Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Neno la Mungu Liko Hai!—Ulitumie

Neno la Mungu Liko Hai!—Ulitumie

“Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.”EBR. 4:12.

1, 2. Yehova alimuambia Musa afanye nini, na alimuhakikishia nini?

UNAWEZA kujisikia namna gani ikiwa unasimama mbele ya mutawala mukubwa zaidi wa dunia ili kutetea watu wa Yehova? Pengine unaweza kuwa na wasiwasi, kujisikia kwamba haustahili, ao hata kuogopa. Utajitayarisha namna gani? Unaweza kufanya nini ili maneno yako yakuwe yenye nguvu na uonekane kabisa kuwa umetumwa na Mungu Mweza-Yote?

2 Musa alijikuta katika hali kama hiyo. Yehova alimuambia Musa, ambaye alikuwa ‘mupole zaidi kuliko watu wote waliokuwa juu ya uso wa inchi,’ kwamba angemutuma kwa Farao ili kukomboa watu wa Mungu kutoka katika utumwa wa Misri. (Hes. 12:3) Mambo yaliyofuata yalionyesha wazi kwamba Farao alikuwa mutu asiyeheshimu wengine, na mwenye kiburi. (Kut. 5:1, 2) Sasa, Yehova alimutuma Musa amuambie Farao aachilie mamilioni ya watu waliokuwa watumwa wake. Tunaelewa sababu gani Musa alimuuliza Yehova hivi: “Mimi ni nani hata niende kwa Farao, nikawatoe wana wa Israeli kutoka Misri?” Musa alijiona kuwa hastahili na kwamba hangeweza kufanya kazi hiyo. Lakini Mungu alimuhakikishia kwamba angemusaidia. Yehova alimuambia hivi: “Nitakuwa pamoja nawe.”—Kut. 3:9-12.

3, 4. (a) Sababu gani Musa aliogopa? (b) Namna gani unaweza kujikuta katika hali inayofanana na ile ya Musa?

3 Sababu gani Musa aliogopa? Ni wazi kwamba Musa aliogopa  kama Farao hangepokea na kusikiliza mutu ambaye Yehova Mungu alituma. Musa aliogopa pia kama hata Waisraeli hawangeamini kwamba Yehova alimutuma ili kuwakomboa kutoka Misri. Kwa hiyo Musa alimuambia Yehova hivi: “Lakini tuseme hawaniamini wala hawaisikilize sauti yangu, kwa sababu watasema, ‘Yehova hakukutokea.’”—Kut. 3:15-18; 4:1.

4 Jibu ambalo Yehova alimutolea Musa na pia mambo yaliyotendeka baadaye yanaweza kufundisha kila mumoja wetu jambo la maana sana. Pengine wewe hautatumwa mbele ya mutawala fulani mwenye mamlaka. Lakini je, kuna wakati unaona kuwa ni vigumu kusema juu ya Yehova na Ufalme wake unapoongea na watu wa kawaida, ambao unakutana nao? Ikiwa umejikuta katika hali kama hiyo, mufano wa Musa unaweza kukufundisha somo la maana sana.

‘NI NINI ILIYO MUKONONI MWAKO?’

5. Mungu alitia nini katika mukono wa Musa, na namna gani jambo hilo lilimusaidia asiwe na woga? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

5 Wakati Musa aliogopa kwamba watu hawangechukua maneno yake kwa uzito, Mungu alimutayarisha ili apambane na magumu ambayo angepata. Kitabu cha Kutoka kinasema hivi: “Yehova akamuambia [Musa]: ‘Ni nini iliyo mukononi mwako?’ Naye akajibu: ‘Fimbo.’ Kisha akasema: ‘Itupe chini.’ Basi akaitupa chini, nayo ikakuwa nyoka; na Musa akaanza kumukimbia. Sasa Yehova akamuambia Musa: ‘Nyoosha mukono wako umukamate kwenye mukia.’ Basi akaunyoosha mukono wake, akamukamata, naye akawa fimbo mukononi mwake. Kisha Mungu akasema: ‘Ili wapate kuamini ya kwamba Yehova . . . amekutokea.’” (Kut. 4:2-5) Ndiyo, Mungu alitia katika mukono wa Musa kitu ambacho kingemusaidia ahakikishe kwamba ujumbe wake ulitoka kwa Yehova. Mungu alitumia nguvu zake ili kufanya fimbo ya Musa ikuwe na uzima, hata kama watu waliiona kuwa fimbo tu! Bila shaka muujiza huo ulifanya maneno ya Musa yakuwe yenye nguvu zaidi, na ulionyesha kwamba Yehova alikuwa anamutegemeza. Kisha, Yehova alimuambia hivi: ‘Fimbo hii utaichukua mukononi mwako ili uitumie kufanya zile ishara.’ (Kut. 4:17) Kwa sababu sasa Musa alikuwa na fimbo hiyo iliyoonyesha kwamba anatumia mamlaka kutoka kwa Mungu, angeweza kuenda na kumutetea Mungu bila woga mbele ya watu wake na mbele ya Farao.—Kut. 4:29-31; 7:8-13.

6. (a) Tunapaswa kuwa na nini mukononi tunapohubiri, na sababu gani? (b) Eleza namna gani “neno la Mungu liko hai” na namna gani “lina nguvu.”

6 Wakati tunaenda kutangazia wengine ujumbe wa Biblia sisi pia tunaweza kuulizwa: ‘Ni nini iliyo mukononi mwako?’ Tunapohubiri, mara nyingi tunakuwa na Biblia katika mukono, na tuko tayari kuitumia. Hata kama watu fulani wanaona Biblia kuwa ni kitabu tu, sisi tunajua kwamba ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake na anaitumia ili kuzungumuza nasi. (2 Pet. 1:21) Biblia inazungumuzia mambo ambayo Mungu anaahidi kufanya kupitia Ufalme wake. Ndiyo sababu mutume Paulo aliandika hivi: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.” (Soma Waebrania 4:12.) Ahadi zote za Yehova hazikose kutimia, kwa sababu Yeye mwenyewe anaendelea kufanya yote ili kuzitimiza. (Isa. 46:10; 55:11) Mutu anapokuwa na maoni hayo juu ya Neno la Yehova, mambo ambayo anasoma katika Biblia yanatenda katika maisha yake.

7. Namna gani tunaweza ‘kulitumia sawasawa neno la kweli’?

7 Yehova ametia katika mukono wetu Neno lake lililo hai ambalo tunaweza kutumia ili kuonyesha kwamba ujumbe wetu ni wa kweli na unatoka kwake. Haishangaze kwamba, kisha kuwaandikia Waebrania, mutume Paulo alimushauria Timotheo ‘afanye kabisa yote aliyoweza  ili kulitumia sawasawa neno la kweli.’ (2 Tim. 2:15) Namna gani tunaweza kulitumia shauri la Paulo? Kwa kusoma kwa sauti maandiko tuliyochagua vizuri, ambayo yanaweza kugusa mioyo ya watu watakaotusikiliza. Trakte zilizotolewa katika mwaka wa 2013 zimetayarishwa ili kutusaidia kufanya hivyo.

CHAGUA VIZURI ANDIKO UTAKALOSOMA!

8. Mwangalizi mumoja wa utumishi alisema nini juu ya trakte zetu mupya?

8 Trakte zote mupya zimepangwa kwa namna moja. Kwa hiyo, tunapojifunza namna ya kutumia trakte moja, tutajua kuzitumia zote. Je, ni vyepesi kuzitumia? Mwangalizi mumoja wa utumishi katika Hawaii, États-Unis, aliandika hivi: “Tulitambua mara moja kwamba vyombo hivyo vipya vinaweza kuwa na matokeo mazuri iwe tunahubiri mahali pa watu wote ao nyumba kwa nyumba.” Ametambua kwamba namna trakte hizo zimepangwa inafanya watu wajibu bila magumu, na kila mara hilo linaongoza kwenye mazungumuzo mazuri. Anafikiri kwamba ni kwa sababu kwenye ukurasa wa kwanza wa trakte kuna ulizo na pia majibu ambayo mutu anaweza kuchagua. Musikilizaji haogope kwamba atatoa jibu lisilo la kweli.

9, 10. (a) Namna gani trakte zetu mupya zinatupatia nafasi ya kutumia Biblia katika mahubiri? (b) Ni trakte gani ambazo zimekusaidia sana katika mahubiri, na sababu gani?

9 Kila trakte inatupatia nafasi ya kusoma andiko lililochaguliwa vizuri. Kwa mufano, ona trakte Kuna Siku Mateso Yataisha?Iwe jibu la musikilizaji ni “ndiyo,” “hapana,” ao “pengine”, fungua trakte, na bila kuongeza jambo lolote, umuambie hivi: “Ona jibu la Biblia.” Kisha soma Ufunuo 21:3, 4.

10 Trakte Una Mawazo Gani juu ya Biblia? inaweza kutumiwa kwa njia ileile hata kama musikilizaji anachagua jibu gani kwenye ukurasa wa kwanza. Fungua trakte hiyo kisha useme hivi: “Biblia inasema kwamba ‘andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.’” Kisha unaweza kuongeza hivi: “Lakini andiko hilo haliishie pale.” Kisha fungua Biblia yako na usome andiko lote la 2 Timotheo 3:16, 17.

11, 12. (a) Kutumia trakte katika mahubiri kutakuletea furaha gani? (b) Namna gani trakte zinaweza kukusaidia ujitayarishe ili kuwarudilia watu?

11 Namna musikilizaji wako anaitikia itakusaidia kujua kiasi cha habari munazoweza kuzungumuzia katika trakte. Unapotumia trakte hizo katika  mahubiri, utafurahi sana kwa sababu utakuwa pia umesomea watu Biblia, hata kama unaweza kusoma andiko moja ao maandiko mawili tu unapowatembelea kwa mara ya kwanza. Baadaye, munaweza kuendelea na mazungumuzo.

12 Kwenye ukurasa wa mwisho wa kila trakte, chini ya kichwa “Pengine Unajiuliza” kuna ulizo na maandiko ya kuzungumuzia wakati wa kumurudilia mutu. Katika trakte Unawaza Maisha Yatakuwa Namna Gani Wakati Unaokuja? ulizo la kuzungumuzia wakati wa kumurudilia mutu ni: “Mungu atafanya nini ili maisha yakuwe mazuri sana katika dunia?” Maandiko ya Mathayo 6:9, 10 na Danieli 2:44 yanatajwa. Katika trakte Watu Waliokufa, Wanaweza Kweli Kuishi Tena? ulizo la kuzungumuzia wakati wa kumurudilia mutu ni: “Sababu gani watu wanazeeka na wanakufa?” Maandiko ya Mwanzo 3:17-19 na Waroma 5:12 yanatajwa.

13. Namna gani unaweza kutumia trakte ili kuanzisha mafunzo ya Biblia?

13 Tumia trakte ili zikusaidie kuanzisha mafunzo ya Biblia. Wakati mutu anatumia chombo cha kusoma alama iliyo kwenye ukurasa wa mwisho wa trakte, ataongozwa mara moja kwenye adresi yetu ya Internete ambayo itamuchochea akubali kujifunza Biblia. Trakte zinataja pia broshua Habari Njema Inayotoka kwa Mungu! na zinaongoza kwenye somo fulani katika broshua hiyo. Kwa mufano, trakte Kwa Kweli, Ni Nani Anayeitawala Dunia? inaongoza kwenye somo la 5 la broshua hiyo. Trakte Ni Nini Inayoweza Kufanya Familia Yako Ikuwe na Furaha? inaongoza kwenye somo la 9. Ukitumia trakte kwa njia inayofaa, utazoea kutumia Biblia wakati unatembelea watu kwa mara ya kwanza, na wakati unawarudilia. Kufanya hivyo kunaweza kukusaidia kuanzisha mafunzo mengi ya Biblia. Unaweza tena kufanya nini ili kutumia vizuri Neno la Mungu unapohubiri?

CHAGUA HABARI INAYOHANGAISHA WATU

14, 15. Namna gani unaweza kumuiga mutume Paulo unapohubiri?

14 Mutume Paulo alitamani sana kuhubiria ‘watu wengi zaidi.’ (Soma 1 Wakorintho 9:19-23.) Paulo alitaka ‘kuwapata Wayahudi . . . , kuwapata wale walio chini ya sheria . . . , kuwapata wale wasio na sheria . . . , na kuwapata walio zaifu.’ Ndiyo, alipenda kupata “watu wa namna zote, ili kwa vyovyote [awaokoe] wengine.” (Mdo. 20:21) Namna gani tunaweza kumuiga mutume Paulo tunapojitayarisha kuwahubiria “watu wa namna zote” katika eneo letu?—1 Tim. 2:3, 4.

15 Kila mwezi Huduma Yetu ya Ufalme inatutolea mapendekezo. Jaribu kuyatumia. Lakini ikiwa kuna habari zingine zinazohangaisha watu katika eneo lako, tayarisha namna ya kuanzisha mazungumuzo ambayo inapatana na mahitaji yao. Fikiria mahali ambapo unaishi, watu wanaoishi mahali hapo, na mambo yanayowahangaisha zaidi. Kisha, tafuta andiko ambalo litawasaidia. Mwangalizi mumoja wa muzunguko anaeleza namna yeye na bibi yake wanakazia Biblia; anasema hivi: “Watu wengi wanaturuhusu tusome andiko ikiwa hatuwachukue wakati mwingi, na ikiwa tunazungumuzia jambo linalowahangaisha. Kisha kumusalimia mutu, tukiwa na Biblia katika mukono, tunamusomea andiko.” Katika mafungu yanayofuata, utaona habari fulani, maulizo, na maandiko ambayo wahubiri fulani wamejaribu kutumia, na ambayo wewe pia unaweza kujaribu kutumia katika eneo lako.

Je,unatumia Biblia na trakte unapohubiri?(Ona fungu la 8 mupaka 13)

16. Eleza namna unaweza kutumia andiko la Isaya 14:7 katika mahubiri.

16 Ikiwa unaishi katika eneo lenye vita, unaweza kumuuliza mutu hivi: “Utajisikia namna gani kama unasikia habari hii kwenye vyombo vya kutangaza habari: ‘Dunia nzima imepumuzika, imekuwa huru kutokana na usumbufu. Watu wamechangamuka kwa vigelegele vya shangwe’? Biblia inazungumuzia jambo hilo katika andiko la Isaya 14:7. Biblia inataja ahadi nyingi za Mungu kuhusu wakati unaokuja wenye amani.” Kisha umusomee katika Biblia, moja kati ya ahadi hizo.

17. Unaweza kusema nini mbele ya kusomea mutu andiko la Mathayo 5:3?

 17 Je, wanaume wengi katika eneo lenu wana magumu ili kutimiza mahitaji ya familia zao? Ikiwa jibu ni ndiyo, unaweza kuanza mazungumuzo kwa kuuliza hivi: “Mutu anahitaji feza ngapi ili familia yake ikuwe na furaha?” Sikiliza jibu, kisha ongeza hivi: “Wanaume wengi wanapata feza nyingi kuliko hizo lakini familia zao hazina furaha. Sasa, mutu anahitaji nini kabisa ili akuwe na furaha?” Soma Mathayo 5:3 na umuambie kama ungependa kumufundisha Biblia.

18. Namna gani unaweza kutumia andiko la Yeremia 29:11 ili kuwatia wengine moyo?

18 Je watu wa eneo lenu wanateseka kwa sababu ya musiba fulani ambao uliwapata hivi karibuni? Unaweza kuanza mazungumuzo kwa kusema: “Ninakutembelea ili tuzungumuzie wazo fulani lenye kutia moyo. (Soma Yeremia 29:11.) Umeona mambo matatu ambayo Mungu anatutakia? ‘Amani,’ ‘wakati ujao,’ na ‘tumaini.’ Hauone kwamba inatia moyo kujua kwamba anataka tukuwe na maisha mazuri? Lakini inawezekana namna gani?” Kisha umuonyeshe katika broshua Habari Njema somo ambalo linajibu ulizo hilo.

19. Eleza namna unaweza kutumia andiko la Ufunuo 14:6, 7 unapozungumuza na watu wanaopendezwa na mambo ya dini.

19 Je, unaishi katika eneo ambamo watu wanapendezwa na mambo ya dini? Ikiwa jibu ni ndiyo, unaweza kuanza mazungumuzo kwa kuuliza hivi: “Kama malaika anakuambia jambo fulani, utasikiliza maneno yake? (Soma Ufunuo 14:6, 7.) Kwa sababu malaika huyo anasema ‘muogopeni Mungu,’ hauone kwamba ingekuwa jambo la lazima tujue Mungu huyo ni nani? Malaika anatusaidia kupata jibu anaposema kwamba ni ‘Yeye aliyezifanya mbingu na dunia.’ Ni nani huyo?” Kisha soma Zaburi 124:8, ambayo inasema: ‘Musaada wetu uko katika jina la Yehova, Mutengenezaji wa mbingu na dunia.’ Endelea na mazungumuzo ukiwa na kusudi la kumuelezea mengi zaidi juu ya Yehova Mungu.

20. (a) Namna gani tunaweza kutumia andiko la Methali 30:4 ili kumufundisha mutu jina la Mungu? (b) Unatumia andiko lingine gani ili kufundisha watu jina la Mungu?

20 Unaweza kuanzisha mazungumuzo pamoja na kijana kwa kusema hivi: “Ningependa kukusomea andiko fulani ambalo lina ulizo moja la maana sana. (Soma Methali 30:4.) Hakuna mwanadamu ambaye anatimiza maneno ya andiko hilo; kwa hiyo linahusu Muumbaji wetu. * Namna gani tunaweza kujua jina lake? Nitafurahi kukuonyesha jina hilo katika Biblia.”

TUMIA NGUVU YA NENO LA MUNGU UNAPOHUBIRI

21, 22. (a) Namna gani andiko ambalo limechaguliwa vizuri linaweza kubadilisha maisha ya mutu? (b) Umeamua kufanya nini kila mara unapohubiri?

21 Hatujue namna watu watatenda tunapowasomea andiko ambalo tumechagua vizuri. Kwa mufano, katika inchi ya Australia ndugu wawili waligonga kwenye mulango wa kijana mumoja mwanamuke. Mumoja kati yao alimuuliza hivi: “Unajua jina la Mungu?” kisha akamusomea Zaburi 83:18. Mwanamuke huyo anasema: “Nilishangaa sana. Kisha wao kuondoka, nilichukua motokari na kuenda kilometre 56 mahali pa kuuzishia vitabu ili nitafute jina hilo katika tafsiri zingine za Biblia; kisha nilitafuta jina hilo katika kamusi ao diksionere. Kwa sababu nilisadiki kwamba jina la Mungu ni Yehova, nilijiuliza kama kulikuwa mambo mengine ambayo nilipaswa kujifunza.” Kisha muda mufupi, mwanamuke huyo pamoja na mwanaume ambaye baadaye alimuoa walianza kujifunza Biblia, na baadaye wakabatizwa.

22 Neno la Mungu linabadilisha maisha ya watu wanaolisoma na kuamini ahadi za Yehova. (Soma 1 Wathesalonike 2:13.) Ujumbe wa Biblia una nguvu kuliko neno lolote ambalo tunaweza kusema ili kugusa mioyo ya watu. Kwa hiyo, kila mara tunapopata nafasi, tunapaswa kutumia Neno la Mungu ambalo liko hai!

^ fu. 20 Ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 7, 1987, ukurasa wa 31.