Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 Masimulizi Kuhusu Maisha Ya Watu

Yehova Amenisaidia Kabisa

Yehova Amenisaidia Kabisa

Mimi na bibi yangu Evelyn, tulishuka kutoka katika treni huko Hornepayne, kijiji kilicho kaskazini mwa Ontario, huko Kanada. Ilikuwa asubuhi sana na kulikuwa baridi sana. Ndugu mumoja wa mahali hapo alitupeleka kwake, na kisha kula chakula kizuri cha asubui pamoja naye, bibi yake, na mutoto wake, tulipita katika barafu na kuhubiri nyumba kwa nyumba. Katika kipindi hicho cha kisha muchana, nilitoa hotuba yangu ya kwanza nikiwa mwangalizi wa muzunguko. Tulikuwa watu watano tu.

BILA shaka, watu hao wachache waliohuzuria hotuba yangu katika mwaka wa 1957 hawakuniogopesha. Kusema kweli, nimekuwa mutu mwenye haya sana siku zote. Nilipokuwa kijana mudogo, nilikuwa ninajificha wageni walipofika kwetu, hata kama nilikuwa ninawajua.

Bila shaka, unaweza kushangaa kujua kwamba migawo mingi ambayo nimepata katika tengenezo la Yehova imenilazimisha kukutana na watu wengi, marafiki na watu ambao sikujua. Lakini, niliendelea kuwa mutu mwenye haya na kufikiri kama sistahili, kwa hiyo, siwezi kujivuna kwa sababu ya matokeo yoyote mazuri ambayo nimepata katika migawo hiyo. Lakini, nimejionea ukweli wa ahadi hii ya Yehova: ‘Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mukono wangu wa kuume wa uadilifu.’ (Isa. 41:10) Njia moja kubwa ambayo Yehova ametumia ili kunisaidia ni kupitia Mashahidi wenzangu. Acheni niwaelezee kuhusu wamoja kati yao, kuanzia wale walionisaidia nilipokuwa mutoto.

BIBLIA NA BUKU NDOGO NYEUSI

Kwenye shamba la familia yetu huko kusini-mangaribi mwa Ontario

Asubuhi moja ya Siku ya Yenga yenye jua kali katika miaka ya 1940, dada Elsie Huntingford alifika nyumbani kwenye shamba la familia yetu kusini-mangaribi mwa Ontario. Mama yangu alifungua mulango; lakini  baba yangu aliyekuwa mwenye haya kama mimi, alibaki nami katika nyumba akisikiliza. Baba aliwaza kwamba Dada Huntingford alikuwa muchuruzi na kwamba Mama alitaka kununua kitu fulani ambacho hatukuhitaji, kwa hiyo, alienda kwenye mulango na kumuambia kwamba hatuna lazima ya kitu. Dada Huntingford alimuuliza baba yangu hivi: “Ni kusema, hamuna lazima ya kujifunza Biblia?” Baba yangu alimujibu hivi “Tuko na lazima ya kujifunza Biblia.

Dada Huntingford alitutembelea kwa wakati unaofaa. Wazazi wangu walikuwa wameshirikiana sana na kanisa linaloitwa Eglise unifiée du Canada, lakini walikuwa wameamua kuachana na kanisa hilo. Sababu gani? Kwa sababu mutumishi mumoja wa kanisa hilo aliandika majina ya wale waliotoa sadaka kulingana na kiasi ambacho walitoa na kuyabandika katika kanisa. Kwa kuwa wazazi wangu hawakuwa matajiri, majina yao yalichukua nafasi ya mwisho-mwisho, na wazee wa kanisa waliwachochea watoe feza nyingi. Mutumishi mwengine wa kanisa hilo alisema kwamba alikuwa akifundisha mambo ambao haamini kabisa ili tu asipoteze kazi yake. Kwa hiyo, tuliachana na kanisa hilo lakini tulikuwa tungali tunatafuta namna ya kumuabudu Mungu vizuri.

Kwa kuwa kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikatazwa katika Kanada, Dada Huntingford aliendelea kujifunza pamoja na familia yetu kwa kutumia Biblia na maandishi fulani yaliyokuwa katika buku lake ndogo nyeusi. Alipotambua baadaye kwamba familia yetu haingemuchongea kwa wakubwa, alianza kututolea vichapo vya Biblia. Kisha kujifunza, tulificha mbali vichapo hivyo. *

Wazazi wangu walikubali kweli kupitia mahubiri ya nyumba kwa nyumba na walibatizwa katika mwaka wa 1948

Ijapokuwa upinzani na vizuizi vingine, Dada Huntingford aliendelea kuhubiri habari njema kwa bidii. Bidii yake ilinishangaza na ilinichochea nikubali kweli. Mwaka mumoja kisha wazazi wangu kubatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova, mimi pia nilibatizwa. Ilikuwa tarehe 27/02/1949, katika chombo cha chuma ambamo wafugaji walitia maji ili wanyama wakunywe. Wakati huo nilikuwa na miaka 17. Kisha kubatizwa, nilipenda sana nianze utumishi wa wakati wote.

YEHOVA ALINISAIDIA NISIOGOPE

Nilishangaa sana nilipoalikwa kwenye Beteli katika mwaka wa1952

Kisha kubatizwa nilisita kuanza mara moja kazi ya upainia. Nilitumika kwenye benki na katika biro fulani kwa sababu nilikuwa ninafikiri kwamba ilikuwa lazima nipate feza  za kunisaidia katika kazi ya upainia. Lakini, kwa kuwa nilikuwa ningali kijana asiye na uzoefu, nilimaliza feza zangu kisha tu kuzipata. Kwa hiyo, ndugu mumoja anayeitwa Ted Sargent alinishauri nisiogope na nimutumainie Yehova. (1 Nya. 28:10) Kwa kuwa alinitia moyo, nilianza kazi ya upainia Mwezi wa 11, 1951. Nilikuwa na dola 40 tu, kinga iliyokuwa imekwisha kutumikishwa, na sakoshe mupya. Lakini siku zote Yehova alinisaidia nipate yale niliyohitaji. Ninafurahi sana kwa kuwa ndugu Ted alinitia moyo ili nianze kazi ya upainia! Kazi hiyo iliniletea baraka nyingi.

Siku moja mangaribi, mwishoni mwa Mwezi wa 8, 1952, mutu fulani wa Toronto aliniita. Ni biro ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Kanada ndiyo iliniita niende kutumika kwenye Beteli Mwezi wa 9. Ijapokuwa nilikuwa mwenye haya na nilikuwa sijatembelea Beteli hapo mbele, nilifurahi sana kwa kuwa mapainia wengine walikuwa wamenielezea mambo mazuri kuhusu Beteli. Mara moja nilizoea maisha ya Beteli.

“ONYESHA NDUGU KAMA UNAWAHANGAIKIA”

Kisha miaka mbili kufika kwenye Beteli, nilichukua nafasi ya ndugu Bill Yacos ambaye alikuwa mutumishi wa kutaniko (anayeitwa leo muratibu wa baraza la wazee) la Shaw Unit huko Toronto. * Nilikua na miaka 23 tu na nilijiona kuwa kijana wa mashambani wa bure-bure. Lakini Ndugu Yacos alinionyesha kwa unyenyekevu na upole mambo ya kufanya. Na Yehova alinisaidia kabisa.

Ndugu Yacos aliyekuwa munene na mwenye kupenda kucheka, aliwapenda sana watu. Alipenda ndugu, nao pia walimupenda. Alizoea kuwatembelea nyumbani kwao, na hakufanya hivyo tu wakati walikuwa na magumu. Bill Yacos alinitia moyo nifanye hivyo pia na nihubiri pamoja na ndugu na dada. Aliniambia hivi: “Ken, onyesha ndugu kama unawahangaikia. Hilo litakusaidia usikazie tu uzaifu wao mbalimbali.”

BIBI MWAMINIFU

Yehova amenisaidia kwa njia ya pekee kuanzia Mwezi wa 1, 1957. Katika mwezi huo nilioa Evelyn, aliyesoma darasa la 14 la Masomo ya Gileadi. Mbele tuoane, Evelyn alikuwa ametumikia katika jimbo la Quebec, ambamo luga ya Kifaransa inazungumuziwa. Katika siku hizo jimbo hilo la Quebec lilikuwa linatawaliwa na Kanisa Katoliki la Roma. Kwa hiyo, Evelyn alikuwa na mugawo mugumu, lakini alishikamana na mugawo wake na Yehova pia.

Evelyn na mimi tulioana katika mwaka wa 1957

Evelyn alishikamana na mimi. (Efe. 5:31) Lakini, uaminifu wake ulijaribiwa kisha tu ndoa yetu! Tulikuwa tumepanga kuenda Florida, Amerika, lakini siku moja tu kisha ndoa yetu, biro ya tawi iliniomba niende kuhuzuria mukutano wa juma moja kwenye Beteli ya Kanada. Bila shaka, mukutano huo ulivuruga mipango yetu, lakini mimi na Evelyn tulitaka kufanya jambo lolote ambalo Yehova anatuomba. Kwa hiyo, tulikatiza safari yetu ya kisha ndoa. Katika juma hilo, Evelyn alihubiri katika eneo lililo karibu na tawi. Hata kama eneo hilo lilikuwa tofauti sana na Quebec, hakuvunjika moyo.

Mwishoni mwa juma hilo, nilishangaa kupokea mugawo wa kuwa mwangalizi wa muzunguko kaskazini mwa Ontario. Nilikuwa ningali mupya katika maisha ya ndoa, nikiwa na miaka  25 tu na sikuwa na uzoefu mwingi, lakini tulimutumainia Yehova na kufunga safari. Katika kipindi cha baridi kali huko Kanada, tulichukua treni ya usiku pamoja waangalizi wengi wenye kusafiri ambao walikuwa na uzoefu waliokuwa wakirudia katika migawo yao. Walitutia moyo sana! Ndugu mumoja hata alitubembeleza tulale mahali ambapo angelala katika treni hiyo ili tusipitishe usiku wote tukiwa wenye kukaa. Asubuhi iliyofuata, siku 15 tu kisha ndoa yetu, tulienda kutembelea kikundi kidogo huko Hornepayne, kama nilivyoeleza mwanzoni mwa habari hii.

Mimi na Evelyn tulilazimika kufanya mabadiliko mengine. Tulipokuwa katika kazi ya wilaya mwishoni mwa mwaka wa 1960, nilialikwa kusoma darasa la 36 la Masomo ya Gileadi, ambayo ingefanya miezi kumi kuanzia Mwezi wa 2, 1961 huko Brooklyn, New York. Bila shaka, nilifurahi, lakini furaha hiyo ilipunguka kidogo kwa kuwa Evelyn hakualikwa. Lakini, kama vile bibi wengine ambao bwana zao walialikwa kwenye masomo hayo, Evelyn aliombwa aandike barua inayoonyesha kwamba alikubali kuishi mbali na mimi kwa muda wa miezi kumi hivi. Evelyn alilia, lakini tulikubali niende kwenye masomo hiyo, na alifurahi kwa sababu ningepata mazoezi mazuri kwenye Masomo ya Gileadi.

Wakati huo, Evelyn alitumikia kwenye Beteli ya Kanada. Alipata pendeleo kubwa la kuishi katika chumba kimoja na dada mumoja mutiwa-mafuta, aliyeitwa Margaret Lovell. Bila shaka, mimi na Evelyn tulitamani sana kuonana tena. Kwa musaada wa Yehova, kila mumoja wetu alibakia kwa muda fulani katika mugawo wake. Nia yake ya kukubali tutumie wakati ambao tungepitisha pamoja ili tushugulikie migawo mbalimbali katika tengenezo la Yehova ilinigusa moyo sana.

Kisha kufanya miezi mitatu hivi kwenye Masomo ya Gileadi, Ndugu Nathan Knorr, aliyekuwa akisimamia kazi ya ulimwenguni pote, alinipatia mualiko mumoja wa pekee. Aliniuliza ikiwa ninaweza furahia kuacha Masomo ya Gileadi ili niende kufundisha kwa muda Masomo ya Huduma ya Ufalme kwenye Beteli ya Kanada. Ndugu Knorr aliniambia kwamba silazimishwe kukubali mualiko huo. Ikiwa nilitaka ningeendelea na Masomo ya Gileadi na pengine ningetumwa baadaye kuwa misionere mahali fulani. Tena aliniambia kwamba nikiamua kurudia Kanada pengine singealikwa tena hata kidogo kwenye Masomo ya Gileadi na baadaye, ningerudi tena katika shamba huko Kanada. Aliniachia wakati wa kuamua kisha kuongea na bibi yangu kuhusu jambo hilo.

Kwa kuwa nilijua mawazo ya bibi yangu Evelyn kuhusu migawo ya kiteokrasi, nilimuambia mara moja Ndugu Knorr hivi: “Jambo lolote ambalo tengenezo la Yehova litatuomba kufanya, tutafurahia kulifanya.” Siku zote tumefikiri kwamba tunapashwa kuenda kila mahali ambapo tengenezo la Yehova litatutuma hata ikiwa si mapendezi yetu.

Kwa hiyo, katika Mwezi wa 4, 1961, nilitoka Brooklyn na kurudia Kanada ili kufundisha  Masomo ya Huduma ya Ufalme. Baadaye, tulianza kutumikia kwenye Beteli ya Kanada. Kisha, nilishangaa kupokea mualiko ili kusoma darasa la 40 la Masomo ya Gileadi, ambalo lingeanza katika mwaka wa 1965. Tena, Evelyn alipashwa kuandika barua inayoonyesha kwamba alikubali tuachane kwa muda. Lakini, kisha majuma machache, tulifurahi sana wakati Evelyn alipata pia mualiko ili kusoma pamoja na mimi.

Kisha kufika kwenye Masomo ya Gileadi, Ndugu Knorr alituambia kwamba wanafunzi wote walioandikwa katika madarasa ya Kifaransa, kama sisi, wangetumwa huko Afrika. Lakini, jambo la kushangaza tulitumwa huko Kanada kisha masomo! Niliwekwa kuwa musimamizi mupya wa tawi (anayeitwa sasa Muratibu wa Halmashauri ya Tawi). Wakati huo nilikuwa na miaka 34 tu na nilimuambia Ndugu Knorr kwamba ningali kijana sana. Lakini aliniambia nisiogope. Mara moja nilianza kuuliza ndugu wenye kukomaa na wenye uzoefu mwingi kwenye Beteli mbele ya kuchukua maamuzi mazito.

KWENYE BETELI NILIJIFUNZA NA KUFUNDISHA

Kutumikia kwenye Beteli kumenitolea nafasi nzuri ya kujifunza kutokana na wengine. Ninaheshimia sana na kupendezwa na washiriki wengine wa Halmashauri ya Tawi. Nimetiwa moyo pia na ndugu na dada wengi wazuri, vijana na wazee ambao tumetumika nao hapa kwenye Beteli na katika makutaniko mbalimbali ambamo tumetumikia.

Ninaongoza ibada ya asubuhi katika familia ya Beteli ya Kanada

Kutumikia kwenye Beteli kumenitolea pia nafasi ya kuwafundisha wengine na kutia nguvu imani yao. Mutume Paulo alimuambia Timotheo hivi: “Endelea katika mambo uliyojifunza.” Pia aliongezea hivi: ‘Na mambo uliyoyasikia kutoka kwangu kwa usibitisho [ao ushuhuda] wa mashahidi wengi, mambo hayo uwakabizi watu waaminifu, ambao nao watakuwa na sifa za kustahili vya kutosha kufundisha wengine.’ (2 Tim. 2:2; 3:14) Wakati fulani ndugu na dada zangu wananiuliza ikiwa nimejifunza nini katika miaka 57 ambayo nimepitisha kwenye Beteli. Ninawajibia tu kwamba ni jambo la maana kuwa tayari kufanya jambo lolote ambalo tengenezo la Yehova linatuomba na kutegemea musaada wake.

Nilipofika kwenye Beteli, nilikuwa kijana asiye na uzoefu na mwenye haya, sasa kumepita miaka mingi, lakini ni kama jana tu. Hata hivyo, miaka hiyo yote Yehova amekuwa ‘akiushika mukono wangu wa kuume.’ Zaidi sana kupitia wema na musaada ambao ndugu na dada wananitolea kwa wakati unaofaa, Yehova anaendelea kunihakikishia hivi: “Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.”—Isa. 41:13.

^ fu. 10 Tarehe 22/05/1945, serikali ya Kanada ilituruhusu tuendelee na kazi yetu ya kuhubiri.

^ fu. 16 Wakati huo, ikiwa kulikuwa makutaniko zaidi ya moja katika muji fulani, kila kutaniko liliitwa kikundi.