Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Utaendelea Kukesha’?

‘Utaendelea Kukesha’?

‘Kwa hiyo, muendelee kukesha kwa sababu hamujue ile siku wala saa.’MT. 25:13.

1, 2. (a) Yesu alisema nini juu ya siku za mwisho? (b) Tutachunguza maulizo gani?

WAZIA unamuona Yesu na wanafunzi wake ine wanakaa kwenye Mulima wa Mizeituni, na wanaangalia hekalu la Yerusalemu. Wakati huo, Yesu anazungumuzia unabii moja kati ya unabii mbalimbali wenye kuvutia. Petro, Andrea, Yakobo na Yohana wanamusikiliza kwa uangalifu wakati anaonyesha kwamba unabii huo utatimia wakati unaokuja. Anawaambia mambo mengi juu ya siku za mwisho za ulimwengu huu muovu, wakati angekuwa anatawala katika Ufalme wa Mungu. Anawaambia kwamba wakati huo wa maana sana, atamuweka ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara’ hapa duniani na kwamba mutumwa huyo atakuwa anapatia wafuasi wake chakula cha kiroho chenye wanahitaji kwa wakati unaofaa.—Mt. 24:45-47.

2 Kisha, katika unabii huohuo, Yesu alitoa mufano wa mabikira kumi. (Soma Mathayo 25:1-13.) Katika habari hii tutachunguza maulizo haya: (1) Mufano huo unatutolea ujumbe gani wa maana? (2) Namna gani Wakristo watiwa-mafuta wametumia shauri la mufano huo, na wamepata matokeo gani? (3) Namna gani kila mumoja wetu anaweza kufaidika na mufano huo leo?

MUFANO WA MABIKIRA KUMI UNATUTOLEA UJUMBE GANI?

3. Zamani, vichapo vyetu vilitumia njia gani ili kufasiria mufano wa mabikira kumi, na inawezekana matokeo ilikuwa nini?

3 Katika habari yenye ilitangulia, tuliona kwamba katika miaka ya hivi karibuni, hatua kwa hatua mutumwa mwaminifu amefasiria habari zenye kuzungumuziwa katika Biblia bila kukazia sana mambo yenye habari hizo zingefananisha wakati unaokuja. Sasa anakazia zaidi sana mambo yenye tunajifunza katika habari hizo. Zamani, vichapo vyetu vilikazia mambo madogo-madogo ya mufano wa Yesu wa mabikira kumi, kama vile, tala, mafuta ya tala, chupa za kutia ndani mafuta, na mambo mengine. Tunaweza kusema kwamba kukazia sana mambo madogo-madogo ya mufano huo, kulikuwa kunatufanya tusielewe ujumbe mwepesi na wa haraka sana wa mufano huo? Kama vile tutaona, jibu la ulizo hilo ni la maana sana.

4. Katika mufano wa mabikira kumi, namna gani tunaweza kutambua (a) bwana-arusi? (b) mabikira?

4 Tuzungumuzie sasa ujumbe wa maana sana wenye kupatikana katika mufano huo wa Yesu. Kwanza, tuone watu wenye kuzungumuziwa sana katika mufano huo. Katika mufano huo, bwana-arusi ni nani? Bila shaka, Yesu alikuwa anazungumuza juu yake mwenyewe. Tunasema hivyo kwa sababu wakati mwingine alijiita kuwa bwana-arusi! (Lu. 5:34, 35) Mabikira wenye kuzungumuziwa katika mufano huo ni nani? Yesu anasema kwamba mabikira wanapaswa kuwa tayari na tala zao wakati bwana-arusi anakuja. Pia, Yesu anatolea “kundi ndogo” la wafuasi watiwa-mafuta shauri hili: ‘Viuno vyenu na vifungwe mishipi na tala zenu ziwe zikiwaka, nanyi mutakuwa kama watu wanaomungoja bwana wao wakati anaporudi kutoka kwenye karamu ya ndoa.’ (Lu. 12:32, 35, 36) Zaidi ya hilo, mutume Paulo na mutume Yohana waliongozwa na roho ya Mungu ili kuandika maneno yenye kuonyesha kwamba wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo ni mabikira safi. (2 Kor. 11:2; Ufu. 14:4) Bila shaka, Yesu alitumia mufano ulio kwenye Mathayo 25:1-13 ili kushauria wafuasi wake watiwa-mafuta na kuwaonya.

5. Namna gani Yesu alionyesha wakati ambao mufano wake utatimia?

5 Pili, tuchunguze namna matukio yanafuatana. Shauri la Yesu linahusu kipindi gani cha wakati? Yesu anatusaidia kuelewa kipindi hicho cha wakati katika maneno ya kumalizia ya mufano wake. Alisema hivi: “Bwana-arusi akafika [akakuja].” (Mt. 25:10) Kama vile tulijifunza katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 7, 2013, neno “kuja” ao kufika kwake, linatumiwa mara munane katika unabii wa Yesu wenye kupatikana kwenye Mathayo sura ya 24 na 25. Na katika unabii huo, ni neno lilelile la Kigiriki ndilo linatumiwa. Katika unabii huo, kila mara Yesu alizungumuzia wakati atakuja, ni kusema, wakati wa ziki kubwa ili kuhukumu na kuharibu ulimwengu huu muovu. Kwa hiyo, tunaweza kusema kwamba mufano huo wa Yesu unahusu siku za mwisho, lakini utatimia kabisa wakati wa ziki kubwa.

6. Ni ujumbe gani wa maana wenye kupatikana katika mufano wa Yesu wa mabikira kumi?

6 Mufano huo wa Yesu unatutolea ujumbe gani wa maana? Tufikirie habari yenye Yesu alizungumuzia mbele ya kutoa mufano huo. Alikuwa ametoka tu kuzungumuza juu ya ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara.’ Mutumwa huyo angekuwa kikundi kidogo cha wanaume watiwa-mafuta wenye wangeongoza wafuasi wa Kristo katika siku za mwisho. Yesu aliwashauria kwamba wanapaswa kubakia waaminifu. Kisha, alitoa mufano wa mabikira kumi ili kuonya wafuasi wote watiwa-mafuta katika siku za mwisho kwamba wanapaswa ‘kuendelea kukesha’ ili wasipoteze zawadi yao nzuri sana. (Mt. 25:13) Acha sasa tuchunguze mufano huo na tuone namna wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo wametumia shauri hilo.

NAMNA GANI WATIWA-MAFUTA WAMETUMIA SHAURI LA MUFANO WA MABIKIRA KUMI?

7, 8. (a) Sababu gani mabikira tano wenye busara walikuwa tayari? (b) Namna gani watiwa-mafuta wameonyesha kwamba wako tayari?

7 Mufano wa Yesu unaonyesha kwamba bwana-arusi aliwakuta mabikira wenye busara wakiwa tayari, lakini wale wapumbavu hawakuwa tayari. Sababu gani mabikira wenye busara walikuwa tayari? Kuna sababu mbili: Walijitayarisha kwa ajili ya kuja kwa bwana-arusi na walikesha. Mabikira kumi hao ambao waliombwa kukesha wakati wa usiku ili kungojea bwana-arusi, walipaswa kuacha tala zao zenye kuwaka, na kuendelea kukesha usiku wote mupaka bwana-arusi afike. Hata hivyo, tofauti na wale mabikira wapumbavu, mabikira tano wenye busara walikuwa tayari kabisa kwa sababu walileta mafuta mengine katika chupa zao kwa ajili ya tala zao. Watiwa-mafuta waaminifu wamejitayarisha hivyo kwa ajili ya kuja kwa Yesu?

8 Bila shaka! Katika siku hizi za mwisho, Wakristo watiwa-mafuta wametenda kama mabikira wenye busara. Wako tayari kutimiza kwa uaminifu mugawo wao mupaka mwisho. Wanaelewa kwamba ili waendelee kumutumikia Mungu kwa uaminifu, wanapaswa kuachana na faida za kimwili zenye ulimwengu wa Shetani unaweza kuwatolea. Wamejitoa ili kumutumikia Yehova kwa uaminifu, si kwa sababu ule mwisho unakaribia, lakini kwa sababu wanamupenda Yehova na Mwana wake. Wanaendelea kuwa washikamanifu kwa kuepuka roho ya ulimwengu huu yenye kuchochea watu kupenda sana vitu vya kimwili, wakuwe na mwenendo mubaya, na waonyeshe roho ya kujipenda wenyewe. Kwa hiyo, wanaendelea kuwa tayari, imara, na kuangaza kama nuru, na hawaone kwamba Bwana-arusi anakawia kuja.—Flp. 2:15.

9. (a) Yesu alitoa shauri gani kuhusu hali ya kusinzia? (b) Namna gani Wakristo watiwa-mafuta wameitikia sauti kubwa yenye kusema, “Huyu hapa bwana-arusi”? (Ona maelezo ya chini.)

9 Mabikira hao walikuwa tayari kwa sababu walikesha. Inawezekana leo Wakristo watiwa-mafuta walale usingizi wakati wa kukesha? Ndiyo. Katika mufano wake, Yesu alisema kwamba mabikira kumi “walisinzia na kuanza kulala” wakati bwana-arusi alionekana kuwa mwenye kukawia. Yesu alijua vizuri kwamba uzaifu wa mwili unaweza kufanya mutu mwenye nia nzuri akose kuendelea kukesha. Wakristo watiwa-mafuta waaminifu wameelewa maana ya onyo hilo, na wamejikaza sana ili kuendelea kukesha. Katika mufano wa Yesu, katikati ya usiku, mabikira wote walisikia sauti kubwa yenye kusema: “Huyu hapa bwana-arusi!” Lakini ni mabikira wenye busara tu ndio walivumilia mupaka mwisho. (Mt. 25:5, 6; 26:41) Tuseme nini juu ya Wakristo watiwa-mafuta leo? Vilevile, tangu siku za mwisho zilianza na kuendelea, Wakristo watiwa-mafuta wameitikia sauti yenye kusema: “Huyu hapa bwana-arusi.” Wako hakika kabisa kwamba Bwana-arusi iko karibu kuja. Kwa hiyo, wamevumilia na kuendelea kuwa tayari zaidi ili kumungojea bwana-arusi. * Hata hivyo, maneno ya kumalizia ya mufano huo inahusu kipindi fulani cha wakati. Namna gani?

MABIKIRA WENYE BUSARA WANAPATA ZAWADI NA WAPUMBAVU WANAAZIBIWA

10. Mazungumuzo kati ya mabikira wapumbavu na mabikira wenye busara yanatokeza ulizo gani lenye linaweza kuwa vigumu kuelewa?

10 Pengine inaweza kuwa vigumu sana kuelewa maneno ya kumalizia ya mufano huo wa Yesu. Katika maneno hayo, mabikira wapumbavu wanaomba musaada kwa wale wenye busara, lakini mabikira wenye busara wanakataa kuwasaidia. (Soma Mathayo 25:8, 9.) Maneno hayo ya kumalizia yanatokeza ulizo hili lenye linaweza kuwa vigumu kuelewa: “Katika historia ya watu wa Mungu, ni wakati gani Wakristo watiwa-mafuta wangekataa kusaidia wale wenye kuwa na lazima ya musaada?” Kuchunguza namna matukio yanafuatana, kunatusaidia tuelewe maneno ya kumalizia ya mufano huo. Tukumbuke kwamba mafasirio mapya yanaonyesha kama Yesu, Bwana-arusi, atakuja kuleta hukumu mbele ziki kubwa imalizike. Inaonekana kwamba maneno hayo ya kumalizia ya mufano huo inahusu mambo fulani yenye itatokea mbele ziki kubwa imalizike. Sababu gani tunasema hivyo? Kwa sababu wakati huo, Wakristo watiwa-mafuta watakuwa wametiwa muhuri kwa mara ya mwisho.

11. (a) Ni mambo gani itatokea mbele ya ziki kubwa kuanza? (b) Mabikira wenye busara walimaanisha nini wakati waliambia wale wapumbavu waende kuuza mafuta ya tala?

11 Kwa hiyo, mbele ziki kubwa ianze Wakristo wote watiwa-mafuta waaminifu watakuwa wametiwa muhuri kwa mara ya mwisho. (Ufu. 7:1-4) Kuanzia wakati huo, watakuwa hakika kwamba wataenda mbinguni. Lakini fikiria miaka ya mbele ziki kubwa kuanza. Wakristo watiwa-mafuta wenye hawakukesha, ni kusema, hawakubaki waaminifu, watapatwa na nini? Watapoteza pendeleo lao la kuenda mbinguni. Ni wazi kwamba, hawatatiwa muhuri kwa mara ya mwisho. Wakati huo, Wakristo wengine watiwa-mafuta watachaguliwa. Inawezekana wakati ziki kubwa itaanza, wale wapumbavu watashituka kuona namna Babiloni Mukubwa anaharibiwa. Labda ni wakati huo tu ndio watatambua kwamba hawakuwa tayari kwa ajili ya kuja kwa Bwana-arusi. Ikiwa watu hao watalilia musaada wakati huo wa mwisho-mwisho, ni nini itatokea? Mufano wa Yesu unatoa jibu lenye kuhuzunisha. Katika mufano huo, mabikira wenye busara wanakataa kuwapatia wale wapumbavu mafuta kwa ajili ya tala zao, na wanawaambia kwamba waende nafasi pa kuuzishia mafuta ya tala. Usisahau kwamba wakati huo ilikuwa “katikati ya usiku.” Wangepata watu wenye kuuzisha mafuta ya tala wakati huo? Hapana. Walikuwa wamechelewa sana.

12. (a) Wakati wa ziki kubwa, ni jambo gani lenye kuhuzunisha litawapata watiwa-mafuta wenye hawakubaki waaminifu mbele ya kutiwa muhuri kwa mara ya mwisho? (b) Wale wenye kufananishwa na mabikira wapumbavu watapatwa na nini?

12 Vilevile, wakati wa ziki kubwa, Wakristo watiwa-mafuta waaminifu hawatasaidia wale wenye hawakuendelea kuwa waaminifu. Hawatapata musaada fulani wakati huo. Watakuwa wamechelewa sana. Kisha, watapatwa na nini? Yesu alionyesha jambo lenye lilitokea wakati mabikira wapumbavu walienda kutafuta mafuta. Alisema hivi: ‘Bwana-arusi akafika, na wale mabikira waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye kwenye karamu ya arusi; nao mulango ukafungwa.’ Wakati Kristo atakuja katika utukufu wake mbele ziki kubwa imalizike, atakusanya wafuasi wake watiwa-mafuta waaminifu huko mbinguni. (Mt. 24:31; 25:10; Yoh. 14:1-3; 1 Tes. 4:17) Bila shaka, mulango utafungwa ili wale wenye hawakuendelea kuwa waaminifu, ni kusema, wale wenye kufananishwa na mabikira wapumbavu, wasiingie. Kwa hiyo, watalia: ‘Bwana, bwana, utufungulie!’ Lakini atawaambia kama vile ataambia wale wenye kufananishwa na mbuzi wakati wa hukumu. Atasema hivi: ‘Ninawaambia ninyi kweli, Siwajue ninyi.’ Itakuwa jibu lenye kuhuzunisha kabisa!—Mt. 7:21-23; 25:11, 12.

13. (a) Sababu gani hatupaswe kusema kwamba wengi kati ya Wakristo watiwa-mafuta hawataendelea kuwa waaminifu? (b) Sababu gani onyo lenye kupatikana katika mufano wa Yesu linaonyesha pia kwamba anawatumainia Wakristo watiwa-mafuta? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

13 Kulingana na mambo yenye tumekwisha kuzungumuzia, tunaweza kusema nini? Yesu alikuwa anasema kwamba Wakristo wengi watiwa-mafuta hawataendelea kuwa waaminifu na kwamba wengine watachukua nafasi yao? Hapana. Kumbuka kwamba, alikuwa ametoka tu kumuonya ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara’ kwamba asigeuke na kuwa mutumwa muovu. Kwa kutoa onyo hilo, Yesu hakumaanisha kwamba mutumwa huyo angegeuka na kuwa mutumwa muovu. Vilevile, mufano huo wa Yesu unatoa onyo kubwa. Kama vile mabikira tano walikuwa wapumbavu na wengine tano walikuwa wenye busara, kila Mukristo mutiwa-mafuta iko na uwezo wa kuchagua ikiwa atakuwa tayari na kuendelea kukesha ao ikiwa atakuwa mupumbavu na kukosa uaminifu. Mutume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu ili atoe mashauri yenye kufanana na hayo wakati aliwaandikia Wakristo wenzake watiwa-mafuta. (Soma Waebrania 6:4-9; linganisha na Kumbukumbu la Torati 30:19.) Ona kwamba mashauri hayo ya mutume Paulo yalikuwa mazito, lakini alitumia pia maneno yenye upendo ili kuonyesha kama alikuwa hakika kwamba ndugu na dada zake Wakristo watapata ‘mambo yaliyo bora [mazuri zaidi]’ yenye kuwa mbele yao. Vilevile, onyo lenye kupatikana katika mufano wa Yesu linaonyesha kwamba anawatumainia kabisa Wakristo watiwa-mafuta. Kristo anajua kwamba kila mufuasi wake mutiwa-mafuta anaweza kubakia mwaminifu na kupata zawadi nzuri sana!

“KONDOO WENGINE” WA KRISTO WANAFAIDIKA NAMNA GANI?

14. Sababu gani “kondoo wengine” wanaweza pia kufaidika na mufano wa mabikira kumi?

14 Kwa sababu mufano wa Yesu wa mabikira kumi unahusu Wakristo watiwa-mafuta, tunaweza kusema kwamba “kondoo wengine” wanaweza pia kufaidika na mufano huo? (Yoh. 10:16) Ndiyo! Kumbuka kwamba mufano huo unatutolea ujumbe huu wenye kuwa wazi: ‘Muendelee kukesha.’ Ujumbe huo unahusu tu Wakristo watiwa-mafuta? Wakati fulani, Yesu alisema hivi: ‘Lile ninalowaambia ninyi ninawaambia wote, Muendelee kukesha.’ (Mk. 13:37) Yesu anaomba wafuasi wake wote watayarishe mioyo yao ili wafanye kazi kwa uaminifu, na anawaomba wote waendelee kukesha. Kwa hiyo, Wakristo wote wanaombwa kufuata mufano wa Wakristo watiwa-mafuta kwa kuendelea kutia kazi ya kuhubiri pa nafasi ya kwanza katika maisha yao. Usisahau kwamba wale mabikira wapumbavu waliomba mabikira wenye busara wawasaidie na mafuta ya tala. Ombi lao lenye halina maana, linatukumbusha kwamba hakuna mutu anaweza kuwa mwaminifu pa nafasi yetu, kubaki katika kweli kwa ajili yetu, ao kuendelea kukesha pa nafasi yetu. Kila mumoja wetu atatoa hesabu mbele ya Yesu Kristo, Muamuzi mwenye haki ambaye Yehova ameweka. Kwa hiyo, tunapaswa kuwa tayari, kwa sababu atakuja hivi karibuni!

Ombi la kuomba mafuta ya tala linatukumbusha kwamba hakuna mutu anaweza kukesha ao kuwa mwaminifu pa nafasi yetu

15. Sababu gani Wakristo wote wa kweli watafurahia ndoa ya Kristo pamoja na bibi-arusi?

15 Wakristo wote wanaweza kufaidika pia na tukio la maana sana lenye kuzungumuziwa katika mufano wa Yesu. Sisi wote tutafurahia ndoa hiyo yenye itafanyika hivi karibuni. Kisha vita ya Har-magedoni, Wakristo watiwa-mafuta watakuwa bibi-arusi wa Kristo huko mbinguni. (Ufu. 19:7-9) Kisha, kila mwanadamu mwenye kuwa na tumaini la kuishi hapa duniani, atafaidika na ndoa hiyo ya mbinguni, kwa sababu itawaletea wanadamu serikali kamilifu. Iwe uko na tumaini la kuenda mbinguni ao la kuishi hapa duniani, sisi wote tuazimie kujifunza somo la maana sana lenye kupatikana katika mufano wa mabikira kumi. Kwa hiyo, tuendelee kuwa tayari kwa kutayarisha mioyo yetu na tuendelee kuwa imara, na kukesha zaidi ili tuweze kufurahia wakati muzuri sana wenye Yehova ametuwekea!

^ fu. 9 Katika mufano huo wa Yesu, kuna kipindi fulani cha wakati kati ya sauti kubwa yenye kusema, “Huyu hapa bwana-arusi!” (mustari wa 6) na kuja kwa bwana-arusi (mustari wa 10). Katika siku hizi za mwisho, Wakristo watiwa-mafuta wenye kukesha wameelewa vizuri alama yenye kuonyesha kuwapo kwa Yesu. Kwa hiyo, wanajua kwamba iko “hapa,” ni kusema, anatawala katika mamlaka ya Ufalme. Wanaendelea kuvumilia mupaka wakati atakuja.