Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Unaendelea Kusonga Mbele Pamoja na Tengenezo la Yehova?

Unaendelea Kusonga Mbele Pamoja na Tengenezo la Yehova?

“Macho ya Yehova yako juu ya waadilifu [ao wenye haki].”1 PET. 3:12.

1. Ni tengenezo gani lililochukua nafasi ya taifa la Israeli ambalo liliasi? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

NI YEHOVA aliyeanzisha kutaniko la Kikristo katika siku za mitume na kurudisha ibada ya kweli katika siku zetu. Kama tulivyoona katika habari iliyotangulia, tengenezo lililofanyizwa na wafuasi wa kwanza-kwanza wa Kristo lilichukua nafasi ya taifa la Israeli ambalo liliasi. Tengenezo hilo lilikuwa taifa la watu kwa ajili ya jina la Yehova. Tengenezo hilo mupya, lililokubaliwa sana na Mungu, liliokoka uharibifu wa Yerusalemu katika mwaka wa 70. (Lu. 21:20 21) Matukio hayo ya siku za mitume yalionyesha mambo ambayo yangewapata watumishi wa Yehova katika siku zetu. Ulimwengu muovu wa Shetani utaharibiwa hivi karibuni, lakini watumishi wa Yehova walio duniani wataokoka siku za mwisho. (2 Tim. 3:1) Ni nini inayotuhakikishia jambo hilo?

2. Yesu alisema nini kuhusu ‘ziki kubwa,’ na itaanza namna gani?

2 Alipozungumuzia kuwapo kwake ambako hakuonekane na mwisho wa ulimwengu huu, Yesu alisema hivi: ‘Kutakuwa na ziki kubwa ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mupaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.’ (Mt. 24:3, 21) Ziki hiyo isiyolinganishwa itaanza wakati Yehova atatumia serikali za ulimwengu ili  kuharibu ‘Babiloni Mukubwa,’ ni kusema, dini zote za uongo. (Ufu. 17:3-5, 16) Kisha kutatokea nini?

SHAMBULIO LA SHETANI LITAONGOZA KWENYE HAR-MAGEDONI

3. Kisha dini za uongo kuharibiwa, Shetani atajaribu kufanyia watumishi wa Yehova nini?

3 Kisha dini za uongo kuharibiwa, Shetani na watu wanaomuunga mukono, watashambulia watumishi wa Yehova. Kwa mufano, kuhusu ‘Gogu wa inchi ya Magogu,’ Maandiko yalitabiri hivi: ‘Utaingia kama zoruba. Utakuwa kama mawingu ya kuifunika inchi, wewe na vikosi vyako vyote na vikundi vingi vya watu pamoja nawe.’ Kwa sababu mashahidi wa Yehova hawana jeshi la kuwapigania na ndio watu wanaopenda sana amani katika ulimwengu, wataonekana kuwa watu walio rahisi kushambuliwa. Lakini kuwashambulia itakuwa kujidanganya kabisa!—Eze. 38:1, 2, 9-12.

4, 5. Yehova atafanya nini Shetani atakapojaribu kuangamiza watumishi wake?

4 Yehova atafanya nini Shetani atakapojaribu kuwaangamiza watumishi wake? Yeye atatumia mamlaka yake akiwa Mutawala Mukubwa wa Ulimwengu Wote ili kuwapigania watumishi wake. Yehova anaona kushambulia watumishi wake kuwa ni kumushambulia yeye. (Soma Zekaria 2:8.) Kwa hiyo, Baba yetu wa mbinguni atatenda haraka ili kutuokoa. Wokovu huo utaonekana waziwazi wakati ulimwengu wa Shetani utaharibiwa kwenye Har-magedoni, ni kusema, ‘vita ya ile siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote.’—Ufu. 16:14, 16.

5 Unabii wa Biblia unasema hivi kuhusu Har-magedoni: ‘Bwana anaanzisha baraza ya mataifa, anawahukumu wanadamu wote; wabaya anawatoa wapigwe upanga. Bwana wa ulimwengu asema hivi: Angalieni, musiba umeenea toka taifa hata taifa, tufani kubwa inatoka mipakani pa dunia. Siku ile watu waliouawa na Bwana watalala toka mupaka wa dunia hata mupaka wake; hawataombolezwa, hawatakusanyiwa, wala hawatazikwa. Watalala juu ya udongo wawe mbolea.’ (Yer. 25:31-33 Verbum Bible) Har-magedoni itaharibu ulimwengu muovu wa Shetani. Ulimwengu wa Shetani utaangamizwa kabisa lakini sehemu ya duniani ya tengenezo la Yehova itaokoka.

SABABU GANI TENGENEZO LA YEHOVA LINAENDELEA KUSONGA MBELE?

6, 7. (a) Wale wanaofanyiza ‘umati mukubwa’ wanapatikana namna gani leo? (b) Kumekuwa na ongezeko gani katika miaka ya hivi karibuni?

6 Tengenezo la Mungu lingali mupaka leo na linaendelea kusonga mbele kwa sababu Mungu anakubali watu wanaofanyiza tengenezo hilo. Biblia inatuhakikishia hivi: “Macho ya Yehova yako juu ya waadilifu [ao wenye haki], na masikio yake yanaielekea dua yao.” (1 Pet. 3:12) Wenye haki hao wanatia ndani ‘umati [ao mukutano] mukubwa’ ambao ‘unatoka katika ile ziki kubwa.’ (Ufu. 7:9, 14) Wale watakaookolewa hawatakuwa “umati” tu, watakuwa ‘umati mukubwa,’ ni kusema, watu wengi sana. Wewe pia unajiwazia kuwa kati ya wale watakaokoka ‘ile ziki kubwa’?

7 Wale wanaofanyiza mukutano mukubwa wanapatikana namna gani? Wanaendelea kukusanywa pamoja kupitia kazi ya kuhubiri. Yesu alitabiri hivi: “Hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14) Hiyo ndiyo kazi ya lazima sana ambayo tengenezo la Mungu linafanya katika siku hizi za mwisho.  Kupitia kazi ya kuhubiri na kufundisha ambayo Mashahidi wa Yehova wanafanya katika dunia yote, mamilioni ya watu wamejifunza kumuabudu Mungu “kwa roho na kweli.” (Yoh. 4:23, 24) Kwa mufano, katika kipindi cha miaka kumi iliyopita hivi karibuni, ni kusema, miaka ya utumishi tangu 2003 mupaka 2012, watu zaidi ya 2707000 walibatizwa ili kuonyesha kwamba wamejitoa kwa Mungu. Leo, kuna Mashahidi wa Yehova zaidi ya 7900000 katika dunia yote, na mamilioni wanajiunga nao kila mwaka, zaidi sana siku ya Ukumbusho. Hatupashwe kujivuna kwa sababu ya hesabu hiyo kwa kuwa ni ‘Mungu anayekuza [ao anayekomalisha].’ (1 Kor. 3:5-7) Ni wazi kwamba mukutano mukubwa unaendelea kuongezeka sana kila mwaka.

8. Sababu gani kuna ongezeko kubwa katika tengenezo la Yehova katika siku zetu?

8 Mashahidi wa Yehova wanaendelea kuongezeka sana kwa sababu Yehova anawategemeza. (Soma Isaya 43:10-12.) Ongezeko hilo lilitabiriwa kupitia maneno haya ya unabii: ‘Mudogo atakuwa elfu, na munyonge atakuwa taifa lenye nguvu. Mimi mwenyewe, Yehova, nitaharakisha jambo hilo kwa wakati wake.’ (Isa. 60:22) Wakati fulani, mabaki ya watiwa-mafuta walikuwa wadogo, lakini hesabu yao iliongezeka kadiri Waisraeli wengine wa kiroho waliendelea kuingizwa katika tengenezo la Mungu. (Gal. 6:16) Kwa kuwa Yehova ameendelea kuwabariki, hesabu ya mukutano mukubwa inaendelea kuongezeka.

YEHOVA ANATUOMBA TUFANYE NINI?

9. Tunapashwa kufanya nini ili kupata baraka za wakati ujao ambazo Mungu ametuahidi katika Neno lake?

9 Iwe sisi ni Wakristo watiwa-mafuta ao wa mukutano mukubwa, tunaweza kupata baraka za wakati ujao wenye furaha ambazo Mungu ametuahidi katika Neno lake. Hata hivyo, ili kupata baraka hizo, tunapashwa kuishi kulingana na sheria za Yehova. (Isa. 48:17, 18) Fikiria Waisraeli waliokuwa wakiongozwa na Sheria ya Musa. Kusudi moja la sheria hiyo lilikuwa kuwalinda Waisraeli kwa kuwapatia maagizo mazuri kuhusu ngono, biashara, kuwatunza watoto, namna ya kuwatendea wanadamu wenzao, na mambo mengine. (Kut. 20:14; Law. 19:18, 35-37; Kum. 6:6-9) Kutii sheria za Mungu kunatuletea sisi pia faida katika mambo hayo. Kwa hiyo, hatuone kufanya mapenzi ya Mungu kuwa muzigo muzito. (Soma 1 Yohana 5:3.) Zaidi ya hilo, kama vile Sheria ilivyowalinda Waisraeli, sisi pia tukitii Sheria na kanuni za Yehova tutalindwa na tutakuwa “na afya katika imani.”—Tito 1:13.

10. Sababu gani ni vizuri kuwa na programu ya kujifunza Biblia na kufanya Ibada ya Familia ya mangaribi kila juma?

10 Sehemu ya duniani ya tengenezo la Yehova inaendelea kusonga mbele katika njia mbalimbali. Kwa mufano, tunaendelea kuelewa vizuri zaidi kweli ya Biblia. Hilo halipashwe kutushangaza kwa sababu ‘njia ya waadilifu ni kama nuru inayongaa, inayozidi kuongezeka mupaka muchana mukamilifu.’ (Met. 4:18) Lakini ni vizuri tujiulize hivi: ‘Je, ninajua mafasirio mapya kuhusu kweli ya Maandiko? Ninazoea kusoma Biblia kila siku? Ninasoma bila kukawia kila kichapo kipya? Mimi na familia yangu tunafanya Ibada ya Familia ya mangaribi ya kila juma?’ Wengi kati yetu wanaweza kukubali kwamba si vigumu sana kufanya mambo yote hayo. Siri ni kuwa tu na programu. Kwa kweli, ni jambo la lazima sana kujifunza kweli ya Biblia, kuitumia, na kufanya maendeleo ya kiroho, zaidi sana leo kwa sababu ziki kubwa inakaribia sana!

11. Namna gani sikukuu za zamani na mikutano na mikusanyiko yetu imewasaidia watumishi wa Mungu?

 11 Tengenezo la Yehova linatutia moyo tufuate shauri hili la mutume Paulo: ‘Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri munavyoona siku ile kuwa inakaribia.’ (Ebr. 10:24, 25) Sikukuu za kila mwaka na mikusanyiko mingine ya kumuabudu Yehova, iliwasaidia Waisraeli wawe na uhusiano muzuri pamoja na Mungu. Zaidi ya hilo, mikusanyiko hiyo kama vile Sikukuu ya pekee ya Vibanda iliyofanywa katika siku za Nehemia ilikuwa wakati wa kufurahi sana. (Kut. 23:15, 16; Neh. 8:9-18) Sisi pia tunapata furaha kama hiyo kwenye mikutano, na mikusanyiko yetu. Acheni tuhuzurie mikutano na mikusanyiko hiyo ili tuwe na hali nzuri ya kiroho na furaha.—Tito 2:2.

12. Namna gani tunapashwa kuona kazi ya kuhubiri?

12 Sisi ambao tumejiunga na tengenezo la Mungu, tunafurahia kufanya “kazi takatifu ya habari njema ya Mungu.” (Rom. 15:16) Tunapofanya ‘kazi hiyo takatifu’ tunakuwa “wafanyakazi” pamoja na Yehova, ambaye ni ‘Mutakatifu.’ (1 Kor. 3:9; 1 Pet. 1:15) Kuhubiri habari njema kunasaidia jina takatifu la Yehova litakaswe. Bila shaka, ni pendeleo kubwa sana kupewa “habari njema yenye utukufu ya Mungu mwenye furaha.”—1 Tim. 1:11.

13. Uhusiano wetu muzuri pamoja na Mungu na maisha yetu yanategemea nini?

13 Mungu anataka tuendelee kuwa na uhusiano muzuri pamoja naye kwa kushikamana naye na kutegemeza tengenezo lake katika njia mbalimbali. Musa aliwaambia Waisraeli hivi: ‘Nachukua mbingu na dunia kuwa mashahidi juu yenu leo, kwamba nimeweka uzima na kifo mbele yako, baraka na laana; nawe lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako, kwa kumupenda Yehova Mungu wako, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye; kwa maana yeye ni uhai wako na urefu wa siku zako, ili ukae katika inchi ambayo Yehova aliwaapia mababu zako Abrahamu, Isaka na Yakobo.’ (Kum. 30:19, 20) Kwa hiyo, maisha yetu yanategemea kufanya mapenzi ya Yehova, kumupenda, kumutii kwa kusikiliza sauti yake, na kushikamana naye.

14. Ndugu mumoja alisema nini kuhusu sehemu inayoonekana ya tengenezo la Mungu?

14 Siku moja, ndugu Pryce Hughes, ambaye aliazimia kushikamana na Mungu na tengenezo Lake, aliandika hivi: “Nafurahi sana kuona kwamba nimeishi kulingana na ujuzi wa makusudi ya Yehova tangu zile siku za mbele tu ya mwaka wa 1914 . . . Jambo ambalo limekuwa la maana sana kwangu ni kuendelea kuwa karibu na sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova. Mambo niliyojionea mwanzoni yalinifundisha kwamba si jambo la hekima kutegemea akili ya mwanadamu. Wakati tu akili yangu ilitambua hivyo, niliazimia kukaa karibu na tengenezo hili la kweli. Ikiwa mutu hategemee tengenezo hili, namna gani anaweza kukubaliwa na kubarikiwa na Yehova?”

ENDELEA KUSONGA MBELE PAMOJA NA TENGENEZO LA MUNGU

15. Toa mufano ulio katika Biblia unaoonyesha namna tunapashwa kutenda tunapotolewa mafasirio mapya kuhusu Maandiko fulani.

15 Ili Yehova atukubali na kutubariki, tunapashwa kutegemeza tengenezo lake na kukubali mafasirio mapya. Fikiria jambo hili: Kisha kifo cha Yesu, Wakristo wengi Wayahudi waliokuwa wanashika sana Sheria waliona kuwa ni vigumu kuachana nayo . (Mdo. 21:17-20) Hata hivyo, barua ya Paulo kwa Waebrania iliwasaidia watambue kwamba hawakutakaswa kupitia zabihu ‘zilizotolewa kulingana na Sheria,’ lakini walitakaswa “kupitia toleo la mwili wa Yesu Kristo mara moja kwa wakati wote.” (Ebr. 10:5-10) Bila shaka, wengi kati ya Wakristo hao Wayahudi walibadilisha mawazo yao na waliendelea kuwa na uhusiano muzuri pamoja na Mungu. Sisi pia tunapashwa kujifunza kwa bidii na kuwa tayari kukubali mafasirio mapya ya Neno la Mungu na maagizo mapya kuhusu kazi yetu ya kuhubiri.

16. (a) Ni baraka gani ambazo zitafanya maisha yawe mazuri katika dunia mupya? (b) Ni ahadi gani ambayo unangojea kwa hamu?

16 Yehova ataendelea kubariki wale wote wanaoendelea kuwa waaminifu kwake na kwa tengenezo lake. Watiwa-mafuta waaminifu watafurahia pendeleo lao la kutawala na Kristo huko mbinguni. (Rom. 8:16, 17) Sisi tulio na tumaini la kuishi duniani, tunaweza kuwazia maisha mazuri ambayo tutapata katika Paradiso. Sisi wote tulio katika tengenezo la Yehova, tunafurahia sana kuwahubiria wengine kuhusu dunia mupya ambayo Mungu ametuahidi! (2 Pet. 3:13) Andiko la Zaburi 37:11 linasema hivi: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” Watu “watajenga nyumba na kukaa ndani yake” na watafurahia “kazi ya mikono yao wenyewe.” (Isa. 65:21, 22) Hakutakuwa tena watu wa kuwatesa wengine, hakutakuwa umaskini, na njaa. (Zab. 72:13-16) Babiloni Mukubwa hatawadanganya tena watu kwa sababu hatakuwa tena. (Ufu. 18:8, 21) Wafu watafufuliwa na kupewa nafasi ya kuishi milele. (Isa. 25:8; Mdo 24:15) Hayo ni matumaini mazuri sana kwa wote ambao wamekwisha amua kumutumikia Yehova. Ili tuone utimizo wa ahadi hizo, tunapashwa kuendelea kufanya maendeleo ya kiroho na kusonga mbele pamoja na tengenezo la Mungu.

Unajiwazia ukiwa katika Paradiso(Ona fungu la 16)

17. Tunapashwa kuwa na maoni gani kuhusu ibada ya Yehova na tengenezo lake?

17 Kwa kuwa mwisho unakaribia sana, ni vizuri tuendelee kuwa na imani yenye nguvu na kupendezwa sana na mipango ambayo Yehova amefanya kwa ajili ya ibada. Mutunga-zaburi Daudi alikuwa na maoni kama hayo alipoimba hivi: ‘Nimemuomba Yehova jambo moja—ndilo nitakalolitafuta, kwamba nipate kukaa katika nyumba ya Yehova siku zote za maisha yangu, ili kuuona uzuri wa Yehova na kulitazama kwa usamini hekalu lake.’ (Zab. 27:4) Acheni kila mumoja wetu aendelee kushikamana na Mungu na watumishi wake, na kusonga mbele pamoja na tengenezo la Yehova.