Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Umutumikie Mungu kwa Uaminifu Ijapokuwa ‘Mateso Mengi’

Umutumikie Mungu kwa Uaminifu Ijapokuwa ‘Mateso Mengi’

‘Lazima tuingie katika Ufalme wa Mungu kupitia ziki nyingi [ao mateso mengi].’—MDO. 14:22.

1. Sababu gani watumishi wa Mungu hawashangae wanapopata mateso?

UNASHANGAA kusikia kwamba utapata ‘ziki nyingi’ mbele upate uzima wa milele? Pengine hilo halikushangaze. Hata kama unamutumikia Yehova tangu zamani ao umeanza hivi karibuni, unajua kwamba katika ulimwengu huu unaotawaliwa na Shetani, hatuwezi kuepuka mateso.—Ufu. 12:12.

2. (a) Zaidi ya magumu yanayofikia wanadamu wote, Wakristo wanapata mateso gani mengine? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.) (b) Ni nani anayetuletea mateso, na namna gani tunajua hivyo?

2 Zaidi ya mateso ambayo ni ya “kawaida kwa watu” wote wasiokamilika, kuna mateso mengine ambayo yanapata Wakristo tu. (1 Kor. 10:13) Ni mateso gani hayo? Ni upinzani mukali ambao wanapata kwa sababu wanamutii Mungu kwa moyo wote. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: ‘Mutumwa si mukubwa kuliko bwana wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.’ (Yoh. 15:20) Ni nani anayeleta upinzani huo? Bila shaka ni Shetani; Biblia inamutaja kuwa ‘simba anayenguruma, akitafuta kumumeza mutu.’ (1 Pet. 5:8) Shetani atatumia kila njia ili ajaribu kuvunja ushikamanifu wa wanafunzi wa Yesu. Tuone mambo yaliyomufikia mutume Paulo.

 MATESO AMBAYO ALIPATA HUKO LISTRA

3-5. (a) Paulo alipata mateso gani huko Listra? (b) Sababu gani maneno ya Paulo kuhusu mateso yalikuwa yenye kutia moyo?

3 Mara nyingi mutume Paulo aliteswa kwa sababu ya imani yake. (2 Kor. 11:23-27) Tuone jambo moja ambalo lilimupata katika muji wa Listra. Kisha kuponyesha mwanaume fulani aliyekuwa kilema tangu kuzaliwa, watu walianza kusifu Paulo na Barnaba kama miungu. Paulo na Barnaba walijaribu kubembeleza watu hao wenye musisimuko ili waache kuwaabudu. Kisha muda kidogo, wapinzani Wayahudi walifika hapo na kuanza kusemea Paulo na Barnaba uongo ili kushawishi watu hao. Mara moja mambo yaliharibika. Watu hao walimupiga Paulo majiwe na kumuacha karibu kufa.—Mdo. 14:8-19.

4 Kisha kutembelea muji wa Derbe, Paulo na Barnaba “walirudi Listra na Ikoniamu na Antiokia, wakizitia nguvu nafsi za wanafunzi, wakiwatia moyo kubaki katika imani na kusema: ‘Lazima tuingie katika Ufalme wa Mungu kupitia ziki nyingi.’” (Mdo. 14:21, 22) Maneno hayo yanaweza kushangaza sana. Kwa kweli, Paulo aliposema kwamba watu watapata ‘ziki nyingi,’ hilo lingeweza kuogopesha watu kuliko kuwatia moyo. Namna gani basi Paulo na Barnaba ‘waliwatia moyo’ wanafunzi kupitia ujumbe huo ulioonyesha kwamba wangepata mateso mengi?

5 Tunaweza kupata jibu kwa kuchunguza maneno ya Paulo kwa uangalifu. Hakusema tu: ‘Lazima tuvumilie ziki nyingi.’ Lakini alisema: ‘Lazima tuingie katika Ufalme wa Mungu kupitia ziki nyingi.’ Kwa hiyo, Paulo alitia wanafunzi moyo kwa kukazia faida ya kubaki waaminifu. Zawadi ambayo wangepata haikuwa ndoto tu. Lakini, Yesu alisema kwamba ‘yule atakayevumilia mupaka mwisho ndiye ataokolewa.’Mt. 10:22.

6. Wale wanaovumilia watapata zawadi gani?

6 Ikiwa tunavumilia tutapata zawadi. Wakristo watiwa-mafuta watapata zawadi ya uzima usioweza kufa watakapotawala pamoja na Yesu huko mbinguni. “Kondoo wengine” watapata zawadi ya uzima wa milele katika dunia ambamo ‘haki itakaa.’ (Yoh. 10:16; 2 Pet. 3:13) Lakini, kama vile Paulo alisema, tutapata kwanza mateso mengi mbele ya kupokea zawadi hiyo. Tuone mateso ya aina mbili.

MASHAMBULIZI YA WAZIWAZI

7. Mashambulizi ya waziwazi ni nini?

7 Yesu alitabiri hivi: ‘Watu watawapeleka mahakamani, nanyi mutapigwa katika masinagogi na kusimamishwa mbele ya magavana na wafalme.’ (Mk. 13:9) Kulingana na maneno hayo, Wakristo fulani watateswa kimwili; pengine, viongozi wa dini ao wakubwa wa serikali ndio watatokeza mateso hayo. (Mdo. 5:27, 28) Tufikirie tena mufano wa Paulo. Je, aliogopa alipofikiria mateso kama hayo? Hapana.—Soma Matendo 20:22, 23.

8, 9. Namna gani Paulo alionyesha kwamba aliazimia kupambana na majaribu, na Mashahidi fulani wa wakati wetu wamefanya hivyo namna gani?

8 Paulo alipambana kwa ujasiri na mashambulizi ya waziwazi ya Shetani, naye alisema hivi: ‘Siifanyi nafsi yangu kuwa kitu chenye samani sana kwangu, kama tu ningepata kumaliza mwendo wangu na huduma niliyopokea kutoka kwa Bwana Yesu, kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fazili zisizostahiliwa za Mungu.’ (Mdo. 20:24) Ni wazi kwamba Paulo hakuogopa alipofikiria mateso ambayo yangemupata. Lakini, aliazimia kupambana na mateso hayo hata kutokee nini. Hangaiko lake kubwa lilikuwa “kutoa ushahidi kamili” ijapokuwa mateso yoyote.

9 Leo, ndugu na dada wengi wameazimia pia kufanya hivyo. Kwa mufano, katika inchi moja,  Mashahidi fulani wamefungwa karibu miaka 20 kwa sababu hawakujiingiza katika vita. Hawakupelekwa kwenye tribinali kwa sababu inchi yao haikuwa na mupango wowote kwa ajili ya wale waliokataa kujiunga na jeshi. Walipokuwa katika gereza, hakuna mutu aliyeruhusiwa kuwatembelea, hata watu wa familia yao; na wamoja kati ya wafungwa hao walipigwa na kuteswa kwa njia mbalimbali.

10. Sababu gani hatupaswe kuogopa majaribu yanayotokea bila kutazamia?

10 Katika maeneo mengine ndugu zetu wanapambana na majaribu yanayotokea bila kutazamia. Usiogope ikiwa wewe pia unapambana na majaribu kama hayo. Fikiria mufano wa Yosefu. Aliuzishwa ili kuwa mutumwa, lakini Yehova ‘alimukomboa kutoka katika ziki zake zote.’ (Mdo. 7:9, 10) Yehova anaweza kukukomboa pia. Usisahau hata kidogo kwamba ‘Yehova anajua namna ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu [wenye kushikamana na Mungu] kutoka katika jaribu.’ (2 Pet. 2:9) Je, utaendelea kumutumainia Yehova, ukijua kwamba anaweza kukuokoa kutoka ulimwengu huu na kukuwezesha kupata uzima wa milele chini ya utawala wa Ufalme wake? Ni jambo lenye kufaa kumutumainia Yehova na kupambana na majaribu kwa ujasiri.—1 Pet. 5:8, 9.

MASHAMBULIZI YASIYOONEKANA WAZI

11. Kuna tofauti gani kati ya mashambulizi yasiyoonekana wazi ya Shetani, na mashambulizi ya waziwazi?

11 Aina ingine ya mateso ambayo tunaweza kupambana nayo ni yale yasiyoonekana wazi. Mateso hayo yanatofautiana namna gani na mashambulizi ya waziwazi? Mashambulizi ya waziwazi ni kama upepo mukali unaopiga muji na kuharibisha nyumba yako mara moja. Mashambulizi yasiyoonekana wazi ni kama vidudu vidogo-vidogo ambavyo vinashambulia nyumba yako na vinaanza kuharibisha mbao za nyumba polepole, mupaka nyumba yote inaanguka. Mufano huo wa pili unaonyesha kwamba, mutu anaweza kukosa kutambua hatari mupaka ajikute amechelewa kabisa.

12. (a) Shetani anatumia njia gani ili kutushambulia, na sababu gani anafanikiwa? (b) Kuvunjika moyo kulikuwa na matokeo gani juu ya Paulo?

12 Shetani anataka kuharibisha urafiki wako pamoja na Yehova kupitia mashambulizi ya waziwazi, ao kwa kuregeza polepole imani yako kupitia mashambulizi yasiyoonekana wazi. Aina moja ya mashambulizi yasiyoonekana wazi ambayo Shetani anatumia ni kutufanya tuvunjike moyo. Mutume Paulo alisema kwamba wakati fulani yeye pia alivunjika moyo. (Soma Waroma 7:21-24.) Sasa, sababu gani Paulo, aliyekuwa “nguvu kiroho,” na inawezekana alikuwa mushiriki wa baraza linaloongoza la wakati wa mitume, anajiita ‘masikini mimi’? Paulo anasema kwamba alijisikia hivyo kwa sababu ya kutokamilika. Alitamani sana kufanya yaliyo sawa, lakini alisikia ndani yake nguvu ingine iliyomupiganisha. Ikiwa wakati fulani wewe pia unajisikia hivyo, hauone kwamba ni jambo lenye kutia moyo kujua kwamba hata mutume Paulo alipambana na magumu kama hayo?

13, 14. (a) Ni nini inafanya watumishi fulani wa Mungu wavunjike moyo? (b) Ni nani anayetaka kuvunja imani yetu, na sababu gani?

13 Wakati fulani, ndugu na dada wengi wanavunjika moyo, wanaogopa, ao pengine wanajisikia kuwa watu bure. Kwa mufano, dada mumoja painia mwenye bidii anasema hivi: “Mara kwa mara, ninakumbuka makosa ambayo nimefanya, na kila mara ninajisikia mubaya sana. Ninapokumbuka makosa yangu, ninajisikia kuwa hakuna mutu ambaye anaweza kunipenda, hata Yehova.”

14 Ni nini inafanya watumishi fulani wa Yehova wenye bidii, kama painia huyo, wavunjike moyo? Kunaweza kuwa sababu nyingi. Pengine mutu anaweza kuwa tu na maoni mabaya juu yake mwenyewe ao juu ya maisha yake. (Met. 15:15) Wengine wanaweza kuwa na tatizo fulani la mwili  linalowafanya wakuwe na huzuni kila mara. Iwe sababu ni gani, tunapaswa kukumbuka ni nani anayetaka tujisikie vile. Kwa kweli, ni nani anayetaka tuvunjike moyo na tuache kupigana vita ya kiroho? Ni nani anapenda ujisikie vile yeye anajisikia kwa sababu ya hukumu kali inayomungojea? (Ufu. 20:10) Bila shaka ni Shetani. Ukweli ni kwamba, iwe Shetani anatumia mashambulizi ya waziwazi ao mashambulizi yasiyoonekana wazi, kusudi lake ni lilelile, ni kusema, anataka kutuogopesha, kuregeza imani yetu, na kutufanya tuvunjike moyo kabisa. Usisahau kwamba watu wa Mungu wako katika vita ya kiroho.

15. Tutaonyesha namna gani kwamba tumeazimia kuendelea kupiganisha hali ya kuvunjika moyo?

15 Usiache hata kidogo Shetani apate ushindi. Endelea kufikiria zawadi utakayopata. Paulo aliandikia Wakristo wa muji wa Korintho hivi: ‘Hatukufe moyo, lakini hata ikiwa mutu tuliye kwa inje anaharibika, hakika mutu tuliye kwa ndani anafanywa upya siku baada ya siku. Kwa maana ingawa ziki ni ya dakika na ni nyepesi, hiyo inatufanyizia utukufu wenye uzito mukubwa zaidi na zaidi na ni wa milele.’—2 Kor. 4:16, 17.

UJITAYARISHE SASA KWA AJILI YA MATESO

Wakristo wote wanajizoeza ili kutetea imani yao(Ona fungu la 16))

16. Sababu gani ni jambo la lazima kujitayarisha tangu sasa kwa ajili ya mateso?

16 Kama vile tuliona, Shetani anatumia njia nyingi za ujanja ili kudanganya watu. (Efe. 6:11) Sisi wote tunapaswa kufuata shauri hili lililo katika andiko la 1 Petro 5:9: ‘Chukueni musimamo mukamupinge yeye.’ Ili kufanya hivyo, ni lazima tutayarishe akili na moyo wetu, na tujizoeze tangu sasa kufanya mambo mema. Tuchukue mufano: Katika jeshi, maaskari wanafanya mazoezi mbele hata ya kuwa katika hatari ya kushambuliwa. Ni hivyo pia katika jeshi la kiroho la Yehova. Hatujue vita ambayo  tutakuwa nayo wakati unaokuja. Kwa hiyo, ni jambo la hekima kujizoeza vizuri wakati kungali kiasi fulani cha amani. Paulo aliwaandikia Wakorintho hivi: ‘Endeleeni kujijaribu kama ninyi muko katika imani, endeleeni kusibitisha ninyi wenyewe namna mulivyo.’—2 Kor. 13:5.

17-19. (a) Namna gani tunaweza kujichunguza? (b) Namna gani vijana wanaweza kujitayarisha ili kutetea imani yao kwenye masomo?

17 Namna moja ya kufuata shauri hilo la Paulo ni kujichunguza kwa uangalifu. Ujiulize hivi: ‘Je, ninaendelea kusali? Wakati ninashawishiwa na marafiki, je, ninamutii Mungu kuwa mutawala kuliko kutii wanadamu? Je, ninahuzuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida? Je, ninahubiri kwa bidii? Je, ninajikaza kabisa kuvumilia makosa ya waamini wenzangu, kama vile wao pia wananivumilia? Je, ninajitiisha kwa wale wanaoongoza kutaniko letu na wale wanaoongoza tengenezo la Mungu katika dunia yote?’

18 Umeona kwamba kati ya maulizo hayo kuna maulizo mawili yanayohusu kutetea imani yetu kwa bidii, na kuepuka kushawishiwa na marafiki. Vijana Wakristo wanapaswa kufanya vile wanapokuwa kwenye masomo. Wamejifunza kutetea imani yao bila haya na bila kuogopa. Wanajitetea kwa bidii. Magazeti yetu yanatoa mapendekezo ya lazima kuhusu jambo hilo. Kwa mufano, gazeti Amuka! la Mwezi wa 7, 2009 linapendekeza kwamba ikiwa mwanafunzi mwenzako anakuuliza sababu gani hauamini mageuzi, unaweza kumujibu kwa kifupi hivi: ‘Sababu gani niamini mageuzi? Hata wanasayansi wenyewe ambao wanajiona kuwa na elimu nyingi hawakubaliane juu ya mageuzi.’ Wazazi, musikose kufanya mazoezi mara kwa mara pamoja na watoto wenu ili kuwatayarisha kwa ajili ya majaribu ambayo watakutana nayo kwenye masomo.

19 Kwa kweli, sikuzote si vyepesi kutetea imani yetu ao kufanya mambo mengine ambayo Yehova anatuomba. Kisha kufanya kazi muchana muzima, inaomba kuwa na roho ya kujitoa ili uende kwenye mikutano. Pia, ili uende katika mahubiri, inaomba kujikaza sana kuamuka asubuhi na kuacha usingizi wako mutamu. Lakini kumbuka kwamba, ukijikaza tangu sasa kuwa na programu nzuri ya kiroho, wakati majaribu makubwa zaidi yatatokea, utakuwa tayari kupambana nayo.

20, 21. (a) Namna gani kufikiri sana juu ya zabihu ya ukombozi kunatusaidia kupambana na hali ya kuvunjika moyo? (b) Unapaswa kujikaza kufanya nini hata kama utapata mateso?

20 Namna gani tunaweza kupambana na mashambulizi yasiyoonekana wazi? Kwa mufano, namna gani tunaweza kupambana na hali ya kuvunjika moyo? Njia kubwa zaidi ya kufanya hivyo ni kufikiri sana juu ya zabihu ya ukombozi. Hilo ndilo jambo ambalo mutume Paulo alifanya. Wakati fulani, alijisikia kuwa mutu bure ao masikini. Alijua pia kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya watenda-zambi; hakukufa kwa ajili ya watu wakamilifu. Paulo alikuwa mumoja kati ya watenda-zambi hao. Kwa hiyo, aliandika hivi: ‘Ninaishi kwa imani ambayo ni kumwelekea Mwana wa Mungu, aliyenipenda mimi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yangu.’ (Gal. 2:20) Ndiyo, Paulo aliona zabihu ya ukombozi kuwa ya maana sana. Alitambua kwamba alifaidika kipekee na zabihu hiyo.

21 Wewe pia utafaidika sana ikiwa unatambua kwamba Yehova alitoa zabihu ya ukombozi kwa ajili yako. Hilo halimaanishe kwamba hautavunjika tena moyo. Wamoja kati yetu wataendelea kupambana na hali ya kuvunjika moyo, mupaka tutakapoingia katika dunia mupya. Lakini kumbuka kwamba wale ambao watavumilia mupaka mwisho watapata zawadi. Tunakaribia sana wakati ambapo Ufalme wa Mungu utarudisha amani katika dunia na kufanya wanadamu waaminifu wafikie ukamilifu. Ujikaze ili uingie katika Ufalme huo, hata kama utaingia kupitia mateso mengi.