Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tusisahau Wale Wanaofanya Utumishi wa Wakati Wote

Tusisahau Wale Wanaofanya Utumishi wa Wakati Wote

‘Sisi tunaendelea kukumbuka kazi yenu ya uaminifu na kazi yenu ya jasho na yenye upendo.’—1 THES. 1:3.

1. Mutume Paulo alisema nini kuhusu watu ambao wanamutumikia Yehova kwa bidii?

MUTUME Paulo alikumbuka wale waliotumika kwa bidii ili kueneza habari njema. Aliandika hivi: ‘Sisi tunaendelea kukumbuka kazi yenu ya uaminifu na kazi yenu ya jasho yenye upendo na uvumilivu wenu kwa sababu ya tumaini lenu katika Bwana wetu Yesu Kristo mbele za Mungu wetu na Baba.’ (1 Thes. 1:3) Ni kweli kwamba, Yehova pia anakumbuka kazi ambayo watumishi wake waaminifu wanafanya kwa bidii na kwa upendo, iwe hali zao zinawaruhusu kufanya mengi ao machache.—Ebr. 6:10.

2. Tutazungumuzia nini katika habari hii?

2 Watumishi wengi wa Yehova, wa zamani na wa leo, wamejitoa sana ili kumutumikia kwa wakati wote. Katika habari hii, tutazungumuzia namna wamoja kati yao walifanya hivyo wakati wa mitume. Tutazungumuzia pia namna mbalimbali za utumishi wa wakati wote katika siku zetu, na namna gani tunaweza kukumbuka ndugu na dada zetu wapendwa wanaojitoa katika utumishi huo.

WAKATI WA MITUME

3, 4. (a) Wakati wa mitume, Wakristo fulani walifanya utumishi gani wa wakati wote? (b) Walipata namna gani mahitaji yao ya kimwili?

3 Muda mufupi kisha kubatizwa, Yesu alianzisha kazi ambayo ingeenea katika dunia yote. (Lu. 3:21-23; 4:14, 15, 43)  Kisha kifo chake, mitume wake waliendelesha kazi hiyo. (Mdo. 5:42; 6:7) Wakristo fulani, kama vile Filipo, walikuwa wamisionere na walihubiri sana katika inchi ya Palestina. (Mdo. 8:5, 40; 21:8) Paulo na Wakristo wengine walienda kuhubiri katika maeneo ya mbali sana. (Mdo. 13:2-4; 14:26; 2 Kor. 1:19) Pia, wengine kama vile Sila, Marko, na Luka walikuwa waandishi. (1 Pet. 5:12) Dada Wakristo walitumika pamoja na ndugu hao waaminifu. (Mdo. 18:26; Rom. 16:1, 2) Mambo ambayo wote hao walifanya na kujionea, yanafanya tufurahie kusoma Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo; pia habari zao zinatuonyesha kwamba Yehova anakumbuka watumishi wake.

4 Wakati wa mitume, namna gani watumishi wa wakati wote walipata mahitaji yao ya kimwili? Wakati fulani, Wakristo wengine waliwapokea katika nyumba zao, na waliwatolea misaada mbalimbali, lakini watumishi wa wakati wote hawakuomba misaada hiyo. (1 Kor. 9:11-15) Wakristo fulani, ao makutaniko yaliwasaidia kwa kujipendea. (Soma Matendo 16:14, 15; Wafilipi 4:15-18.) Ili kupata mahitaji yao ya lazima, Paulo na wale waliosafiri pamoja naye walifanya kazi fulani ya kimwili isiyochukua wakati mwingi.

WAKATI WETU

5. Ndugu mumoja na bibi yake walisema nini kuhusu maisha yao katika utumishi wa wakati wote?

5 Leo, ndugu na dada wengi wanafanya aina mbalimbali za utumishi wa wakati wote. (Ona kisanduku chenye kichwa ““ Aina Mbalimbali za Utumishi wa Wakati Wote.”) Wanajisikia namna gani kuhusu utumishi wao? Unaweza kuwauliza ulizo hilo; majibu yao yanaweza kukusaidia sana. Tuchukue mufano huu: Ndugu mumoja ambaye amekuwa painia wa kawaida, painia wa pekee, misionere, na ambaye leo anatumika kwenye beteli katika inchi ya kigeni anaeleza hivi: “Ninaona kwamba, nilichagua vizuri sana nilipoamua kufanya utumishi wa wakati wote. Wakati nilikuwa na miaka 18, nilipaswa kuchagua kati ya kusoma masomo ya juu, kufanya kazi ya kimwili, ao kuwa painia. Sasa nimejionea kwamba Yehova hawezi kusahau hata kidogo mutu ambaye anajitoa ili kufanya utumishi wa wakati wote. Nimepata nafasi ya kutumia uwezo ambao Yehova amenipatia; singepata nafasi ya kutumia uwezo huo katika kazi yoyote ya kimwili kama vile ninautumia leo.” Bibi yake pia anasema hivi: “Kila mugawo ambao tulipewa umenisaidia kukomaa kiroho. Mara nyingi sana, tumeona namna Yehova ametulinda na kutuongoza. Hatungepata baraka hizo ikiwa hatukuamua kufanya utumishi wa wakati wote. Ninamushukuru Yehova kila siku kwa kutupatia pendeleo la kufanya utumishi wa wakati wote.” Je, wewe pia ungependa kuwa na maisha kama hayo?

6. Yehova anaona namna gani utumishi ambao tunamutolea?

6 Ni kweli kwamba, hali za ndugu na dada fulani haziwaruhusu kufanya utumishi wa wakati wote. Tunaamini kabisa kwamba Yehova anapendezwa sana na mambo wanayotimiza kulingana na uwezo wao. Fikiria wale ambao mutume Paulo anataja katika andiko la Filemoni 1-3, na wale wote waliokuwa katika kutaniko la Kolosai. (Soma.) Paulo alipendezwa nao; Yehova pia alipendezwa nao. Vilevile, Baba yetu wa mbinguni anapendezwa sana na utumishi wako. Namna gani wewe unaweza kuwasaidia wale walio katika utumishi wa wakati wote?

KUSAIDIA MAPAINIA

7, 8. Mapainia wanatimiza nini, na namna gani wengine katika kutaniko wanaweza kuwasaidia?

7 Kama vile tu watumishi wa Yehova wa wakati wa mitume, sisi pia tunatiwa moyo sana tunapokuwa na mapainia wenye bidii katika kutaniko. Mapainia wa kawaida wanajikaza kuhubiri saa 70 kila mwezi. Unaweza kuwasaidia namna gani?

8 Dada mumoja painia anayeitwa Shari  alisema hivi: “Mapainia wanaonekana kuwa nguvu kiroho kwa sababu wanahubiri kila siku. Hata hivyo, wanahitaji kutiwa moyo.” (Rom. 1:11, 12) Dada mwengine ambaye alikuwa painia kwa miaka fulani alisema hivi juu ya mapainia katika kutaniko lake: “Mapainia wanaendelea kuhubiri kwa bidii. Mapainia wanafurahi sana wakati wengine wanawabeba katika motokari ili kuenda katika mahubiri, wanapowaalika kula chakula, wanapowanunulia essence ao kuwapatia musaada fulani wa feza. Hilo linaonyesha kwamba wengine wanawahangaikia kabisa.”

9, 10. Wakristo fulani wamefanya nini ili kusaidia mapainia katika makutaniko yao?

9 Je, ungependa kuhubiri pamoja na mapainia? Painia mumoja anayeitwa Bobbi alisema hivi: “Tuko na lazima ya watu wa kuhubiri pamoja nasi katika juma.” Painia mwengine katika kutaniko hilo alisema hivi: “Ni vigumu sana kupata mutu wa kuhubiri naye kisha midi.” Dada mumoja ambaye sasa anatumikia kwenye Beteli ya Brooklyn anaeleza kwa furaha namna alisaidiwa wakati alikuwa painia. Anasema hivi: “Dada mumoja ambaye alikuwa na motokari aliniambia hivi: ‘Ukikosa mutu wa kuhubiri naye, uniite, miye nitahubiri pamoja na weye.’ Kwa kweli, dada huyo alinisaidia niendelee kuwa painia.” Dada mwengine anayeitwa Shari anasema hivi: “Kisha kumaliza kazi, mara nyingi mapainia ambao hawajaoa ao kuolewa wanajisikia kuwa peke yao. Mara kwa mara munaweza kualika mapainia kama hao kwenye ibada yenu ya familia. Mukifanya nao mambo mengine pia, mutawasaidia waendelee kuwa na nguvu.”

10 Dada mumoja ambaye alifanya utumishi wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 50 anakumbuka musaada ambao yeye na dada wengine mapainia ambao walikuwa hawajaolewa walipata. Anasema hivi: “Wazee wa kutaniko letu walikuwa na programu ya kutembelea mapainia kwa ukawaida kisha miezi fulani. Wakati walitutembelea, walituuliza juu ya afya yetu, kazi yetu ya kimwili, na walitafuta kujua kama tulikuwa na shida fulani. Walichukua mambo hayo kwa uzito. Mara kwa mara walifika katika nyumba yetu ili waone kama tulikuwa na lazima ya musaada fulani.” Pengine hilo linakukumbusha namna Paulo alikuwa mwenye shukrani sana kwa mambo ambayo familia moja ilimutendea alipokuwa katika muji wa Efeso.—2 Tim. 1:18.

11. Mapainia wa pekee wanatimiza nini?

11 Makutaniko fulani yamepata pendeleo la kuwa na mapainia wa pekee. Mapainia wa pekee wengi wanajikaza kuhubiri saa 130 kila mwezi.  Kwa sababu wanatumia wakati mwingi sana katika mahubiri na katika mambo mengine ya kiroho, hawana wakati wa kufanya kazi ya kimwili. Kila mwezi, biro ya tawi inawatumia feza kidogo ili kuwasaidia waendelee kushugulikia tu kazi ya kuhubiri.

12. Namna gani wazee na ndugu na dada wengine katika kutaniko wanaweza kusaidia mapainia wa pekee?

12 Namna gani tunaweza kusaidia mapainia wa pekee? Ndugu mumoja ambaye ni muzee kwenye Beteli na ambaye mara nyingi anaonana na mapainia wa pekee alisema hivi: “Wazee wanapaswa kuongea na mapainia wa pekee, kujua hali zao, ili waone namna gani wanaweza kuwasaidia. Mashahidi fulani wanawaza kama mapainia wa pekee hawakose kitu kwa sababu biro ya tawi inawatumia feza; lakini ndugu na dada wanaweza kuwasaidia katika njia nyingi.” Kama vile mapainia wa kawaida, mapainia wa pekee wanafurahi sana wanapopata mutu wa kuhubiri pamoja nao. Je, unaweza kusaidia mapainia wa pekee kwa kuhubiri pamoja nao?

KUSAIDIA WAANGALIZI WANAOSAFIRI

13, 14. (a) Ni lazima tukumbuke nini juu ya waangalizi wa muzunguko, na bibi zao? (b) Namna gani wewe unaweza kusaidia waangalizi wanaosafiri, na bibi zao?

13 Ndugu na dada wengi wanawaza kama waangalizi wa muzunguko, na bibi zao, ni watu walio nguvu kiroho na wanaweza kuvumilia hali ngumu. Hiyo ni kweli, lakini wao pia wanalazima ya kutiwa moyo, kupata watu wa kuhubiri pamoja nao, na kupata nafasi ya kujifurahisha pamoja na wengine. Tunaweza kufanya nini ikiwa wanagonjwa na kupangishwa kwenye hopitali, pengine ili wafanyiwe upasuaji ao wapate matunzo mengine? Wanafurahi sana wakati ndugu na dada wanawasaidia na kuwaonyesha kwamba wanawahangaikia. Tunaweza kufikiria namna Luka, ambaye aliandika kitabu cha Matendo, na ambaye alikuwa ‘tabibu [ao muganga] mupendwa,’ alimuhangaikia sana Paulo na wengine ambao walisafiri pamoja naye.—Kol. 4:14; Mdo. 20:5–21:18.

14 Waangalizi wanaosafiri, na bibi zao, wanahitaji kuwa na marafiki, na wanafurahia sana jambo hilo. Mwangalizi mumoja wa muzunguko aliandika hivi: “Inaonekana kwamba marafiki wangu wanatambua wakati niko na lazima ya kutiwa moyo. Wananiuliza maulizo kwa hekima, na hilo linanisaidia niweze kuwaambia mambo ambayo yananihangaisha. Wananisaidia sana kwa sababu wananisikiliza ninapoongea nao.” Waangalizi wa muzunguko, na bibi zao, wanafurahi sana wakati wanatambua kwamba ndugu na dada wanawahangaikia.

KUSAIDIA WANABETELI

15, 16. Wanabeteli na wale wanaotumika kwenye Majumba ya Mikusanyiko wanatimiza nini, na namna gani tunaweza kuwasaidia?

15 Wale wanaotumika kwenye Beteli ao kwenye Majumba ya Mikusanyiko, wanatimiza mambo ya maana sana katika kazi inayoongozwa na tawi ya inchi yao. Ikiwa katika kutaniko ao muzunguko wenu kuna Wanabeteli, namna gani unaweza kuonyesha kwamba unawakumbuka?

16 Wakati ndugu na dada hao wanafika kwenye Beteli, wanaweza kujisikia kuwa mbali na familia na marafiki wao. Wanafurahi sana wakati Wanabeteli wenzao, na ndugu na dada katika kutaniko lao jipya wanafanya nao urafiki. (Mk. 10:29, 30) Kwa kawaida, programu yao ya kazi inawaachia wakati wa kukusanyika na kuhubiri kila juma pamoja na kutaniko lao. Lakini, wakati fulani Wanabeteli wanaweza kuwa na kazi nyingi sana. Ikiwa wengine katika kutaniko wanaelewa jambo hilo, na wanaonyesha kwamba wanapenda Wanabeteli na wanafurahia yale ambayo wanatimiza, wote wanaweza kufaidika.—Soma 1 Wathesalonike 2:9.

KUSAIDIA WALE WANAOTUMIKIA KATIKA INCHI ZA KIGENI

17, 18. Wale wanaotumikia katika inchi za kigeni wanapewa migawo gani?

17 Wale wanaotumikia katika inchi za kigeni, wanaweza kukuta  chakula, luga, na hali za maisha zenye kuwa tofauti kabisa na zenye walizoea. Sababu gani wanakubali kuishi katika hali hizo?

18 Wamoja kati yao ni wamisionere ambao kwa kawaida wanatumwa katika maeneo ambamo watu wengi wanaweza kufaidika na mazoezi ambayo wamisionere hao wamepata. Biro ya tawi inapatia wamisionere makao na feza kidogo kwa ajili ya mahitaji yao ya lazima. Wengine wanatumikia kwenye biro ya tawi ao wanasaidia kujenga nyumba za Beteli, biro za watafsiri, Majumba ya Mikusanyiko, ao Majumba ya Ufalme. Wanapewa chakula, makao, na mambo mengine ya lazima. Wao pia wanakusanyika na kuhubiri pamoja na kutaniko lao; kwa hiyo wanaweza kusaidia wengine katika njia mbalimbali.

19. Tunapaswa kukumbuka nini juu ya wale wanaotumikia katika inchi za kigeni?

19 Namna gani unaweza kukumbuka wale wanaotumikia katika inchi za kigeni? Ni vizuri ukumbuke kwamba, pengine ndugu na dada hao hawajazoea chakula fulani, zaidi sana ikiwa hawajakawia katika eneo lenu. Usisahau jambo hilo wakati unapenda kuwaalika kula chakula. Unaweza kuwauliza ni chakula gani wanapenda kula ao wangependa kuonja. Ukuwe muvumilivu kwa sababu hawajajua vizuri luga ambayo munasema katika eneo lenu. Pengine hawataelewa mara moja mambo yote ambayo unasema, lakini unaweza kuwasaidia kwa kuwafundisha kusema vizuri maneno ya luga yenu. Wao pia wanapenda kujifunza.

20. Namna gani tunaweza kusaidia watumishi wa wakati wote na wazazi wao?

20 Kisha miaka mingi, watumishi wa wakati wote ambao wanatumikia mbali na kwao wanaweza kufikiria namna ya kusaidia wazazi wao ambao wamezeeka. Ikiwa wazazi wao ni Mashahidi, inawezekana kwamba wanapenda watoto wao waendelee kufanya utumishi wa wakati wote. (3 Yoh. 4) Ni kweli kwamba watumishi wa wakati wote wanafanya yote ambayo wanaweza ili kutembelea wazazi wao mara kwa mara na kuwasaidia. Hata hivyo, ikiwa wale wanaoishi karibu na wazazi hao wanawasaidia, wanasaidia pia watumishi wa wakati wote. Usisahau kwamba watumishi wa wakati wote wana mambo mengi ya kufanya katika kazi ya lazima zaidi ambayo inafanyika leo katika dunia. (Mt. 28:19, 20) Je, wewe ao kutaniko lenu munaweza kusaidia wazazi waliozeeka wa ndugu ao dada aliye katika utumishi wa wakati wote?

21. Watumishi wa wakati wote wanajisikia namna gani wakati wengine wanawasaidia?

21 Wale wanaochagua kufanya utumishi wa wakati wote, hawafanye hivyo ili wapate feza, lakini wanapenda kutumikia Yehova na kusaidia wanadamu wenzao. Kwa hiyo, wanafurahia sana musaada wowote ambao unaweza kuwatolea. Dada mumoja anayetumikia katika inchi ya kigeni anaeleza namna yeye na watumishi wengine wa wakati wote wanajisikia: “Wakati wengine wanakuandikia barua fupi tu ya shukrani unaona kwamba wanakuhangaikia na wanafurahia mambo ambayo unafanya.”

22. Uko na maoni gani juu ya utumishi wa wakati wote?

22 Kufanya utumishi wa wakati wote ndio njia nzuri zaidi ya kutumia maisha yetu. Haiko vyepesi kufanya hivyo, lakini utumishi huo unasaidia mutu ajifunze mambo mengi, na unaleta furaha kubwa sana. Tena, utumishi huo unatutayarisha kwa ajili ya utumishi ambao tutamutolea Yehova milele na kwa furaha wakati Ufalme wake utatawala dunia yote. Kwa hiyo basi, tuendelee ‘kukumbuka kazi ya uaminifu na kazi ya jasho yenye upendo’ ya wale wanaofanya utumishi wa wakati wote.—1 Thes. 1:3.