Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Furahia Ndoa ya Mwana​-Kondoo!

Furahia Ndoa ya Mwana​-Kondoo!

“Acheni tushangilie na kuwa wenye shangwe mno . . . kwa sababu ndoa ya Mwana​-Kondoo imefika.”​—UFU. 19:7.

1, 2. (a) Ni ndoa ya nani itakayoleta furaha huko mbinguni? (b) Tutazungumuzia maulizo gani?

 MARA nyingi kutayarisha ndoa kunachukua wakati. Lakini tunataka kuzungumuzia ndoa ya pekee sana, ni kusema, ndoa ya Mufalme. Ndoa hiyo imetayarishwa kwa kipindi cha miaka 2 000 hivi. Karibuni bwana​-arusi atajiunga na bibi​-arusi. Nyumba ya Mufalme itajaa nyimbo zenye kupendeza, na viumbe walio mbinguni wataimba hivi: ‘Musifuni Yah, kwa sababu Yehova Mungu wetu, Mweza​-Yote, ameanza kutawala akiwa mufalme. Acheni tushangilie na kuwa wenye shangwe mno, na tumupe yeye utukufu, kwa sababu ndoa ya Mwana​-Kondoo imefika na muke wake amejitayarisha.’​—Ufu. 19:6, 7.

2 Yesu Kristo ndiye yule “Mwana​-Kondoo” ambaye ndoa yake italeta furaha huko mbinguni. (Yoh. 1:29) Ni mavazi ya namna gani atakayovaa kwa ajili ya ndoa? Bibi​-arusi wake ni nani? Namna gani bibi​-arusi huyo ametayarishwa kwa ajili ya ndoa? Ndoa hiyo itafanywa wakati gani? Kwa kuwa ndoa hiyo italeta furaha huko mbinguni, je, wale walio na tumaini la kuishi milele duniani wataifurahia pia? Kwa kuwa tunangojea kwa hamu tukio hilo, acheni tuzungumuzie maulizo hayo tunapoendelea kuchunguza Zaburi ya 45.

‘MAVAZI YAKE YAMETIWA MANUKATO’

3, 4. (a) Mutunga​-zaburi anasema nini kuhusu mavazi ambayo bwana​-arusi anavaa kwa ajili ya ndoa, na ni nini inayomufanya afurahi zaidi? (b) “Binti za wafalme” na “malkia” wanaofurahi pamoja na Bwana-arusi ni nani?

3 Soma Zaburi 45:8, 9. Bwana​-arusi, Yesu Kristo, atavaa mavazi yake ya kifalme yenye utukufu ya ndoa. Bila shaka, mavazi yake yanatoa harufu nzuri kama ile ya “manukato bora zaidi” kama vile manemane na kida, ambayo ilikuwa kati ya vitu vilivyotumiwa ili kutengeneza mafuta matakatifu ya kutia mafuta yaliyotumiwa katika Israeli.​—Kut. 30:23-25.

4 Muziki wa mbinguni unaopigwa katika nyumba ya Mufalme unamufanya Bwana​-arusi afurahi zaidi anapongojea ndoa yake. “Malkia” anafurahi pia pamoja naye. Malkia huyo ni sehemu ya mbinguni ya tengenezo la Mungu linalotia ndani “binti za wafalme,” ambao ni malaika watakatifu. Inapendeza sana kusikia sauti za mbinguni zikisema: “Acheni tushangilie na kuwa wenye shangwe mno . . . kwa sababu ndoa ya Mwana-Kondoo imefika”!

BIBI-ARUSI ANATAYARISHWA KWA AJILI YA NDOA

5. ‘Muke wa Mwana​-Kondoo’ ni nani?

5 Soma Zaburi 45:10, 11. Tumejua Bwana​-arusi, lakini bibi​-arusi wake ni nani? Bibi​-arusi huyo ni washiriki wa kutaniko wanaoongozwa na Yesu Kristo. (Soma Waefeso 5:23, 24.) Watatawala pamoja naye katika Ufalme wake wa Kimasiya. (Lu. 12:32) Wakristo hao watiwa​-mafuta 144 000 ‘wanaendelea kumufuata Mwana​-Kondoo popote anapoenda.’ (Ufu. 14:1-4) Wanakuwa ‘muke [ao bibi] wa Mwana​-Kondoo’ na wataishi pamoja naye mbinguni.​—Ufu. 21:9; Yoh. 14:2, 3.

6. Sababu gani watiwa​-mafuta wanaitwa ‘binti ya mufalme,’ na sababu gani wanaambiwa kwamba wanapaswa ‘kusahau watu wao’?

6 Bibi-arusi anaitwa ‘Ewe binti,’ lakini pia ‘binti ya mufalme.’ (Zab. 45:13) ‘Mufalme’ huyo ni nani? Ni Yehova. Anawakubali Wakristo watiwa​-mafuta kuwa “watoto” wake. (Rom. 8:15-17) Kwa kuwa watakuwa bibi​-arusi wa Kristo huko mbinguni, watiwa​-mafuta wanaambiwa hivi: ‘Muwasahau watu wenu na nyumba ya baba yenu [wa kimwili].’ Wanapaswa kuendelea ‘kukaza akili zao juu ya mambo yaliyo juu, si juu ya mambo yaliyo duniani.’​—Kol. 3:1-4.

7. (a) Namna gani Kristo amekuwa akimutayarisha yule atakayekuwa bibi-arusi wake? (b) Namna gani bibi-arusi anamuona yule atayekuwa bwana​-arusi wake?

7 Kwa miaka mingi, Kristo amekuwa akimutayarisha bibi-arusi wake kwa ajili ya ndoa itakayofanywa mbinguni. Mutume Paulo alisema kwamba Kristo ‘alilipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake, ili alitakase, akilisafisha na kuliosha kwa maji kwa njia ya neno, ili kujipa mwenyewe kutaniko likiwa na fahari, likiwa bila doa ao kunyanzi au lolote la mambo hayo, bali ili liwe takatifu na bila dosari.’ (Efe. 5:25-27) Mutume Paulo aliwaambia Wakristo watiwa​-mafuta katika Korintho hivi: ‘Nina wivu juu yenu kwa wivu wa kimungu, kwa maana mimi binafsi niliwachumbia ninyi mume mumoja ili niwatoe mukiwa bikira safi kiadili kwa Kristo.’ (2 Kor. 11:2) Bibi​-arusi anamutolea Mungu ibada safi na yenye kukubalika, kwa hiyo Yesu Kristo anamuona kuwa mwenye sura nzuri. Na bibi​-arusi ‘anamuinamia’ Yesu Kristo na kumukubali kuwa “bwana” yake wa wakati ujao.

BIBI-ARUSI ‘ANAPELEKWA’ KWA MUFALME

8. Sababu gani bibi-arusi anatajwa kuwa “mwenye utukufu wote”?

8 Soma Zaburi 45:13, 14a. Bibi-arusi anatajwa kuwa “mwenye utukufu wote” kwa ajili ya ndoa ya Mufalme. Katika andiko la Ufunuo 21:2, bibi​-arusi anafananishwa na muji, Yerusalemu Mupya, na ‘amepambwa kwa ajili ya mume wake.’ Muji huo wa mbinguni una “utukufu wa Mungu” na unangaa, ‘kama jiwe la samani zaidi, kama jiwe la yaspi lenye kungaa kwa uangavu kama fuwele.’ (Ufu. 21:10, 11) Kitabu cha Ufunuo kinazungumuzia kwa njia yenye kupendeza uzuri wa Yerusalemu Mupya. (Ufu. 21:18-21) Ndiyo sababu mutunga​-zaburi anasema kwamba bibi​-arusi ni mwenye kupendeza kabisa! Tunatazamia awe hivyo kwa sababu ndoa ya Mufalme itafanywa huko mbinguni.

9. Bibi-​arusi anapelekwa kwa ‘mufalme’ gani, na amevaa namna gani?

9 Bibi​-arusi anapelekwa kwa Bwana​-arusi wake, ni kusema, Mufalme wa Kimasiya. Amekuwa akimutayarisha bibi​-arusi wake, kwa ‘kumusafisha na kumuosha kwa maji kwa njia ya neno.’ Yeye ni ‘mutakatifu na hana dosari [ao kasoro].’ (Efe. 5:26, 27) Bibi​-arusi wake anapaswa pia kuvaa vizuri kwa ajili ya tukio hilo, na amefanya hivyo. Kwa kweli ‘mavazi yake yamepambwa kwa zahabu’ na ‘atapelekwa kwa mufalme akiwa na mavazi yaliyofumwa.’ “Amepewa ruhusa ya kupambwa kitani bora, changavu, safi” kwa ajili ya ndoa ya Mwana​-Kondoo, ‘maana hicho kitani bora kinamaanisha matendo ya uadilifu ya watakatifu.’​—Ufu. 19:8.

“NDOA IMEFIKA”

10. Ndoa ya Mwana​-Kondoo inapaswa kufanywa wakati gani?

10 Soma Ufunuo 19:7. Ndoa ya Mwana-Kondoo inapaswa kufanywa wakati gani? Hata ikiwa andiko la Ufunuo 19:7 linaonyesha kwamba ‘muke wake amejitayarisha’ kwa ajili ya ndoa, mistari inayofuata haizungumuzie ndoa. Lakini, inatoa maelezo yaliyo wazi kuhusu sehemu ya mwisho ya ziki kubwa. (Ufu. 19:11-21) Je, hilo linamaanisha kwamba ndoa hiyo itafanywa mbele ya Bwana​-arusi Mufalme kukamilisha ushindi wake? Hapana. Matukio yanayozungumuziwa katika kitabu cha Ufunuo hayaandikwe namna yatakavyofuatana. Zaburi ya 45 inaonyesha kwamba ndoa hiyo itafanywa kisha Mufalme, Yesu Kristo, kufunga upanga wake na ‘kuendelea mupaka afanikiwe [ao ashinde]’ maadui wake.​—Zab. 45:3, 4.

11. Kristo atakapokamilisha ushindi wake, matukio yatafuatana namna gani?

11 Kwa hiyo, tunaweza kusema kwamba matukio yatafuatana hivi: Kwanza, yule “kahaba,” Babiloni Mukubwa, ni kusema, dini zote za uongo, ataharibiwa. (Ufu. 17:1, 5, 16, 17; 19:1, 2) Kisha, Kristo ataharibu sehemu itakayobaki ya ulimwengu muovu wa Shetani kwenye ‘vita vya ile siku kubwa ya Mungu Mweza​-Yote’ inayoitwa Har-magedoni. (Ufu. 16:14-16; 19:19-21) Mwishowe, Mufalme​-Shujaa atakamilisha ushindi wake kwa kumutupa Shetani na mashetani wake katika abiso, ni kusema, katika hali ya kutotenda iliyo kama kifo, ili wasiweze tena kuwadanganya watu.​—Ufu. 20:1-3.

12, 13. (a) Ndoa ya Mwana​-Kondoo itafanywa wakati gani? (b) Ni nani watakaofurahia ndoa ya Mwana​-Kondoo huko mbinguni?

12 Wakristo watiwa-mafuta wanaobaki waaminifu mupaka kifo katika siku hizi za mwisho, wanafufuliwa mara moja na kuenda mbinguni. Wakati fulani kisha kuharibiwa kwa Babiloni Mukubwa, Yesu atawakusanya kwake washiriki wa bibi​-arusi watakaokuwa wangali duniani. (1 Thes. 4:16, 17) Kwa hiyo, mbele vita ya Har-magedoni ianze, washiriki wote wa “bibi​-arusi” watakuwa wamefika mbinguni. Kisha vita hiyo, ndoa ya Mwana​-Kondoo itafanywa. Ndoa hiyo itakuwa yenye kufurahisha kabisa! Andiko la Ufunuo 19:9 linasema kwamba ‘wenye furaha ni wale walioalikwa kwenye mulo wa jioni wa ndoa ya Mwana​-Kondoo.’ Bila shaka, Washiriki 144 000 wa bibi​-arusi watafurahi kabisa. Na Bwana​-arusi Mufalme atafurahi sana ‘kula na kunywa mezani pake [kwa njia ya mufano] katika ufalme wake’ pamoja na wale wote watakaotawala pamoja naye. (Lu. 22:18, 28-30) Lakini, ndoa ya Mwana​-Kondoo haitashangiliwa tu na Bwana​-arusi na bibi-arusi wake.

13 Kama tulivyoona hapo mbele, sauti za mbinguni zitaimba hivi kwa umoja: ‘Acheni tushangilie na kuwa wenye shangwe mno, na tumupe yeye [Yehova] utukufu, kwa sababu ndoa ya Mwana​-Kondoo imefika na muke wake amejitayarisha.’ (Ufu. 19:6, 7) Lakini, tuseme nini kuhusu watumishi wa Yehova walio duniani? Je, nao watafurahia pia ndoa hiyo?

“WATAPELEKWA KWA FURAHA”

14. ‘Rafiki mabikira’ wa bibi-arusi wanaotajwa katika Zaburi ya 45 ni nani?

14 Soma Zaburi 45:12, 14b, 15. Nabii Zekaria alitabiri kwamba katika siku za mwisho, watu wa mataifa wangejiunga kwa furaha na mabaki ya Israeli wa kiroho. Aliandika hivi: “Katika siku hizo watu kumi kutoka katika luga zote za mataifa watashika, ndiyo, wataushika sana upindo wa nguo ya mutu aliye Muyahudi, wakisema: ‘Tunataka kwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.’” (Zek. 8:23) Andiko la Zaburi 45:12 linawataja hao “watu kumi” kuwa “binti za Tiro” na watu “walio matajiri kati ya watu.” Wanawaletea watiwa​-mafuta zawadi, wanatafuta kukubaliwa na kusaidiwa kiroho. Tangu mwaka wa 1935, mabaki ya watiwa​-mafuta ‘wameleta’ mamilioni ya watu ‘kwenye uadilifu,’ ni kusema, wamewafundisha ukweli kuhusu Yehova. (Dan. 12:3) Watu hao waaminifu wanaoshirikiana na Wakristo watiwa​-mafuta wamekuwa mabikira kiroho kwa sababu wameepuka ibada yoyote ya uongo katika maisha yao. ‘Rafiki hao mabikira’ wa bibi​-arusi wamejitoa wenyewe kwa Yehova na wameonyesha kwamba wao ni raia wanaomutii kwa uaminifu Bwana​-arusi Mufalme.

15. Namna gani ‘rafiki mabikira’ wanatumika pamoja na washiriki wa bibi​-arusi ambao wangali duniani?

15 Mabaki ya bibi-arusi wanapendezwa sana na ‘rafiki mabikira’ kwa sababu wanawasaidia kwa bidii kuhubiri “habari njema ya Ufalme” katika dunia yote. (Mt. 24:14) “Roho na bibi-arusi huendelea kusema: ‘Njoo [ao kuja]!’” na wale wote wanaosikia wanasema: “Njoo!” (Ufu. 22:17) “Kondoo wengine” wamesikia bibi-arusi, ni kusema, Wakristo watiwa​-mafuta wakisema “Njoo!” na wamejiunga na bibi​-arusi kwa kuwaambia wakaaji wote wa dunia “Njoo!”​—Yoh. 10:16.

16. Yehova amewatolea kondoo wengine pendeleo gani?

16 Mabaki ya watiwa​-mafuta wanawapenda kondoo wengine na wanafurahi kujua kwamba Yehova, Baba ya Bwana​-arusi, ametolea pia kondoo wengine hao pendeleo la kufurahia ndoa ya Mwana​-Kondoo itakayofanywa huko mbinguni. Ilitabiriwa kwamba ‘rafiki mabikira’ hao “watapelekwa kwa furaha na shangwe.” Bila shaka, kondoo wengine, walio na tumaini la kuishi milele duniani, watafurahi pamoja na viumbe wote wakati ndoa ya Mwana​-Kondoo itafanywa huko mbinguni. Kitabu cha Ufunuo kinawaonyesha washiriki wa ‘umati mukubwa’ wakiwa “wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana​-Kondoo.” Wanamutolea Yehova utumishi mutakatifu katika uwanja wa duniani wa hekalu lake kubwa la kiroho.​—Ufu. 7:9, 15.

‘Rafiki mabikira’ wa bibi​-arusi watafurahia pia ndoa ya Mwana​-Kondoo (Ona fungu la 16)

“MAHALI PA MABABU ZAKO PATACHUKULIWA NA WANA WAKO”

17, 18. Namna gani wengine watafaidika na ndoa ya Mwana​-Kondoo katika ulimwengu mupya, na atakuwa baba ya wanani wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu?

17 Soma Zaburi 45:16. ‘Rafiki mabikira’ wa bibi-arusi wa Kristo watafurahi zaidi watakapoona mambo mazuri ambayo ndoa ya Mwana​-Kondo itatimiza katika ulimwengu mupya. Bwana​-arusi atakazia sasa uangalifu juu ya dunia na kuwafufua “mababu zake.” Kwa kuwa atawafufua, “mababu zake” watakuwa “wana” wake. (Yoh. 5:25-29; Ebr. 11:35) Atawafanya wengine kati yao kuwa ‘wakubwa katika dunia yote.’ Bila shaka, Kristo atachagua wazee fulani waaminifu kati ya wazee wanaosimamia makutaniko leo ili waongoze mambo katika ulimwengu mupya.​—Isa. 32:1.

18 Kristo atakuwa baba ya wengine pia wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu. Kwa kweli, wale wote ambao watapata uzima wa milele duniani wataupata kwa sababu wameonyesha imani katika zabihu ya ukombozi ya Yesu. (Yoh. 3:16) Kwa hiyo, Yesu atakuwa ‘Baba yao wa Milele.’​—Isa. 9:6, 7.

WANACHOCHEWA ‘KUJULISHA JINA’ LA MUFALME

19, 20. Namna gani matukio yanayozungumuziwa katika Zaburi ya 45 yanawahusu Wakristo wote wa kweli?

19 Soma Zaburi 45:1, 17. Bila shaka, matukio yanayozungumuziwa katika Zaburi ya 45 yanawahusu Wakristo wote. Watiwa​-mafuta ambao wangali duniani wanatazamia kwa furaha kuungana hivi karibuni na ndugu zao na Bwana​-arusi wao huko mbinguni. Kondoo wengine wanatiwa moyo waendelee kutii Mufalme wao mwenye utukufu na wanafurahia sana pendeleo lao kutumika pamoja na washiriki wa bibi-arusi ambao wangali duniani. Kisha ndoa yake, Kristo na watawala wenzake wataletea wakaaji wa dunia baraka nyingi sana.​—Ufu. 7:17; 21:1-4.

20 Tunapoendelea kungojea “jambo jema” linalohusiana na Mufalme wa Kimasiya, je, hilo halituchochee ‘kujulisha jina lake’? Tujikaze ili tuwe kati ya wale ‘watakaomusifu Mufalme mupaka wakati usio na kipimo.’