Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Maulizo ya Wasomaji Wetu

Maulizo ya Wasomaji Wetu

Yesu aliambia Masadukayo kwamba watu watakaofufuliwa ‘hawataoa wala kuolewa.’ (Lu. 20:34-36) Je, alikuwa anazungumuzia ufufuo utakaofanyika duniani?

Ulizo hilo ni la maana, zaidi sana kwa wale ambao wamepoteza bibi ao bwana yao. Watu hao wanangojea kwa hamu kuonana tena na bwana ao bibi yao katika dunia mupya. Mwanaume mumoja ambaye bibi yake alikufa alisema hivi: “Miye na bibi yangu hatukutaka ndoa yetu iishe. Tulipenda kabisa tuendelee kuishi pamoja, na kumuabudu Yehova sikuzote. Hata leo ninaendelea kuwa na mawazo hayo.” Je, tunaweza kabisa kuamini kwamba watu ambao watafufuliwa wataweza tena kuoa ao kuolewa? Kwa kifupi, hatuwezi kuhakikisha jambo hilo.

Tangu miaka mingi, vichapo vyetu vimesema kwamba wakati Yesu alisema juu ya kuoa ao kuolewa kisha ufufuo, inawezekana alikuwa anazungumuzia ufufuo ambao utafanyika duniani, na kwamba wale watakaofufuliwa duniani hawataoa ao kuolewa. * (Mt. 22:29, 30; Mk. 12:24, 25; Lu. 20:34-36) Hata kama hatuwezi kuhakikisha jambo hilo, je, inawezekana Yesu alikuwa anazungumuzia wale ambao watafufuliwa ili waishi mbinguni? Tuchunguze yale ambayo alisema.

Yesu alisema maneno hayo katika hali gani? (Soma Luka 20:27-33.) Masadukayo, ambao hawakuamini ufufuo, walijaribu kumutega Yesu kwa kumuuliza kuhusu ufufuo na ndoa kati ya mutu na bibi ya ndugu yake. * Yesu alijibu hivi: ‘Watoto wa mufumo huu wa mambo wanaoa na kuolewa, lakini wale ambao wamehesabiwa kustahili kuupata mufumo ule wa mambo na ufufuo kutoka kwa wafu hawaoe wala hawaolewe. Kwa kweli, wala hawawezi kufa tena kamwe, kwa maana wao ni kama malaika, nao ni watoto wa Mungu kwa kuwa watoto wa ufufuo.’ Lu. 20:34-36.

Sababu gani vichapo vyetu vilisema kwamba inawezekana Yesu alikuwa anazungumuzia ufufuo utakaofanyika duniani? Kuna sababu mbili. Kwanza, inaonekana kwamba Masadukayo walikuwa wanafikiria ufufuo utakaofanyika duniani; kwa hiyo, inawezekana jibu ambalo Yesu alitoa linahusu ufufuo huo. Pili, Yesu alimalizia jibu lake kwa kutaja Abrahamu, Isaka, na Yakobo, ambao bila shaka watafufuliwa ili waishi duniani.—Lu. 20:37, 38.

Hata hivyo, inaonekana Yesu alikuwa anasema juu ya ufufuo wa wale watakaoishi mbinguni. Sababu gani tunasema hivyo? Tuone mambo mawili ya maana katika maneno ya Yesu.

“Wale ambao wamehesabiwa kustahili kuupata . . . ufufuo kutoka kwa wafu.” Watiwa-mafuta waaminifu ‘wamehesabiwa kuwa wanastahili ufalme wa Mungu.’ (2 Thes. 1:5, 11) Wamehesabiwa kuwa wenye haki na wanastahili kupata uzima kwa musingi wa zabihu ya ukombozi; kwa hiyo, wanapokufa hawana hatia ya zambi. (Rom. 5:1, 18; 8:1) Watiwa-mafuta wanatajwa kuwa ‘wenye furaha na watakatifu’ na wanastahili kufufuliwa ili waishi mbinguni. (Ufu. 20:5, 6) Lakini hata watu “wasio waadilifu” watafufuliwa ili waishi duniani. (Mdo. 24:15) Hatuwezi kusema kwamba watu wasio waadilifu “wanastahili” kufufuliwa.

 “Hawawezi kufa tena kamwe.” Yesu hakusema: “Hawatakufa tena kamwe.” Lakini alisema: “Hawawezi kufa tena kamwe.” Tafsiri zingine za Biblia zimeandika maneno hayo hivi: “Wao ni watu wasiokufa” ao “kifo hakina tena nguvu juu yao.” Watiwa-mafuta ambao wanakufa wakiwa waaminifu wanafufuliwa ili kuishi mbiguni, na wanapewa hali ya kutoweza kufa, ni kusema, uzima ambao hautakuwa na mwisho na ambao hauwezi kuharibika. (1 Kor. 15:53, 54) Kifo hakina tena nguvu yoyote juu ya wale watakaofufuliwa ili waishi mbinguni. *

Mambo ambayo tumekwisha kuzungumuzia yanatufundisha nini? Inawezekana maneno ya Yesu kuhusu kuoa na kuolewa baada ya ufufuo yanahusu ufufuo wa wale watakaoishi mbinguni. Ikiwa ni hivyo, maneno hayo yanaweza kutufundisha mambo mengi juu ya wale watakaofufuliwa ili waishi mbinguni: Hawataoa ao kuolewa, hawawezi kufa, na kwa namna fulani, wako kama malaika, ni kusema, wataishi katika makao ya kiroho. Jambo hilo linatokeza maulizo mengine.

Ulizo la kwanza: Sababu gani Yesu alizungumuzia ufufuo wa wale watakaoishi mbinguni, wakati alikuwa anajibu Masadukayo, ambao pengine walikuwa wanafikiria ufufuo utakaofanyika duniani? Wakati fulani Yesu hakuwa anajibu moja kwa moja maulizo ya wapinzani wake. Kwa mufano, wakati Wayahudi walimuomba afanye ishara fulani, alisema hivi: “Libomoeni hekalu hili, na katika siku tatu nitalisimamisha.” Inaonekana Yesu alijua kwamba Wayahudi hao waliwaza anasema juu ya jengo la hekalu, “lakini alikuwa akiongea juu ya hekalu la mwili wake.” (Yoh. 2:18-21) Pengine Yesu hakupenda tu kujibu Masadukayo hao wanafiki ambao hawakuamini ufufuo na hawakuamini hata kama kuna malaika. (Met. 23:9; Mt. 7:6; Mdo. 23:8) Lakini Yesu alipenda kufundisha wanafunzi wake kuhusu ufufuo wa wale watakaoishi mbinguni, kwa sababu wao pia wangepata ufufuo huo.

Ulizo la pili: Sababu gani Yesu alimalizia maneno yake kwa kutaja Abrahamu, Isaka, na Yakobo, ambao watafufuliwa ili waishi duniani? (Soma Mathayo 22:31, 32.) Umeona katika andiko hilo kwamba mbele Yesu ataje Abrahamu, Isaka, na Yakobo, alisema kwanza hivi: “Kwa habari ya ufufuo wa wafu.” Maneno hayo yanaonyesha kwamba Yesu alitaka sasa kuzungumuzia jambo lengine. Kisha, Yesu alitaja mambo ambayo Musa aliandika, na ambayo hata Masadukayo walisema kwamba wanaamini; alirudilia maneno ambayo Yehova alimuambia Musa katika kichaka kilichokuwa kinawaka moto, ili kuhakikisha kwamba ufufuo wa duniani utafanyika.—Kut. 3:1-6.

Ulizo la tatu: Ikiwa maneno ya Yesu yanahusu ufufuo wa wale watakaoishi mbinguni, je, wale watakaofufuliwa ili waishi duniani wataweza tena kuoa ao kuolewa? Neno la Mungu halijibu moja kwa moja ulizo hilo. Ikiwa Yesu alizungumuzia ufufuo wa wale watakaoishi mbinguni, maneno yake hayaonyeshe kama watu watakaofufuliwa ili waishi duniani wataoa na kuolewa, ao hapana.

Kwa sasa, tunajua kwamba Neno la Mungu linasema wazi kama, ikiwa bwana ao bibi anakufa, ndoa yao inaishia pale. Kwa hiyo, ikiwa mutu ambaye amefiwa na bwana ao bibi anaamua kuoa ao kuolewa tena na mutu mwengine, hafanye kosa hata kidogo. Huo ni uamuzi wa mutu mwenyewe, na hatupaswe kusema vibaya juu ya mutu ambaye anaamua kuoa ao kuolewa tena.—Rom. 7:2, 3; 1 Kor. 7:39.

Inaeleweka kwamba tunaweza kuwa na maulizo mengi juu ya maisha katika dunia mupya. Lakini kuliko kujisumbua kwa kuwazia-wazia majibu, inafaa tungojee tu wakati unaokuja. Lakini tunaweza kuamini kabisa kwamba Yehova hatakosa kutosheleza tamaa na mahitaji yote ya watu wanaomutii.— Zab. 145:16.

^ fu. 4 Ona Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 Mwezi wa 6, mwaka wa 1987, ukurasa wa 30-31.

^ fu. 5 Wakati wa zamani, ikiwa bwana alikufa bila kuzaa watoto, ndugu yake alipaswa kuoa yule mwanamuke aliyefiwa na kuzaa naye watoto ili kuendelesha familia ya yule aliyekufa.—Mwa. 38:8; Kum. 25:5, 6.

^ fu. 9 Wale watakaofufuliwa ili waishi duniani watapewa uzima wa milele, lakini hawatapewa hali ya kutoweza kufa. Ukipenda kujua tofauti kati ya hali ya kutoweza kufa, na uzima wa milele, soma Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 Mwezi wa 4, 1984, ukurasa wa 30 na wa 31 (Kifaransa).