Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Daraka la Wanawake Katika Mupango wa Yehova

Daraka la Wanawake Katika Mupango wa Yehova

“Wanawake wanaotangaza habari njema ni jeshi kubwa.”ZAB. 68:11.

1, 2. (a) Mungu alimupatia Adamu zawadi gani? (b) Sababu gani Mungu alimupatia Adamu mwanamuke? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

YEHOVA alikuwa na kusudi fulani alipoumba dunia. “Aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isa. 45:18) Mungu aliumba mwanadamu wa kwanza, Adamu, akiwa mukamilifu na alimupatia makao mazuri, ni kusema, bustani ya Edeni. Adamu alifurahia sana miti mikubwa-mikubwa, mito midogo-midogo iliyokuwa inateremuka, na wanyama waliokuwa wanaruka-ruka! Lakini alikosa jambo fulani la lazima sana. Yehova alionyesha jambo hilo wakati alisema hivi: ‘Si vema huyo mwanaume aendelee kuwa peke yake. Nitamufanyia musaidizi, awe kikamilisho chake.’ Kisha Mungu akamufanya Adamu alale usingizi muzito, akachukua mufupa mumoja wa ubavu wa Adamu, na ‘akaufanya kuwa mwanamuke.’ Wakati Adamu aliamuka, alifurahi sana! Alisema hivi: ‘Mwishowe huyu ni mufupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu. Huyu ataitwa Mwanamuke, kwa sababu huyu alitolewa katika mwanaume.’—Mwa. 2:18-23.

2 Mwanamuke ni zawadi ya pekee ambayo Mungu alimupatia mwanaume, kwa sababu yeye ni musaidizi anayefaa kabisa kwa mwanaume. Angekuwa pia na pendeleo la pekee la kuzaa watoto. Kwa hiyo, ‘Adamu alimuita muke wake Hawa [ao Eva], kwa sababu ndiye angekuja kuwa mama ya kila mutu anayeishi.’ (Mwa. 3:20) Mungu aliwatolea Adamu na Eva zawadi ya pekee kabisa! Walikuwa na uwezo wa kuzaa wanadamu wengine wakamilifu. Kwa njia hiyo, dunia ingekuwa  paradiso iliyojaa watu wakamilifu ambao wangetawala viumbe vingine.—Mwa. 1:27, 28.

3. (a) Adamu na Eva walipaswa kufanya nini ili Mungu awabariki, lakini ni nini ilitokea? (b) Tutazungumuzia maulizo gani?

3 Ili Yehova awabariki, Adamu na Eva walipaswa kumutii na kukubali utawala wake. (Mwa. 2:15-17) Ni kwa kufanya hivyo tu ndipo wangetimiza daraka ambalo Mungu aliwapatia. Hata hivyo, inahuzunisha kwamba walishawishiwa na Shetani, “yule nyoka wa zamani,” na walimukosea Mungu. (Ufu. 12:9; Mwa. 3:1-6) Uasi huo umekuwa na matokeo gani juu ya wanawake? Wanawake wa zamani waliomutumikia Mungu walitimiza nini? Sababu gani wanawake Wakristo leo wanaitwa “jeshi kubwa”?—Zab. 68:11.

MATOKEO YA UASI

4. Kati ya Adamu na Eva, ni nani alilaumiwa kwa sababu ya zambi ambayo walifanya?

4 Alipoulizwa sababu gani aliasi, Adamu alijaribu kujitetea kwa kusema hivi: ‘Mwanamuke uliyenipa awe pamoja nami, alinipa tunda kutoka katika ule muti nami nikakula.’ (Mwa. 3:12) Adamu hakukubali makosa yake, lakini alijaribu kuyatia juu ya mwanamuke ambaye Mungu alimupatia, na juu ya Mungu ambaye ni Mutoaji mwenye upendo! Adamu na Eva walifanya zambi, lakini ni Adamu ndiye alilaumiwa kwa sababu ya zambi hiyo. Ndiyo sababu, mutume Paulo aliandika kwamba ‘kupitia mutu mumoja [Adamu] zambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia zambi.’—Rom. 5:12.

5. Utawala wa wanadamu umeonyesha nini?

5 Adamu na Eva walishawishiwa kufikiri kwamba hawakuhitaji Utawala wa Yehova. Hilo lilitokeza ulizo hili: Ni nani aliye na haki ya kutawala? Ili kujibu ulizo hilo mara moja kwa yote, Mungu aliruhusu wanadamu wajitawale kwa muda fulani. Alijua kwamba wanadamu wangejionea wenyewe kama hawawezi kujitawala. Kwa miaka mingi, utawala wa wanadamu umeleta matatizo mengi sana. Katika miaka 100 hivi iliyopita, karibu watu milioni mia moja wamekufa katika vita; na kati ya watu hao kuna wanaume, wanawake, na watoto wasio na kosa. Kwa hiyo, imeonekana wazi kwamba “mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yer. 10:23) kwa hiyo, tunatambua kwamba Yehova ndiye ana haki ya kuwa Mutawala wetu.—Soma Methali 3:5, 6.

6. Wanawake wanatendewa namna gani katika maeneo mengi?

6 Wanadamu wote, iwe wanaume ao wanawake wanatendewa vibaya katika ulimwengu huu unaotawaliwa na Shetani. (Mhu. 8:9; 1 Yoh. 5:19) Kuwatendea wanawake vibaya ni moja ya mambo ya kinyama ambayo watu wanafanya. Duniani pote, karibu wanawake 30 kati ya wanawake 100, wanatendewa vibaya na wanaume. Watoto wanaume wanapendelewa kuliko watoto wanawake kwa sababu watu wanasema kwamba watoto wanaume wanapokomaa wataendeleza jamaa na kuchunga wazazi wao na wazazi wa wazazi wao. Katika maeneo fulani, watu hawapendi kuzaa watoto wanawake; watu wanatosha mimba nyingi za watoto wanawake kuliko mimba za watoto wanaume.

7. Mwanzoni, Mungu alikuwa na kusudi gani juu ya wanaume na wanawake?

7 Mungu hafurahi hata kidogo anapoona wanawake wanatendewa vibaya. Yeye anatendea wanawake kwa haki na anawaheshimu. Yehova anawahangaikia wanawake; hilo linaonekana wazi kwa kuwa alimuumba Eva akiwa mukamilifu na kwa namna ambayo hangekuwa mutumwa lakini angekuwa musaidizi wa Adamu. Hiyo ni moja ya sababu zilizofanya kwamba, mwishoni mwa siku ya sita ya uumbaji, Mungu ‘aliona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.’ (Mwa. 1:31) Ndiyo,   “kila kitu” ambacho Yehova alifanya kilikuwa “chema sana.” Tangu mwanzo, Mungu alitaka wanaume na wanawake wakuwe na maisha mazuri!

WANAWAKE WALIOKUBALIWA NA MUNGU

8. (a) Wanadamu wana mwenendo wa namna gani leo? (b) Tangu zamani, Mungu amekubali watu wa namna gani?

8 Kisha uasi katika Edeni, wanaume na wanawake wamekuwa na mwenendo mubaya; na katika miaka 100 iliyopita, mwenendo wao umeharibika sana kuliko wakati mwingine wowote. Biblia ilitabiri kwamba katika “siku za mwisho” mwenendo wa watu ungeendelea kuharibika. Matendo mabaya ya wanadamu yameenea sana, na hilo linafanya siku hizi kuwa “nyakati za hatari.” (2 Tim. 3:1-5) Lakini tangu zamani, “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova” amekubali wanaume na wanawake ambao wamemutumainia, wametii sheria zake, na wamejitiisha kwake na kumukubali kuwa Mutawala wao.—Soma Zaburi 71:5.

9. Ni watu ngapi waliokoka Garika, na sababu gani?

9 Wakati Mungu aliharibu ulimwengu muovu wa zamani kupitia Garika ya wakati wa Noa, ni watu wachache sana ndio waliokoka. Ikiwa ndugu na dada za Noa waliishi wakati huo, wao pia walikufa katika Garika. (Mwa. 5:30) Hesabu ya wanawake waliookoka garika ni sawa na hesabu ya wanaume waliookoka. Noa, bibi yake, watoto wake watatu, na bibi za watoto wake, ndio waliokoka. Waliokolewa kwa sababu walimuogopa Mungu na walifanya mapenzi yake. Watu wote wanaoishi leo wanatokana na watu hao munane ambao walikubaliwa na Yehova.—Mwa. 7:7; 1 Pet. 3:20.

10. Sababu gani Sara na Rebeka walikubaliwa na Yehova?

10 Kisha miaka mingi, wanawake waliomuogopa Mungu ambao waliolewa na watumishi wa Yehova, walikubaliwa pia na Mungu. Haingekuwa hivyo ikiwa wanawake hao walikuwa wananungunika juu ya hali yao. (Yuda 16) Hatuwezi hata kidogo kufikiri kwamba Sara, muke wa Abrahamu, alianza kunungunika wakati waliondoka katika muji muzuri wa Uru na kuishi ndani ya mahema katika inchi ya kigeni. Lakini, ‘Sara alimutii Abrahamu, akimuita bwana.’ (1 Pet. 3:6) Fikiria pia Rebeka, mwanamuke mwenye sifa nzuri, ambaye Yehova alipatia Isaka. Haishangaze kwamba Isaka ‘alimupenda, na . . . alipata faraja baada ya kumupoteza mama yake.’ (Mwa. 24:67) Sisi pia tunafurahi sana tunapoona kati yetu wanawake ambao kama Sara na Rebeka, wanamuogopa Mungu!

11. Namna gani wanawake wawili Waebrania walionyesha kwamba wanamuogopa Mungu?

11 Wakati walikuwa katika utumwa huko Misri, Waisraeli waliongezeka sana; kwa hiyo, Farao aliamuru watoto wote wanaume Waebrania wauawe wanapozaliwa. Lakini, tufikirie Shifra na Pua, wanawake Waebrania, ambao inaonekana walisimamia kazi ya kuzalisha. Walikataa kabisa kuua watoto hao, kwa sababu walimuogopa Yehova. Kwa hiyo, Yehova aliwabariki kwa kuwapa familia.—Kut. 1:15-21.

12. Debora na Yaeli walifanya mambo gani ya maana sana?

12 Wakati wa waamuzi katika Israeli, nabii Debora alikuwa mwanamuke aliyekubaliwa na Mungu. Alimutia moyo Muamuzi Baraka na alisaidia Waisraeli wakombolewe kutokana na maadui wao, lakini alitabiri kwamba haiko Baraka ndiye angepata ushindi juu ya Wakanaani. Lakini, Mungu angemutoa Sisera, mukubwa wa jeshi la Wakanaani, ‘katika mukono wa mwanamuke.’ Jambo hilo lilitendeka wakati Yaeli   mwanamuke asiye Muisraeli, alimuua Sisera.—Amu. 4:4-9, 17-22.

13. Biblia inasema nini juu ya Abigaili?

13 Abigaili alikuwa pia mwanamuke mwenye sifa nzuri ambaye aliishi kati ya mwaka wa 1001 na 1100 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. Alikuwa na hekima, lakini Nabali, bwana yake, alikuwa mukali, mwenye matendo mabaya, na asiye na akili. (1 Sam. 25:2, 3, 25) Wakati fulani Daudi na watu wake walichunga mifugo ya Nabali; lakini wakati walimuomba chakula, ‘aliwakemea kwa sauti kali’ na hakuwapatia kitu chochote. Daudi alikasirika sana na alipanga kumuua Nabali na watu wake. Aliposikia jambo hilo, Abigaili aliwabebea Daudi na watu wake chakula na vinywaji, na hivyo akazuia mauaji. (1 Sam. 25:8-18) Kisha Daudi akamuambia Abigaili hivi: “Abarikiwe Yehova Mungu wa Israeli, aliyekutuma leo unipokee!” (1 Sam. 25:32) Nabali alipokufa, Daudi alimuoa Abigaili.—1 Sam. 25:37-42.

14. Binti za Shalumu waliunga mukono kazi gani, na namna gani wanawake Wakristo wanafanya hivyo leo?

14 Wanaume, wanawake, na watoto wengi walikufa wakati jeshi la Wababiloni liliharibu Yerusalemu na hekalu katika mwaka wa 607 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. Kazi ya kujenga tena ukuta wa Yerusalemu ilianza katika mwaka wa 455 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, na ilisimamiwa na Nehemia. Kati ya wale waliosaidia kujenga, kulikuwa binti za Shalumu, mukubwa wa wilaya ya Yerusalemu. (Neh. 3:12) Walikuwa tayari kufanya kazi ya hali ya chini. Tunapendezwa sana na wanawake wengi Wakristo ambao wanategemeza kwa furaha kazi za ujenzi zinazofanywa na tengenezo la Yehova!

WANAWAKE WALIOMUOGOPA MUNGU WAKATI WA MITUME

15. Mungu alimupatia Maria pendeleo gani?

15 Wakati wa mitume, na mbele kidogo ya wakati huo, Yehova alibariki wanawake wengi kwa kuwapatia mapendeleo ya pekee. Kati yao kulikuwa bikira aliyeitwa Maria. Alipokuwa anachumbiwa na Yosefu, alipata mimba kwa njia ya muujiza kupitia roho takatifu. Sababu gani Mungu alimuchagua ili akuwe mama wa Yesu? Bila shaka ni kwa sababu alikuwa na sifa za kiroho ambazo zingemusaidia kumukomalisha mutoto wake mukamilifu. Maria alipata pendeleo kubwa kabisa la kuwa mama wa mutu mukubwa zaidi aliyeishi duniani.—Mt. 1:18-25.

16. Toa mufano unaoonyesha namna Yesu aliwatendea wanawake.

16 Yesu aliwatendea wanawake vizuri sana. Kwa mufano, fikiria mwanamuke fulani aliyekuwa anatokwa damu kwa miaka 12. Alikuja nyuma ya Yesu katika kikundi kikubwa cha watu na kugusa nguo yake. Yesu hakumukemea, lakini alimuambia kwa upole hivi: “Binti yangu, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani, na uwe na afya njema kutokana na ugonjwa wako wenye kuhuzunisha.”—Mk. 5:25-34.

17. Ni muujiza gani uliofanyika kwenye Pentekoste ya mwaka wa 33?

17 Wanawake fulani ambao walikuwa wanafunzi wa Yesu walimutumikia, na pia walitumikia mitume wake. (Lu. 8:1-3) Na kwenye Pentekoste ya mwaka wa 33, karibu wanaume na wanawake 120 walipokea roho takatifu ya Mungu kwa njia ya pekee. (Soma Matendo 2:1-4.) Kutolewa kwa roho takatifu kulikuwa kumetabiriwa katika maneno haya: ‘[Mimi Yehova] nitaimimina roho yangu juu ya kila namna ya mwili, na wana wenu na binti zenu watatoa unabii . . . Na hata juu ya watumishi wa kiume na juu ya wajakazi nitaimimina roho yangu.’ (Yoe. 2:28, 29) Kupitia muujiza huo wa siku ya Pentekoste, Mungu alionyesha kwamba alikuwa amekataa taifa la Israeli ambalo liliasi, na kwamba alikuwa amekubali “Israeli wa Mungu,” inayofanyizwa na wanaume na wanawake. (Gal. 3:28; 6:15, 16) Wakati wa mitume, kati ya wanawake Wakristo waliounga mukono kazi ya kuhubiri kulikuwa binti ine wa Filipo mweneza-injili.—Mdo. 21:8, 9.

 “JESHI KUBWA” LA WANAWAKE

18, 19. (a) Mungu amewapatia wanaume na wanawake pendeleo gani? (b) Mutunga-zaburi alisema nini juu ya wanawake wanaotangaza habari njema?

18 Katika miaka ya 1870, wanaume na wanawake fulani walionyesha kwamba walipendezwa sana na ibada ya kweli. Walitangulia wale ambao leo wanatenda kulingana na unabii huu wa Yesu: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mt. 24:14.

19 Kikundi kidogo cha Wanafunzi wa Biblia kimeongezeka, na leo kimekuwa Mashahidi wa Yehova milioni 8 hivi. Watu wengine zaidi ya milioni 11 wanaonyesha kwamba wanapendezwa na Biblia, na kazi yetu, kwa kuhuzuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu unaofanywa kila mwaka. Katika maeneo mengi, kati ya watu wanaohuzuria, wanawake ndio wengi. Duniani pote kuna wahubiri wa wakati wote zaidi ya milioni moja; na kati ya wahubiri hao wanawake ndio wengi zaidi. Mungu amewapatia wanawake waaminifu pendeleo la kutenda kupatana na maneno haya ya mutunga-zaburi: “Yehova mwenyewe anasema neno hili; wanawake wanaotangaza habari njema ni jeshi kubwa.”—Zab. 68:11.

Kwa kweli, wanawake wanaotangaza habari njema ni “jeshi kubwa”(Ona fungu la 18 na la 19)

BARAKA AMBAZO WANAWAKE WAAMINIFU WATAPATA

20. Tunaweza kupanga kujifunza habari gani?

20 Katika habari hii hatuwezi kuzungumuzia wanawake wote waaminifu ambao Biblia inataja. Lakini sisi wote tunaweza kusoma habari yao katika Neno la Mungu na katika vichapo vyetu. Kwa mufano, tunaweza kutafakari juu ya uaminifu wa Ruthu. (Rut. 1:16, 17) Kusoma kitabu cha Biblia kinachoitwa kwa jina la Malkia Esta, na kusoma habari juu yake katika vichapo vyetu kunaweza kutia nguvu imani yetu. Tutapata faida kubwa tukipanga kujifunza habari kama hizo wakati wa Ibada yetu ya Familia ya mangaribi. Ikiwa unaishi peke yako, unaweza kuchunguza habari hizo wakati wa funzo lako la pekee.

21. Wakati wa majaribu, namna gani wanawake waliomuogopa Yehova walionyesha uaminifu wao kwake?

21 Bila shaka Yehova anabariki kazi ya kuhubiri ambayo wanawake Wakristo wanafanya, na anawategemeza wakati wa majaribu. Kwa mufano, alisaidia wanawake waliomuogopa waendelee kuwa waaminifu wakati wa utawala wa Nazi na wa Wakomunisti, wakati wengi kati yao waliteswa na wengine hata waliuawa kwa sababu walitaka kumutii Mungu. (Mdo. 5:29) Leo pia, dada zetu pamoja na waabudu wengine wa Yehova wanaunga mukono utawala wa Mungu. Kama vile tu ilikuwa wakati wa Waisraeli, Yehova anakamata mukono wao wa kuume na anawaambia: ‘Musiogope, kwa maana mimi niko pamoja nanyi.’—Isa. 41:10-13.

22. Tunangojea baraka gani wakati unaokuja?

22 Hivi karibuni, wanaume na wanawake wanaomuogopa Mungu watafanya dunia hii kuwa paradiso, na watasaidia watu wengi ambao watafufuliwa wajifunze kusudi za Yehova. Mbele wakati huo ufike, iwe sisi ni wanaume ao wanawake, tuendelee kufurahia pendeleo letu la kumutumikia Yehova “bega kwa bega.”—Sef. 3:9.