Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Unaona Uriti Wako wa Kiroho Kuwa wa Lazima Sana?

Unaona Uriti Wako wa Kiroho Kuwa wa Lazima Sana?

‘Tulipokea . . . roho inayotoka kwa Mungu, ili tuyajue mambo ambayo Mungu ametupa sisi kwa fazili.’1 KOR. 2:12.

1. Kwa kawaida watu wana mawazo gani?

WATU wengi wamesikia mawazo kama haya: ‘Kitu kinaonwa kuwa cha lazima wakati hakiko tena.’ Wakati fulani wewe pia unajisikia hivyo? Kwa kawaida, mutu haone vitu vyenye alipata wakati alikuwa angali mutoto kuwa vya lazima sana. Kwa mufano, mutu mwenye alikomalia katika familia tajiri anaona vitu vyenye iko navyo kuwa vya kawaida. Vilevile, vijana wanaweza kukosa kutambua mambo ya lazima zaidi katika maisha kwa sababu ya kukosa uzoefu.

2, 3. (a) Vijana Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu ili kuepuka jambo gani? (b) Ni nini inaweza kutusaidia tuone uriti wetu wa kiroho kuwa wa lazima sana?

2 Ikiwa wewe ni kijana, pengine mwenye miaka 20 hivi, ni mambo gani unaona kuwa ya lazima sana? Katika ulimwengu, watu wengi wanafikiri kwamba maisha inategemea vitu vya kimwili, ni kusema, mushahara muzuri, nyumba nzuri, ao kupata chombo fulani cha kiteknolojia cha sasa na cha hali ya juu. Hata hivyo, ikiwa tunahangaikia tu vitu hivyo, tunakosa jambo la lazima sana, ni kusema, utajiri wa kiroho. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba leo watu wengi sana hawajaanza hata kutafuta utajiri huo. Ninyi vijana ambao mulizaliwa katika familia ya Kikristo munapaswa kuwa waangalifu sana ili musikose kutambua kwamba  uriti wenu wa kiroho ni wa lazima sana. (Mt. 5:3) Kukosa kuona uriti wenu wa kiroho kuwa wa lazima sana kunaweza kuwa na matokeo mabaya katika maisha yenu yote.

3 Hata hivyo, unaweza kuzuia jambo hilo litokee. Ni nini itakusaidia uone uriti wako wa kiroho kuwa wa lazima sana? Tuchunguze sasa mifano fulani ya Biblia yenye inaweza kutusaidia tutambue sababu gani ni jambo la hekima kuona uriti wetu wa kiroho kuwa wa lazima sana. Mifano yenye tunataka kuchunguza inaweza kusaidia vijana na Wakristo wengine wote waone uriti wao wa kiroho kuwa wa lazima sana.

WALIZARAU URITI WAO WA KIROHO

4. Andiko la 1 Samweli 8:1-5 linasema nini juu ya watoto wa Samweli?

4 Biblia inazungumuzia mifano ya watu fulani wenye walizarau uriti wao wa kiroho. Jambo hilo lilitendeka katika familia ya nabii Samweli, ambaye alimutumikia Yehova tangu utoto wake na ambaye alikuwa na sifa nzuri mbele ya Mungu. (1 Sam. 12:1-5) Samweli aliwaachia watoto wake, Yoeli na Abiya, mufano muzuri. Lakini, hawakuiga mufano wake, na wakakuwa watu wabaya. Biblia inasema kwamba tofauti na baba yao, ‘walipotosha hukumu.’—Soma 1 Samweli 8:1-5.

5, 6. Watoto wa Yosia na mujukuu wake walitenda namna gani?

5 Watoto wa Mufalme Yosia walizarau pia uriti wao wa kiroho. Yosia aliwaachia mufano muzuri kuhusu namna ya kumuabudu Yehova. Wakati kitabu cha Sheria kilipatikana na kusomewa mbele yake, Mufalme Yosia alifanya yake yote ili kutumikisha maagizo ya Yehova. Alitumika kwa bidii ili kutosha ibada ya sanamu na uchawi katika inchi, na aliwatia moyo watu wamutii Yehova. (2 Fal. 22:8; 23:2, 3, 12-15, 24, 25) Bila shaka, huo ulikuwa uriti muzuri sana wa kiroho ambao watoto wake walipata. Kisha muda fulani, watoto tatu kati ya watoto wake na mujukuu (ao munkana) wake mumoja wakakuwa wafalme, lakini hakuna hata mumoja wao mwenye aliona uriti huo kuwa wa lazima.

6 Kisha Yosia kufa, Yehoahazi, mutoto wake, alikuwa mufalme, lakini ‘alifanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova.’ Alitawala kwa muda wa miezi tatu tu, kisha Farao Mufalme wa Misri akamukamata na kumutia katika gezeza. Alikufa katika inchi ya Misri akiwa mufungwa. (2 Fal. 23:31-34) Kisha, Yehoyakimu ndugu yake akatawala kwa muda wa miaka 11. Yeye pia hakuona uriti wake wa kiroho kuwa wa lazima. Kwa sababu ya mwenendo mubaya wa Yehoyakimu, Yeremia alitabiri hivi juu yake: “Atazikwa kwa maziko ya punda-dume.” (Yer. 22:17-19) Sedekia, mutoto wa Yosia, na Yehoyakini, mujukuu wake walitawala kisha yeye kufa; wakakuwa watu wabaya na hakuna hata mumoja mwenye alifuata mufano wa Yosia.—2 Fal. 24:8, 9, 18, 19.

7, 8. (a) Namna gani Sulemani alipoteza uriti wake wa kiroho? (b) Mifano ya Biblia ya watu wenye walizarau uriti wao wa kiroho inaweza kutufundisha nini?

7 Mufalme Sulemani alipata uriti muzuri sana wa kiroho kutoka kwa Daudi, baba yake. Sulemani alizaliwa katika familia yenye ilikuwa na hali nzuri ya kiroho na alianza vizuri, lakini mwishowe alizarau uriti wake wa kiroho. ‘Wakati Sulemani alikuwa muzee, wake zake wakawa wameugeuza moyo wake ukaifuata miungu mingine; na moyo wake haukuwa mukamilifu kwa Yehova Mungu wake, kama moyo wa Daudi baba yake.’ (1 Fal. 11:4) Kwa hiyo, hakuendelea kukubaliwa na Yehova.

8 Wanaume hao wenye tumezungumuzia waliriti hali nzuri ya kiroho na walikuwa na nafasi ya kufanya mambo yenye kumufurahisha Yehova. Lakini jambo la kuhuzunisha ni kwamba walizarau uriti wao wa kiroho. Lakini haiko vijana wote wenye wanazungumuziwa katika Biblia ndio walizarau uriti wao wa kiroho, na ni hivyo pia leo. Tuchunguze sasa mifano fulani mizuri yenye vijana Wakristo wanaweza kuiga.

 HAWAKUZARAU URITI WAO WA KIROHO

9. Watoto wa Noa walituachia mufano gani muzuri sana? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

9 Watoto wa Noa walituachia mufano muzuri sana. Baba yao alipewa amri ya kujenga safina na kuingiza familia yake ndani. Watoto wa Noa waliona kwamba ni jambo la lazima sana kufanya mapenzi ya Yehova. Bila shaka walimuunga baba yao mukono. Walimusaidia kujenga safina, na kisha wakaingia ndani. (Mwa. 7:1, 7) Sababu gani walifanya hivyo? Andiko la Mwanzo 7:3 linasema kwamba waliingiza wanyama ndani ya safina ‘ili kuhifazi hai uzao juu ya uso wa dunia yote.’ Wanadamu pia waliokolewa. Kwa sababu watoto wa Noa waliona uriti wao wa kiroho kuwa wa lazima sana, walipewa pendeleo la kusaidia wanadamu waendelee kuwa duniani na walipewa pia pendeleo la kurudisha ibada ya kweli katika dunia iliyosafishwa.—Mwa. 8:20; 9:18, 19.

10. Wakati walikuwa huko Babiloni, namna gani vijana ine Waebrania walionyesha kwamba mafundisho yenye walipokea yalikuwa ya lazima sana?

10 Kisha miaka mingi, vijana ine Waebrania walionyesha kwamba mambo yenye walikuwa wamejifunza ilikuwa ya lazima sana. Hanania, Mishaeli, Azaria, na Danieli walipelekwa katika utumwa huko Babiloni katika mwaka wa 617 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. Walikuwa wenye sura nzuri, wenye akili, na hawangekuwa na magumu ya kujipatanisha na maisha ya Wababiloni. Lakini hawakufanya hivyo. Walionyesha kupitia matendo yao kwamba walikumbuka uriti wao, ni kusema, mambo yenye walikuwa wamefundishwa. Vijana hao ine walibarikiwa sana kwa sababu waliendelea kushikamana na mafundisho ya kiroho yenye walipokea wakati walikuwa watoto wadogo.—Soma Danieli 1:8, 11-15, 20.

11. Namna gani watu wengine walifaidika na mambo yenye Yesu alijifunza?

11 Kati ya watu wenye waliona uriti wao wa kiroho kuwa wa lazima sana, Yesu Kristo ndiye mufano muzuri zaidi. Alijifunza mambo mengi kutoka kwa Baba yake, na aliyaona kuwa ya lazima sana. Maneno yake inaonyesha jambo hilo. Alisema hivi: “Kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.” (Yoh. 8:28) Na alipenda watu wengine wafaidike na mambo yenye alijifunza. Aliambia kikundi cha watu wengi hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Lu. 4:18, 43) Alisaidia wasikilizaji wake waone kwamba ni lazima wasikuwe “sehemu ya ulimwengu,” kwa sababu watu wa ulimwengu wanazarau mambo ya kiroho.—Yoh. 15:19.

USIZARAU URITI WAKO WA KIROHO

12. (a) Andiko la 2 Timotheo 3:14-17 linahusu namna gani vijana wengi leo? (b) Vijana Wakristo wanapaswa kujiuliza maulizo gani?

12 Kama vijana wenye tumezungumuzia, inawezekana wewe pia ulikomalia katika familia ya watumishi wa Yehova Mungu. Ikiwa ni hivyo, mambo yenye Biblia inasema juu ya Timotheo inaweza kukuhusu pia. (Soma 2 Timotheo 3:14-17.) Ni wazazi wako ndio walikufundisha kuhusu Mungu wa kweli na kuhusu namna ya kumupendeza. Inawezekana wazazi wako walianza kukufundisha tangu wakati ulikuwa mutoto mudogo. Bila shaka hilo lilikusaidia sana ‘ukuwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu kupitia imani kuhusiana na Kristo Yesu’ na lilikusaidia ukuwe “na vifaa kamili” kwa ajili ya kazi ya Mungu. Ulizo la maana ni hili: Unaona uriti wako wa kiroho kuwa wa lazima sana? Inaomba kujichunguza ili kujua. Ujiulize maulizo kama haya: ‘Ninajisikia namna gani wakati ninafikiria pendeleo langu la kuhesabiwa pamoja na mashahidi wengi waaminifu wenye waliishi mbele yangu? Ninajisikia namna gani wakati ninafikiria pendeleo langu la kuwa kati ya watu wachache walio duniani na ambao Mungu anajua? Ninaona kwamba kujua kweli ni  pendeleo kubwa sana?’

Unajisikia namna gani juu ya pendeleo la kuwa kati ya mashahidi waaminifu wa Mungu?(Ona fungu la 9, 10, na 12)

13, 14. Vijana fulani Wakristo wamejaribu kufanya nini, na sababu gani kujiingiza katika ulimwengu ni kukosa hekima? Toa mufano.

13 Vijana fulani wenye walikomalia katika familia za Kikristo wanaweza kukosa kutambua tofauti kubwa kati ya paradiso yetu ya kiroho na ulimwengu wa Shetani wenye kujaa giza. Wamoja kati yao wamejaribu hata kuingia katika ulimwengu ili kujionea. Unaweza kujitupa mbele ya motokari yenye inatembea mbio ili tu uone ikiwa motokari hiyo inaweza kukuumiza ao kukuua? Bila shaka hapana! Vilevile, hakuna lazima ya kujiingiza katika mwenendo wenye kupotoka wa ulimwengu huu ili kujionea maumivu makali yenye mwenendo huo unaweza kutokeza.—1 Pet. 4:4.

14 Gener, ndugu mwenye anaishi katika Asia, alikomalia katika familia ya Kikristo. Alibatizwa wakati alikuwa na miaka 12. Hata hivyo, kisha muda fulani, alianza kuvutiwa na tabia za ulimwengu huu. Anasema hivi: “Nilipenda kujionea ‘uhuru’ ambao ulimwengu unatoa.” Gener alianza kuwa na maisha ya unafiki. Wakati alikuwa na miaka 15 hivi, alianza kuiga tabia za marafiki wake wabaya. Kama wao, alianza kunywa pombe na kutukana watu. Mara nyingi, Gener alikuwa anarudi usiku sana nyumbani, kisha kucheza muchezo wa biyar (billard) na michezo fulani ya ordinatere yenye kuchochea watu kuuana ao kupigana. Lakini kisha kipindi fulani, alianza kutambua kwamba ulimwengu huu haulete furaha ya kweli. Alitambua kwamba namna yake ya kuishi haikuwa na maana. Sasa amerudi katika kutaniko. Anasema hivi: “Ningali ninapambana na magumu mengi, lakini baraka za Yehova ni nyingi sana kuliko magumu hayo.”

15. Vijana Wakristo wenye hawakukomalia katika familia za Kikristo wanapaswa kufikiria jambo gani?

15 Bila shaka, kuna vijana wengine katika kutaniko ambao hawakukomalia katika familia za Kikristo. Ikiwa wewe ni mumoja wao, fikiria pendeleo kubwa lenye unapata tangu sasa kwa sababu unamujua Muumbaji na unamutumikia! Kuna watu zaidi ya bilioni saba (7000000000) duniani. Kwa hiyo, ni baraka kubwa kuwa kati ya watu wenye Yehova amevuta kwake na ambao amefunulia kweli ya Biblia. (Yoh. 6:44, 45) Karibu mutu mumoja tu juu ya kila watu 1000 ambao wanaishi leo ndiye ana ujuzi sahihi wa kweli; na wewe ni mumoja wao. Jambo hilo linaweza kutuletea sisi wote furaha, hata kama tulijifunza kweli namna gani. (Soma 1 Wakorintho 2:12.) Gener anasema hivi: “Wakati ninafikiria jambo hilo ninaona  kwamba nimepewa pendeleo kubwa sana. Mimi ni nani ili nijulikane na Yehova, Yule mwenye aliumba ulimwengu wote muzima?” (Zab. 8:4) Dada mumoja wa eneo hilohilo alisema hivi: “Wanafunzi wanafurahi sana wakati wanajulikana na mwalimu wao. Sisi tunafurahi zaidi wakati tunafikiria pendeleo kubwa zaidi la kujulikana na Yehova, Mufundishaji Mukubwa.”

UTAFANYA NINI?

16. Vijana Wakristo wanaweza kuchagua kufanya jambo gani la hekima?

16 Kwa kufikiria pendeleo kubwa lenye umepewa, hauone kwamba unapaswa kuazimia hata zaidi kuwa kati ya watu wachache wenye wametumia vizuri maisha yao? Kwa kufanya hivyo, utahesabiwa kati ya watumishi wengi waaminifu wa Mungu. Ni jambo la hekima zaidi kufanya hivyo kuliko kufuata vijana wengi ambao wanatumia maisha yao ovyoovyo katika ulimwengu huu wenye unakaribia kuharibiwa.—2 Kor. 4:3, 4.

17-19. Ni nini itakusaidia kuwa na maoni yenye kufaa kuhusu kuwa tofauti na ulimwengu?

17 Bila shaka, hilo halimaanishe kwamba sikuzote itakuwa vyepesi kujitenga na ulimwengu. Hata hivyo, ukifikiri sana juu ya jambo hilo, utaona kwamba ni jambo la hekima kujitenga na ulimwengu. Tuchukue mufano wa mwanamichezo ya Olimpike. Bila shaka, anapaswa kuwa tofauti na wengine ili afikie muradi wake. Ili apate wakati mwingi wa kujizoeza, anapaswa kujiima mambo mengi yenye inaweza kumuchukua wakati na kumukengeusha. Tena, kwa sababu iko tayari kuwa tofauti na wengine, ataweza kujizoeza zaidi ili afikie muradi wake.

18 Watu wa ulimwengu hawafikirie matokeo mabaya ya matendo yao. Kufikiri juu ya wakati unaokuja kutakusaidia ukuwe tofauti na ulimwengu kwa kuepuka mwenendo wake muchafu na mazoea yenye kuharibu hali ya kiroho; kwa kufanya hivyo ‘utaushika imara uzima ulio wa kweli.’ (1 Tim. 6:19) Dada mwenye tumekwisha kutaja anasema hivi: “Ikiwa unashikamana kabisa na mambo yenye unaamini, utajisikia vizuri sana mwishoni mwa siku. Hilo litaonyesha kwamba umepata nguvu ya kujitenga na ulimwengu wa Shetani. Zaidi ya yote, itakuwa kama vile unamuona Yehova anapendezwa na wewe na anakutazama na sura yenye furaha. Na wakati huo unajisikia vizuri sana kwa sababu uko tofauti na ulimwengu huu!”

19 Maisha haina maana ikiwa mutu anahangaikia tu mambo yenye anaweza kupata sasa. (Mhu. 9:2, 10) Ikiwa wewe ni kijana na unafikiri sana juu ya kusudi na urefu wa maisha yako, hauone kwamba ni vizuri uepuke “kutembea kama vile mataifa,” lakini ni jambo la hekima uishi maisha yenye kuwa na maana?—Efe. 4:17; Mal. 3:18.

20, 21. Tutapata nini ikiwa tunafanya maamuzi mazuri, na Yehova anatuomba tufanye nini?

20 Ikiwa tunafanya maamuzi mazuri, tutakuwa na maisha yenye furaha tangu sasa na ‘tutariti dunia,’ ni kusema, tutapata uzima wa milele. Tutapata baraka nyingi sana kuliko hata namna tunawazia. (Mt. 5:5; 19:29; 25:34) Tunapaswa kujua kwamba, Mungu hatatupatia baraka hizo bila sisi kufanya kitu fulani. Kuna mambo yenye anatuomba tufanye. (Soma 1 Yohana 5:3, 4.) Lakini, anastahili tumutumikie kwa uaminifu!

21 Ni pendeleo kubwa sana kuona mambo mengi yenye Yehova ametupatia! Tunajua vizuri sana Neno la Mungu na tunaelewa vizuri ukweli juu yake na makusudi yake. Tunafurahia pendeleo la kuitwa kwa jina lake na kuwa Mashahidi wake. Mungu anatuhakikishia kwamba iko upande wetu. (Zab. 118:7) Iwe sisi ni vijana ao hapana, sisi wote tuonyeshe kwamba tunaona uriti wetu wa kiroho kuwa wa lazima sana. Tutafanya hivyo kwa kuonyesha katika maisha yetu kwamba tunapenda kabisa kumutolea Yehova “utukufu milele.”—Rom. 11:33-36; Zab. 33:12.