Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Chakula Changu Ni Kufanya Mapenzi ya Mungu’

‘Chakula Changu Ni Kufanya Mapenzi ya Mungu’

Ni jambo gani unalofurahia sana? Je, ni ndoa, kulea watoto ao kufanya urafiki na watu? Pengine unafurahia kula chakula pamoja na watu unaowapenda. Hata hivyo, kwetu sisi watumishi wa Yehova, jambo la lazima sana ni kufanya mapenzi ya Mungu, kujifunza Neno lake, na kuhubiri habari njema, sivyo?

Katika wimbo wake wa kumusifu Muumbaji wake, Mufalme Daudi wa Israeli, aliimba hivi: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.” (Zab. 40:8) Ijapokuwa Daudi alipata matatizo na mahangaiko mengi katika maisha yake, alifurahia kabisa kufanya mapenzi ya Mungu. Bila shaka, si Daudi tu aliyefurahia kumutumikia Mungu wa kweli.

Mutume Paulo alitumia maneno ya Zaburi 40:8 kuhusu Masiya, ao Kristo. Paulo aliandika hivi: “Wakati yeye [Yesu] anapokuja katika ulimwengu anasema: ‘“Zabihu na toleo wewe haukutaka, bali ulinitayarishia mwili. Haukukubali matoleo mazima ya kuteketezwa na toleo la zambi.” Ndipo nikasema, “Tazama! Nimekuja (katika kitabu cha kukunjwa imeandikwa juu yangu) ili kufanya mapenzi yako, Ee Mungu.”’”—Ebr. 10:5-7.

Alipokuwa duniani, Yesu alifurahia kutazama uumbaji, kupitisha wakati pamoja na marafiki, na kula pamoja na wengine. (Mt. 6:26-29; Yoh. 2:1, 2; 12:1, 2) Lakini, jambo ambalo alihangaikia sana na kufurahia zaidi lilikuwa kufanya mapenzi ya Baba yake wa mbinguni. Ndiyo sababu Yesu alisema hivi: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yoh. 4:34; 6:38) Wanafunzi wa Yesu walijifunza kutokana na Bwana wao siri ya kupata furaha ya kweli. Walifurahia sana kuwahubiria wengine habari njema ya Ufalme, na walifanya hivyo bila kulazimishwa na kwa bidii.—Lu. 10:1, 8, 9, 17.

‘NENDENI MUKAFANYE WANAFUNZI’

Yesu aliwaamuru wafuasi wake: ‘Nendeni mukafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mukiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mupaka umalizio wa mufumo wa mambo.’ (Mt. 28:19, 20) Kutii amri ya Yesu kunamaanisha kuwahubiria  watu kila mahali ambapo wanaweza kupatikana, kurudilia wale waliopendezwa, na kujifunza Biblia pamoja nao. Kufanya kazi hivyo kunaweza kutuletea furaha nyingi.

Upendo unatuchochea tuendelee kuhubiri hata kama watu fulani wanakataa kusikiliza ujumbe wetu

Watu wasikilize ujumbe wetu ao hapana, kuwa na maoni mazuri kunaweza kutusaidia sana tufurahie mahubiri. Sababu gani tunaendelea kuhuburi habari njema hata kama watu fulani wanakataa kusikiliza ujumbe wetu? Kwa sababu tunajua kwamba tunapohubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi tunaonyesha kwamba tunamupenda Mungu na jirani yetu. Zaidi ya hilo, uzima wetu na wa majirani wetu uko katika hatari. (Eze. 3:17-21; 1 Tim. 4:16) Acheni tuzungumuzie mambo fulani ambayo yamewasaidia ndugu na dada zetu fulani waendelee kuhubiri ao kuongeza bidii yao katika maeneo ambamo watu hawafurahie ujumbe wetu.

TUMIA KILA NAFASI INAYOJITOKEZA

Mara nyingi, tunapata matokeo mazuri katika mahubiri tunapotumia maulizo vizuri. Asubuhi moja, dada Amalia aliona mwanaume mumoja akisoma gazeti katika bustani. Alimukaribia na kumuuliza ikiwa amekwisha kusoma habari fulani njema. Mwanaume huyo aliposema hapana, dada Amalia alimuambia hivi: “Ninakuletea habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu.” Hilo lilimufanya apendezwe na ujumbe, na alikubali kujifunza Biblia. Kwa hiyo, dada Amalia alianzisha mafunzo matatu ya Biblia katika bustani.

Dada Janice amefanya mahali pake pa kazi kuwa eneo lake la mahubiri. Walinzi wawili walipopendezwa na habari zinazochapishwa katika Munara wa Mulinzi, dada aliamua kuwapelekea magazeti kwa ukawaida. Alimupelekea pia mufanyakazi mwenzake aliyependezwa na habari mbalimbali katika Munara wa Mulinzi na Amuka! Mufanyakazi mwengine alipoona hivyo aliomba pia magazeti. Dada Janice anasema hivi: “Hii ni baraka kabisa kutoka kwa Yehova.” Mwishowe, alikuwa na watu 11 wa kuachia magazeti mahali pa kazi.

UWE NA MAONI YANAYOFAA

Mwangalizi mumoja mwenye kusafiri alisema kwamba katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba, wahubiri hawapashwe kumaliza mazungumuzo kwa kumuambia tu musikilizaji kwamba watarudia kumuona siku ingine. Lakini wanaweza kumuuliza musikilizaji hivi: “Ninaweza kurudia tena ili kukuonyesha namna gani tunajifunza Biblia?” ao wanaweza kusema hivi: “Ninaweza kufika siku gani na saa ngapi ili tuendelee na mazungumuzo yetu?” Mwangalizi huyo alisema kwamba kwa kutumia njia hiyo, ndugu na dada wa kutaniko ambamo alikuwa akitumikia walianzisha mafunzo ya Biblia 44 katika juma moja.

Kurudilia watu tuliohubiria bila kukawia, hata kisha siku chache tu, kunaweza kuleta matokeo mazuri. Sababu gani? Kwa sababu kufanya hivyo kunaonyesha kwamba tunapenda kuwasaidia kabisa watu wanaostahili waelewe Biblia. Mwanamuke  mumoja alipoulizwa sababu gani alikubali kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, alisema hivi: “Nilianza kujifunza kwa sababu walinihangaikia kabisa na kunionyesha upendo.”

Unaweza kumuuliza musikilizaji hivi: “Ninaweza kurudia tena ili kukuonyesha namna gani tunajifunza Biblia?”

Muda mufupi kisha kusoma Masomo ya Mapainia, dada Madaí alianza kuongoza mafunzo ya Biblia 15 na alikuwa amegawia wahubiri wengine mafunzo mengine 5. Wanafunzi wake wengi walianza kukusanyika kikawaida. Ni jambo gani ambalo lilimusaidia kuanzisha mafunzo mengi hivyo? Masomo hayo yalimuonyesha ulazima wa kuendelea kuwarudilia watu mupaka atakapowapata wale waliopendezwa hapo mbele. Shahidi mwengine ambaye amewasaidia watu wengi wajue kweli ya Biblia anasema hivi: “Nimetambua kwamba kuendelea kurudilia watu ni jambo la maana sana ili kuwasaidia wale wanaotaka kumujua Yehova.”

Kurudilia watu tuliohubiria bila kukawia kunaonyesha kwamba tunapendezwa kabisa na wale wanaotaka kuelewa Biblia

Inaomba kuwa na bidii nyingi sana ili kuwarudilia watu na kuongoza mafunzo ya Biblia. Hata hivyo, baraka ambazo tunapata zinashinda sana jitihada ambazo tulifanya. Ikiwa tunahubiri kwa bidii ujumbe wa Ufalme, tunaweza kuwasaidia wengine ‘wapate ujuzi sahihi wa kweli’ ambao utawasaidia waokolewe. (1 Tim. 2:3, 4) Sisi pia, tunaweza kutosheka na kupata furaha kubwa sana.