Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Ona Uzuri wa Yehova’

‘Ona Uzuri wa Yehova’

Matatizo yanaweza kuwa na matokeo mabaya juu yetu. Yanaweza kutuhangaisha akili, kuturegeza, na kubadilisha maoni yetu kuhusu maisha. Mufalme Daudi wa Israeli alipatwa na magumu mengi yaliyomuhangaisha sana. Namna gani alipambana nayo? Katika wimbo wake wenye kugusa moyo, Daudi anajibu hivi: ‘Kwa sauti yangu, nilimuomba Yehova musaada; kwa sauti yangu, nilianza kumulilia Yehova anionyeshe kibali. Mbele zake niliendelea kumwanga hangaiko langu; mbele zake niliendelea kutangaza juu ya taabu yangu mwenyewe, roho yangu ilipozimia ndani yangu. Ndipo wewe mwenyewe ulipoijua [ao uliichunguza] barabara yangu.’ Bila shaka, Daudi alisali kwa unyenyekevu Mungu amusaidie.​—Zab. 142:1-3.

Daudi alipopambana na matatizo, alisali Yehova kwa unyenyekevu amusaidie

Katika wimbo mwingine, Daudi aliimba hivi: ‘Nimemuomba Yehova jambo moja—​ndilo nitakalolitafuta, kwamba nipate kukaa katika nyumba ya Yehova siku zote za maisha yangu, ili kuuona uzuri wa Yehova na kulitazama kwa usamini hekalu lake.’ (Zab. 27:4) Daudi hakuwa Mulawi, lakini wazia namna alivyojisikia aliposimama inje ya hekalu takatifu karibu na mahali ambapo watu walimuabudu Yehova. Moyo wa Daudi ulijaa shukrani nyingi hivi kwamba alitaka kupitisha siku zinazobaki za maisha yake mahali hapo ili kuendelea “kuuona uzuri wa Yehova.”

Neno “uzuri” linatumiwa kuhusiana na hali “yenye kupendeza ao yenye kufurahisha moyo, akili, ao mwili.” Siku zote Daudi alipendezwa sana na mupango ambao Mungu alifanya kwa ajili ya ibada. Tunaweza kujiuliza, ‘Je, ninapendezwa na ibada ya Yehova kama Daudi?’

‘TAZAMA KWA USAMINI’ MUPANGO WA MUNGU

Leo, hatumuabudu Yehova katika hekalu lenye kuonekana. Lakini, tunafanya hivyo katika hekalu kubwa la kiroho, ni kusema mupango ambao Mungu amefanya ili kutusaidia tumuabudu kwa njia inayofaa. * Ikiwa ‘tunatazama kwa usamini’ mupango huo, sisi pia tunaweza “kuuona uzuri wa Yehova.”

Fikiria mazabahu ya shaba ya toleo la kuteketezwa iliyokuwa mbele ya mwingilio wa hema la ibada. (Kut. 38:1, 2; 40:6) Mazabahu hayo yaliwakilisha utayari wa Mungu wa kukubali uzima wa kibinadamu wa Yesu kuwa zabihu ya ukombozi. (Ebr. 10:5-10) Fikiria namna jambo hilo linavyotuhusu sisi leo! Mutume Paulo aliandika hivi: “Tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kupitia kifo cha Mwana wake.” (Rom. 5:10) Ikiwa tunaonyesha imani katika damu iliyomwangwa ya Yesu, Mungu anaweza kutukubali na kututumainia kwa sababu tumekuwa marafiki wake. Kisha, tunaweza kuwa na “urafiki wa karibu pamoja na Yehova.”​—Zab. 25:14.

Kwa sababu ‘zambi zetu zinafutwa,’ tunaweza kufurahia ‘majira ya kuburudisha kutoka kwa Yehova.’ (Mdo. 3:19) Hali yetu inafanana na ile ya mufungwa anayengojea kifo, lakini ambaye anasikitikia matendo yake ya zamani na kufanya haraka mabadiliko. Muamuzi mwenye huruma anapoona hilo, anamuondolea hukumu ya kifo. Mufungwa huyo anajisikia kama vile muzigo muzito umeondolewa kwenye mabega yake na anafurahi sana! Yehova anafanya kama muamuzi huyo, anawakubali wanadamu wanaotubu na kuwaondolea hukumu ya kifo.

FURAHIA IBADA YA KWELI

Alipokuwa kwenye nyumba ya Yehova, Daudi alijionea namna Waisraeli wengi walivyokusanyika, namna Sheria ilivyosomwa na kuelezwa mbele ya watu, namna uvumba ulivyochomwa, na kazi mbalimbali za makuhani na Walawi. Hayo yalikuwa kati ya mambo ya maana ya ibada ya kweli. (Kut. 30:34-38; Hes. 3:5-8; Kum. 31:9-12) Mambo hayo yaliyokuwa ya maana katika ibada ya kweli huko Israeli yanalingana na yale yanayofanywa leo.

Kama vile zamani, ni jambo lenye ‘kupendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja’ leo! (Zab. 133:1) Kumekuwa ongezeko kubwa katika ‘ushirika wetu wa ndugu’ wa duniani pote. (1 Pet. 2:17) Neno la Mungu linasomwa na kufasiriwa mbele ya watu kwenye mikutano yetu. Kupitia tengenezo lake, Yehova ameendelea kututolea mafundisho mazuri. Tunapata pia chakula kingi cha kiroho kupitia vichapo ambavyo tunaweza kutumia katika funzo la pekee na funzo la familia. Mushiriki mumoja wa Baraza Linaloongoza alisema hivi: “Kutafakari juu ya Neno la Yehova, kufikiri kuhusu maana yake na kutafuta hekima na uelewaji ndiyo mambo ambayo yametajirisha sana maisha yangu na kunifanya nitosheke kiroho.” Bila shaka, ‘ujuzi unaweza kupendeza nafsi yetu.’​—Met. 2:10.

Leo, sala zenye kukubalika za watumishi wa Mungu zinamufikia Yehova kila siku. Sala hizo ni kama harufu ya uvumba wenye harufu nzuri. (Zab. 141:2) Inapendeza sana kujua kwamba Yehova Mungu anafurahi sana tunapomukaribia kwa unyenyekevu katika sala!

Musa alisali hivi: “Uzuri wa Yehova Mungu wetu na uwe juu yetu, na kazi ya mikono yetu uifanye imara juu yetu.” (Zab. 90:17) Tunapoendelea kuhubiri kwa bidii, Yehova anabariki kazi yetu. (Met. 10:22) Pengine tumewasaidia watu fulani ili wajifunze kweli. Ao tumeendelea kuhubiri kwa miaka mingi ijapokuwa kutopendezwa kwa watu, magonjwa, kuvunjika moyo, ao upinzani. (1 Thes. 2:2) Hata hivyo, tumejionea “uzuri wa Yehova” na tumetambua kwamba Baba yetu wa mbinguni anasamini kabisa yale tunayofanya, sivyo?

Daudi aliimba hivi: ‘Yehova ni sehemu yangu, fungu langu nililogawiwa, na kikombe changu. Unaulinda uriti wangu. Umenipimia mahali penye kupendeza.’ (Zab. 16:5, 6) Daudi alifurahia ‘sehemu’ yake, ni kusema, uhusiano muzuri pamoja na Yehova na pendeleo la kumutumikia. Kama Daudi, tunaweza kupatwa na matatizo, lakini tunafurahia baraka nyingi sana za kiroho! Acheni siku zote tuendelee kufurahia ibada ya kweli na ‘kutazama kwa usamini’ hekalu kubwa la kiroho la Yehova.

^ Soma Munara wa Mulinzi wa tarehe 01/07/1996, ukurasa wa 14-24.