu waliosema “mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (2 Kor. 11:4, 13; Mdo. 20:30) Baadaye, Yesu alisifu kutaniko la Efeso kwa sababu ‘halikuvumilia watu wabaya.’ Wakristo wa Efeso ‘waliwajaribu’ watu hao na kutambua kwamba walikuwa mitume wa uongo. (Ufu. 2:2) Inapendeza kuona kwamba, katika barua yake ya pili kwa Wathesalonike, mutume Paulo alitoa shauri hili: ‘Sasa tunawapa ninyi maagizo, akina ndugu, katika jina la Bwana Yesu Kristo, mujiepushe na kila ndugu anayetembea bila utaratibu.’ Kisha alizungumuzia Wakristo ambao ‘hawakutaka kufanya kazi.’ (2 Thes. 3:6, 10) Ikiwa walipaswa kuepuka watu fulani waliokuwa wavivu na ambao hawakutaka kufanya kazi, basi lilikuwa jambo la maana hata zaidi kuepuka watu ambao walikuwa wameanza kutenda kama waasi-imani. Bila shaka, kufanya urafiki wa karibu pamoja na watu hao kulikuwa jambo la hatari na la kuepuka. Na ndivyo ilivyo leo pia.​—Met. 13:20.

9. Sababu gani tunapaswa kufanya angalisho ikiwa mutu fulani anaanza kutoa maoni yake kuhusu mambo ambayo Biblia haizungumuzie waziwazi ao kuchambua tengenezo la Yehova?

9 Kwa kuwa tunakaribia sana mwanzo wa ziki kubwa na mwisho wa ulimwengu huu muovu, maonyo hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu ambayo yalitolewa wakati wa mitume ni ya maana sana kwetu. Hatutaki hata kidogo ‘kukosa kusudi’ la fazili zisizostahiliwa za Yehova na kupoteza tumaini la uzima wa milele, iwe ni mbinguni ao duniani. (2 Kor. 6:1) Ikiwa mutu fulani anayehuzuria mikutano yetu anaanza kutuingiza katika mabishano kuhusu mambo ambayo Biblia haizungumuzie waziwazi ao anaanza kuchambua tengenezo la Yehova, tunapaswa kabisa kufanya angalisho.​—2 Thes. 3:13-15.

‘ENDELEA KUSHIKA MAPOKEO ULIYOFUNDISHWA’

10. Wakristo wa Thesalonike walitiwa moyo kushika mapokeo gani?

10 Mutume Paulo alionya Wakristo wa Thesalonike ‘wasimame imara’ na kushika yale ambayo walikuwa wamefundishwa. (Soma 2 Wathesalonike 2:15.) Ni “mapokeo” gani ambayo walikuwa wamefundishwa? Bila shaka, hayakuwa mafundisho ambayo dini ya uongo inafundisha na ambayo watu wanafikiri kwamba inatoka katika Biblia. Lakini, mutume Paulo alikuwa anazungumuzia mafundisho ambayo yeye na wengine walikuwa wamepokea kwa Yesu na vilevile yale ambayo Mungu aliwachochea waandike. Mengi ya mafundisho hayo yalikuja kuwa sehemu ya Maandiko matakatifu. Mutume Paulo aliwasifu ndugu katika kutaniko la Korintho kwa sababu, kama alivyoandika, ‘katika mambo yote munanikumbuka na munayashika sana mapokeo kama vile nilivyowapa ninyi.’ (1 Kor. 11:2) Mafundisho hayo yalitokana na Yehova na Yesu na kwa hiyo yalipaswa kutumainiwa.

11. Watu fulani wanadanganywa namna gani?

11 Alipoandikia Waebrania, mutume Paulo alizungumuzia njia mbili ambamo Mukristo anaweza kupoteza imani na kushindwa kusimama imara. (Soma Waebrania 2:1; 3:12.) Alizungumuzia ‘kupeperushwa’ na ‘kujiondoa.’ Kwa mufano, inaweza kuwa vigumu kutambua namna mashua inavyopeperushwa mbali kutoka kwenye inchi kavu. Pole kwa pole, inaweza kuenda mbali. Kwa upande mwingine, mutu pia anaweza kusukuma mashua yake kutoka kwenye inchi kavu. Mifano hiyo miwili inaonyesha namna mutu anavyoweza kudanganywa, kwa kuanza kuwa na mashaka kuhusu kweli.

12. Ni mambo gani yanayoweza kuharibu hali yetu ya kiroho leo?

12 Inaonekana kwamba Wathesalonike fulani walikuwa katika hali hiyo. Namna gani leo? Kuna mambo mengi yenye kupoteza wakati. Fikiria wakati mwingi ambao watu wanapitisha ili kuzungumuza na marafiki wao kwenye Internete, ili kusoma na kujibu ujumbe kwenye Internete, ili kutafuta habari za hivi karibuni kuhusu michezo ao kufanya mambo wanayopenda kufanya kama vile kupiga gitari, kusoma vitabu, kutazama televizyo, kusikiliza muziki na mengine. Mambo yote hayo yanaweza kukengeusha akili ya Mukristo na kupunguza bidii yake. Matokeo yanaweza kuwa nini baadaye? Anaweza kukosa wakati wa kusali, kujifunza Neno la Mungu, kuhuzuria mikutano, na kuhubiri. Tunaweza kufanya nini ili akili yetu isikitikiswe ao kudanganywa hivyo kwa urahisi?

MAMBO YA KUSAIDIA AKILI YETU ISITIKISWE

13. Kama ilivyotabiriwa, watu wana maoni gani leo kuhusu siku za mwisho, na ni nini itasaidia imani yetu isiregee?

13 Hatupaswe kusahau kwamba tunaishi katika siku za mwisho na kwamba ni hatari kufanya urafiki na watu wanaokataa kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” Mutume Petro aliandika hivi kuhusu wakati wetu: “Watakuja wazihaki na zihaka zao, wakiendelea kulingana na tamaa zao wenyewe na kusema: ‘Huku kuwapo kwake kulikoahidiwa kuko wapi? Kwani, tangu siku mababu zetu walipolala katika kifo, mambo yote yanaendelea sawasawa kama tangu mwanzo wa uumbaji.’” (2 Pet. 3:3, 4) Kusoma Biblia kila siku na kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida kutatusaidia tuendelee kukumbuka kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” Uasi-imani uliotabiriwa ulionekana waziwazi zamani na ungali mupaka leo. ‘Mutu wa uasi-sheria’ angali na anaendelea kupinga watumishi wa Mungu. Kwa hiyo, huu ndio wakati wa kuendelea kungojea siku ya Yehova inayokaribia sana.​—Sef. 1:7.

Kujitayarisha vizuri na kushiriki katika kazi ya kuhubiri kunatusaidia tusitikiswe upesi kutoka kwenye kufikiri kwetu (Ona fungu la 14 na la 15)

14. Namna gani kufanya mengi katika kazi ya kuhubiri kunatulinda?

14 Ushuhuda umeonyesha kwamba njia kubwa ya kusaidia akili yetu isitikiswe ao tusidanganywe ni kuhubiri kwa ukawaida habari njema ya Ufalme. Ndiyo maana, wakati Yesu, ambaye ni Kichwa cha kutaniko, aliwaamuru wafuasi wake wafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, wawafundishe kushika mambo yote aliyokuwa amewafundisha, alikuwa akiwatolea shauri ambalo lingewalinda wasidanganywe. (Mt. 28:19, 20) Kutenda kulingana na agizo hilo kunatuchochea kuwa na bidii katika kazi ya kuhubiri. Je, unafikiri kwamba ndugu zetu wa Thesalonike wangefurahia kuhubiri na kufundisha kijuu-juu tu, kama watu wanaofanya kazi fulani kwa sababu tu wanalazimishwa kuifanya? Kumbuka maneno haya ambayo mutume Paulo aliwaandikia: ‘Musiuzime moto wa roho. Musiyatendee kwa zarau maneno ya unabii.’ (1 Thes. 5:19, 20) Bila shaka, unabii mbalimbali ambao tunajifunza na kuelezea wengine ni wenye kupendeza sana!

15. Tunaweza kuzungumuzia mambo gani ya maana wakati wa ibada ya familia?

15 Bila shaka, tunataka kusaidia washiriki wa familia zetu wafanye namna yao ya kuhubiri iwe nzuri. Ndugu na dada wengi wametambua kwamba njia moja ya kusaidia washiriki wa familia zao ni kutumia wakati fulani wanapofanya ibada ya familia ili kujitayarisha kwa ajili ya mahubiri. Munaweza kuzungumuzia namna washiriki wa familia wanaweza kurudilia wale waliopendezwa na ujumbe wa Biblia. Watazungumuzia nini watakapowarudilia? Ni habari gani ambazo zitawasaidia wale watakaorudiliwa waendelee kupendezwa na ujumbe wa Biblia? Ni wakati gani unaofaa kabisa ili kuwarudilia watu hao? Wengi wanatumia pia wakati fulani wa ibada yao ya familia ili kutayarisha mikutano, hilo linawasaidia wajue mambo yatakayozungumuziwa kwenye mikutano hiyo. Je, unaweza kujitayarisha vizuri ili kutoa maelezo kwenye mikutano? Kutoa maelezo kutatia nguvu imani yako na kutasaidia akili yako isitikiswe. (Zab. 35:18) Kwa kweli, kuhuzuria ibada ya familia kutatusaidia tuepuke kuwazia​-wazia mambo ambayo Biblia haizungumuzie waziwazi na kutilia mashaka mafundisho ya kweli.

16. Ni nini inayowachochea Wakristo watiwa​-mafuta waendelee kulinda uwezo wao wa kufikiri?

16 Kufikiria namna ambavyo Yehova amebariki watu wake kwa miaka mingi kwa kuwasaidia waelewe vizuri unabii wa Biblia, kunaweza kutusaidia tusamini baraka ambazo tunangojea. Watiwa​-mafuta wanangojea kujiunga na Kristo huko mbinguni. Tumaini hilo linawachochea waendelee kulinda uwezo wao wa kufikiri! Maneno haya ambayo mutume Paulo aliwaandikia Wathesalonike yanawahusu: ‘Sisi tuna wajibu wa kumushukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu, akina ndugu munaopendwa na Yehova, kwa sababu Mungu aliwachagua ninyi . . . kwa kuwatakasa ninyi kwa roho na kwa imani yenu katika kweli.’​—2 Thes. 2:13.

17. Unatiwa moyo namna gani na maneno yanayopatikana kwenye 2 Wathesalonike 3:1-5?

17 Pia, wale wote walio na tumaini la kuishi milele duniani wanapaswa kujikaza kulinda akili yao isitikiswe kwa urahisi. Ikiwa unatumaini la kuishi duniani, endelea kutii maneno yenye kutia moyo ambayo mutume Paulo aliwatolea watiwa-mafuta wenzake katika Thesalonike. (Soma 2 Wathesalonike 3:1-5.) Kila mumoja wetu anapaswa kusamini sana maneno hayo yenye kutia moyo. Bila shaka, barua za Paulo kwa Wathesalonike zinatutolea maonyo ya maana sana kuhusu kuwazia​-wazia mambo ambayo Biblia haizungumuzie waziwazi na kuamini mawazo yenye kuleta mashaka. Kwa kuwa tunakaribia sana mwisho, acheni tusamini sana maonyo hayo.

^ Kama tunavyosoma katika Matendo 20:29, 30, mutume Paulo alionyesha kwamba kutoka katika makutaniko ya Kikristo, ‘watu wangesimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate.’ Historia inaonyesha kwamba kadiri siku zilivyopita, tofauti kati ya viongozi wa dini na waamini wengine ilianza kuonekana. Kisha mwaka wa 200, ilionekana wazi kwamba ‘mutu wa uasi-sheria’ ni viongozi wa dini zinazojiita kuwa za Kikristo.​—Soma Munara wa Mulinzi wa 01/02/1990, ukurasa wa 10-14.