Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Rudi na Uwatie Nguvu Ndugu Zako’

‘Rudi na Uwatie Nguvu Ndugu Zako’

PETRO alilia kwa uchungu kisha kumukana Yesu. Hata kama Petro alipaswa kujikaza kutengeneza tena hali yake ya kiroho, Yesu alitaka kumutumia ili kusaidia wengine. Yesu alikuwa amemuambia hivi: ‘Mara tu utakapokuwa umerudi, uwatie nguvu ndugu zako.’ (Lu. 22:32, 54-62) Petro alitegemeza kutaniko la wakati wa mitume. (Gal. 2:9) Vilevile, ndugu ambaye zamani alikuwa muzee wa kutaniko anaweza tena kurudilia madaraka yake na kupata furaha ya kuwatia nguvu kiroho ndugu na dada.

Ndugu ambao wakati fulani walikuwa wazee wameachishwa madaraka, na hilo linaweza kufanya wajisikie kuwa hawafae kitu. Julio, * ambaye alikuwa muzee huko Afrika ya Kusini kwa miaka 20, alisema hivi: “Kutayarisha hotuba, kutembelea ndugu na dada, na kuwashugulikia kiroho ilikuwa sehemu kubwa ya maisha yangu. Kisha, mara moja nilipoteza madaraka yangu; nilijisikia kuwa nimepoteza jambo la maana sana katika maisha. Kwa kweli, huo ulikuwa wakati mugumu sana.” Leo, Julio ni muzee tena.

“ONENI YOTE KUWA SHANGWE”

Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: ‘Oneni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, munapokutana na majaribu ya namna mbalimbali.’ (Yak. 1:2) Yakobo alikuwa anazungumuzia majaribu ambayo tunapata kwa sababu ya upinzani na kutokamilika. Alitaja tamaa za kibinafsi, upendeleo, na mambo mengine. (Yak. 1:14; 2:1; 4:1, 2, 11) Wakati Yehova anaturekebisha, tunaweza kuhuzunika. (Ebr. 12:11) Lakini majaribu hayo hayapaswe kutukosesha furaha.

Hata kama tumepoteza madaraka yetu katika kutaniko, tunaweza kuonyesha kwamba tuna imani yenye nguvu na kwamba tunamupenda Yehova. Tunaweza  pia kuchunguza sababu zilizotufanya tutumikie madaraka hayo. Je, ilikuwa ni kwa faida yetu wenyewe, ao ni kwa sababu tunamupenda Mungu na tunasadiki kwamba kutaniko ni lake na linastahili kushugulikiwa vizuri? (Mdo. 20:28-30) Wale ambao zamani walikuwa wazee na ambao wanaendelea kumutumikia Mungu kwa furaha, wanaonyesha kwamba wanamupenda kweli Yehova.

Wakati Mufalme Daudi alirekebishwa kwa sababu ya zambi alizofanya, alikubali na alisamehewa. Daudi aliimba hivi: ‘Mwenye furaha ni mutu ambaye amesamehewa maasi yake, ambaye zambi yake imefunikwa. Mwenye furaha ni mutu ambaye Yehova hamuhesabie kosa, na ambaye katika roho yake hamuna udanganyifu.’ (Zab. 32:1, 2) Daudi alirekebishwa, na bila shaka hilo lilimusaidia achunge vizuri watu wa Mungu.

Mara nyingi, ndugu ambao wamerudilia madara yao wanakuwa wachungaji wazuri zaidi. Muzee mumoja anasema hivi: “Sasa ninaelewa muzuri namna ya kushugulikia watu ambao wanafanya kosa.” Muzee mwengine alisema hivi: “Sasa ninachukua kwa uzito pendeleo la kutumikia ndugu na dada.”

UNAWEZA TENA KUWA MUZEE?

Mutunga-zaburi aliandika kwamba Yehova “hataendelea kutafuta makosa wakati wote.” (Zab. 103:9) Kwa hiyo, tusiwaze kama Mungu hawezi tena kutumainia mutu ambaye amefanya kosa kubwa. Ricardo ambaye aliachishwa madaraka baada ya kuwa muzee wa kutaniko kwa miaka mingi anasema hivi: “Nilivunjika moyo sana. Kwa muda murefu, nilijisikia kuwa sifae kitu, na hilo lilinizuia kurudilia madaraka yangu na kutumikia tena ndugu na dada. Sikuamini kama ningekuwa tena mutu mwenye kutumainika. Lakini, kwa kuwa ninapenda kusaidia wengine, niliongoza mafunzo ya Biblia, nilitia wengine moyo kwenye Jumba la Ufalme, na nilihubiri pamoja nao. Hilo lilinisaidia niache kujisikia kuwa sifae kitu, na sasa nimekuwa tena muzee.”

Yehova amesaidia ndugu wakuwe na furaha na nia ya kuongoza tena kutaniko

Kuendelea kuwa na kinyongo ao kuendelea kukasirika kunaweza kuzuia ndugu akuwe tena muzee. Ni vizuri kabisa kuiga Daudi, ambaye alikimbia Mufalme Sauli mwenye wivu. Daudi  hakumutendea Sauli vibaya, hata wakati nafasi zilijitokeza. (1 Sam. 24:4-7; 26:8-12) Wakati Sauli alikufa katika vita, Daudi alilia sana, na kusema kwamba Sauli na Yonathani mutoto wake ni “watu wenye kupendwa na wenye kupendeza.” (2 Sam. 1:21-23) Daudi hakuendelea kukasirika.

Ikiwa unafikiri kwamba ulitendewa bila haki, usiache hasira ikutawale. Kwa mufano, wakati William aliachishwa madaraka kisha kuwa muzee kwa miaka 30 katika Uingereza, aliwakasirikia wazee fulani. Ni nini ilimusaidia William aache kuwakasirikia? Anasema hivi: “Kusoma kitabu cha Ayubu kulinitia moyo. Ikiwa Yehova alimusaidia Ayubu kufanya amani pamoja na rafiki zake watatu, bila shaka atanisaidia pia nifanye amani pamoja na wazee hao.”—Ayu. 42:7-9.

MUNGU ANABARIKI WALE WANAOKUWA TENA WAZEE

Ikiwa wewe mwenyewe uliamua kuacha kuchunga kundi la Mungu, ni vizuri uchunguze sababu zilizokufanya uamue hivyo. Je, ni kwa sababu ulikuwa na mambo mengi ya kufanya? Je, ulitia mambo mengine pa nafasi ya kwanza katika maisha yako? Ulivunjika moyo kwa sababu ya makosa ya wengine? Iwe ni kwa sababu gani, kumbuka kwamba, ulipokuwa muzee, ulikuwa na nafasi nzuri ya kusaidia ndugu na dada. Hotuba zako ziliwatia nguvu, mufano wako muzuri uliwatia moyo, na kazi zako za uchungaji ziliwasaidia wapambane na majaribu yao. Ulipokuwa muzee mwaminifu, ulifurahisha moyo wa Yehova, na hilo lilikuletea furaha.—Met. 27:11.

Onyesha kwamba unamupenda Yehova kwa kujitoa kabisa katika utumishi mutakatifu

Yehova amesaidia ndugu wakuwe na furaha na nia ya kuongoza tena kutaniko. Iwe uliamua kuacha kuwa muzee ao uliachishwa, unaweza tena “kufikia cheo cha [ao kazi ya] mwangalizi.” (1 Tim. 3:1) Mutume Paulo ‘hakuacha kusali’ ili Wakristo Wakolosai wajazwe na ujuzi sahihi wa mapenzi ya Mungu ‘ili watembee kwa kumustahili Yehova kwa kusudi la kumupendeza yeye kikamili.’ (Kol. 1:9, 10) Ikiwa unapewa tena pendeleo la kuwa muzee, umuombe Yehova akupatie nguvu, uvumilivu, na furaha. Katika siku hizi za mwisho, watu wa Mungu wanahitaji musaada wa kiroho wa wachungaji wenye upendo. Je, una uwezo, na unataka kutia nguvu ndugu na dada zako?

^ fu. 3 Majina fulani yamebadilishwa.