Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Fanya Njia ya Miguu Yako Iwe ‘Laini’ ili Ufanye Maendeleo

Fanya Njia ya Miguu Yako Iwe ‘Laini’ ili Ufanye Maendeleo

WAKATI watu wa Mungu walitoka huko Babiloni katika mwaka wa 537 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, Yehova alifikiria barabara yao ya kuenda Yerusalemu. Aliwaambia hivi: “Fungueni njia ya watu. Fanyeni matuta, fanyeni matuta kwa ajili ya njia kuu. Ondoeni mawe juu yake.” (Isa. 62:10) Wazia namna Wayahudi fulani walipaswa kufanya kazi hiyo. Wayahudi fulani walioenda mbele walipaswa kujenga barabara, pengine kufunika mashimo na kulainisha njia na nafasi zisizokuwa nzuri. Kufanya hivyo kungesaidia ndugu zao waliowafuata wapite katika barabara nzuri ili kurudia katika inchi yao.

Tunaweza kutumia habari hiyo kuwa mufano wa njia inayoongoza kwenye miradi ya kiroho. Yehova anataka watumishi wake wote watembee katika njia hiyo bila kitu chochote cha kuwazuia. Neno lake linatushauri hivi: ‘Lainisha mapito ya muguu wako, nazo njia zako zote na zifanywe imara.’ (Met. 4:26) Iwe sisi ni vijana ao hapana tutaona kwamba ni jambo la hekima kufuata shauri hilo nzuri kutoka kwa Mungu.

TAYARISHA NJIA KWA KUCHUKUA MAAMUZI MUZURI

Pengine umesikia watu fulani wakisema hivi kuhusu vijana: ‘Una nafasi nyingi za kufanikiwa katika maisha yako.’ Kwa kawaida vijana wana afya nzuri, akili mwepesi na wanatamani sana kufanikiwa katika maisha. Ndiyo sababu Biblia inasema hivi: “Uzuri wa vijana ni nguvu zao.” (Met. 20:29) Kijana anayetumia uwezo ao nguvu zake ili kumutumikia Yehova anaweza kufikia miradi ya kiroho na kupata furaha ya kweli.

Hata hivyo, kama vile unajua, uwezo wa vijana wetu unatamaniwa sana katika dunia hii. Wakati kijana Shahidi anatumika vizuri kwenye masomo, mushauri wa masomo, mwalimu ao mwanafunzi mwenzake anaweza kumuchochea asome masomo ya juu ili kupata maisha mazuri katika ulimwengu huu muovu. Ao ndugu ao dada kijana aliye na  uwezo katika michezo mbalimbali kama vile kukimbia, anaweza kutambua kwamba watu fulani wanamuchochea ili ajiandikishe katika kikundi cha wachezaji. Je, umejikuta katika hali hiyo ao unamujua kijana fulani anayepambana na hali kama hiyo? Ni nini inaweza kumusaidia kijana Mukristo achukue maamuzi mazuri?

Mafundisho ya Biblia yanaweza kumusaidia kijana ajitayarishe ili atembee katika barabara nzuri sana katika maisha. Andiko la Mhubiri 12:1 linasema hivi: ‘Mukumbuke, sasa, Muumba wako Mukubwa katika siku za ujana wako.’ Namna gani wewe ao rafiki yako munaweza kabisa ‘kumukumbuka Muumba wenu Mukubwa’?

Fikiria jambo lililomupata Eric * wa Afrika-Mangaribi. Alipenda sana kucheza kabumbu. Alipokuwa na miaka 15, Eric alichaguliwa ili kucheza katika timu ao ekipe ya taifa. Pengine alipenda kupata nafasi nzuri ya kuenda kupata mazoezi mazuri sana ya kucheza huko Ulaya ili awe muchezaji mwenye kujulikana sana. Lakini namna gani shauri la ‘kumukumbuka Muumba wake Mukubwa’ lilimusaidia? Habari hiyo inaweza kuwafundisha somo gani wewe na marafiki zako?

Eric alikuwa angali anasoma wakati alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Kupitia funzo la Biblia, Eric alivumbua kwamba Muumbaji wake atamaliza kabisa matatizo yote ya wanadamu. Eric alianza kutambua kwamba ni jambo la maana atumie wakati na nguvu zake ili kufanya mapenzi ya Mungu. Kwa hiyo, aliona kwamba ni vizuri kufanya mapenzi ya Mungu, kuliko kufuatia tu michezo katika maisha yake. Kisha, akabatizwa na kufanya maendeleo ya kiroho. Alifikia kuwa mutumishi wa huduma na kisha alialikwa kwenye Masomo ya Biblia kwa Ajili ya Ndugu Wasio na Bibi.

Ikiwa Eric angefutilia michezo ya kabumbu, pengine angepata utajiri na angejulikana sana. Lakini alielewa ukweli wa kanuni hii ya Biblia: ‘Vitu vyenye samani vya tajiri ni muji wake wenye nguvu, navyo ni kama ukuta wa ulinzi katika mawazo yake.’ (Met. 18:11) Bila shaka, usalama ambao mutu anaweza kupata kupitia utajiri si usalama wa kweli kabisa. Zaidi ya hilo, wale wanaofuatilia utajiri kwa pupa mara nyingi ‘wanajichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.’—1 Tim. 6:9, 10.

Inapendeza kuona kwamba vijana wengi wamepata furaha na usalama wenye kuendelea kwa kufanya kazi ya utumishi wa wakati wote. Eric anasema hivi: “Nimejiunga na ‘timu’ kubwa ya watumishi wa wakati wote. Hiyo ndiyo timu nzuri sana ambayo nimejiunga nayo, na ninamushukuru Yehova kwa kunionyesha njia moja tu ya kupata furaha ya kweli na kufanikiwa katika maisha.”

Namna gani wewe? Kuliko kufutilia miradi katika ulimwengu huu, sababu gani usifanye imara “njia zako” mbele za Yehova kwa kufanya kazi ya upainia?—Soma kisanduku “ Nimepata Faida Ambazo Singepata Kwenye Masomo ya Juu.”

ONDOA VIZUIZI KATIKA NJIA YAKO

Walipotembelea biro ya tawi ya Amerika, ndugu mumoja na bibi yake waliona furaha ya Wanabeteli wanaomutumikia Yehova kwenye tawi hiyo. Baadaye bibi yake aliandika hivi: “Tulikuwa tumefurahia sana programu yetu.” Ndugu huyo na bibi yake waliamua kutumia wakati na nguvu zao ili kufanya mengi katika utumishi wa Yehova.

Mwanzoni, ilionekana kuwa vigumu kwa ndugu huyo na bibi yake kufanya mabadiliko. Lakini siku moja, walifikiria Andiko fulani la siku hiyo. Andiko hilo lilikuwa Yohana 8:31, ambalo lina maneno haya ya Yesu: ‘Mukikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu.’ Wakiwa na mawazo ya andiko hilo katika akili yao, walifikiri hivi: “Jambo lolote tutakalofanya ili kurahisisha maisha yetu ni zabihu ya maana.” Waliuzisha nyumba yao kubwa, na vitu vingine ambavyo waliona kuwa si vya lazima, kisha walihamia katika kutaniko lililohitaji kusaidiwa. Leo, wao ni mapainia, lakini pia wanasaidia katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme na ni wajitoleaji kwenye mikusanyiko ya wilaya. Wanajisikia namna gani? Wanasema hivi: “Tunashangazwa na furaha ambayo tumepata kwa kuishi maisha rahisi, na kufanya tu yale ambayo tengenezo la Yehova linatutia moyo tufanye.”

BAKI KWENYE BARABARA HIYO

Mufalme Sulemani aliandika hivi: ‘Macho yako yatazame mbele moja kwa moja, ndiyo, macho yako yenye kungaa yanapaswa kutazama mbele yako moja kwa moja.’ (Met. 4:25) Kama vile shofere anavyokazia macho kwenye barabara, tunapaswa kuepuka jambo linaloweza kutukengeusha na kutuzuia tusifuatilie miradi ya kiroho na kuifikia.

Ni miradi gani ya kiroho unayoweza kujiwekea na kufikia? Kuanza utumishi wa wakati wote ni muradi muzuri  sana. Unaweza pia kutumikia katika kutaniko la karibu lililo na lazima ya wahubiri wenye ufundi ili kuhubiri eneo lao kubwa. Ao kutaniko fulani linaweza kuwa na wahubiri wenye ufundi lakini halina wazee na watumishi wa huduma wa kutosha. Je, unaweza kutumia njia moja kati ya hizo ili kusaidia? Sababu gani usizungumuze na mwangalizi wa muzunguko ili aone ikiwa unaweza kusaidia? Ikiwa unafurahia kutumikia katika maeneo ya mbali, unaweza kuomba mafasirio kuhusu makutaniko ya mbali yanayohitaji kusaidiwa. *

Tufikirie tena habari inayopatikana kwenye Isaya 62:10. Wayahudi fulani walipaswa kutumika sana ili kulainisha na kusafisha barabara iliyoelekea kwenye inchi yao ili watu wa Mungu wafike katika inchi yao. Ikiwa unajikaza ili ufikie miradi katika utumishi mutakatifu, usichoke. Mungu anaweza kukusaidia ufikie miradi hiyo. Endelea kumuomba Yehova hekima unapojaribu kuondoa vizuizi vyovyote mbele yako. Bila shaka, utaona namna Mungu anaweza kukusaidia ‘Kulainisha mapito ya muguu wako.’—Met. 4:26.

^ fu. 8 Jina limebadilishwa.

^ fu. 18 Soma kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova, ukurasa wa 111-112.