Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Sikiliza Sauti ya Yehova Popote Ulipo

Sikiliza Sauti ya Yehova Popote Ulipo

“Masikio yako yatasikia neno nyuma yako likisema: ‘Hii ndiyo njia.’”ISA. 30:21.

1, 2. Tunapata muongozo wa Yehova namna gani?

BIBLIA inazungumuzia watu waliopokea muongozo wa Yehova kwa njia mbalimbali. Kuna wale ambao walisikia sauti ya Yehova kupitia malaika ao katika maono ao ndoto. Kupitia njia hizo Yehova aliwafunulia mambo ambayo yangetokea baadaye. Tena, Yehova aliwapatia kazi fulani za kufanya. (Hes. 7:89; Eze. 1:1; Dan. 2:19) Wengine walipokea muongozo wa Yehova kupitia wajumbe wake hapa duniani. Wale wote waliopokea maagizo ya Yehova walibarikiwa.

2 Leo, Yehova anaongoza watu wake kupitia Biblia, roho takatifu, na kutaniko. (Mdo. 9:31; 15:28; 2 Tim. 3:16, 17) Muongozo tunaopokea kutoka kwake uko wazi sana; ni kama vile “masikio yetu yanasikia neno nyuma yetu likisema: ‘Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.’” (Isa. 30:21) Yehova anatumia pia Yesu ili atufikishie sauti yake. Yesu anatumia kutaniko analoongoza kupitia ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara.’ (Mt. 24:45) Tunapaswa kuchukua muongozo huo kwa uzito, kwa sababu tutapata uzima wa milele ikiwa tu tunafuata muongozo huo.—Ebr. 5:9.

3. Ni mambo gani yanayoweza kutuzuia kufuata muongozo wa Yehova? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

3 Shetani anataka kutuzuia kufuata muongozo wa Yehova ili tukose uzima wa milele. Tena,  ‘moyo wetu wenye hila’ [ao mudanganyifu] unaweza kutuzuia kufuata muongozo wa Yehova. (Yer. 17:9) Kwa hiyo, tuzungumuzie namna tunaweza kupambana na mambo yanayoweza kutuzuia kusikiliza sauti ya Mungu. Tutazungumuzia pia namna gani kusali kwa ukawaida kutalinda urafiki wetu pamoja na Yehova hata tukuwe katika hali gani.

TUEPUKE NJIA ZA UDANGANYIFU ZA SHETANI

4. Namna gani Shetani anajaribu kuvuruga akili za watu?

4 Shetani anajaribu kuvuruga akili za watu kwa kueneza habari za uongo. (Soma 1 Yohana 5:19.) Vyombo kama vile, magazeti, vitabu, radio, televizyo, na Internete vinaeneza habari katika dunia yote. Hata kama vyombo hivyo vinazungumuzia mambo yenye kupendeza, mara nyingi vinachochea watu wafuate mwenendo ambao unavunja kanuni za Yehova. (Yer. 2:13) Kwa mufano, vyombo vya habari na mashirika yanayotengeneza mambo ya kujifurahisha yanasema waziwazi kwamba mwanaume kulala na mwanaume na mwanamuke kulala na mwanamuke ni mambo yenye kukubalika. Na watu wengi wanafikiri kwamba Biblia inapitisha kipimo inapokataza mambo hayo.—1 Kor. 6:9, 10.

5. Namna gani tunaweza kuepuka kushawishiwa na habari za uongo za Shetani?

5 Namna gani wale wanaopenda haki wanaepuka kushawishiwa na habari za Shetani za uongo ambazo zinaenea leo? Namna gani wanaweza kujua tofauti kati ya mambo mabaya na mazuri? ‘Kwa kujilinda kulingana na neno la Mungu.’ (Zab. 119:9) Biblia inaweza kutuongoza vizuri ili kutofautisha habari za kweli na habari za uongo. (Met. 23:23) Yesu alirudilia andiko fulani la Biblia aliposema kwamba “mwanadamu ataishi . . . kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mt. 4:4) Ni lazima tujifunze namna ya kutumia kanuni za Biblia katika maisha yetu. Kwa mufano, miaka mingi mbele Musa aandike sheria ya Yehova juu ya uasherati, kijana Yosefu alijua kwamba kufanya uasherati ni kumutendea Mungu zambi. Hakufikiria hata kidogo kumukosea Yehova wakati bibi ya Potifa alijaribu kumushawishi afanye naye uasherati. (Soma Mwanzo 39:7-9.) Hata kama bibi ya Potifa alimukaza mara nyingi, Yosefu hakuruhusu sauti ya mwanamuke huyo imuzuie kusikiliza sauti ya Mungu. Ili kusikiliza sauti ya Yehova na kuepuka habari za kuchukiza zinazoenezwa na Shetani, ni lazima tujue kutofautisha mambo mazuri na mabaya.

6, 7. Tunapaswa kufanya nini ili kuepuka kushawishiwa na Shetani?

6 Dunia inajaa mafundisho ya dini na imani zenye kupingana; kwa hiyo watu wanaona kwamba haiwezekane kupata dini ya kweli. Lakini, Yehova ametoa muongozo ulio wazi kwa wale wanaotaka kuufuata. Tunapaswa kuamua tutasikiliza sauti ya nani. Kwa sababu haiwezekane kusikiliza sauti mbili wakati uleule, ni lazima ‘tujue sauti’ ya Yesu na kuisikiliza. Ni yeye ambaye  alipewa daraka la kuongoza kondoo za Yehova.—Soma Yohana 10:3-5.

7 Yesu alisema hivi: ‘Sikilizeni kwa makini [ao kwa uangalifu] mambo ambayo munasikia.’ (Mk. 4:24) Shauri la Yehova liko wazi na ni lenye kufaa, lakini tunapaswa kutayarisha moyo wetu ili kusikiliza na kukubali shauri hilo. Ikiwa hatuko waangalifu, tunaweza kusikiliza shauri mbaya la Shetani kuliko kusikiliza shauri la Mungu. Usiruhusu hata kidogo maisha yako yaongozwe na muziki wa ulimwengu, video za ulimwengu, televizyo, vitabu, marafiki, walimu, ao watu wanaojiwazia kuwa wenye ujuzi.—Kol. 2:8.

8. (a) Namna gani moyo wetu unaweza kutuongoza katika njia za udanganyifu za Shetani? (b) Tunaweza kupatwa na nini ikiwa tunapuuza alama zinazoonyesha kwamba tunakaribia kufanya kosa nzito?

8 Shetani anajua kwamba tuna mwelekeo wa kufanya zambi; kwa hiyo anajaribu kutushawishi ili tufanye zambi. Wakati Shetani anatumia njia hiyo, inakuwa vigumu kwetu kubaki waaminifu. (Yoh. 8:44-47) Namna gani tunaweza kupambana na jaribu hilo? Wazia ndugu ao dada anayepitisha wakati mwingi sana katika mambo ya kujifurahisha, kisha anafikia kufanya jambo ambalo hakuwazia hata siku moja kwamba angeweza kufanya. (Rom. 7:15) Ni nini inayoweza kumufikisha mutu katika hali hiyo? Pengine, mutu huyo aliacha hatua kwa hatua kusikiliza sauti ya Yehova. Ao inawezekana hakutambua alama zilizoonyesha kwamba moyo wake ulikuwa umeanza kudanganyika, ao alizarau tu alama hizo. Kwa mufano, pengine hakuwa anasali tena, hakuwa anahubiri tena kwa ukawaida, ao alianza kukosa mikutano. Mwishowe, aliongozwa na tamaa zake na kufanya mambo ambayo alijua kwamba ni mabaya. Tunaweza kuepuka kosa kama hilo ikiwa tunaendelea kuwa waangalifu sana ili kuvumbua alama yoyote inayoweza kutuonyesha kwamba tunakaribia kufanya kosa nzito, na kurekebisha mambo bila kukawia. Pia, tukisikiliza sauti ya Yehova, hatutakuwa na mawazo yoyote ya uasi-imani.—Met. 11:9.

9. Sababu gani ni jambo la maana sana kuvumbua mbele ya wakati mambo yanayoweza kutuongoza kwenye zambi?

9 Magonjwa yakivumbuliwa mbele ya wakati, hilo linaweza kuokoa uzima. Vilevile, tunaweza kuepuka hatari ya kiroho ikiwa tunavumbua haraka mambo ambayo yanaweza kutuongoza kwenye zambi. Ikiwa tunatambua hali hiyo, ni vizuri kutenda bila kukawia mbele ‘tushikwe [na Shetani] tukiwa hai kwa ajili ya mapenzi yake.’ (2 Tim. 2:26) Tutafanya nini ikiwa tunatambua kwamba tumeacha akili yetu na tamaa zetu zituongoze kutenda tofauti na mapenzi ya Yehova? Tunapaswa kuwa wanyenyekevu ili kumurudilia Yehova bila kuchelewa, tunapaswa kufungua masikio yetu ili kusikiliza vizuri mashauri yake na kumusikiliza kwa moyo wetu wote. (Isa. 44:22) Tujue kwamba kuchukua maamuzi mabaya kunaweza kutuacha na huzuni ambayo  itadumu muda murefu. Ni vizuri kabisa kutenda bila kuchelewa, ili tuepuke hali hiyo yenye kuhuzunisha.

Kuwa na programu nzuri ya kiroho kunaweza kutulinda namna gani na njia za Shetani za udanganyifu?(Ona fungu la 4 mupaka fungu la 9)

TUEPUKE KIBURI NA PUPA

10, 11. (a) Ni nini inaonyesha kwamba mutu anakuwa na kiburi? (b) Habari ya Kora, Dathani na Abiramu inatufundisha nini?

10 Tunapaswa kujua kwamba moyo wetu unaweza kutupoteza. Mwelekeo wetu wa kufanya zambi una nguvu nyingi. Chukua mufano wa kiburi na pupa (ao tamaa isiyofaa). Tuzungumuzie namna tabia hizo mbaya zinaweza kutuzuia kusikiliza sauti ya Yehova na kutuongoza katika hatari ya kiroho. Mutu mwenye kiburi anajiona kuwa wa maana sana. Anaweza kufikiri kwamba ana haki ya kufanya kile anachopenda na kwamba hakuna mutu anayepaswa kumuambia jambo la kufanya. Kwa hiyo, anaweza kufikiri kwamba hana lazima ya muongozo wala shauri kutoka kwa Wakristo wenzake, wazee, ao hata tengenezo la Mungu. Mutu kama huyo hasikie tena vizuri sauti ya Yehova.

11 Waisraeli walipokuwa katika safari yao katika jangwa, Kora, Dathani na Abiramu waliasi mamlaka ya Musa na Haruni. Kwa sababu ya kiburi, waasi hao walifanya mipango yao wenyewe ya kumuabudu Yehova. Yehova alitenda namna gani? Aliwaua wote. (Hes. 26:8-10) Hilo linatufundisha somo la maana sana. Kumuasi Yehova kunaongoza kwenye hatari. Tusisahau pia kwamba ‘roho ya majivuno inatangulia kujikwaa.’—Met. 16:18; Isa. 13:11.

12, 13. (a) Toa mufano unaoonyesha kwamba pupa inaweza kuleta hatari. (b) Eleza namna tamaa inaweza kukomaa haraka ikiwa hatuizuie.

12 Tuzungumuzie pia pupa. Mara nyingi mutu mwenye pupa anafanya yale anayotaka, na anavunja kanuni za mwenendo muzuri. Wakati Naamani, mukubwa wa jeshi la Siria, aliponyeshwa ukoma wake, alimutolea nabii Elisha zawadi, lakini Nabii Elisha alikataa zawadi hizo. Gehazi, mutumishi wa Elisha, alitamani zawadi hizo. Alisema hivi: ‘Kama Yehova anavyoishi, nitakimbia nimufuate [Naamani], nichukue kitu fulani kutoka kwake.’ Bila kumujilisha Elisha, Gehazi alikimbia na kumufuata Naamani, kisha alisema uongo ili kumuomba ‘talanta moja ya feza na mavazi mawili.’ Gehazi alipatwa na nini kwa sababu alitenda hivyo na sababu alidanganya nabii wa Yehova? Gehazi alipatwa na ukoma wa Naamani.—2 Fal. 5:20-27.

13 Pupa inaweza kuanza polepole, lakini kama mutu haizuie, inaweza kukomaa haraka na kumutawala. Habari ya Biblia juu ya Akani inaonyesha namna pupa inaweza kutawala mutu. Pupa ya Akani ilikomaa haraka. Yeye alisema hivi: ‘Nilipoona katikati ya nyara vazi rasmi kutoka Shinari, lenye kupendeza, na shekeli 200 za feza na kipande kimoja cha zahabu, uzito wake ukiwa shekeli 50, ndipo nikavitamani vitu hivyo, halafu nikavichukua.’ Kuliko kuepuka tamaa hiyo mbaya, Akani aliiba vitu hivyo na kuvificha katika hema yake. Wakati kosa la Akani lilijulikana, Yoshua alimuambia kwamba Yehova ataleta musiba juu yake. Akani na watu wa familia yake waliuawa siku ileile kwa kupigwa majiwe. (Yos. 7:11, 21, 24, 25) Pupa inaweza kutupata kila wakati. Kwa hiyo, tunapaswa ‘kujilinda na kila namna ya tamaa.’ (Lu. 12:15) Hata kama wakati fulani tunaweza kuwa na mawazo mabaya kama vile kuwaza juu ya mambo ya uasherati, ni jambo la maana tutoshe mawazo hayo katika akili yetu na tusiruhusu tamaa zetu mbaya zituongoze kwenye zambi.—Soma Yakobo 1:14, 15.

14. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunatambua kwamba tunaanza kuwa na roho ya kiburi na pupa?

14 Kiburi na pupa vinaweza kumuingiza mutu katika hatari kubwa. Kufikiria matokeo ya mwenendo mubaya   kutatusaidia tusiruhusu kiburi na pupa vituzuie kusikiliza sauti ya Yehova. (Kum. 32:29) Katika Biblia, Mungu wa kweli anatuonyesha mwenendo muzuri wa kufuata; anatuonyesha pia faida za kufuata mwenendo huo na matokeo ya kufuata mwenendo mubaya. Moyo wetu ukituchochea tutende kwa kiburi ao kwa pupa, ni jambo la hekima tufikirie matokeo mabaya ya matendo hayo! Tunapaswa kufikiria namna zambi inaweza kuwa na matokeo mabaya juu yetu, juu ya wale wanaotupenda, na zaidi sana namna inaweza kuharibu urafiki wetu pamoja na Yehova.

TUZUNGUMUZE NA YEHOVA KWA UKAWAIDA

15. Yesu alizungumuza na Baba yake katika sala kwa ukawaida; hilo linatufundisha nini?

15 Yehova anatutakia mema. (Zab. 1:1-3) Anatutolea uongozi unaofaa kwa wakati unaofaa. (Soma Waebrania 4:16.) Hata ikiwa Yesu alikuwa mukamilifu, alizungumuza na Yehova kwa ukawaida katika sala. Yehova alimusaidia na kumuongoza katika njia za ajabu. Alituma malaika wamusaidie, alimusaidia kupitia roho takatifu, na alimuongoza alipochagua mitume 12. Sauti ya Yehova ilisikika kutoka mbinguni, akionyesha kwamba angemutegemeza mwana wake na kwamba alimukubali. (Mt. 3:17; 17:5; Mk. 1:12, 13; Lu. 6:12, 13; Yoh. 12:28) Kama Yesu, tunapaswa kumuelezea Mungu mambo yote yaliyo katika moyo wetu. (Zab. 62:7, 8; Ebr. 5:7) Kupitia sala, tunaweza kuendelea kuzungumuza na Mungu na kupata matokeo mazuri tunapofanya mapenzi yake ili kumuletea heshima.

16. Namna gani Yehova anatusaidia tusikilize sauti yake?

16 Hata ikiwa Yehova anafanya iwe vyepesi kupata mashauri yake, yeye halazimishe mutu yeyote kuyafuata. Tunapaswa kumuomba roho yake takatifu, na atatupatia. (Soma Luka 11:10-13.) Kwa hiyo, ni jambo la maana ‘tukazie uangalifu jinsi tunavyosikiliza.’ (Lu. 8:18) Kwa mufano, ikiwa tunamuomba Yehova musaada wa kushinda tabia fulani inayoweza kutuongoza katika uasherati, lakini tunaendelea kutazama ponografia ao filme zinazoonyesha uasherati, tunatenda kwa unafiki. Tunapaswa kuwa katika hali ao mahali ambapo tunaweza kupata roho ya Yehova. Tunajua kwamba tunaweza kupata roho yake tunapohuzuria mikutano. Watumishi wengi wa Yehova waliepuka kufanya jambo mbaya kwa sababu walimusikiliza kwenye mikutano. Kwa kufanya hivyo, walitambua tamaa mbaya zilizokuwa zikikomaa katika mioyo yao na wakafanya mabadiliko.—Zab. 73:12-17; 143:10.

TUENDELEE KUSIKILIZA SAUTI YA YEHOVA KWA UANGALIFU

17. Sababu gani kujitumainia ni jambo la hatari?

17 Fikiria mufano wa Mufalme Daudi. Wakati alikuwa kijana, alipata ushindi juu ya Goliathi, Mufilisti mwenye nguvu nyingi. Daudi akakuwa askari, mufalme, mulinzi, na mutu aliyechukua maamuzi kwa ajili ya taifa la Israeli. Lakini wakati Daudi alijitumainia, moyo wake ulimudanganya na alifanya uzinifu na Bath-sheba, na kufanya hata mipango ili bwana yake, Uria akufe. Wakati alirekebishwa, Mufalme Daudi alikubali kwa unyenyekevu kosa lake, na alitengeneza tena urafiki wake pamoja na Yehova.—Zab. 51:4, 6, 10, 11.

18. Ni nini inayoweza kutusaidia tuendelee kusikiliza sauti ya Yehova?

18 Ili tuepuke kujitumainia kupita kipimo, tunapaswa kufuata shauri ambalo tunapata katika 1 Wakorintho 10:12. Kwa kuwa hatuna uwezo wa ‘kuongoza hatua zetu;’ tunaweza kusikiliza ao sauti ya Yehova ao sauti ya Adui wake. (Yer. 10:23) Tuendelee basi kusali kwa ukawaida, kufuata muongozo wa roho takatifu, na kusikiliza kwa uangalifu sauti ya Yehova sikuzote.